Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) imepewa siku 90 kuhakikisha adha ya uchafuzi wa mazingira inayosababishwa na uunganishaji wa mifumo ya maji kiholela fukwe ya Dengu na Fukwe ya Barabara ya Obama jirani na Hospitali ya Aghakan jijini Dar es Salaam inatatuliwa.

Agizo hilo limetolewa leo tarehe 26 Machi, 2024 na Naibu Katibu Mkuu ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Bi. Christina Mndeme alipokuwa akiongea na Waandishi wa Habari katika ziara yake iliyohudhuriwa pia na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) la kuhakikisha DAWASA wanajenga eneo la kutibu maji kabla ya kuingia baharini ili kulinda Afya ya viumbe wa baharini na Ikolojia ya bahari kwa ujumla.

Amesema ni wajibu wa DAWASA kuhakikisha wanatenganisha mfumo wa majitaka ya bomba lao na bomba la maji ya mvua la Jiji la Dar es Salaam ili kulinda ikolojia ya bahari na mimea iliyo ndani yake kwa mstakabali wa maendeleo endelevu ya bahari nchini.

Aidha amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Mhe. Elihuruma Mabelya kupanda miti katika eneo lote la fukwe hiyo ili kuleta hewa safi na rafiki kwa Viumbe hai.

Ziara hiyo ya Naibu Katibu Mkuu (Muungano na Mazingira) ilihusisha watendaji kutoka NEMC, DAWASA, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.










Share To:

Post A Comment: