Tanzania ina mifumo kadhaa ya kisheria na udhibiti inayoongoza sekta ya mawasiliano na TEHAMA ili kuhakikisha huduma ya intaneti ya kasi inawafikia wananchi wote huku Serikali ikiendelea kuhakikisha usalama katika matumizi ya mtandao kwa wananchi na wadau wote wa ndani na nje ya nchi. 

Akihutubia wakati akifungua Kongamano la C2C (Connect2Connect) leo Septemba 18, 2024 jijini Arusha, Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Jerry William Silaa (Mb) amesema kuwa Serikali inawekeza katika Sekta ya TEHAMA kwa kuwa ni nyenzo muhimu ya nchi kuwa na uchumi wa kidijitali.

Amesema kuwa Mkutano wa Connect2connect kwa mwaka 2023 uliofanyika katika Hoteli ya Madinat Al Bahr huko Zanzibar na kuhudhuriwa na washiriki kutoka nchi 20 uliangazia juhudi za pamoja zinazohitajika kuziba pengo la kidigitali na kukuza maendeleo endelevu barani Afrika.

Mhe. Silaa ametoa rai kwa washiriki wa Kongamano la mwaka huu kuchangia mawazo na kujadili kwa kina namna ya bora ya kuunganisha nchi za bara la Afrika na miundombinu ya kidijitali ili kuwezesha maendeleo endelevu ya uchumi wa kidigitali. 

Naye Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Extensia Limited, Bw. Tariq Malik amesema kuwa Kongamano la mwaka huu chini ya kauli mbiu ya 'Maunganisho yenye manufaa' unalenga kujadili vipengele muhimu vya maendeleo ya TEHAMA vinavyosukuma ukuaji wa uchumi, ujumuishi wa kijamii, na maendeleo endelevu barani Afrika. 

Ameongeza kuwa mada zitakazojadiliwa ni pamoja na hali ya sekta, athari za uchumi wa kidijitali kwa Tanzania, na nafasi ya vituo vya data katika mabadiliko ya kidijitali ili kubadilishana maarifa muhimu kuhusu mipango ya ukuaji wa baadaye na mfumo wa ikolojia ya TEHAMA ili kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bw. Mohammed Khamis Abdulla amesema kuwa Kongamano la C2C limekuwa taa ya maendeleo, likituongoza kuelekea siku zijazo ambapo teknolojia inakuwa kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Ameongeza kuwa kupitia ushirikiano wa Wizara hiyo, kampuni ya Extensia ya Uingereza na washirika wengine matokeo makubwa yameonekana katika kupanua wigo wa miundombinu ya mawasiliano nchini ambapo kwa mwaka huu Kongamano hilo litahusisha mahitaji muhimu ya miundombinu na uunganishaji wa mipakani, ambayo ni muhimu sana kwa kuharakisha ajenda ya TEHAMA ya Afrika.

Katika hatua nyingine Mhe. Silaa amewakaribisha washiriki wa kongamano hilo kushiriki katika Kongamano la Nane la mwaka la TEHAMA litakalofanyika jijini Dar es Salaam, tarehe 13 hadi 17 Oktoba, 2024 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa  Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan lenye kaulimbiu "Kufungua Nguvu ya Akili Mnemba na Roboti kwa Mabadiliko ya Kiuchumi na Kijamii".



Share To:

Post A Comment: