๐ Serikali kuwezesha Sera, Sheria kwa wawekezaji wa Nishati Safi ya kupikia
๐ Ahamasisha matumizi ya Nishati ya Safi ya kupikia nchini
๐Ampongeza Mkurugenzi Mtendaji TANESCO kwa kuunganisha watumishi
Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amewataka Wanawake kuwa mabalozi wa nishati safi ya kupikia, ili kuhakikisha familia na jamii zote zinatumia nishati salama kwa afya na kwa ustawi wa vizazi vijavyo.
Dkt. Biteko amebainisha hayo wakati wa Kongamano la kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa umeme leo Machi 4, 2025 jijini Dar es Salaam.
"Nimefahamishwa kuwa Kongamano hili limeanza kwa mjadala mzito juu ya nafasi ya wanawake katika ajenda ya nishati safi ya kupikia ya umeme. Kupitia mijadala kama hii, tunaibua hoja muhimu na tunashirikiana na wadau wote muhimu kuweka mikakati ya kuhakikisha tunafikia lengo la asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034," Amesema Dkt. Biteko.
Dkt. Biteko amewataka kutumia fursa hiyo ya Siku ya Wanawake vyema na kuwasihi wanawake wote kuibeba ajenda hiyo muhimu ambayo Mheshimiwa Rais amekuwa akiipa kipaumbele akiwa ndani na nje ya Nchi.
Ameongeza kuwa, kupitia mfuko wa Nishati safi ya kupikia, Serikali itahakikisha kuwa wanawake wanapata mikopo yenye riba nafuu ili waweze kushiriki kikamilifu katika biashara za nishati safi.
Pia, Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa Sera na Sheria mbalimbali zinakuwa rafiki kwa wawekezaji wa nishati safi ya kupikia ili waweze kushiriki kikamilifu katika biashara ya nishati safi ya kupikia.

Naye, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga amewataka watanzania hususan wanawake kuendelea kuiunga mkono ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa kutumia na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa watanzania wote.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mha. Gissima Nyamo - Hanga amesema kuwa Serikali imeweka msukumo katika matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa kutumia nishati ya umeme kwa kuwa ni nafuu zaidi na imefika kila mahali nchini.
Aidha, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TANESCO, Mhe. Balozi Zuhura Bundala amesema kuwa wanawake ndio wahusika wakuu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Amesema nishati safi ya kupikia ina gharama nafuu na ni rahisi kwa matumizi.
Jukwaa hilo limelenga kuhakikisha kwamba kila Mtanzania, hususani mwanawake, anapata fursa ya kutumia nishati safi kwa kupikia.





Post A Comment: