Wakuu wa Idara ya Ununuzi na Wakuu wa Idara ya  Mipango wametakiwa kutumia mafunzo waliyoyapata kuhusu Sheria mpya ya ununuzi, Sheria  ya Ubia  kati ya  Sekta ya  Umma na Sekta Binafsi na Matumizi sahihi  ya Takwimu wakati wa utekelezaji  majukumu yao na kuwa mabalozi kwa wengine ambao hawajapata fursa hiyo.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, wakati akifungua mafunzo kuhusu Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura  Na. 410, Sheria  ya Ubia  kati ya  Sekta ya  Umma na Sekta Binafsi,Sura NA. 103 na  Matumizi sahihi  ya Takwimu ulioandaliwa na Wizara ya Fedha katika ukumbi wa Halmashauri ya Jiji,Mtumba, Dodoma.

Alisema kuwa Sheria mpya ya Ununuzi imejikita zaidi katika kulinda maslahi ya Taifa hususan katika kuwanufaisha watanzania, ambapo kumewekwa upendeleo kwa makundi mbalimbali ya kijamii.

“Makundi hayo yametengewa asilima thelathini ya bajeti ya ununuzi ya kila taasisi ya umma lengo kuu likiwa ni kuyawezesha makundi hayo kushiriki katika zabuni za umma na hatimaye yaweze kukuza kipato chao pamoja na kujenga uwezo”, alisema Mhe. Senyamule.

Aliongeza kuwa upande wa miradi ya PPP pamoja na mambo mengine, Sheria ya PPP sura 103 imefanyiwa marekebisho kwa kuweka mazingira wezeshi ili kuimarisha ushiriki wa Sekta Binafsi katika kutekeleza miradi ya ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta ya Binafsi. 

Mhe. Senyamule alifafanua kuwa  Sheria hiyo inaruhusu Wawekezaji katika miradi ya ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi kunufaika na vivutio vya kikodi na visivyokuwa vya kikodi, sawa na wale wanaopata vivutio chini ya Sheria ya Uwekezaji Tanzania, Sura 38.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Bi. Jenifa Christian Omolo alisema kuwa Wizara ya Fedha inaendesha mikutano kwa watendaji wa Serikali waliopo katika ngazi za Mikoa pamoja na Halmashauri za Majiji, Miji na Wilaya.

“Serikali imeona changamoto mbalimbali  zinazohusu utekelezwaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura 410, Sheria ya Ubia Kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi pamoja na matumizi sahihi ya takwimu zinazoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu,”alisema Bi. Omolo.

Alisema kuwa Mkutano huo umehusisha mawasilisho ya mada tatu, ikiwemo  utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2023, Sheria ya Ubia baina ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi na matumizi sahihi ya takwimu.

Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye ni Mkuu wa Idara ya Ununuzi Manispaa ya Singida,  Bw. Simon Haule, aliipoongeza Serikali kwa kufanya marekebisho ya Sheria na Kanuni zake.

“Kupitia mafunzo haya,  tunaahidi kuwa Mabalozi wazuri kwa wenzetu  na tutawafundisha Watendaji wengine katika Taasisi tulizotoka ambao hawajashirikia mafunzo haya ili lengo la Serikali liweze kufanikiwa kupitia sisi”, alisema Bw. Haule.

Mkutano huo umewashirikisha Wakuu wa Taasisi mbalimbali wa Wizara za Kisekta, Wakuu wa Idara ya Ununuzi na Wakuu wa Idara ya Mipango iliyojumuisha Kanda ya Kati katika Mikoa ya Dodoma, Singida na Iringa.

Share To:

Post A Comment: