Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Daniel Mushi, amesema upatikanaji wa mabasi ya watumishi yatasaidia sana katika kuweka mazingira salama na wezeshi ya utendaji.
Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kujali watumishi na kuboresha mazingira ya kazi.
Amesisitiza kuwa watumishi ni nguzo kuu ya kufikia malengo kwani ndio watekekezaji wa mipango na maono wizara hivyo, Wizara inaendelea kuweka mazingira stahiki na jumuishi kwa watumishi wote.
"Rais wetu amesisitiza kazi iende sambamba na kujali utu, na hivi ndio tunatekeleza kauli mbiu ya Kazi na Utu tunasonga mbele kwa kuweka mazingira yanayovutia utendaji kwa watumishi" amesema Prof. Mushi.
Prof. Mushi amewahimiza watumishi kutumia mabasi hayo na kuyatunza ili yaweze kurahisisha utendaji kazi na kutumika kwa muda mrefu.Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Edith Rwiza amesema ununuzi wa mabasi matatu (3) mapya kwa ajili ya usafiri wa watumishi ni hatua muhimu ya kuboresha mazingira ya kazi kwa Wizara.
Akizungumza jijini Dodoma Aprili 28, 2026 katika uzinduzi wa mabasi ya watumishi, Mkurugenzi huyo amesema mabasi hayo yamenunuliwa na Wizara kwa kushirikiana na Mradi wa Kuimarisha na Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi Tanzania Bara (BOOST) kwa zaidi ya Shilingi milioni 500 kwa lengo la kuwezesha watumishi katika safari za kila siku za kwenda kazini na kurudi nyumbani pamoja na ziara za kikazi.
"Kabla ya hatua hii, watumishi walilazimika kutumia kati ya shilingi 10,000 hadi 15,000 kwa siku kufika ofisini hali iliyoleta ugumu wa maisha na kupunguza morali ya kazi" amesema Dkt. Rwiza
Mkurugenzi Rwiza amesema upatikanaji wa mabasi haya ni sehemu ya jitihada za wizara kuhakikisha watumishi wanafanya kazi katika mazingira bora na yenye ufanisi.
Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikalin na Afya (TUGHE), Bw. Moshi Kisinga ameushukuru uongozi wa Wizara hiyo kwa kununua magari kwa ajili ya watumishi.
"Kwa niaba ya watumishi wenzangu tumepokea magari haya kwa furaha na hakika tumeondokana na changamoto kubwa ya usafiri", amesema Kisinga.
Ametoa rai kwa watumishi kufanya kazi kwa juhudi na maarifa akisisitiza uwajibikaji katika majukumu ya kila siku.

























