Na Chedaiwe Msuya, WF, Mwanga


Vikundi vya Kijamii na Huduma Ndogo za Fedha katika Kata ya Lembeni Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro, vimetakiwa kujisajili katika mfumo wa Wezesha Portal ambao umeanza kutumika tangu mwezi Oktoba, 2023, ili kurahisisha usajili kwa njia ya kidigitali  ambapo vikundi vinaweza kusajili bila kufika Ofisi za Halmashauri.
 
Akizungumza katika mwendelezo wa program ya elimu ya fedha kwa umma iliyotolewa kwa wananchi wa Halmashauri ya Manispaa ya Mwanga, Afisa Usimamizi wa Fedha katoka Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha - Wizara ya Fedha, Bw. Kelvin Kalengela, alisema ni muhimu watoa huduma ndogo za fedha wasajili na kupata leseni ya kutoa huduma hizo kwa wananchi kwa mujibu wa Sheria za Benki Kuu ya Tanzania.
 
‘’ Wito kwa Taasisi za huduma ndogo za fedha ni muhimu wasajiliwe kwa mujibu wa Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania, vilevile vikundi vyote vya huduma ndogo za fedha na vile vya kijamii ni lazima visajiliwe kwa mujibu wa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ili viweze kunufaika na fursa mbalimbali za uwezeshaji kiuchumi zinazotolewa na Serikali’’. Alisema Bw. Kalengela
 
Bw. Kalengela aliongeza kuwa ni vyema vikundi vya kijamii na huduma ndogo za fedha vikaharakisha kujisajili kwenye mfumo wa Wezesha Portal kwa kufanya hivyo kutawasaidia kuunganishwa na fursa mbalimbali zilizopo kwenye mifuko na program za uwezeshaji wananchi kiuchumi pamoja na Taasisi za fedha zinazotoa mikopo kwa riba nafuu inayotolewa kwa vijana wajasiriamali na makundi maalum.
 
Vilevile Afisa Usimamizi wa Fedha katoka Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha - Wizara ya Fedha, Bw. Stanley Kibakaya alisema kuwa lengo la Programu ya Elimu ni kutoe Uelewa kwa Wananchi kuhusu masuala ya fedha na kuonyesha fursa zinazopatikana katika Sekta ya Fedha ikiwemo umuhimu wa kusajili vikundi vya huduma ndogo ya fedha kwa njia ya mfumo.
 
“ Programu hii ni ya Nchi mzima na Lengo la Wizara hadi kufikia Mwaka 2025/26 ni kuwafikia Wananchi asilimia 80 kwa kuwapatia Elimu ya Fedha na kutambua fursa zilizopo kwenye Sekata ya Fedha, kuna fursa kwa makundi yote”. Alisema Bw. Kibakaya

Nae Afisa Maendeleo ya Jamii, Bw. Samwel Daniel Kateri, ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Fedha kuweza kutoa elmu ya fedha katika Wilaya ya Mwanga kwa wananchi wake.

“Napenda kutoa pongezi za dhati kwa Wizara ya Fedha kwa jitihada zake za kutoa elimu ya fedha kwa wananchi wa Wilaya ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro. Hatua hii ni muhimu katika kuimarisha uelewa wa wananchi kuhusu usimamizi wa fedha, uwekezaji, mikopo, na itawawezesha kufikia malengo yao ya kifedha ”.

Program ya elimu ya fedha inatolewa kwa wananchi jinsi ya kutumia fedha zao kwa njia bora na wana uwezekano mkubwa wa kuchangia maendeleo ya jamii. Kwa mfano, wanaweza kushirikiana katika miradi ya maendeleo ya kijamii kama vile ujenzi wa shule, hospitali, au miundombinu.
Share To:

Post A Comment: