Na. Farida Ramadhani na Joseph Mahumi, WF, Mbeya.


Wakazi wa Jiji la Mbeya wametakiwa kutumia elimu waliyoipata katika Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Kitaifa kubadilisha maisha yao hususan katika masuala ya usimamizi wa fedha.

Rai hiyo imetolewa na Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Dkt. Charles Mwamwaja, wakati akifunga maadhimisho hayo Jijini Mbeya.

Dkt. Mwamwaja alisema kwamba elimu waliyoipata inatakiwa iwabadilishe kwa kuacha mambo yote waliyokuwa wakiyafanya awali kwa kufuata utaratibu na maamuzi sahihi wanaposhighulikia masuala yao ya kifedha.

“Wataalam wanasema mikopo siyo mibaya, lakini kabla hujakopa lazima uwe na malengo, usikope kwa sababu fedha zipo mahala fulani, ukope ukiwa na mpango. Naamini hii ni sehemu mojawapo ya kubadilika”, alisisitiza Dkt. Mwamwaja.

Alisisita wananchi wanapochukua mikopo wahakikishe wanasoma mikataba na kuchukua nakala za mikataba hiyo ili kuepuka madhara mbalimbali yanayotokana na mikop yenye masharti magumu maarufu kama mikopo umiza. 

Dkt. Mwamwaja pia alitoa rai kwa wananchi hao kutumia huduma rasmi za fedha kwa kuhakikisha kila wanachokifanya katika shughuli zao za masuala ya kifedha ziwe zimerasimishwa.

“Kama ni kikoba ni jambo zuri na kinaungwa mkono lakini hicho kikoba kisajiliwe ili kiwe rasmi”, aliongeza Dkt. Mwamwaja.

Aliwasihi kutumia elimu waliyoipata kuwaelimisha wengine ambao hawakuweza kufika katika maadhimisho hayo kwa kuwa elimu ya fedha ni endelevu na haitolewi kwenye maadhimisho hayo pekee. 

Aidha, alisema utoaji wa elimu ya fedha ni endelevu ingawa utoaji wa elimu hiyo kwenye Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa hutolewa mara moja kwa mwaka. 

“Maadhimisho haya ambayo tunamaliza leo sio mwisho wa kutoa elimu, bado tutaendelea na kutumia njia mbalimbali katika kutoa elimu ya fedha, tusitoke hapa tukasema baada ya maadhimisho haya fursa hii ya kutoa elimu inafungwa hadi mwakani, Hapana. Utoaji wa elimu ya fedha ni endelevu”, alisema Dkt. Mwamwaja.

Alisema Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeteua Waratibu wa Huduma Ndogo za Fedha katika kila mkoa na halmashauri nchini ambao wamekuwa wakitoa elimu ya fedha kwa wananchi.

Maadhimisho hayo ni ya nne kufanyika nchini ambayo ni utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa Mwaka 2020/21 – 2029/30 na yanalenga kutoa elimu ya fedha kwa umma na kuongezeka kwa mchango wa Sekta ya Fedha kwenye ukuaji wa Uchumi.
Share To:

Post A Comment: