MWANZA

Wadau wa Sekta ya Milki mkoani Mwanza wamesisitizwa kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia sheria, taratibu na misingi ya taaluma ya milki ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kutoa huduma bora na zenye kuaminika kwa wananchi.

Msisitizo huo umetolewa leo Machi 17, 2026 mkoani Mwanza na Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Mkoa huo, Bw. Wilson Luge, wakati akifunga kikao kazi cha wadau wa Sekta ya Milki kilichoandaliwa na Kitengo cha Milki kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Amesema mafunzo na semina zinazotolewa kwa wadau wa Sekta ya Milki yana mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa kitaalamu pamoja na kuimarisha utendaji kazi katika kutoa huduma bora kwa wananchi, hususan katika masuala yanayohusu tathmini ya mali na usimamizi wa milki.

“Tunapenda kuishukuru Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki kwa kutoa semina na mafunzo kwa wadau wetu wa Sekta ya Milki. Mafunzo haya yatawasaidia kuongeza ujuzi na kuimarisha weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” amesema Luge.

Aidha, amewasisitiza wadau hao wa sekta ya milki kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao na kujiepusha na vitendo vinavyokiuka sheria ikiwemo kujihusisha na masuala ya utakatishaji fedha, huku akielezea umuhimu wa kufuata taratibu zote za kisheria na kitaaluma katika kutoaji huduma za tathmini ya mali.

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki (Real Estate) inaendesha mijadala ya pamoja na wadau kwa lengo la kupata maoni kuhusu utambuzi na usajili wa Wadau wa Sekta ya Milki ili kuboresha na kukuza sekta ya milki nchini.

Mijadala hiyo inalenga kutoa elimu, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazoikabili sekta ya milki nchini ambapo tayari kitengo hicho kimefanya vikao vya mijadala katika mkoa wa Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Tanga, Mwanza na Morogoro.


Zaidi ya wakazi 57,000 wilayani Mkinga mkoa wa Tanga wanatarajiwa kunufaika na mradi mkubwa wa maji wa Mkinga-Horohoro uliofikia asilimia 65 ya utekelezaji wake huku kijiji kimoja cha Mtimbwani kikiwa tayari kinapata huduma hiyo.

Mradi huo unatekelezwa na mkandarasi mzawa STC kwa gharama ya shilingi bilioni 35 ambapo utakapokamilika utaongeza huduma ya majisafi wilayani Mkinga kufikia asilimia 88.

Hayo yamebainishwa na Meneja wa RUWASA mkoa wa Tanga Mha. Upendo Lugongo wakati akitoa taarifa ya mradi kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira iliyofanya ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo Machi 17, 2026 ambapo alisema jumla ya vijiji 37 vinatarajiwa kunufaika baada ya mradi kukamilika.

Alisema katika awamu ya kwanza jumla ya vijiji 27 vitanufaika na tayari wakazi wa kijiji kimoja cha Mtimbwani wameshaanza kufurahia huduma ya maji ikiwemo shule na zahanati za kijiji hicho ambazo nazo zimeunganishiwa majisafi ya bomba.




Furaha imetanda kwa kinamama wa taasisi ya JAI baada ya kupokea sadaka ya Iftar kutoka kwa taasisi ya Ramadhani Charity Program 2026, ikiwa ni sehemu ya kuendelea kusaidia jamii katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Akizungumza wakati wa kukabidhi sadaka hiyo, Mwenyekiti wa Ramadhani Charity Program 2026, Ahmed Misanga, aliwapongeza kinamama wa JAI kwa kuwa mstari wa mbele katika kujitolea na kusaidia jamii.
Misanga alisema kuwa JAI ni washirika wa karibu wa Ramadhani Charity Program, hivyo wameona ni vyema kufika na kuwapatia sadaka ya Iftar kama ishara ya kutambua mchango wao mkubwa katika kusaidia jamii.
Aidha, alitumia fursa hiyo kumuombea dua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na viongozi wengine wa nchi ili waendelee kuiongoza Tanzania kwa amani, umoja na mafanikio.
Kwa upande wake, Kiongozi wa JAI Mkoa, Bi. Aisha Ramadhani, alisema tukio hilo ni faraja kubwa kwao kwani linaonyesha kuwa kazi wanazozifanya za kujitolea zinatambuliwa na kuthaminiwa.
Alimshukuru Ahmed Misanga na Ramadhani Charity Program kwa kuwapatia sadaka hiyo, akisema Allah atawalipa kwa wema huo na wao wataendelea kuwaombea dua kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kusaidia watu wenye uhitaji katika jamii.
Katika hafla hiyo, kinamama wa JAI walipokea msaada wa vyakula vikiwemo tambo, ngano na tende, pamoja na fedha kwa ajili ya mboga kwa ajili ya Iftar.
 
 


Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesisitiza kuwa uhuru wa vyombo vya habari nchini upo, unalindwa kisheria na unatambuliwa katika Katiba pamoja na Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, huku ikitoa wito kwa wanahabari kuzingatia maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kauli hiyo ya JAB imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo, Wakili Patrick Kipangula, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha moja kwa moja cha Hatua za Ushindi kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha Hope Channel Tanzania, leo Machi 17, 2026 jijini Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa kifungu cha 7 cha Sheria ya Huduma za Habari kinaweka bayana haki na uhuru wa vyombo vya habari, ikiwa ni pamoja na haki ya mwandishi wa habari kutafuta, kuchakata na kusambaza taarifa, huku wananchi wakiwa na haki ya kupata taarifa sahihi kuhusu maendeleo yanayowazunguka.

“Uhuru wa vyombo vya habari upo na unalindwa kisheria. Mwandishi ana haki ya kutafuta na kusambaza taarifa, na mwananchi ana haki ya kupata taarifa. Huu ndio msingi wa uwazi na uwajibikaji katika jamii,” amesema Wakili Kipangula.

Hata hivyo, amesisitiza kuwa uhuru huo unaambatana na wajibu wa kuzingatia maadili ya taaluma, akibainisha kuwa dhana ya uwajibikaji haipaswi kuchanganywa na kile kinachoitwa ukandamizaji wa vyombo vya habari.

Amebainisha kuwa baadhi ya malalamiko ya ukandamizaji yanatokana na kutokuzingatia misingi ya kitaaluma, hususan pale ambapo taarifa zinapotolewa bila uthibitisho, uwiano au kwa lugha isiyozingatia maadili.




“Ni muhimu kutofautisha kati ya uwajibikaji na ukandamizaji. Usipozingatia maadili ya taaluma, usiseme unakandamizwa. Uwajibikaji ni sehemu ya taaluma, na haupaswi kutafsiriwa kama kubanwa kwa uhuru wa habari,” amesisitiza Kipangula.

Katika hatua nyingine, Wakili Kipangula ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya sekta ya habari kupitia mageuzi ya kisheria na kisera, ikiwemo kufutwa kwa Sheria ya Magazeti iliyokuwa ikitajwa kuwa kandamizi na kuanzishwa kwa Sheria ya Huduma za Habari inayolenga kuimarisha uhuru, uwajibikaji na weledi katika tasnia hiyo.

Amesema maboresho hayo yameleta mwelekeo mpya unaowezesha vyombo vya habari na wanahabari kufanya kazi zao kwa uhuru zaidi, huku wakizingatia viwango vinavyokubalika kitaaluma na kisheria.

Aidha, ametoa wito kwa wanahabari kuendelea kuilinda taaluma yao kwa kuzingatia ukweli, usahihi na uwiano katika utoaji wa taarifa, sambamba na kuheshimu haki za wananchi za kupata taarifa sahihi na kwa wakati kwa mujibu wa Sheria ya Kupata Taarifa.

Amesisitiza umuhimu kwa waajiri kote nchini kuhakikisha wanapata wataalamu wenye sifa stahiki kuingia katika menejimenti zao, sanjari na kuwatumia waandishi wenye ithibati, katika kazi zote za kihabari ili kulinda na kuipa thamani taaluma ya uandishi wa habari.

  



Na OWM - TAMISEMI, Arusha

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI, Mhe. Florent Kyombo ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mkoa na Serikali za Mitaa (OWM- TAMISEMI), kwa usimamizi mzuri wa utekelezaji wa miradi ya TACTIC katika Jiji la Arusha, miradi ambayo imeweka kiwango bora cha utekelezaji wa miradi ya aina hiyo ambayo inatekelezwa katika miji na majiji 45 nchini.

Mhe.  Kyombo ametoa pongezi hizo leo Machi 17, 2026 mara baada ya kamati yake kutembelea, kukagua na kuridhishwa na usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani (Bondeni City Bus Terminal), ujenzi wa soko la Mrombo, ujenzi wa soko la Kilombero pamoja na ujenzi wa mradi wa uboreshaji wa bustani ya mapumziko Themi.

“Naungana na wajumbe wenzangu kutoa pongezi za dhati kwa utekelezaji mzuri wa miradi ya TACTIC katika jiji la Arusha, hakika utekelezaji wa miradi hii umeweka kiwango bora cha namna ya kutekeleza miradi ya aina hii nchini,” amesistiza Prof. Shemdoe.

Aidha, Mhe. Kyombo amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha za utekelezaji wa miradi pamoja na kumpa dhamana ya usimamizi wa miradi hiyo Prof. Shemdoe na watendaji wanaomsaidia, ambao wanaitendea haki dhamana waliyopewa na Mheshimiwa Rais.

Sanjari na hilo, Mhe. Kyombo amempongeza Mkandarasi wa Kampuni ya M/S MOHAMMEDI BUILDERS LIMITED kwa kiwango kizuri cha utekelezaji wa miradi yote minne ya TACTIC inayotekelezwa katika jiji la Arusha, ambayo itachochea ukuaji wa uchumi ndani ya jiji hilo.

Akizungumzia suala la ushirikishaji wa wadau katika miradi hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema kuwa kabla ya kuanza kutekelezwa miradi hiyo,  timu ya kuandaa mazingira ya utekelezaji wa mradi hupita ikiwa na fomu maaluum ya kupokea maoni ya wadau kuhusiana na mradi husika, na kuongeza kuwa maoni ya wadau yalizingatiwa kwani hicho ni kigezo muhimu cha miradi yote inayotekelezwa na Benki ya Dunia.

Naye mmoja wa Wajumbe wa Kamati hiyo ya Bunge ya Kudumu ya TAMISEMI Mhe. Hawa Mwaifunga, amesema amefarijika kuona hatua nzuri iliyofikiwa ya Ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani  na kuongeza kuwa kituo hicho kitakapokamilika kitakuwa na manufaa kwa wananchi wa Jiji la Arusha.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI Mhe. Jafari Chege ameupongeza uongozi wa mkoa na Jiji la Arusha kwa kutekeleza vizuri miradi ya TACTIC ambayo imelenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kukuza uchumi wa wananchi wa Jiji la Arusha.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Diwani wa Kata ya Themi Mhe. Melance Kinabo, amemshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kulijali Jiji la Arusha kwa kuliletea fedha za utekelezaji wa miradi minne ya TACTIC, ambayo ikikamilika itaongeza wigo wa wananchi kupata ajira zitakazowaingizia kipato.

 



Na Mwandishi Wetu, Tanga.


Wananchi wa Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga wanatarajiwa kunufaika zaidi kiuchumi kupitia uwekezaji wa Serikali katika sekta ya kilimo cha mwani, hatua inayolenga kuongeza thamani ya mazao ya bahari na kuboresha maisha ya jamii za pwani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kaushio jipya na mashine mbili za kisasa za kusaga mwani uliofanyika tarehe 16 Machi 2026 katika Kijiji cha Kichaka Miba, Wilaya ya Mkinga, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy H. Nderiananga, amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuimarisha uchumi wa wananchi wa maeneo ya pwani.

Mradi wa Kuimarisha Usalama wa Bahari unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), na unatekelezwa na Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Tawi la Mwanza kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ambapo Lengo lake ni kuimarisha ufuatiliaji na ulinzi wa bahari pamoja na kuongeza thamani ya rasilimali za baharini kwa manufaa ya jamii.

Mhe. Nderiananga amesema kupitia mradi huo, Serikali imenunua boti mbili za doria, kujenga kaushio la kisasa la mwani, kusimika mashine za kusaga mwani na kutoa mafunzo kwa vikundi vya wakulima. Ameongeza kuwa hatua hizo zitaboresha ubora wa mwani, kupanua masoko, kuongeza kipato cha wakulima na kusaidia kuzuia vitendo vya kihalifu baharini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP), Dkt. Guvenail Mkonoko, amesema kabla ya utekelezaji wa mradi huo wataalamu walifanya tathmini iliyobaini changamoto za mbinu duni za kilimo, ukaushaji usio salama na ukosefu wa miundombinu ya kisasa ya uchakataji. 





Naye mwakilishi wa wakulima wa mwani, Bi. Mwamvua Bwebwe, Ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kuongeza uzalishaji, kupunguza upotevu wa mazao na kuboresha kipato chao.


Morogoro:

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo imeongoza kampeni ya kupanda miti mkoani Morogoro ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani, inayofikia kilele chake kila mwaka tarehe 22 Machi, kwa lengo la kulinda vyanzo vya maji na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza wakati zoezi hilo, Wilfred Mwakalosi, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, alisema taasisi hiyo kwa kushirikiana na Ofisi ya Bonde la Maji la Wami Ruvu na Wakala wa Huduma za Misitu ( TFS) wamefanikiwa kupanda miti zaidi ya 5,000 katika eneo linalozunguka mto Lukulunge, Kata ya Mzumbe, mkoani Morogoro.

Mwakalosi alibainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuhifadhi mazingira, vyanzo vya maji na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji kqtika maeneo mbalimbali nchini. “Morogoro ni miongoni mwa maeneo yaliyokuwa na vyanzo vingi vya maji hapo awali, lakini kwa sasa hali imebadilika kwa kiasi kikubwa kutokana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, hivyo kutishia upatikanaji wa maji kwa wakazi wake” alieleza.

Mhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) wa Wilaya ya Morogoro, Stanley Kweka, alisema uharibifu wa misitu umechangia kupungua kwa kina cha maji katika Bwawa la Mindu, huku mmomonyoko wa udongo ukiendelea kuwa tatizo kubwa hivyo upandaji wa miti ni suluhisho muhimu katika kulinda kingo za mito na kuhakikisha vyanzo vya maji vinabaki salama kwa matumizi ya sasa na baadaye.

Naye  Meneja wa Uratibu wa Mazingira na Jumuiya za Watumia Maji kutoka Bodi ya Bonde la ya Maji la Wami/Ruvu Janeth Kisoma,alisema mto Lukulunge ni chanzo muhimu kinachochangia maji katika Bwawa la Mindu, ambalo linahudumia zaidi ya asilimia 75 ya wakazi wa Manispaa ya Morogoro, hivyo uhifadhi wake unahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali.

 


Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Tawala wa Mikoa na  Serikali wa Mitaa - TAMISEMI,  wameridhishwa na kupongeza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa shule mpya ya sekondari ya wasichana Longido Samia Girl's, wilaya ya Longido Mkoa wa Arusha, mradi uliotekelezwa na Serikali kwa gharama ya shilingu Bilioni 4.4, kupitia programu ya SEQUIP.

Akizungumza mara baada ya kukagua mradi huo mapema leo machi 17,2026, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Florent Kyombo (Mb), licha ya kuridhishwa na ubora wa mradi huo, ameipongeza Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi za kuboresha miundonu ya elimu nchini huku Mkoa wa Arusha ukiwa ni miongoni mwa wanufaika. 

Ameweka wazi kuwa, lengo la serikali ni kuhakisha watoto wa kitanzania wanapata elimu kwenye mazingira rafiki na dhamira ya dhati Dkt.Samia ni kuwahamasisha watoto wa kike nchini kusoma masomo ya Sayansi ili kuzalisha watalamu wengi katika fani za Sayansi.

Hata hivyo wajumbe hao, wameshauri mkoa kuwa na msimamizi wa majengo 'Estate Manager' atakayekuwa na dhamani ya kusimami majengo yote ya serikali yaliyokamilika, ili kuhakikisha yanaendelea kutunzwa na kuendelea kuwa bora pamija na kushugulikia masuala ya ukarabati wa majengo hayo. 

Naye mkuu wa wilaya ya Longido Mhe.  Ally Kali, amewashukuru wajumbe wa kamati hiyo kwa niaba ya wananchi wake, kwa kuwatembelea na kukagua mradi huo wa shule, mradi ambao amekiri ni muhimu kwa watoto wa jamii ya Kimaasai, jamii ambao hapo awali wasichana wengi walikosa nafasi ya kupata elimu.

Mhe. Kali, amesisitiza kufanyia kazi maelekezo na ushauri ulmntolewa na wajumbe ikiwa ni pamoja na kupeleka maombi ya mahitaji ya shule hiyo kwenye Kamati ya Bajetii ili yaingizwe kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha

Awali shule ya wasichana Longdo Samia Girl ni miongoni mwa shule 26 za kimkoa,ukiwa na lengo la kuongeza idadi ya shule na kuboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji nchini, iliyoanza kupokea wanafunzi mwaka 2024 ina wanafunzi 681 wa kidato cha 1-6 kwa mchepuo wa Sayansi.