Serikali ya Tanzania kwa mara ya kwanza katika historia imetenga Shilingi Bilioni 6.3 kwa ajili ya miradi ya utafiti wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, huku Shilingi Milioni 600 zikielekezwa katika miradi ya usalama wa chakula.

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dkt. Amos Nungu, amebainisha hayo katika mkutano na wanahabari kuelekea maadhimisho ya miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, kupitia ushirikiano wa kimkakati kati ya Serikali ya Tanzania na nchi rafiki pamoja na taasisi za kimataifa, COSTECH imepokea Shilingi Bilioni 5.65 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya utafiti wa pamoja kati ya watafiti wa Tanzania na washirika wao.

Serikali imeendelea kuwekeza katika sekta ya sayansi, teknolojia na ubunifu ambapo Shilingi Bilioni 25.7 zimetengwa kwa tafiti, ubunifu na maendeleo ya teknolojia kupitia COSTECH. Zaidi ya tafiti 50 katika sekta za elimu, kilimo, afya, na mazingira zimefadhiliwa ili kuhakikisha maarifa haya yanatumika kuboresha maisha ya Watanzania.

Mbali na hayo, Serikali kupitia COSTECH imeimarisha vituo vya ubunifu 111 na kufanikisha usajili wa kampuni mpya 70 zinazotokana na wabunifu waliowezeshwa na serikali.

Dkt. Nungu amesisitiza kuwa hatua hii inathibitisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuifanya Tanzania kuwa taifa linalowekeza katika sayansi, teknolojia na ubunifu kwa maendeleo endelevu.

Share To:

OKULY BLOG

Post A Comment: