Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Ridhiwani Kikwete amepongeza LESCO kwa kuendelea kusimamia haki na uwajibikaji wa masuala ya kazi, uchumi na kijamii.

“Nitumie fursa hii kuwapongeza kwa moyo wa dhati kwa kutekeleza vema majukumu yenu kwa ufanisi ili kuhakikisha malengo ya kuanzishwa LESCO yanatimia” amesema. 
Mhe. Ridhiwani ametoa pongezi hizo leo Septemba 4, 2024 Jijini Dodoma alipokutana na Wajumbe wa Baraza la  Ushauri wa Masuala ya Kazi, Uchumi na Kijamii (LESCO) kwa lengo la kufahamiana na kuagana nao wajumbe wa baraza hilo ambalo uongozi wake umefikia ukomo.

Aidha, amesema katika kipindi cha miaka 3, LESCO imefanya kazi nzuri ya kuishauri serikali kuhusu sera zinazohusu masuala ya Ajira na Kazi; upangaji wa kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi; Uridhiaji wa mikataba ya Shirika la Kazi Duniani; na ushirikishwaji wa wadau wa Utatu (Serikali, Waajiri na Wafanyakazi) katika masuala  ya  kazi, Uchumi na jamii.
Vile vile, Mhe. Ridhiwani ametoa rai kwa wajumbe wa baraza hilo kuendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri ili kuhakikisha sekta ya kazi na ajira inazingatia misingi ya kazi zenye staha kwa maslahi ya wafanyakazi na waajiri.

Awali akizungumza Mwenyekiti wa LESCO Dkt. Samwel Nyantahe ameishukuru Serikali kwa kutoa ushirikiano katikia kipindi chote cha utekelezaji wa majukumu yao.







Share To:

Post A Comment: