Na: Josephine Majura, WF, Mwanza


Wakuu wa Idara ya Ununuzi na Wakuu wa Idara ya Mipango wameahidi kwenda kutekeleza kwa vitendo yote waliyojifunza kupitia mafunzo ya kuwajengea uwezo katika Sheria mpya ya Ununuzi, Sheria ya Ubia  kati ya  Sekta ya  Umma na Sekta Binafsi na Matumizi sahihi ya Takwimu yaliyohusisha mikoa ya Mwanza, Geita na Kagera yaliyofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti baada ya kupatiwa mafunzo hayo Afisa Mipango na Uratibu kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba, Bw. Rogatevane Kipigapasi,  aliishukuru Serikali kwa kuwajengea uwezo kuhusu Sheria hizo kwa kuwa mafunzo hayo yatawaongezea uwezo na weledi katika kutekeleza majukumu yao.

“Kulikuwa na mada nzuri binafsi nimejifunza fursa zilizopo kupitia Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, marekebisho katika Sheria hii yanatoa fursa kwa wazawa kushiriki katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo”, alisema Bw. Kipigapasi.

Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato, Bi. Maria Ndohelo, alishauri  mafunzo hayo yawe endelevu kwa kutolewa mara kwa mara ili kuhakikisha Sheria, Kanuni na Taratibu zinajulikana vizuri kwa watumiaji wakuu wa Sheria hizo ili iwe rahisi wakati wa utekelezaji.

“Nina waasa Washiriki wenzangu wa mafunzo haya kwenda  kuyatumia vizuri tutakaporudi katika Vituo vyetu  vya kazi kwa kuwa Serikali ina matarajio makubwa kwetu sisi baada ya mafunzo haya”, alisema Bi. Ndohelo.

Alifafanua kuwa Serikali inawategemea kama wataalamu waliopewa dhamana katika kupanga Mipango ya Serikali na kusimamia Manunuzi mbalimbali ya Umma hivyo ni jukumu la kila mshiriki wa mafunzo kwenda kufanya kazi kwa weledi kama walivyoelekezwa katika mafunzo.

Mafunzo hayo yamewashirikisha Wakuu wa Idara ya Ununuzi na Wakuu wa Idara ya Mipango wa mikoa ya Mwanza, Geita na Kagera yaliyofunguliwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Bw. Kusirie Swai katika ukumbi wa Ofisi  ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Bw. Kusirie Swai, aliwataka Washiriki wa mafunzo kwenda kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu.

Bw. Swai alisema kuwa Serikali hutunga sheria ili kuhakikisha wanaotekeleza majukumu kwa niaba ya Serikali wanazifuata, ili kupata matokeo chanya yanayotarajiwa na Serikali.

Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Taasisi zake ikiwemo Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC) na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wanaendelea kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo Wakuu wa Idara ya Ununuzi na Mipango nchi nzima katika mikoa ya Kikanda ikiwemo Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kati, Kanda ya Pwani, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Kusini, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini na Kanda ya Magharibi.

Share To:

Post A Comment: