. _Amshukuru Rais Samia kwa kuwezesha upatikanaji wa magari hayo_
. _Ataka magari hayo yasaidie kukuza utalii na ufuatiliaji wa mapato_
. _Aelekeza Halmashauri kushirikiana na TAWA, TANAPA na wadau wa utalii kukuza utalii_
Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla leo Jumanne Juni 30, 2026 amekabidhi magari mawili ya usimamizi na ufuatiliaji wa Utalii na mapato kwa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli, akimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha upatikanaji wa magari hayo mawili yenye jumla ya thamani ya Shilingi 440,611,400.
Mhe. Makalla amekabidhi magari hayo wakati wa ziara yake Wilayani Monduli, akiagiza matumizi sahihi na yaliyokusudiwa kwa magari hayo ikiwa ni pamoja na kusaidia katika kukuza utalii Wilayani Monduli pamoja na ufuatiliaji na ukusanyaji wa mapato ya serikali.
Katika hatua nyingine, Mhe. Makalla akisisitiza kuhusu ukuzaji wa utalii Mkoani Arusha, ameielekeza Halmashauri ya Wilaya ya Monduli kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania TAWA, Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) na wadau wengine wa utalii katika kukuza utalii Wilayani Monduli sambamba na kuhifadhi vivutio vya utalii vilivyopo Wilayani Monduli.
Magari yaliyokabidhiwa ni pamoja na Toyota Land Cruiser Hardtop (5 door) likiwa na gharama ya Shilingi 235, 606,600 na Toyota Land Cruiser (Pick up) likiwa na gharama ya Shilingi 205, 004,800 pamoja na pikipiki aina ya Yamaha YBR iliyotolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii, vyote kwa pamoja vikitajwa kuongeza chachu ya ukusanyaji wa mapato kwa mwaka wa fedha 2026/27 na kuhakikisha doria za maliasili zinafanyika kikamilifu.
Awali katika maelezo yake Afisa mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli Bw. Jeofrey Mwambasi amemshukuru Rais Samia na Uongozi wa Halmashauri hiyo kwa kuwezesha kupatikana kwa magari hayo, akiahidi kuwa Halmashauri hiyo itayatunza magari na pikipiki hiyo pamoja na kuhakikisha yanatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na serikali katika ukusanyaji wa mapato pamoja na uhifadhi.















































