Na. Saidina Msangi, Chalinze, Pwani.


Wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze wameishukuru Serikali kwa kuwafikishia elimu ya fedha itakayowasaidia kujikwamua kiuchumi kwa kutumia fursa za uwekezaji ili kujiongezea kipato na kuongeza thamani ya akiba zao.

Wananchi hao walitoa shukrani hizo baada ya kupata mafunzo ya elimu ya fedha yaliyoratibiwa na Wizara ya Fedha, yenye kauli mbiu "Elimu ya fedha ni msingi wa maendeleo ya kiuchumi" ambayo yametolewa kwa siku mbili katika ukumbi wa mikutano wa Wilaya ya Halmashauri ya Chalinze.

                                                  
Akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake, Bi. Mery Leonard Chiwiko, aliishukuru Wizara ya Fedha kwa kuwapa elimu hiyo muhimu, akisema kuwa hapo awali hawakuwa na uelewa mzuri kuhusu masuala ya fedha, mikopo na uwekezaji.


"Tunaishukuru Wizara ya Fedha kwa kutupatia elimu hii, itatusaidia sana katika kuimarisha maisha yetu ya kifedha, kuepukana na mikopo umiza na pia tumejifunza kuwa hata kama una kipato kidogo inawezekana kuweka akiba na kuwekeza akiba hiyo na kupata faida," alisema Chiwiko.


Wananchi hao waliiomba Serikali kuona namna ya kuwafikishia mafunzo ya elimu ya fedha ikiwezekana mara mbili kwa mwaka kutokana na umuhimu wake katika kuwawezesha kukabiliana na changamoto za kiuchumi.


Timu ya Maafisa kutoka kutoka Wizara ya Fedha imetoa mafunzo ya elimu ya fedha ikiwemo namna ya kuweka akiba na mbinu za usimamizi wa fedha na uwekezaji kwa washiriki zaidi ya 800 ambao wanatarajiwa kuwa mabalozi wa kuwafikishia wenzao elimu hiyo ili nao waweze kunufaika na kujikwamua kiuchumi.


Share To:

Post A Comment: