Na. Joseph Mahumi na Peter Haule, WF, Dodoma


Serikali imesema inaendelea kuweka mikakati na mbinu mbalimbali za muda mfupi, wa kati na mrefu katika kushughulikia changamoto ya uhaba wa Fedha za Kigeni (Forex), ikiwemo kuainisha baadhi ya sekta ambazo zinaweza kuleta mapato zaidi ambayo yatatoa suluhisho la kudumu la uhaba wa fedha za kigeni.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi mpya wa Uingereza nchini Tanzania, Mhe. Marrianne Young aliyefika Ofisini kwake Jijini Dodoma kwa ajili ya kujitambulisha.

Mhe. Dkt. Nchemba amesema kuwa, katika bajeti inayoendelea, Serikali imeweka vipaumbele kwa baadhi ya sekta ambazo ni za kuongeza mapato ya fedha za kigeni japokuwa kama nchi kuna hali tofauti na baadhi ya nchi nyingine zinazoizunguka Tanzania kwakuwa inatekeleza miradi mikubwa ya kimkakati.

Aliongeza kuwa, hali hiyo imesababishwa na kutokuwa na uwiano katika uingizaji wa bidhaa nchini na uuzaji wa bidhaa nje ya nchi, lakini pia imetokana na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati kama mradi wa kuzalisha umeme wa Bwawa la Nyerere, mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) na Daraja la Busisi.

“Ni wazi kwamba kila unapokuwa na tofauti yoyote kati ya kile unachouza nje na kile unachoagiza kutoka nje, kutakuwa na shinikizo kwenye fedha za kigeni, na hicho ndicho kinachotokea na pia mikakati na hatua zinazochukuliwa zitasaidia kupata suluhisho la kudumu siku za karibuni” alisema Mhe. Dkt. Nchemba.

Aidha Mhe. Dkt. Nchemba alitumia fursa hiyo kumpongeza Balozi huyo kwa kuteuliwa kuwa Balozi wa Uingereza nchini na kuahidi kuendelea kufanya kazi pamoja ili kuendeleza ushirikiano kati ya Tanzania na Uingereza katika kuhakikisha maendeleo endelevu ya kiuchumi. 

“Dhamira ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuendelea kushirikiana na Serikali ya Uingereza ili kuimarisha ushirikiano muhimu wa maendeleo” alisema Dkt. Nchemba.

Mhe. Dkt. Nchemba aliongeza kuwa, Uingereza ni mdau muhimu wa maendeleo kwa kuendelea kutekeleza ajenda ya Maendeleo ya Kitaifa kama ilivyoainishwa chini ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/22–2025/26 (FYDP III).

“Tunashukuru sana kwa msaada thabiti ambao Serikali ya Uingereza imekuwa ikitoa kwa Tanzania, hususan katika maeneo ya ulinzi wa kijamii kupitia Mpango wa TASAF awamu ya II, Sekta ya Elimu, Afya kupitia Mfuko wa Pamoja wa Afya na Msaada wa Mpango wa Kupambana na Rushwa ambao umechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo endelevu ya kiuchumi nchini Tanzania” alisema Dkt. Nchemba.

Kwa Upande wake, Balozi huyo mpya wa Uingereza nchini, Mhe. Marrianne Young, amemshukuru Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu kwa kumkaribisha na kuahidi kuendeleza ushirikiano kati yao katika kusukumu gurudumu la maendeleo ya kiuchumi kwa Tanzania.

“Ningependa kuwapongeza kwa sera imara za uchumi wa jumla na maendeleo, Ninaelewa kwamba tumekuwa na msaada wa muda mrefu kutoka Mamlaka ya Mapato na Forodha ya Uingereza (HMRC) katika eneo hili na tunafanya kazi zaidi ili kusaidia juhudi za Serikali ya Tanzania za kuongeza wigo wa mapato”

Kikao hicho kimehudhuriwa na Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Madeni Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, viongozi wandamizi wa Wizara ya Fedha na Maafisa kutoka Ubalozi wa Uingereza.
Share To:

Post A Comment: