Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefanya kikao kazi na watumishi wa taasisi hiyo kutoka kampasi zote, akisisitiza umuhimu wa uwajibikaji, umoja na mshikamano katika kufanikisha malengo ya taasisi.

WATUMISHI  wa Tume ya Ushindani Ofisi ya Kanda ya Ziwa wametoa elimu kwa wadau mbalimbali, wakiwemo wanafunzi, waandishi wa habari na wafanyabiashara, walipotembelea Banda la Kliniki ya Walaji katika Manispaa ya Musoma Mkoani Mara.

Banda hilo limegeuka kuwa kitovu cha maarifa, likiwavutia wengi waliotaka kuelewa kwa undani haki zao kama walaji pamoja na namna bora ya kushiriki katika soko kwa uadilifu na uelewa mpana.

Akitoa elimu hiyo, Mkuu wa Kanda ya Ziwa FCC, Bw. Mdimi, amesisitiza umuhimu wa walaji kuwa na uelewa wa haki zao ili kujilinda dhidi ya bidhaa duni, huduma zisizo na viwango na vitendo vya udanganyifu vinavyoweza kujitokeza sokoni.

"Amebainisha kuwa elimu kwa walaji ni silaha muhimu katika kujenga uchumi imara unaozingatia haki na usawa kwa wote."amesema Bw.Mdimi

Kwa upande wa wafanyabiashara, wamekumbushwa umuhimu wa kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia sheria za ushindani wa haki, wakielezwa kuwa uaminifu kwa wateja ni msingi wa mafanikio ya biashara yoyote endelevu.

Elimu hiyo imewajengea uelewa mpya kuhusu wajibu wao katika kulinda maslahi ya walaji.

Wanafunzi  wameahidi kuwa mabalozi wa elimu hiyo katika jamii zao, huku waandishi wa habari wakiahidi kueneza ujumbe huo kwa umma kupitia vyombo vyao.

Elimu hiyo  ni sehemu ya maandalizi kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026, yakilenga kuendelea kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kulinda haki za walaji na kuimarisha ushindani wa haki sokoni.

Kwa ujumla, juhudi hizi zinaakisi dhamira ya Tume ya Ushindani kuhakikisha kuwa kila mlaji anakuwa na sauti, analindwa na anapata huduma bora, huku biashara zikikua katika mazingira ya haki na uwazi.

 


Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Nolasco Mlay, ameshiriki mafunzo maalum kwa waandaaji wa maudhui (content creators) yanayofanyika leo Machi 24, 2026 mkoani Dar es Salaam, yakilenga kuwajengea uwezo waandaaji hao wa maudhui ili kuboresha ubunifu na kuongeza tija ya kazi zao.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, huku Wizara ya Nishati ikiwa miongoni mwa wawezeshaji.


Uwezeshaji wa Wizara ya Nishati katika mafunzo hayo ni kielelezo cha kutambua kazi zinazofanywa na waandaaji hao wa maudhui ambao ni daraja muhimu la kutoa elimu na kuhamasisha kupitia majukwaa yao kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Mafunzo yanayotolewa leo yanalenga kuwasaidia watengeneza maudhui kuboresha kazi zao kupitia kubiasharisha maudhui mtandaoni (Content Monetization & Sustainability), kujiongezea thamani binafsi na chapa (Personal Branding na Channel Optimization), pamoja na masuala ya hakimiliki.

Aidha, waandaji hao wa maudhui watapata elimu ya namna ya kufikia masoko ya kimataifa, maadili na miongozo ya utoaji huduma mtandaoni, pamoja na usalama wa taarifa binafsi katika utengenezaji wa maudhui.

 


Dubai, Machi 2026
KAMPUNI ya Airtel Africa kwa kushirikiana na SpaceX wametangaza kufanikiwa kwa majaribio ya huduma za data na ujumbe (SMS) kupitia Starlink Mobile nchini Kenya, hatua muhimu inayofungua njia ya kuleta mawasiliano ya satelaiti moja kwa moja kwenye simu za mkononi kwa mamilioni ya wananchi katika nchi 14 ambako Airtel inafanya kazi barani Afrika.

Majaribio hayo yalifanyika katika maeneo yasiyokuwa na mtandao wa kawaida wa simu, yaani maeneo ambayo minara ya mawasiliano ya ardhini haikuwa na mawimbi. Katika maeneo hayo, huduma ya Starlink Mobile iliwezeshwa moja kwa moja na kuruhusu simu janja zinazotumia teknolojia ya 4G kuunganishwa na mtandao wa satelaiti zaidi ya 650 zilizokwisha kurushwa angani, hivyo kuwezesha watumiaji kuendelea kuwa na mawasiliano hata katika maeneo ya mbali kabisa.

Katika kipindi cha majaribio, huduma hiyo iliweza kusaidia matumizi ya data nyepesi kama vile kupiga na kutuma ujumbe kupitia WhatsApp, kutumia ramani, Facebook Messenger pamoja na kufanya miamala ya kifedha kupitia programu ya Airtel App. Watumiaji waliweza kuendelea kutumia huduma muhimu hata walipokuwa katika maeneo ambayo kwa kawaida hayana mtandao wa simu.

Akizungumzia mafanikio hayo, Mtendaji Mkuu wa Airtel Africa, Sunil Taldar, alisema hatua hiyo inaonesha utekelezaji wa vitendo baada ya tangazo la ushirikiano kati ya Airtel Africa na SpaceX. Alisema majaribio yaliyofanyika nchini Kenya yanaonesha dhamira ya kampuni hiyo kupanua upatikanaji wa mawasiliano kwa watu wengi zaidi barani Afrika.

Aliongeza kuwa kwa kuunganisha teknolojia ya Starlink Mobile, Airtel Africa inahakikisha wateja wake wanaendelea kuwa na mawasiliano hata wanaposafiri nje ya maeneo yenye mtandao wa kawaida wa simu.

Baada ya majaribio hayo nchini Kenya, Airtel Africa na Starlink Mobile wanatarajia kutumia uzoefu walioupata kupanua huduma hiyo katika nchi zote 14 ambako Airtel inafanya kazi, kulingana na vibali vya mamlaka za mawasiliano za kila nchi. Aidha, kampuni hizo zinapanga kuanzisha huduma za kupiga simu kwa sauti pamoja na huduma za data zenye uwezo mkubwa zaidi kupitia teknolojia ya Starlink Mobile V2, ambayo itawawezesha watumiaji kupata huduma ya intaneti ya kasi moja kwa moja kwenye simu zao bila kutegemea minara ya kawaida ya mawasiliano.

 


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, ametoa wito kwa wadau na waandaaji wa majukwaa mbalimbali ya wanawake nchini kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, pamoja na kutoa elimu itakayosaidia kuwaokoa wanawake dhidi ya changamoto zitokanazo na matumizi ya nishati isiyo safi.

Salome Makamba ameyasema hayo leo, tarehe 25 Machi 2026, katika hafla ya maadhimisho ya miaka 10 ya Malkia wa Nguvu Legacy Mark 2026 iliyoandaliwa na Clouds Media Group, inayofanyika katika Hoteli ya Serena, jijini Dar es Salaam.

Ameitaka pia Jukwaa la Malkia wa Nguvu kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ni mhamasishaji namba moja barani Afrika wa ajenda hiyo.

“Malkia wa Nguvu Levels isimuache Mwanamke wa Kitanzania akaendelea kuteketea kwa kutumia Nishati isiyo safi. Wizara ya Nishati tunacho kipaumbele cha kuhakikisha kufikia mwaka 2030 Watanzania zaidi ya asilimia 80 wawe wanatumia nishati safi ya kupikia” amesema Salome Makamba.

Aidha, Salome ameeleza kuwa juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali zinahitaji kuungwa mkono na majukwaa mengine kama Malkia wa Nguvu, ambayo yana nafasi muhimu ya kuwa sehemu ya suluhisho kwa kuweka kipaumbele katika utoaji wa elimu kuhusu matumizi ya nishati safi.

Amesisitiza kuwa nishati safi inaleta mapinduzi makubwa katika maisha ya mwanamke kwa kuondoa madhara yatokanayo na moshi wa kuni na mkaa, kufungua fursa za biashara, kuongeza kipato, pamoja na kupunguza hatari na unyanyasaji unaoweza kujitokeza wakati wa kutafuta nishati katika maeneo hatarishi.

“Tukiamua kwa pamoja, tunaweza kuhakikisha hakuna mwanamke anayebaki nyuma kimaendeleo. Tushirikiane na kuwezeshana ili siku moja tujivunie jitihada hizi za kumkomboa mwanamke na kuona matunda yake yakinufaisha jamii nzima,” amesisitiza Mhe. Salome.

 


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amewasili katika hafla ya maadhimisho ya miaka 10 ya Malkia wa Nguvu Legacy Mark 2026 iliyoandaliwa na Clouds Media Group, inayofanyika katika Serena Hotel. Leo tarehe 25 Machi 2026.

Mhe. Salome ndiye mgeni rasmi katika hafla hiyo, ambapo ameambatana na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara ya Nishati, Nteghenjwa Hosseah.

Jukwaa la Malkia wa Nguvu ni mpango maalum unaolenga kuwawezesha wanawake katika nyanja za kiuchumi, kijamii na maendeleo binafsi. Kupitia jukwaa hili, wanawake hupata fursa ya kujifunza, kushirikishana uzoefu na kujenga mitandao itakayowasaidia kukua katika biashara, uongozi na maisha kwa ujumla.

 Aidha, jukwaa hilo huibua mijadala ya masuala muhimu yanayowagusa wanawake na kuwapa motisha ya kujitambua, kujiamini na kutumia fursa zilizopo ili kufikia mafanikio.













Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) imepokea ugeni kutoka Chuo Kikuu cha Limerick cha nchini Ireland , ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika elimu, tafiti na ubunifu kupitia mpango wa Samia Scholarship Extended Data Science and Artificial Intelligence (SSE DS/AI+).

Akizungumza wakati wa mapokezi hayo, Naibu Makamu Mkuu wa NM-AIST anayesimamia Taaluma, Utafiti na Ubunifu, Profesa Anthony Mshandete, amesema ujio wa ugeni huo umefungua fursa mpya katika maeneo ya kipaumbele, ikiwemo ubiasharishaji wa matokeo ya tafiti pamoja na kuendeleza programu za akili unde (Artificial Intelligence) na sayansi kwa ujumla, hatua itakayochochea maendeleo ya kiteknolojia nchini.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Chuo Kikuu cha Limerick anayeshughulikia Ushirikiano wa Kimataifa na Jamii, Profesa Colin Fitzpatrick, amesema wamefurahishwa kukutana na wanafunzi wenye vipaji na viwango vya juu katika NM-AIST. Ameeleza kuwa Chuo Kikuu cha Limerick huvutia wanafunzi mahiri kutoka sehemu mbalimbali duniani na kuwapa uzoefu wa kimataifa. Ameongeza kuwa ameridhishwa na maandalizi ya wanafunzi hao pamoja na mfumo bora wa ufadhili wa masomo unaowawezesha kufanikiwa katika taaluma zao.

Naye Mratibu wa Bootcamp katika NM-AIST na Mkuu wa Shule ya Biashara (BuSH), Profesa Lilian Pasape, amesema ujio wa chuo hicho ni fursa muhimu kwa wanafunzi. Amebainisha kuwa Chuo Kikuu cha Limerick ni miongoni mwa vyuo vinavyoongoza duniani kwa kuunganisha masomo na sekta ya viwanda pamoja na makampuni. Amesema kupitia mpango wa Samia Scholarship Extended Data Science and Artificial Intelligence (SSE DS/AI+), wanafunzi 32 kati ya 50 wamechaguliwa kujiunga na chuo hicho, hali inayoonyesha ubora wa programu hiyo na kuongeza uwezekano wa wahitimu kupata ajira mara baada ya kuhitimu.

Akitoa shukrani kwa niaba ya wanufaika wa ufadhili huo, mwanafunzi Anita Kulwa amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imewawezesha vijana wengi kupata elimu bora ya juu. Ameahidi kutumia ipasavyo fursa hiyo kwa kujituma katika masomo yake, hususan katika maeneo ya sayansi ya data na akili unde, ili kuchangia maendeleo ya Taifa.

Kwa ujumla, ziara hiyo inatarajiwa kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma, kuongeza ubunifu na kuchochea maendeleo ya teknolojia nchini kupitia programu za pamoja kati ya Tanzania na Ireland.

    

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuwasilisha Randama ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/2026 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii tarehe 23 Machi 2026 jijini Dodoma. Kushoto ni Naibu Waziri wa Ardhi Mhe. Kaspar Mmuya na kulia ni Katibu Mkuu Mhandisi Anthony Sanga.

Na Munir Shemweta, WANMM

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imewasilisha Randama ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Bajeti kuu ya Serikali. Akiwasilisha randama hiyo leo tarehe 23 Machi, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo amesema wizara yake imejipanga kuendelea kutekeleza vipaumbele muhimu vinavyolenga kuboresha sekta ya ardhi, ikiwa ni pamoja na kuongeza kasi ya upimaji wa ardhi, utoaji wa hati miliki, pamoja na kudhibiti migogoro ya ardhi nchini. Ameongeza kuwa, katika mwaka wa fedha 2026/2027, wizara inalenga kuimarisha mifumo ya kidijitali katika usimamizi wa ardhi ili kuongeza uwazi, ufanisi na mapato ya Serikali. Aidha, juhudi zaidi zitaelekezwa katika kupanga, kupima na kumilikisha ardhi katika maeneo ya mijini na vijijini. Uwasilishaji wa Randama hiyo ni hatua muhimu katika mchakato wa kupitia na kuboresha Bajeti ya Wizara kabla ya kuwasilishwa rasmi bungeni kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuwasilisha Randama ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/2026 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii tarehe 23 Machi 2026 jijini Dodoma. Kushoto ni Naibu Waziri wa Ardhi Mhe. Kaspar Mmuya na kulia ni Katibu Mkuu Mhandisi Anthony Sanga.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Mhe. Timotheo Mnzava akisisitiza jambo wakati wa uwasilishwaji Randama ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 tarehe 23 Machi 2026 jijini Dodoma. Kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Mary Masanja.
Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Netho Ndilito akizungumza wakati wa kuwasilisha Randama ya Wizara ya Ardhi mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii tarehe 23 Machi 2026 jijini Dodoma.
Sehemu ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii wakifuatilia uwasilishwaji wa Randama ya Wizara ya Ardhi jijini Dodoma tarehe 23 Machi 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

Mrajis wa Vyama vya Ushirika, Dkt. Benson Ndiege amevitaka Vyama vya Ushirika vya Mazao nchini kutumia mizani za kidigitali katika kupima mazao ya wakulima ili kuondoa udanganyifu na kumlinda mkulima. Mrajis ametoa maelekezo hayo kupitia barua ya tarehe 13 Machi, 2026 aliyowaandikia Wenyeviti na Wajumbe wa Bodi wa Vyama vya Ushirika vya mazao Tanzania Bara kuhakikisha kuwa vinatumia mizani za kidigitali kwa lengo la kuondoa udanganyifu kwenye upimaji wa mazao ya wakulima na kurahisisha upatikanaji wa takwimu sahihi za makusanyo/mauzo ya mazao. Vyama vya Ushirika wa Mazao vitakavyobainika kuwa na Mizani ya kidijitali na havitumii Mizani hizo au kuzitumia kwa matumizi tofauti na malengo yaliyokusudiwa, vitachukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria; na wakulima wanatakiwa kuhakikisha mazao yao yanapimwa kwa kutumia Mizani zilizounganishwa na Mfumo wa Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (MUVU) ili kuwawezesha kupata malipo stahiki ya mazao yao. Aidha, Dkt. Ndiege amevitaka Vyama vyote vya Ushirika wa Mazao ambavyo bado havijatekeleza maelekezo ya ununuzi wa Mizani za kidijitali kuhakikisha kuwa vinanunua Mizani hizo kwa kufuata utaratibu wa manunuzi na Mwongozo wa Ofisi ya Mrajis kuhusu Ununuzi wa Mizani hadi kufikia Juni 31, 2026. Tume ya Maendeleo ya Ushirika inaendelea na jitihada za kuimarisha Usimamizi wa Vyama vya Ushirika nchini ambapo kwa sasa moja ya kipaumbele kinachotiliwa mkazo ni kuratibu na kuhimiza Vyama vya Ushirika vya Mazao, kuweka utaratibu wa ununuzi wa Mizani za Kidijitali sambamba na matumizi sahihi ya mizani hizo.

 


Kuelekea uzinduzi wa WazoHuru Air BnB Apartments Mtaa wa Unyankae-Miembeni Manispaa na Mkoa wa Singida, Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Wazohuru Media Group Limited amechangia vifaa vya michezo kwenye shule za msingi katika Manispaa ya Singida vyenye gharama ya shilingi Milioni 4.2

Vifaa hivyo vya michezo ni pamoja na jezi Jozi moja yenye jezi 16 na mpira mmoja katika shule ya Msingi Tumaini Viziwi, S/M Ukombozi, S/M Kindai, S/M Sumaye, S/M Mtipa na S/M Unyankae.

Pia amechangia Jozi moja yenye jezi 16 na mpira mmoja kwa timu ya Umoja wa Michezo na Taaluma Tanzania kwa Shule za Msingi (UMITASHUMTA) Manispaa ya Singida kwa ajili ya kuanza mashindano ya michezo hiyo mwaka huu 2026.

Akizungumza mara baada ya makabidhiano hayo, Mathias Canal amesema kuwa Lengo kuu la zoezi hilo ni kuhamasisha michezo mashuleni, kukuza vipaji vya wanafunzi, pamoja na kuchangia maendeleo ya afya na ustawi wa watoto.

Ameeleza kuwa pamoja na mambo mengine lakini pia kampuni yake imekabidhi vifaa hivyo vya michezo ikiwa ni sehemu ya mrejesho katika jamii baada ya kukamilika kwa ujenzi wa majengo 7 ya WazoHuru Apartments.

Mathias amebainisha kuwa tarehe 28 Machi 2026, kuanzia saa kumi na mbili kamili jioni (12:00) mradi huo wa eneo hilo la makazi ya kisasa utazinduliwa ambapo mgeni rasmi katika tukio hilo atakuwa ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe Halima Dendego.