SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Vijana,Ajira na wenye Ulemavu imewaomba Wananchi wote wa Jiji la Mwanza pamoja na Mikoa iliyopo jirani kujitokeza kwa wingi katika viwanja vya furahisha Jijini Mwanza ili kuungana na Mh Kassim Majaliwa ambaye ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuadhimisha Wiki ya Vijana inayokutanisha vijana Nchi nzima kwa lengo la kumuenzi Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.


Hayo yameelezwa mapema Leo hii Oktoba 9,2024 Jijini Dodoma na Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Vijana,Ajira, Kazi na wenye ulemavu Mhe Ridhiwani Kikwete alipokuwa akizungumza na Wanahabari wakati akitoa taarifa juu ya Maadhimisho hayo yaliyobeba kauli mbiu inayosema "VIJANA NA MATUMIZI YA FURSA ZA KIDIJITALI KWA MAENDELEO ENDELEVU" ambapo amesema kupitia jukwaa hili vijana hupata nafasi ya kujadili masuala mbalimbali yanayowahusu ikiwemo kuonesha vipaji,bunifu na kazi wanazozifanya.

Aidha ameongeza kuwa mbali na lengo la kumuenzi Baba wa Taifa pia yapo malengo Mahsusi ya Wiki ya vijana ambayo ni kutoa fursa kwa vijana kukutana na vijana wenzao,Vijana kuonesha vipaji,bunifu na kazi wanazofanya katika maeneo yao,kuhamasisha vijana katika jamii kushiriki katika programu mbalimbali za usaidizi wa jamii kwa njia ya kujitolea,Kujenga uwezo katika uongozi kupitia Semina za kujenga uwezo,Kutoa hamasa kwa vijana ili watambue kuwa wao ni sehemu ya jamii na kuhamasisha ushiriki wa Wizara,Idara na Taasisi za Serikali,Sekta Binafsi,Mashirika ya Kiraia,Mashirika ya Umoja wa Mataifa,Washirika wa maendeleo na Mashirika yasiyo ya Kiserikali katika kuwaendeleza vijana.

"Serikali inawaomba Wananchi wote wa Mwanza na Mikoa ya jirani kujitokeza kwa wingi uwanja wa Furahisha na kuungana na Mhe Kassim Majaliwa (mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kufanikisha shughuli hiyo muhimu ya Kitaifa".

"Taifa letu huadhimisha Wiki ya Vijana ikiwa ni jukwaa linalowakutanisha vijana Nchi nzima kwa lengo la kumuenzi Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Kupitia jukwaa hili vijana hupata nafasi ya kujadili masuala mbalimbali yanayowahusu,kuonesha vipaji,bunifu na kazi wanazozifanya na kuwakutanisha na wadau mbalimbali wa maendeleo ya Vijana".

"Malengo ya Wiki ya Vijana ni,kutoa fursa kwa vijana kukutana na vijana wenzao,kufahamiana na kajadili fursa na chanagamo mbalimbali zinazokabili maendeleo yao ya kiuchumi na kijamii,Vijana kuonesha vipaji,bunifu na kazi wanazofanya katika maeneo yao,kuwakutanisha vijana na viongozi na wadau wa maendeleo mbalimbali na kuweza kueleza changmoto zinazowahusu".

Pia Waziri Kikwete ameeleza kuwa katika kuadhimisha Wiki ya Vijana Kitaifa kutakuwa na mambo mbalimbali yakifanyika ikiwemo Kongamano la vijana la siku 2 litakalofanyika tarehe 10 na 12 Oktoba 2024, ambalo litahusisha vijana 1,500 watakaojengewa uelewa katika maene mbalimbali kama vile Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007,Toleo la mwaka 2024 na mkakati wake wa utekelezaji,Ushiriki na Ushirikishwaji wa vijana katika Maamuzi, Fursa za ujasiliamali na Ubunifu wa Kidijitali katika kujifunza na kujiajiri, Teknolojia na Afya ya Uzazi,Akili Mnemba,fursa na changamoto na Teknolojia na Afya ya akili kwa vijana.

Wiki ya Vijana Kitaifa ilianzishwa mwaka 2000 Mkoani Kilimanjaro kufuatia tamko rasmi lililotolewa na Raisi wa awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Benjamin William Mkapa. Katika kutambua umuhimu wa vijana katika maendeleo ya nchi, na limekuwa likiendeshwa kwa miaka 24 mpaka na huadhjmishwa kuanzia tarehe 8 hadi 14 Oktoba kila mwaka.
Share To:

Post A Comment: