Afisa Tarafa wa Idodi,Mapesah Makala amewaomba wananchi wajitokeze kujiandikisha kwenye daftari la mkazi ili apate haki ya kugombea nafasi mbalimbali na kumchagua kiongozi
Afisa Tarafa wa Idodi,Mapesah Makala amewaomba wananchi wajitokeze kujiandikisha kwenye daftari la mkazi ili apate haki ya kugombea nafasi mbalimbali na kumchagua kiongozi

Na Fredy Mgunda, Idodi Iringa.


WANANCHI wa tarafa ya Idodi wameshauriwa kujitokeza kujiandikisha kwenye daftari la makazi ili aweze kupata haki ya kuchagua viongozi bora na kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji kwa ajili ya maendeleo ya miaka mitano ijayo.

Akizungumza wakati wa mkutano wa kuhamasisha kushiriki kikamilifu uchaguzi huo,Afisa Tarafa wa Idodi, Mapesah Makala alisema kuwa ni muhimu kila mwananchi ajitokeze kujiandikisha kwenye daftari la mkazi ili apate haki ya kugombea nafasi mbalimbali na kumchagua kiongozi anayemtaka.


Makala alieleza kuwa zoezi la uandikishaji lililoanza tarehe 11 Oktoba litaendelea hadi tarehe 20 Oktoba 2024, na alihimiza wananchi wasipoteze fursa hii muhimu.

Katika maelezo yake, Afisa Mapesah Makala aliongeza kuwa Serikali za Mitaa zina mchango mkubwa katika maendeleo ya jamii, na kwa kuwaandikisha wapiga kura wengi, wakazi wa Makifu watakuwa na nafasi ya kuchagua viongozi wanaoweza kusukuma mbele ajenda za maendeleo katika eneo hilo. Alitoa wito maalum kwa vijana na wanawake kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi ili kupaza sauti zao katika uchaguzi ujao.

Makala aliwahakikishia wakazi wa Makifu kuwa serikali imeweka mipango thabiti ya kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa uwazi na haki, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kudumisha amani na utulivu wakati wa kipindi hiki cha uchaguzi.

Share To:

mwangaza wa hbari

Post A Comment: