Mbunge wa Jimbo la Gairo, Ahmed Shabiby, ameupongeza Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) kwa kazi kubwa inayofanya katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma na bidhaa zenye vipimo sahihi, hatua ambayo amesema imeendelea kuimarisha ulinzi wa maslahi ya walaji pamoja na wafanyabiashara nchini.
Akichangia leo Mei 22,bungeni Dodoma wakati wa mjadala wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Shabiby amesema WMA imeendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa huku ikishirikiana kikamilifu na wadau mbalimbali kuhakikisha mfumo wa usimamizi wa vipimo nchini unakuwa imara na wa kuaminika.
Shabiby amesema WMA imekuwa mstari wa mbele kutoa ushirikiano wa karibu kila inapohitajika, jambo lililochangia kuongezeka kwa ufanisi katika usimamizi wa vipimo nchini na kuimarisha imani ya wananchi kwa taasisi hiyo.. Aidha, amempongeza Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, kwa uongozi wake wenye weledi, uwajibikaji na ushirikiano mzuri katika kusimamia majukumu ya wakala huo muhimu kwa maendeleo ya sekta ya biashara na viwanda.Hata hivyo, mbunge huyo ameitaka WMA kuongeza umakini zaidi katika kudhibiti ubora wa bidhaa za chuma, hususan nondo zinazozalishwa na baadhi ya viwanda nchini, akieleza kuwa bado kuna changamoto ya uwepo wa bidhaa zisizokidhi viwango vya vipimo vinavyotakiwa.
Amesema baadhi ya viwanda vinavyoendeshwa na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi vinaendelea kuzalisha nondo zenye upungufu wa vipimo, hali inayoweza kuhatarisha usalama wa majengo pamoja na maisha ya wananchi. “Tusibaki kwenye kutoa faini pekee. Viwanda vinavyotengeneza nondo zisizokidhi vipimo vinapaswa kuchukuliwa hatua kali ikiwemo kufungiwa, ili kulinda usalama wa wananchi na kuhakikisha ubora wa ujenzi nchini,” amesema Shabiby. Ameongeza kuwa usimamizi madhubuti wa vipimo vya bidhaa za ujenzi ni msingi muhimu katika kukuza sekta ya viwanda, kulinda miundombinu na kuhakikisha maendeleo endelevu ya taifa.Wakala wa Vipimo Tanzania umeendelea kusimamia matumizi sahihi ya vipimo nchini kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura ya 340, ikiwa ni jitihada za kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa sahihi kulingana na thamani ya fedha wanazolipa.
Serikali kupitia Wakala wa Vipimo (WMA) imeendelea kuimarisha huduma za uhakiki wa vipimo nchini kwa kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Uhakiki kilichopo eneo la Misugusugu, mkoani Pwani, ambacho kimegharimu jumla ya shilingi bilioni 7.3.
Kituo hicho kilichojengwa katika eneo lenye ukubwa wa hekta 2.4 ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kusogeza karibu huduma za vipimo kwa wananchi na wadau wa kibiashara, sambamba na kuimarisha miundombinu ya kitaifa ya udhibiti wa ubora wa vipimo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa Bungeni, kituo hicho kitahusika na uhakiki wa vifaa mbalimbali vinavyotumika katika sekta za nishati na maji, ikiwemo matenki ya magari yanayosafirisha vimiminika, mita mpya za umeme pamoja na dira za maji kabla ya kufungwa kwa watumiaji.
Lengo kuu la uhakiki huo ni kuhakikisha kuwa vifaa hivyo vinakidhi viwango vilivyowekwa kitaifa na kimataifa, na hivyo kuhakikisha usahihi wa vipimo, kulinda haki za watumiaji na wauzaji, pamoja na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa rasilimali za umma.
Hata hivyo, WMA imebainisha kuwepo kwa changamoto mbalimbali zinazokwamisha utekelezaji wake, ikiwemo mwitikio hafifu kutoka kwa baadhi ya wazabuni wa mita za umeme kushindwa kutekeleza takwa la kisheria la kuwasilisha mita hizo kwa ajili ya uhakiki kabla ya kusambazwa kwa taasisi nunuzi.
Changamoto nyingine ni malimbikizo ya muda mrefu ya madai ya malipo ya huduma za uhakiki wa dira za maji kutoka kwa baadhi ya kampuni zilizopewa zabuni, hali inayoweza kuathiri uendelevu wa huduma na ufanisi wa taasisi hiyo.
Akizungumza Bungeni, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mariam Ditopile, amesema kamati yake imebaini hatua nzuri zilizofikiwa na WMA katika kuboresha huduma zake, ikiwemo ujenzi wa kituo hicho cha kisasa cha Misugusugu.
Ditopile amesema kuwa kamati imepongeza juhudi za Serikali katika kuimarisha miundombinu ya uhakiki wa vipimo, lakini pia imesisitiza umuhimu wa kuongeza ufuatiliaji wa wazabuni ili kuhakikisha wanazingatia matakwa ya kisheria kabla ya kusambaza vifaa kwa wananchi.
Aidha, alibainisha kuwa changamoto ya malimbikizo ya madeni ya huduma za uhakiki inapaswa kushughulikiwa kwa haraka ili kuepusha athari katika uendeshaji wa taasisi na utekelezaji wa majukumu yake ya msingi.
Kamati hiyo pia imeitaka Serikali kuendelea kuimarisha usimamizi wa sekta ya vipimo ili kuhakikisha vifaa vyote vinavyotumika nchini vinakuwa sahihi na vinakidhi viwango vilivyowekwa, hatua itakayosaidia kuongeza ufanisi katika sekta mbalimbali za uchumi.
Kwa ujumla, ujenzi wa Kituo cha Misugusugu unatajwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya vipimo nchini, ukiwa na lengo la kuongeza uwazi, usahihi na ulinzi kwa watumiaji wa huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Ofisi ya Makamu wa Rais inatarajiwa kuzindua Programu ya Kitaifa ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania katika kilele cha Siku ya Mazingira Duniani (WED) ambapo kitaifa itafanyika jijini Dodoma, Juni 5, 2026.
Akizungumza katika uzinduzi wa usafi wa Mazingira kuelekea siku hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni alisema lengo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi ya mfano duniani katika suala la Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira.
Alisema Programu hiyo inalenga kutekeleza Dira, 2050 hususan nguzo ya tatu kuhusu Uhifadhi wa Mazingira na Ustahimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi ikiwa na lengo la kupanda miti bilioni 2 kwa mwaka, kuimarisha Biashara ya Kaboni, Uanzishaji wa Bustani za Kijani katika Miji na shughuli zingine za Kijani.
“Pia program hii inatarajia kuongeza ajira zinazoweza kufikia zaidi ya elfu ishirini na tano (25,000) ifikapo 2030 kupitia sekta za taka, misitu, kaboni na nishati safi,”alisema Mhe. Masauni.
Alifafanua kuwa tukio hilo ni sehemu ya juhudi za Kitaifa na Kimataifa za kulinda mazingira, kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kujenga jamii yenye afya na ustahimilivu.
Aidha, alileza Dira, 2050 imeweka maono ya Taifa kuwa hadi kufikia mwaka 2050 Tanzania iwe kinara katika matumizi endelevu ya rasilimali, Taifa linalotumia taka kama malighafi kwa manufaa ya kiuchumi na Taifa kinara katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuimarisha ustahimilivu na uendelevu wa mazingira.
“Juhudi zinahitajika ili kutekeleza shughuli za mazingira kwa njia jumuishi inayohusisha makundi yote ya kijamii bila kujali jinsia au umri. Kwa jiji la Arusha, tafiti za mwaka 2020 zinaonesha kuwa jiji linazalisha takribani tani 550 za taka ngumu kwa siku, ambapo zaidi ya asilimia 60 ya taka hizo zinaweza kurejelezwa ikiwa zitadhibitiwa vizuri kupitia uchumi rejeshi,"aliongeza.
"Kwa ngazi ya Kitaifa, Tanzania inakadiriwa kupoteza takribani hekta 469,420 za misitu kila mwaka kutokana na shughuli mbalimbali zisizo endelevu ikiwa ni pamoja na matumizi makubwa ya kuni na mkaa, kilimo kisicho endelevu, ufugaji holela pamoja na shughuli nyingine za kibinadamu zinazosababisha uharibifu wa mazingira hali inayochangia kuongezeka kwa gesi joto, kuharibu vyanzo vya maji na kuhatarisha usalama wa bioanuwai,".
Alieleza Upandaji wa miti yenye matumizi mbalimbali una mchango mkubwa katika kufyonza gesi ya kaboni, kupunguza mmomonyoko wa udongo, kuhifadhi vyanzo vya maji, kutoa matunda pamoja na kuongeza kipato kwa wananchi kupitia bishara ya Kaboni na kuongeza ustahimilivu dhidi ya athari za Mabadiliko ya Tabianchi.
"Matumizi ya nishati safi ya kupikia ni hatua muhimu katika kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa ambao umeendelea kuwa miongoni mwa sababu kuu za uharibifu wa misitu nchini.
“Kuimarisha upatikanaji na matumizi ya nishati safi kama vile gesi asilia, umeme, biogas na teknolojia bora za kupikia kutasaidia kupunguza kasi ya ukataji miti, kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kuboresha afya za wananchi hususan wanawake na watoto ambao huathirika zaidi na moshi unaotokana na matumizi ya nishati isiyosafi," alisisitiza.
Naye Mkuu wa Wilaya Arusha Mhe. Joseph Mkude alisema kila mmoja ana wajibu wa kutunza na kuhifadhi mazingira na kuzingatia matumizi ya nishati safi ya kupikia na kusema taasisi nyingi zinatekeleza agizo hilo.
Amesema arusha imekuwa ikifanya kila jitihada kuhakikisha jiji hilo linakuwa safi na kushirikisha jamii yote kutambua umuhimu wa utunzaji wa mazingira ndio maana wanafunzi wamepewa kipaumbele.

Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam
Tume ya Taifa ya Mipango kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP leo Mei 22, imefanya mjadala uliyowakutanisha wadau wa maendeleo, sekta binafsi, asasi za kiraia, watafiti na taasisi za elimu ya juu kujadili hatua mbalimbali na afua zinazoweza kutumika ili kukabiliana na athari za mgogoro wa ukanda wa Ghuba.
Akifungua mjadala huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amesema kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti na za kimkakati ili kupunguza athari zinazotokana na mgogoro wa Ghuba kiuchumi na kwa wananchi.
Mhe. Mkumbo amesema hayo leo Mei, 22 jijini Dar es Salaam katika mjadala wa kitaalamu ulioandaliwa na Tume ya Taifa ya Mipango kwa kushirikiana na Umoja wa Mataifa UNDP kwa lengo la kujadili athari, uhimilivu na fursa zinazotokana na mgogoro huo.
Akitaja hatua hizo, Prof. Mkumbo amesema kuwa ni pamoja na kufuatilia kwa karibu bei na upatikanaji wa mafuta, chakula, mbolea na usafiri, kulinda kaya zilizo katika mazingira hatarishi, kuimarisha akiba na usambazaji wa biadhaa muhimu.
“tutahakikisha wananchi wanaendelea kupata chakula cha kutosha na mbolea kwa bei himilivu, vile vile tutaendelea kufanya uthibiti wa gharama za nishati, ikiwa ni pamoja na kutumia fursa za maliasili tulizonazo kama Gesi asilia, madini, utalii na fursa ya miundombinu ya usafiri kuimarisha uchumi wa taifa” amesema Prof. Mkumbo.
Hatua hizo, zinalenga kukabiliana na athari kama vile kupanda kwa bei ya mafuta, usafirishaji na mbolea kunakoweza kuathiri maisha ya wananchi, uzalishaji na bajeti ya Serikali, hivyo Serikali itaendelea kuchukua hatua za haraka ili kuwalinda.
Aidha, Mheshimiwa Waziri ameeleza kuwa pamoja na changamoto hizo, mgogoro huo wa Ghuba unatoa fursa ya kipekee ya kiuchumi kwa Tanzania na bara la Afrika kwa ujumla, hasa katika kuvutia uwekezaji mpya kwenye sekta ya nishati.
"Mgogoro huu unatoa mwanya mkubwa wa uwekezaji katika miundombinu ya mafuta, ikiwemo ujenzi wa viwanda vya kikanda vya kusafisha na kuchakata mafuta (regional refineries)," amesema Prof. Mkumbo.

Awali akimkaribisha Mhe. Waziri, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alieleza kuwa mkutano huo unahusisha wadau wa maendeleo, sekta binafsi, asasi za kiraia, watafiti na taasisi za elimu ya juu kujadili hatua mbalimbali na afua zinazoweza kutumika ili kukabilia na athari za mgogoro huo.
Majadiliano hayo yalihudhuriwa na Mratibu Mkaazi wa Umoja wa Mataifa Bi. Susan Namondo na Mwakalishi Mkaazi wa Umoja wa Mtaifa, na Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania Bw. Shigeki Komatsubaram.







๐Ni ule wa kuboresha kituo cha kufua umeme
๐Amuagiza kuongeza kasi ya utekelezaji wa Mradi huo
Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kutoridhishwa na kasi ya mkandarasi anayetekeleza mradi wa maboresho ya Kituo cha Kufua Umeme cha Hale kutokana na kuchelewa kukamilika kwa Mradi huo ulioanza kutekelezwa tangu mwaka 2022.
Bw. Twange ameyasema hayo leo Aprili 22, 2026 wakati wa ziara yake ya ukaguzi katika mradi wa Hale pamoja na mradi wa usafishaji wa bwawa la Mto Pangani iliyopo katika Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga ambapo amemtaka mkandarasi wa Mradi wa Hale kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo ikiwa ni pamoja na kuongeza wafanyakazi pamoja na muda wa kufanya kazi ili ukamilike kwa wakati.
“Siridhishwi sana na mwenendo wake. Mkandarasi amewahi kuomba nyongeza ya muda mara mbili na nimepata taarifa kuwa yuko kwenye hatua za kuomba nyongeza nyingine ya tatu. Ndio maana nimekuja kuona kuna nini,” amesema Bw. Twange.
Amesema mradi huo una maeneo saba ya utekelezaji ambapo maeneo mawili tayari yamekamilika huku mengine yakiendelea na utekelezaji.
“Nimezungumza na msimamizi wa mradi, mhandisi mshauri pamoja na mkandarasi na nimewaelekeza wakae pamoja kuhakikisha ifikapo mwisho wa mwezi Julai mradi huu uwe umekamilika,” amesema Bw. Twange
Aidha, kuhusu mradi wa usafishaji wa bwawa la Pangani, Bw. Twange amesema matarajio ya TANESCO ni kuhakikisha kazi hiyo inakamilika ndani ya muda uliopangwa ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa msimu wa mvua.
“Matarajio yetu ni kutoupitiliza mwaka mmoja ili tumalize kabla ya msimu unaokuja wa mvua,” ameongeza.
Katika hatua nyingine, Bw. Twange amesema TANESCO kwa sasa inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ya umeme nchini yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 13.4.
Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Mradi wa Hale Mha. Kulwa Byemelo amesema maagizo yaliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji yatatekelezwa ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.
“Mradi huu utakapokamilika utaimarisha upatikanaji wa umeme katika wilaya mbalimbali zinazochukua umeme kutoka kituo cha Hale pamoja na wilaya za Handeni, Muheza na Korogwe,” amesema Byemelo.
Ziara hii ni moja ya mikakati ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme pamoja na kubaini changamoto zinazojitokeza na kuhakikisha zinatatuliwa kwa wakati na miradi ina kamilika ili watanzania waweze kuendelea kufurahia upatikanaji wa umeme wa uhakika.
NAIBU Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali kupitia TANESCO inaendelea kubadilisha nguzo chakavu kwa kuweka nguzo imara zaidi, zikiwemo nguzo za zege na chuma, pamoja na kuimarisha misingi ya nguzo katika maeneo yenye udongo laini ili kukabili changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme.
Salome ameeleza hayo leo, Mei 22, 2026, Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mhe. Sara Msafiri Ally, Mbunge wa Mvomero, aliyetaka kujua ni lini Serikali itatatua changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme katika Tarafa ya Mgeta.
Akijibu swali hilo, Salome amesema Serikali inatambua uwepo wa changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme katika baadhi ya maeneo ya Tarafa ya Mgeta kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo mvua nyingi, uwepo wa udongo usiohimilivu pamoja na uchakavu wa baadhi ya nguzo.
Amesema Serikali kupitia TANESCO inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa miundombinu ya umeme ili kubaini na kushughulikia changamoto hizo mapema pindi zinapojitokeza.
Aidha, Salome amefafanua kuwa Serikali kupitia Wizara ya Nishati imetenga bajeti maalum ya kubadilisha nguzo za miti katika maeneo yote yenye unyevunyevu pamoja na maeneo yenye shughuli mbalimbali za kibinadamu.
Kadhalika, ametoa wito kwa wananchi kuacha matumizi mabaya ya ardhi, ikiwemo kuchoma moto ovyo mashambani, jambo ambalo limekuwa likiathiri miundombinu ya umeme kwa kuunguza nguzo za umeme.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna-DODOMA
Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imeweka mikakati kabambe ya kuimarisha utendaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala katika mwaka wa fedha 2026/2027, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza ufanisi wa masoko ya mazao na kulinda ubora wa bidhaa nchini.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026-2027,bungeni Waziri wa Viwanda na Biashara,Judith Kapinga,amesema kuwa WRRB inalenga kuhakikisha mfumo huo unafanya kazi kwa viwango vya juu zaidi kupitia usimamizi madhubuti wa ubora wa bidhaa zinazoingia na kutoka katika maghala mbalimbali nchini.
Amesema mpango huo, Bodi itaongeza ufuatiliaji wa karibu wa watendaji wa mfumo huo wakiwemo waendesha maghala, wakaguzi pamoja na mameneja dhamana, ili kuhakikisha kunakuwa na uwajibikaji na uzingatiaji wa kanuni zilizowekwa.
"WRRB imejipanga kuendeleza kampeni za elimu kwa umma na uhamasishaji kuhusu matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, hatua inayolenga kuongeza uelewa kwa wakulima na wafanyabiashara kuhusu faida za mfumo huo katika uhifadhi na uuzaji wa mazao."amesema Mhe.Kapinga
Vilevile, Bodi hiyo inaendelea na mchakato wa kupata cheti cha ithibati ya ubora wa kimataifa (ISO), hatua inayotarajiwa kuongeza uaminifu wa mfumo huo ndani na nje ya nchi pamoja na kuufanya uwe na ushindani katika masoko ya kikanda na kimataifa.
Serikali inaamini kuwa uboreshaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala utaongeza thamani ya mazao ya wakulima, kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno, na kuimarisha mapato ya wananchi pamoja na pato la taifa kwa ujumla.
WRRB imeeleza kuwa utekelezaji wa mipango hiyo ni sehemu ya juhudi za muda mrefu za kuifanya sekta ya kilimo kuwa na tija zaidi kupitia mifumo ya kisasa ya uhifadhi, usimamizi na uuzaji wa mazao nchini.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna-DODOMA
Serikali imefikia hatua muhimu katika utekelezaji wa Mradi mkubwa wa Chuma wa Liganga na Makaa ya Mawe wa Mchuchuma baada ya kukamilisha majadiliano na mwekezaji mpya wa mradi huo, hatua inayotajwa kuwa ya kihistoria katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026-2027,bungeni Waziri wa Viwanda na Biashara,Judith Kapinga,amesema Serikali imekamilisha mazungumzo na kampuni ya Shudao Investment Group Company Limited (SDIG), kampuni inayomilikiwa na Serikali ya China, kwa ajili ya kuendeleza mradi huo kwa kushirikiana na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC).
Kampuni hiyo imechukua nafasi ya kampuni ya awali ya Sichuan Hongda Group Company Limited (SHG), iliyokuwa imeanza majadiliano ya utekelezaji wa mradi huo miaka iliyopita.
Amesema kuwa pande zote zimefikia mwafaka katika maeneo muhimu ya uwekezaji ikiwemo mgawanyo wa hisa, kiwango cha mtaji wa mradi, muundo wa usimamizi, muda wa mikataba pamoja na namna ya kuongeza thamani ya madini hapa nchini.
Madini yatakayoongezwa thamani nchini ni pamoja na chuma, vanadium na titanium, hatua inayotarajiwa kuongeza mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa Taifa pamoja na kuchochea maendeleo ya viwanda vya ndani.
Aidha, rasimu za mikataba ya ubia na wanahisa kwa ajili ya shughuli za uchimbaji na ujenzi wa kiwanda cha kuzalisha bidhaa za chuma tayari zimekamilika, huku hatua za mwisho za idhini kutoka mamlaka husika zikiendelea.
Serikali imeeleza kuwa mikataba hiyo inatarajiwa kusainiwa katika nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha 2026/2027, kabla ya kuanza rasmi kwa ujenzi wa mradi ambao unatarajiwa kuchukua miaka mitatu kukamilika.
Mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati kuwahi kutekelezwa nchini kutokana na manufaa yake makubwa kiuchumi.
Taarifa zinaonesha kuwa utekelezaji wake utawezesha Tanzania kuokoa zaidi ya dola za Marekani bilioni 1.22, sawa na shilingi trilioni 3.2, ambazo kwa sasa hutumika kuagiza bidhaa za chuma kutoka nje ya nchi.
Bidhaa za chuma zimeendelea kuwa miongoni mwa bidhaa zinazoongoza kwa matumizi makubwa ya fedha za kigeni baada ya mafuta ya petroli.
Mbali na kupunguza utegemezi wa bidhaa za nje, mradi huo pia unatarajiwa kufungua mlolongo mkubwa wa viwanda vitakavyotumia malighafi za chuma, makaa ya mawe na madini mengine yatakayozalishwa ndani ya nchi.
Vilevile, Serikali inaamini kuwa kuanza kwa uzalishaji wa chuma nchini kutasaidia kupunguza matumizi ya chuma chakavu kinachochangia uharibifu wa miundombinu katika maeneo mbalimbali.
Amesema tathmini ya awali ya kifedha iliyofanywa kwa pamoja na wataalamu wa Serikali na mwekezaji, Serikali inatarajia kupata mapato makubwa kupitia kodi na mirahaba ndani ya kipindi cha miaka 25 ya utekelezaji wa mradi huo.
Makadirio yanaonesha kuwa Serikali inaweza kukusanya hadi dola za Marekani trilioni 1.99 kupitia kodi mbalimbali na malipo ya mrahaba yatakayotokana na mauzo ya umeme, makaa ya mawe, bidhaa za chuma, titanium, vanadium pamoja na aluminium sulphate.
Aidha, utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa kuzalisha ajira za moja kwa moja zipatazo 6,500 na nyingine zaidi ya 26,000 zisizo za moja kwa moja, hatua inayotarajiwa kuongeza kipato kwa wananchi na kukuza uchumi wa maeneo ya mradi.
Wakati huo huo, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo imeendelea kusimamia utekelezaji wa Mradi wa Magadi Soda katika bonde la Engaruka wilayani Monduli.
Hatua zilizofikiwa hadi sasa ni pamoja na ulipaji wa fidia kwa wananchi wanaopisha mradi pamoja na upatikanaji wa mwekezaji wa mradi huo.
Ameeleza kuwa hadi Aprili 2026, Serikali ilikuwa imelipa shilingi bilioni 5.82 sawa na asilimia 98.7 ya fedha za fidia kwa wananchi 513 kati ya 594 waliotakiwa kulipwa.
Zoezi la kukamilisha malipo linaendelea kwa wananchi waliobaki huku Serikali ikieleza kuwa baadhi yao bado wanakamilisha nyaraka muhimu za mirathi na umiliki.
Aidha, Timu ya Serikali ya Majadiliano inaendelea na mazungumzo ya mwisho ya mkataba wa ubia na kampuni iliyoshinda zabuni ya kuendeleza mradi huo.
Mradi wa Magadi Soda unatarajiwa kuokoa zaidi ya dola za Marekani milioni 121 zinazotumika kila mwaka kuagiza malighafi ya magadi soda pamoja na bidhaa zake kutoka nje ya nchi.
Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa CRDB Bank Plc kutoka mataifa ya Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Falme za Kiarabu na Rwanda wamerejea Nyumbani Ngorongoro kushuhudia asili ya mababu zao iliyosheheni vivutio vya utalii vya Wanyamapori, Malikale, Urithi wa Utamaduni na Jiolojia vilivyopo Ngorongoro ambayo ni Kivutio bora cha Utalii Afrika mwaka 2023 na 2025.
Wakiwa ndani ya hifadhi hiyo maarufu duniani, Wakurugenzi hao wamefurahishwa na mandhari, uoto wa asili, wanyamapori pamoja na huduma bora za utalii zinazotolewa ndani ya hifadhi na kusisitiza kuwa uzoefu walioupata umeacha alama inayowafanya kurudi tena na familia zao.
Akizungumza kwa niaba ya ujumbe huo, Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB Prof. Neema Mori amesema ujumbe huo umeichagua Ngorongoro kuwa sehemu yao ya mapumziko kutokana na upekee wake usiofananishwa na eneo lolote duniani kwa kuwa Ngorongoro si tu kivutio cha Utalii bali ni hazina ya historia, utamaduni na asili inayoishi.
Akiwa na Ujumbe huo Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Utalii na Masoko Mariam Kobelo amesema kuwa Ngorongoro ndio eneo lenye ushahidi wa kisayansi na Kimazingira kuwa binadamu wa kwanza alisimama kwa miguu yake miwili zaidi ya miaka Milioni 3.6 iliyopita huku hifadhi hiyo ikipambwa na wanyama wakubwa watano "Big Five", Spishi za Wanyama mbalimbali, Ndege, maua na mimea.
Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Prof. Haruni Mapesa amewataka wanataaluma kuacha tabia ya kuchapisha makala zao kwenye Majarida yasiyotambulika ili kuzuia upotezaji wa nguvu na rasilimali za uchapishaji wa Tafiti.
Prof. Mapesa ameyasema hayo wakati akifungua Semina ya Uwasilishaji wa Makala Mijadala za a Kitaaluma iliyoandaliwa na Idara ya Lugha na Fasihii Chuoni hapo hafla iliyofanyika katika Kampasi ya Kivukoni jijini Dar es salaam.
Mkuu huyo wa Chuo amesema kuwa sasa Tasisi ipo katika hatua za ukuaji ikiwemo kuidhinishwa kwa Kitivo cha Uchumi na Biashara, ambapo chuo kimetenga kiasi cha shilingi milioni 120 kwa ajili ya tafiti na kuna mpango wa kuongeza fedha hizo ili kuwekeza zaidi kwa wahadhiri watakaofanya tafiti mbalimbali.
Naibu Mkuu wa Chuo anayesimamia Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaaluma Prof. Richard Kangalawe amekipongeza Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Jamii kupitia Idara ya Lugha na Fasihi kwa kuandaa semina hiyo na kuwahimiza washiriki kutumia fursa hiyo kuimarisha mawazo ya kitafiti, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha tafiti zote zinasajiliwa rasmi na machapisho yawe yenye ubora wa hali.
Kwa upande wake, Naibu Mkuu wa Chuo Mipango, Fedha na Utawala Prof. Evaristo Haulle amewataka Wanataaluma kubadilika na kuanza kufikiria namna ya kuchangia asilimia 30 ya mapato ya ndani kupitia Tafiti na Miradi wanayoifanya badala ya kutegemea rasilimali na fedha za ndani za chuo pekee.
Akiwasilisha taarifa ya Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Jamii, Mtiva wa Kitivo hicho Dkt. Luzabeth Kitali ameishukuru Menejimenti ya Chuo kwa Maelekezo na Ushauri na kuahidi kuwa idara yake imejipanga kikamilifu kusimamia ubora wa Tafiti, kuendeleza Uandishi ikiwa ni pamoja na kushiriki katika makongamano ya kitaaluma.
Imetolewa na;
Kitengo cha Mawasiliano na Masoko
CHUO CHA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE
21.05.2026
Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Mhe. Stephen Wasira ameipongeza Menejimenti ya Chuo hicho kwa Kujenga ofisi za Walimu na kumbi za Mihadhara kwa kutumia Makusanyo ya Mapato ya ndani, na hivyo kusaidia kupunguza changamoto ya Ofisi na Madarasa iliyokuwa inaikabili Taasisi hiyo.
Mhe. Wasira ameyasema hayo leo baada ya kuzindua jengo lenye ofisi zinazoweza kutumiwa na Walimu zaidi ya Sabini na kumbi mbili za Mihadhara zenye uwezo wa kuchukua wanafunzi Mia sita kwa mara moja kwa kila kumbi.
Kwa upande wake Mkuu wa Chuo Prof. Haruni Mapesa amesema kuzinduliwa kwa ofisi na kumbi za Mihadhara kutasaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa vyumba vya kufundishia na ofisi ambazo zitatumiwa na Watumishi.
Mkuu huyo wa Taasisi amebanisha kuwa dhamira kuu ya ujenzi huo ni kuboresha ustawi na kutoa huduma bora kwa Wanafunzi na Wafanyakazi.
Ameongeza kuwa ujenzi huo utasaidia kuongeza mapato ndani ya Taasisi kwani chuo kitaongeza udahili wa Wanafunzi pamoja na kuendeleza mazingira bora, rafiki na safi kwa Ustawi wa jamii ya Chuo.
Mradi huo umegharimu kiasi cha Shilingi Bilioni Moja na Milioni Sitini na Saba.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano na Masoko
Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere
21.05.2026
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonn-DODOMA
WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Serikali inaendelea kuimarisha uzalishaji wa sukari nchini ili kupunguza utegemezi wa kuagiza sukari kutoka nje ya nchi kupitia upanuzi wa viwanda vya sukari.
Akiwasilisha Mpango wa bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Kapinga amesema viwanda viwili vya Mkulazi Holding Company Limited na Kilombero Sugar Company Limited vimefanya upanuzi mkubwa wa uzalishaji utakaoongeza upatikanaji wa sukari nchini.
Amesema baada ya upanuzi huo, Kiwanda cha Kilombero kitaongeza uwezo wa kuzalisha sukari kutoka tani 123,000 hadi tani 226,000 kwa mwaka, huku majaribio ya uzalishaji yakiwa yamekamilika na uzalishaji rasmi unatarajiwa kuanza mwezi Juni, 2026.
Kapinga amesema kwa upande wa Kiwanda cha Mkulazi, kimeongeza mtambo mpya utakaowezesha uzalishaji wa sukari ya viwandani (industrial sugar) kwa ajili ya matumizi ya viwanda mbalimbali nchini.
Amesema majaribio ya mitambo hiyo tayari yamefanyika kwa mafanikio na kiwanda kimefanikiwa kuzalisha tani 256 za sukari ya viwandani.
“Upanuzi huu utawezesha kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, kupunguza uagizaji kutoka nje pamoja na kuchochea ukuaji wa sekta ya viwanda,” amesema Kapinga.
Aidha, amesema kukamilika kwa miradi hiyo kutazalisha ajira za moja kwa moja 8,500 pamoja na ajira zisizo za moja kwa moja 25,000, hatua ambayo itaongeza kipato kwa wananchi na kuchochea maendeleo ya uchumi wa nchi.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna-DODOMA
WIZARA ya Viwanda na Biashara imeliomba Bunge kuidhinisha bajeti ya Shilingi bilioni 137.8 kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kutekeleza majukumu mbalimbali ya maendeleo ya sekta ya viwanda na biashara nchini.
Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 104.1 zimetengwa kwa matumizi ya kawaida, ambapo Shilingi bilioni 78.0 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi na Shilingi bilioni 26.0 kwa matumizi mengineyo ya uendeshaji.
Akiwasilisha bajeti hiyo Bungeni leo Mei 22, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Shilingi bilioni 33.6 zimetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo, huku fedha zote za maendeleo zikitokana na vyanzo vya ndani vya Serikali.
Amesema bajeti hiyo inalenga kuendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji, kuongeza uzalishaji wa viwanda vya ndani, kukuza biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na nje ya nchi.











.jpeg)



