Wadaia kugawa hongo kati ya Sh.5000 na Sh.50,000 ,Mbunge mwenyewe atoa majibu
Na Shomari Binda,Rorya
WAKATI joto la uchaguzi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), likianza kupanda kwa baadhi ya majimbo imeelezwa katika Jimbo la Rorya
mkoani Mara wajumbe waliokuwa wakipatiwa mafunzo ya utendaji ndani ya Chama hicho wamedaiwa kupewa fedha kati ya Sh.5000 hadi Sh.50,000 kama sehemu ya kuwashawishi wajumbe hao kuelekea uchaguzi mkuu.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopo zinaeleza kwamba juzi katika mafunzo ya watendaji ndani ya Chama Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Rorya, Ongujo Wakibara kwa kushirikiana na mbunge wa Jimbo hilo, Jafari Chege wanadaiwa kuyavuruga kwa kumwaga hongo kwa wajumbe wa mafunzo hayo.
Wakati wa mafunzo hayo inadaiwa Mbunge Chege na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Rorya, Ongujo Wakibara waliingilia katika semina ya makatibu wa matawi na kata iliyofanyika Februari 20, 2025 ambapo wanadaiwa kugawa posho kiasi cha Shilingi 50,000 kwa kila katibu aliyehudhuria mafunzo hayo.
Tuko hilo ambalo liliibua mjadala katika makundi sogozi ya ya WhatsApp ya CCM Mkoa wa Mara ambapo yameeleza utaratibu huo unakiuka maelekezo kutoka makao makuu ya CCM Taifa.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa mafunzo hayo ya watendaji yasiingiliwe na viongozi au wanasiasa kwa sababu ni mafunzo ya kiutendaji na chama kilisema kitagharamia kila kitu ikiwemo chakula na posho.
“Lengo la chama kufanya hivyo ilikuwa ni kuondoa urasimu wa wagombea kutumia nafasi hiyo kutoa rushwa kinyume chake Mwenyekiti wa chama na mgombea wake ambaye ndiye mbunge kwa sasa wamevamia ukumbi na kutoa posho hizo.
“Jambo hili halijawafurahisha hata wakufunzi haswa kauli za Mwenyekiti na Mbunge baada ya kuzuiwa na wakalazimisha kufanya kwa nguvu,” imesema sehemu ya taarifa katika makundi hayo sogezi ya WhatsApp
Hata kupitia Gazeti tando la George Marato Tv, imefatilia taarifa hiyo na kuzungumza na Mbunge wa Jimbo la Rorya, Jafar Chege kwa njia ya simu na kudai yupo msibani toka asubuhi na hajaudhuria kikao hicho na kushangazwa na taarifa hiyo.
Hata hivyo Chege alikiri kuiona taarifa hiyo kwenye makundi sogozi ya CCM lakini hajui lengo lake.”Nimeshangazwa na taarifa hiyo,nipo msibani na nimeambiwa kikao hicho kimeenda vizuri na kimalizika salama hizo taarifa ni za uongo,” amejibu Chege alipokuwa akielezea taarifa hiyo.
Alipotafutwa Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Rorya, Ongujo Wakibara hakupatikana kwenye simu yake ya mkono hivyo jitihada za kumtafuta kuzungumzia jambo hili zinaendelea ili kupata ukweli wa madai ya taarifa hizo.
Hata hivyo pamoja na hali Mwenyekiti huyo wa CCM anadaiwa kuwa amekuwa akiwasimamisha viongozi hovyo hovyo na hivi karibuni katika Kata za Mkoma, Kirogo, Kinyenche, Nyathorogo, Goribe na Tai aliwasimamisha vongozi wa matawi bila kuihusisha kamati ya siasa.
Wakati kwa Mbunge Chege amekuwa akizunguka katika baadhi ya kata na matawi na kukutana na wajumbe moja kwa moja na kugawa fedha kiasi cha Shilingi 5,000 hadi Sh.50,000 kulingana na uwezo na hadhi ya mjumbe.
Post A Comment: