Wakuu wa wilaya na Wakurugenzi wametakiwa kusimamia kikamilifu suala la lishe katika maeneo yao ili kuwa na Taifa lenye watu wenye afya bora pamoja na utimamu wa akili.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa wilaya ya Karatu Dadi Kolimba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Paul Christian Makonda katika kikao cha tathmini ya lishe Mkoa wa Arusha.
Kolimba amesema kuwa agenda ya Mheshiwa Rais ni kuhakikisha kila mtanzania anakuwa na afya njema ili kuweza kusaidia kuwa na Taifa lenye watu waliosalama kiafya .
"Mheshiwa Rais ameingia mkataba na wakuu wa mikoa,wakuu wa wilaya na wakurugenzi ambapo imeenda mpaka kwa watendaji wa kata kwasababu ya usalama wa nchi yetu kuanzia usalama wa mama na mtoto kabla na baada ya kuzaliwa"Alisema
Aidha amewaeleza wadau hao wa lishe kuangalia afua za lishe kila wilaya kuona kama zinatekelezwa ili kuwa na tija.
Kwa upande wake Afisa lishe Mkoa Dotto Mirembe anasema kuwa taarifa ya utekelezaji ya viashiria vinavyosimamiwa na mkataba kwa kipindi cha July hadi Desemba 2024 hadi 2025 ambapo mkoa umeweza kutenga bajeti ya afua za lishe ambapo Mkoa umetenga kiasi cha shilingi Milioni 947 ambapo ni sawa na shilingi 2490.4 kwa kila mtoto.
Dotto amesema tathmini ya lishe kwenye ngazi ya kata Mkoa wa Arusha wanafanya vizuri kwa kuwa mpaka sasa wameweza kuvuka lengo la Taifa katika suala la lishe.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt Charles Mkombachepa kwa niaba ya Katibu tawala wa Mkoa wa Arusha Mussa Misaile amepongeza Afua za lishe kwa kuendelea kufanya vizuri na kuwataka kutobweteka na kuendelea kushika nafasi nzuri katika masuala ya lishe kimkoa.
Post A Comment: