Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imejidhatiti katika kuboresha maisha ya walimu nchini, hususan katika maeneo ya maslahi na mazingira ya kazi.
Mhe. Mchengerwa ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na viongozi pamoja na wajumbe wa mkutano mkuu wa Chama cha Walimu Wilaya ya Rufiji, mara baada ya walimu hao kufanya uchaguzi wa viongozi katika Ukumbi wa Chuo cha Maendeleo Ikwiriri.
"Tumedhamiria kuboresha maisha yenu. Binafsi, tangu nikiwa Waziri wa UTUMISHI hadi sasa nikiwa Waziri wa TAMISEMI, nimekuwa mstari wa mbele kupigania madaraja yenu na maslahi ya walimu kwa ujumla," amesisitiza.
Aidha, Waziri Mchengerwa amebainisha kuwa Taifa lina bahati ya kuwa na Rais anayewajali na kuwathamini walimu na kwamba baada ya kupokea ombi la kuwapandisha madaraja walimu, Rais hakusita kulitekeleza, licha ya ukweli kuwa hatua hiyo ilisababisha ongezeko katika bajeti ya mishahara.
Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Walimu Mkoa wa Pwani, Susan Shesha, amemshukuru Waziri Mchengerwa kwa juhudi zake za kupigania maslahi ya walimu tangu akiwa Waziri wa UTUMISHI na kueleza kuwa katika nafasi yake ya sasa kama Waziri wa TAMISEMI, ameendelea kutoa kipaumbele kwa walimu kwa kusimamia miradi ya elimu kwa uadilifu, ili kuhakikisha kuwa inawanufaisha wananchi kwa ujumla.
Post A Comment: