Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Christina Mndeme ameupongeza uongozi wa Wilaya ya Gairo mkoani Morogoro namna jitihada zinavyochukuliwa katika kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.

Uongozi wa Wilaya ya Gairo umeandaa Tamasha ‘Samia Kilimo Biashara Expo 2024’ ambapo wananchi hupewa elimu mbalimbali ikiwemo faida ya matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia sambamba na athari zitokanazo na matumizi ya Nishati isiyo salama ya kupikia ya kutumia kuni na mkaa.

Bi. Mndeme ambaye alikuwa mgeni rasmi katika tamasha hilo Oktoba 10,2024 ameupongeza uongozi wa wilaya kwa namna ambavyo wamekuwa mstari wa mbele kwa kutoa elimu kwa wananchi wao juu ya matumizi ya nishati safi sambamba na kushirikiana na wadau wake ambapo wananchi wameanza kunufaika kwa kupata majiko ya gesi kwa bei nafuu na majiko banifu yakigawiwa bure kwa baadhi ya wananchi.

“Kila mmoja wetu anafahamu kwamba kinara namba mojoa wa uhamasisha wa matumizi ya nishati safi ni Rais wetu ambaye amekuwa akionesha mfano kwa vitendo na hiyo yote sababu ya upendo wake kwa wananchi ili kuepuka athari zitokanazo na matumizi ya kuni na mkaa.

“Niwaombe elimu hii na ugawaji wa majiko haya ifanyike hadi vijijini ili kila mtu anufaike na punguzo hii ambayo hapa tumeshuhudia wenzetu wakiipata kwani kwa kufanya hivyo tutaokoa watu wengi hasa kina mama ambao asilimia kubwa ndio tunaoshinda jikoni kuandaa chakula cha familia,” amesema Bi. Mndeme.

Kw aupande wake Mkuu wa Wilaya ya Gairo Mhe. Jabir Makame amesema kwa kutambua umuhimu wa tamasha hilo wanashirikisha wadau mbalimbali ikiwemo wanaohusika na mazingira lengo ikiwa kuwasogezea fursa wananchi wa wilaya hiyo.

“Ajenda moja wapo iliyobebwa katika tamasha hili ni kuhusu nishati safi, ajenda ambayo imesisitizwa na kutolewa maelekezo na viongozi wetu na katika Wilaya ya Gairo tumeweza kuipa kipaumbele na kuifanyia kampeni na katika tamasha hili kila siku tumekuwa tukitoa elimu,” amesema Mhe. Makame.

Kaulimbiu ya tamasha hilo inasema “Tunza Mazingira na Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo na Mifugo.

Share To:

Post A Comment: