Wananchi wa Wilaya ya Longido Mkoani Arusha wameiomba serikali kujengea uzio shule zote za serikali za bweni zilizopo katika wilaya hiyo lengo ni kuimarisha ulinzi na kuthibiti vitendo vya uchomaji moto mabweni vinavyokithili katika wilaya hiyo.

Agosti 26 mwaka huu bweni moja la shule ya sekondari mchanganyiko ya Enduiment iliyopo Kijiji cha Lerangwa Kata ya Olmology Tarafa ya Enduiment wilayani humo liliungua moto na septemba mosi mwaka huu bweni lingine moja tena liliungua moto na kufanya wazazi wa wanafunzi hao kuwa na wasiwasi na Maisha ya watoto wao wakiwa shule.

Mmoja wa Mzazi wa Wanafunzi hao aliyejitambulisha mbele ya Naibu Waziri wa Madini na Mbunge wa Longido,Dkt Steven Kiruswa aliyekwenda tena shuleni hapo kuangalia uhalibifu huo wa Moto uliochoma bweni hilo,Oliver Pallangyo alisema alisema shule hiyo haina uzio hivyo ni wakati wa shule zote za bweni Longido kuwekwa uzio na kuwa na walinzi ili kulinda mali za shule na wanafunzi.

Pallangyo alisema vitendo vya uchomaji moto mabweni ya wanafunzi vinapaswa kuthibitiwa na wahusika wanapaswa kusakwa na kuchukuliwa hatua kwani leo inaweza kuwa hapa na kesho inaweza kuwa sehemu nyingine hivyo ni wakati wa kujengea uzio wa umeme kwa shule zote Longido ili wanafunzi waweze kusoma kwa amani.

Alisema na kumshukuru Mbunge Kiruswa kwa kuendelea kutoa misaada kwa wanafunzi hao na wamemwomba Mbunge huyo kutochoka na kuhimiza uongozi wa serikali wilaya ya Longido na serikali Kuu kuangalia hilo la uzio ili wazazi wasiwe na wasiwasi wanafunzi wakiwa shuleni.

Naye Mtawa{Sister}wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Arusha,Sister Bertha Shirima yeye aliunga mkono wazo la wazazi wenzake waliotangulia na kusisitiza kuwa hilo ni wazo jema ambalo linapaswa kufanyiwa kazi na serikali kwa kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Longido ili wanafunzi waweze kuzingatia masomo wakiwa shule.

Shirima alisema uthibiti wa uchomwaji moto shule za bweni Longido unapaswa kuimarishwa kwa sasa na wahusika wanapaswa kusakwa usiku na mchana ili hatua zichukuliwe dhidi yao kwani hawana lengo zuri kwa longido na nchi kwa ujumla.

Naye Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM na Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi {UVCCM} Mkoa wa Arusha,Tezra Furaha pamoja na kuunga mkono wazo la uzio pia alitoa msaada wa magodoro 50 na mablanketi 50 kwa shule hiyo huku akisisitiza kuwa na ushirikiano na Mbunge Kiruswa katika kuleta maendeleo kwa wananchi wa Longido.

Alisema Mbunge Kiruswa ni Mbunge wa mfano katika Mkoa wa Arusha kwani ni Mbunge mwenye kutatua changamoto za wananchi wake kwa haraka na mwenye kujali hivyo anapaswa kuungwa mkono kwa hali na mali hivyo wanapaswa kumlinda kwa gharama yoyote.

Naye Kiruswa mbali ya kutoa magodoro kwa wanafunzi wote 485 na blanket ya idadi hiyo hiyo alisisitiza kupata taarifa sahihi ya wale wanaoihujumu shule hiyo kwa kuchoma moto ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa haraka.

Alisema serikali iko tayari kujenga Miundombinu ya shule hiyo lakini kwanza inataka kupata ushirikiano wa kutosha kwa kuwataja wale wote wanaofanya hujumu ya uchomaji moto shule hiyo ili serikali isiweze kupata hasara pindi inapojenga Miundombinu.

‘’Leo hapa sitoki hadi mje muninong’oneze kwa siri akina nani wanahujumu shule kwa kuchoma moto mabweni ili hatua zichukuliwe maana serikali ikijenga halafu wahuni wanachoma itakuwa kazi bure hivyo wahusika wanapaswa kujulikana’’ alisema Kiruswa

Waziri huyo alisema kuwa Waziri wa Elimu ,Professa Aldof Mkenda ametoa fedha taslimu shilingi milioni moja ili ziweze kununuwa magodoro na baadhi ya wabunge wameahidi kuchangia ununuaji wa magodoro na blanketi ili wanafunzi watakaporudi shuleni kila kitu kiwe sawa kwa ajili ya kuendelea na masomo.

Awali bweni moja liliteketea kwa moto n abweni hilo lilikuwa likichukua wanafunzi 340,vitanda 170 na magodoro 340 mali zote zimeteketea kwa moto lakini hakukuwa na maafa.

Afisa Elimu Sekondari Wilaya ya Longido,Gilbert Sombe alisema shule hiyo inahitajika kujengwa mabweni matatu kwa gharama shilingi milioni 390,vitanda 170 vinapaswa kununuwa kwa gharama ya shilingi milioni 142 na magodoro 340 yanapaswa kununuliwa kwa gharama ya shilingi milioni milioni 60.



Share To:

Post A Comment: