Mkuu wa wilaya ya Ilala, Mheshimiwa Edward Mpogolo, ambaye amemuwakilisha Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Mheshimiwa Albert Chalamila, amepongeza na kuwashukuru viongozi wa dini kwa mchango wao mkubwa wa kuimarisha na kudumisha amani lengo kuleta maendeleo katika jamii.

Akizungumza katika maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 19 ya kanisa la WRC Kivule tarehe,6 April, DC Mpogolo alisema licha ya changamoto mbalimbali viongozi wa dini wameendelea kujitoa na kushirikiana na serikali pale wanapohitajika.

Aidha alimpongeza mgeni rasmi, Deus Sangu, Waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu kazi na ajira , ambaye alimuwakilisha makamu wa raisi Mheshimiwa Emmanuel Nchimbi kwa kushiriki katika maadhimisho hayo.

DC Mpongolo ameipongeza serikali chini ya Mheshimiwa raisi Dkt Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kuleta maendeleo kwa utoaji wa fedha katika mkoa huo na kusisitiza kuwa mafanikio hayo yasingewezekana bila uwepo wa amani, maadili na mchango wa viongozi wa dini.

Aliongeza kuwa viongozi wa dini wamekuwa nguzo muhimu katika kuleta amani, utulivu, upendo na mshikamano miongoni mwa wananchi na kujenga jamii kupitia hofu ya Mungu hali inayochangia kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa malengo ya serikali.

“Mgeni rasmi kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam tufikishie salamu kwa raisi wetu amekuwa na mafanikio makubwa lakini mafanikio haya ni kutokana na maombi ya viongozi wetu na waumini”

Mheshimiwa Mpogolo aliwataka waumini na wananchi kwa ujumla kuendelea kumuombea Rais pamoja na kudumisha amani, akibainisha kuwa mafanikio ya Taifa yanatokana na ushirikiano wa viongozi wa dini na wananchi kwa ujumla.













 



Na Oscar Assenga, Tanga

Askofu Mkuu wa Kanisa la (FPCT) Tanzania, Stevie Mulenga, amewataka viongozi wa dini nchini, wakiwemo maaskofu, kutumia majukwaa ya kidini kuhubiri amani badala ya ujumbe unaoweza kuleta uchonganishi.

Askofu Mulenga alitoa wito huo leo wakati wa ibada ya Sikukuu ya Pasaka iliyofanyika katika kanisa hilo. Alisisitiza kuwa Yesu Kristo hakukuja kuleta uchonganishi, bali alikuja kuleta amani, hasa kupitia kufufuka kwake.

Alieleza kuwa viongozi wa dini wanapaswa kuhubiri amani, upendo, uvumilivu na mshikamano miongoni mwa jamii, ili watu waweze kuishi kwa utulivu. Alisema huo ndio ushauri wake mkubwa kwa viongozi hao katika kipindi hiki cha Sikukuu ya Pasaka.

“Tunamshukuru Mungu kwa sababu haki ya kuabudu inaendelea kuheshimiwa nchini. Ingawa serikali haina dini, wananchi wake wana dini, na wanaendelea kuabudu bila kuvunja sheria. Wana uhuru mkubwa wa kuabudu mchana na usiku,” alisema Askofu Mulenga.

Aidha, aliwataka wananchi kulinda amani iliyopo na kuepuka vitendo vinavyoweza kusababisha fitina au vurugu. Alisisitiza kuwa ibada zinapaswa kuwa sehemu ya kufundisha neno la Mungu, siyo majukwaa ya kuchochea chuki au upendeleo kwa watu fulani.

Kwa upande mwingine, Askofu Mulenga alisema chanzo kikubwa cha mmomonyoko wa maadili ni tamaa  binafsi, ambazo husababisha matukio mbalimbali yanayoshangaza hata jamii ya kimataifa.

Aliongeza kuwa viongozi wa dini wanapaswa kuwaelimisha waumini wao juu ya kuepuka ukatili wa kijinsia, huku wakisisitiza umuhimu wa kuishi kwa amani, utulivu na kufuata matendo mema.



 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mkutano mkubwa wa kitaifa utakaowakutanisha wauzaji chakula (Mamalishe na Babalishe) kutoka mikoa yote nchini.

Mkutano huo umepangwa kufanyika Aprili 11, 2026 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na vyombo vya habari leo Jumamosi Aprili 4,2026 jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Wauzaji Chakula nchini kupitia Umoja wa Mamalishe na Babalishe Tanzania (UMALITA), Avijawa Omari, amesema kuwa wanaiomba Serikali kuwatambua rasmi kama kundi muhimu katika uchumi wa nchi.

Amesema kuwa utambuzi huo utawawezesha wanachama kupata mikopo, fursa za kiuchumi na kukuza ajira kwa vijana na wanawake nchini.

“Tunaomba Serikali ituone rasmi. Utambuzi utarahisisha upatikanaji wa mikopo na kutupa nafasi ya kupanua biashara zetu ili tuzalishe ajira zaidi,” amesema.

Bi Omari ameongeza kuwa mkutano huo utakuwa jukwaa muhimu kwa mamalishe na babalishe kuwasilisha moja kwa moja changamoto zao kwa viongozi wa Serikali kwa lengo la kuongeza kipato, kupanua biashara na kuchangia ukuaji wa ajira nchini.

Aidha, amewataka wanachama na wauzaji chakula wote nchini kujitokeza kwa wingi Aprili 11 katika ukumbi wa JNICC ili kujenga kwa pamoja mustakabali wa biashara zao.

Mkutano huo utafanyika chini ya kaulimbiu “Pika Kishua, Vaa Kishua” (Cook Smart, Dress Smart), inayolenga kuboresha viwango vya utoaji huduma na kuimarisha taswira ya kitaalamu ya wauzaji chakula nchini.

“Sisi ni wajasiriamali tunaojitegemea, na tunalisha taifa asubuhi, mchana, jioni hadi usiku. Tunaomba jamii itambue mchango wetu na kuheshimu kazi tunayoifanya,” aliongeza.

Ameeleza pia kuwa sekta hiyo imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo hatari za kiafya na mazingira magumu ya kazi, lakini sasa wameanza kuelekea katika matumizi ya nishati safi na mbinu bora za upishi ili kulinda afya na kukuza biashara.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Babalishe, Ndugu Ngosha, amesisitiza umuhimu wa umoja na ushirikiano miongoni mwa wanachama ili kufikia malengo yao ya kiuchumi na kijamii.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa wa kihistoria kwa kuwaunganisha wadau wakuu wa sekta isiyo rasmi na viongozi wa juu wa Serikali kujadili mustakabali wa ajira na ujasiriamali nchini.



NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) wamekamata magari mawili yaliyokuwa yamepakia mazao kwa kutumia magunia yenye uzito unaozidi kipimo kinachoruhusiwa, katika operesheni ya kushtukiza iliyofanyika katika masoko ya Ilala na Temeke, jijini Dar es Salaam.

 


Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhandisi Maryprisca Mahundi amesema Serikali itaendelea kuwaunga mkono wafanyabiashara ndogondogo nchini wakiwemo wasusi, waendesha bodaboda, mama lishe na baba lishe kwa kuwawezesha kupata mikopo yenye masharti nafuu inayotolewa katika halmashauri mbalimbali.

Mahundi ameyasema hayo alipohudhuria tamasha la “Urembo na Ibada” lililoandaliwa na mjasiriamali na  mmiliki wa saluni, Maria Wilson maarufu kama Chido Point, jijini Dar es Salaam na kukutanisha zaidi ya wanawake 300 Aprili 03, 2026.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara ndogondogo ili wajikwamue kiuchumi.

“Niwasihi mfike kwenye halmashauri zenu kufuata utaratibu wa mikopo hiyo na kuchangamkia fursa zilizopo. Aidha, nikiwa Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Mbeya, nitaendelea kushirikiana na Chido Point katika kuandaa na kuratibu tamasha hili, linalotarajiwa kufanyika mwezi Julai mwaka huu mkoani Mbeya,” amesema Mahundi.

Kwa upande wake muandaaji wa tamasha hilo, Maria Wilson amesema lengo la tamasha hilo ni kuwaunganisha wasusi kutoka mikoa mbalimbali ili kubadilishana uzoefu na kukuza taaluma ya ususi nchini na ameishukuru Serikali pamoja na Wizara ya Maendeleo ya Jamii kwa kuendelea kuwajali wasusi, huku akiomba wizara nyingine ikiwemo Wizara ya Afya kuangalia ustawi wao hasa katika masuala ya afya na usalama kazini.

“Tamasha hili linalenga kuwaunganisha wasusi na kuwahamasisha wazazi kuwapa kipaumbele watoto wao wenye vipaji vya ususi waweze kujiajiri na kuchangia maendeleo ya taifa” amesema Maria Wilson.

Baadhi ya washiriki wa tamasha hilo wameeleza kufurahishwa na jukwaa hilo pamoja na juhudi za Serikali, wakisema limewapa maarifa na motisha ya kukuza biashara zao na elimu waliyoipata  imewapa mbinu mpya zitakazowasaidia kuboresha kazi zao.




Na Oscar Assenga

Kampuni ya Taifa Gesi imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuunga mkono sera ya Serikali ya kuhamasisha matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira.

Akizungumza katika tamasha lililofanyika wilayani Handeni, Mkurugenzi wa Masoko wa Taifa Gesi, Oscar Shelukindo, alisema kampuni hiyo imekuwa ikishiriki katika matamasha ya kijamii tangu mwaka jana kwa lengo la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya gesi safi.

Alisema kuwa katika tamasha hilo, wameelekeza nguvu zaidi kwa wakazi wa Handeni, hususan Kata ya Mdoe, ili kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwapa uelewa sahihi kuhusu faida za kutumia nishati hiyo.

“Tunafurahi kuwa hapa leo kutoa elimu ya matumizi ya gesi safi, kuondoa hofu kwa wananchi na kuwahamasisha kuachana na matumizi ya nishati zisizo rafiki kwa mazingira. Pia tunatoa gesi kwa bei nafuu ili kuwavutia zaidi kuitumia,” alisema Shelukindo.

Alifafanua kuwa bado kuna wananchi wengi ambao wana hofu au uelewa mdogo kuhusu matumizi ya gesi ya kupikia, hali inayowafanya kuendelea kutumia nishati kama kuni na mkaa, ambazo si rafiki kwa mazingira na pia zina madhara kiafya.


Kwa mujibu wa Shelukindo, utoaji wa elimu hiyo unalenga kubadili mtazamo wa jamii na kuwasaidia wananchi kuelewa kuwa gesi ni salama, nafuu kwa muda mrefu na rahisi kutumia.

Aidha, alisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mchango wa sekta binafsi katika kusaidia juhudi za Serikali za kulinda mazingira, kupunguza ukataji wa miti na kuboresha afya za wananchi kupitia matumizi ya nishati safi.

Wananchi waliohudhuria tamasha hilo walipata fursa ya kuuliza maswali, kujifunza matumizi sahihi ya gesi pamoja na kununua bidhaa za gesi kwa bei iliyopunguzwa.

Kwa ujumla, jitihada za Taifa Gesi zinaonesha namna sekta binafsi inavyoweza kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi, hatua inayotarajiwa kuleta mabadiliko chanya katika jamii, hususan maeneo ya vijijini.

Wataalamu kutoka Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) wamehitimisha mafunzo maalum ya ulinzi na usalama dhidi ya mionzi kwa wafanyakazi wa Maweni Limestone Company. Mafunzo haya, yaliyofunguliwa na Meneja wa Idara ya Ubora wa kampuni hiyo, yalilenga kuwajengea uwezo wafanyakazi wanaoshughulika moja kwa moja na vifaa vya X-Ray Fluorescence (XRF) na nuclear gauges.

Kwa muda wa siku kadhaa, washiriki walipata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu utambulisho wa mionzi ayonishi, kiasi cha mionzi na vipimo, matumizi ya mionzi, athari zake kiafya, kanuni za ulinzi, mfumo wa kisheria wa Tanzania, majukumu ya Afisa Usalama wa Mionzi (RSO), pamoja na usalama wa nyuklia na udhibiti wa usafirishaji haramu.

Katika hotuba ya kufunga mafunzo, wataalamu wa TAEC walisisitiza umuhimu wa kuimarisha utamaduni wa usalama kazini. “Tunataka kuona kila mfanyakazi akibeba jukumu la kulinda afya yake, wenzake na jamii kwa ujumla. Usalama wa mionzi si jambo la hiari, ni wajibu wa kitaifa,” alieleza Ndugu Mungubariki Nyaki, mkufunzi na msimamizi wa Ofisi ya TAEC Jijini Tanga.

Washiriki walionekana wenye shauku na ari ya kupeleka maarifa mapya kazini. Baadhi walikiri kuwa mafunzo haya yamewapa ujasiri wa kushughulika na vifaa vya mionzi kwa umakini zaidi, huku wengine wakisisitiza umuhimu wa kushirikiana na TAEC ili kuhakikisha viwango vya kitaifa na kimataifa vinazingatiwa.

Mafunzo haya pia yaligusia hatua za dharura endapo ajali za mionzi zitatokea, jambo lililowapa washiriki uelewa wa namna ya kukabiliana na changamoto kwa utulivu na ufanisi.

Kwa ujumla, kufungwa kwa mafunzo haya kumeacha taswira ya matumaini na uwajibikaji. Kampuni ya Maweni Limestone imeonyesha dhamira ya dhati ya kulinda wafanyakazi wake na jamii kwa kuhakikisha teknolojia za kisasa zinatumika kwa usalama na kwa manufaa ya Taifa.





Tamasha la Pasaka ‘Mtoko na Christina Shusho

Na Mwandishi Wetu

WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi Aprili 5, 2026, siku ya Jumapili ya Pasaka, katika tamasha la ‘Mtoko na Christina Shusho Pasaka’ litakalofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam ambapo wananchi wataruhusiwa kuingia bure.

Kauli mbiu ya tamasha hilo ni “Ushindi wa Milele.”

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Machi 30, 2026, Meneja wa msanii wa muziki wa injili Christina Shusho, Humphrey Gatimu, amesema maandalizi ya tamasha hilo yamekamilika kwa asilimia 100 na kusisitiza kuwa wananchi wote wanakaribishwa kushiriki bila malipo yoyote.

Amesema tamasha hilo litawakutanisha waimbaji mbalimbali wa muziki wa injili akiwemo Rose Muhando, Joel Lwaga, The Voice, Bella Kombo, Ambwene Mwasongwe, Neema Gospel Choir, Paul Clement na wengine wengi.
“Milango ya ukumbi itafunguliwa rasmi saa nane mchana, hivyo tunawaomba wananchi kujitokeza kwa wingi na kuwahi mapema ili kuepuka changamoto ya kukosa nafasi ndani,” amesema Gatimu.
Aidha, Gatimu amebainisha kuwa matarajio ya waandaaji ni kupanua wigo wa tamasha hilo mwakani kwa kulipeleka katika mikoa mitatu tofauti, huku wakiahidi kuweka wazi maeneo hayo wakati utakapofika.
Kwa upande wake, mwimbaji wa nyimbo za injili, Shusho amesema tamasha hilo ambalo hufanyika kila mwaka kipindi cha Pasaka, limekuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wasanii wa muziki wa injili, waumini pamoja na familia kwa lengo la kusherehekea sikukuu hiyo na kuinua vipaji vipya.
Amesema mafanikio ya tamasha hilo yanatokana na amani iliyopo nchini Tanzania, akimshukuru Mungu kwa kumpatia kibali cha kufanya tamasha pamoja na viongozi wa serikali kwa kuendelea kudumisha utulivu na maendeleo ya taifa.
“Tunawahimiza watu kufika mapema ili waweze kushiriki kikamilifu ibada ya sifa na kuabudu pamoja nasi, kwani kuna mambo mengi mazuri yameandaliwa kwa ajili ya kumtukuza Mungu,” amesema Shusho.
Naye mwimbaji kutoka kundi la The Voice, Obedi Mark amesema tamasha hilo limekuwa chachu kwa wasanii wengi kukuza vipaji vyao sambamba na kueneza ujumbe wa injili kupitia muziki.
Kwa upande wake mwanakwaya wa kwaya ya Mt Cecilia Makuburi, Joseph Atanasi amesema wao kama kwaya watashiriki kikamilifu katika tamasha hilo wakiwa wamejiandaa vyema kuendelea kumsifu Mungu kupitia uimbaji.
 

Na.Mwandishi Wetu

TUME ya Ushindani (FCC) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini imeadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani kwa kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Shughuli hiyo imefanyika tarehe 31 Machi, 2026 ambapo FCC imekabidhi vifaa tiba vinne vya Oxygen Flow Meter vitakavyosaidia wagonjwa wanaohitaji huduma ya hewa tiba, hususan wale wanaopata changamoto ya kupumua.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mkuu wa FCC Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Bw.Dickson Mbanga, amesema kuwa tukio hilo ni sehemu ya kuadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani pamoja na kutimiza miaka mitatu tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo katika ukanda huo.

Mbanga ameeleza kuwa FCC imeona ni vyema kutumia maadhimisho hayo kwa kutoa mchango wa kijamii utakaoleta tija moja kwa moja kwa wananchi, hasa katika sekta ya afya ambayo ni nyeti na muhimu kwa ustawi wa jamii.

 "Vifaa hivyo vitasaidia kuongeza uwezo wa hospitali katika kuhudumia wagonjwa wanaohitaji msaada wa hewa tiba, hivyo kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa utoaji wa huduma hizo."amesema Bw.Mbanga

Kwa upande wake, akipokea vifaa hivyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, Muuguzi Kiongozi Ndg. Petro Seme ametoa shukrani za dhati kwa FCC kwa msaada huo muhimu.

Seme amesema kuwa vifaa hivyo ni vya kisasa na vina uwezo wa kuhudumia wagonjwa wawili kwa wakati mmoja, jambo ambalo litarahisisha upatikanaji wa huduma ya hewa tiba na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wagonjwa.


Katibu Mkuu-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt Tausi M. Kida ametoa wito kwa watendaji wa Tume hiyo kufanya kazi kwa weledi, ubunifu na ushirikiano ili kuishi dhana ya kufanya kazi isivyokawaida ili kuyafikia matarajio ya Taifa jumuishi, lenye ustawi, haki na linalojitegemea.

‎Dkt Kida ametoa wito huo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Mipango.

Aidha, amesisitiza ‎kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan inayo matarajio makubwa kwa Tume ya kuhakikisha inatekeleza ipasavyo majukumu yake kwa weledi, ari na kuzingatia utu.

‎Mkutano huo, umeongozwa na kauli mbiu isemayo: Utumishi Imara ni Msingi wa Utekelezaji wa Dira 2050.