Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Mhe. Fatuma Toufiq akizungumza wakati Kamati hiyo ilipotembelea na kukagua maendeleo ya mradi wa uzalishaji Sukari wa Mkulazi Holding  Company, Mbigiri Mkoani Morogoro.

 Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Mhe. Fatma Toufiq amepongeza uwekezaji uliofanywa katika kiwanda cha sukari cha Mkulazi.


Mhe. Fatma ametoa pongezi hizo wakati wa ziara ya kamati hiyo ya kukagua maendeleo ya kiwanda hicho kilichojengwa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa ubia na Jeshi la Magereza.

"Tumeona uwekezaji mkubwa sana ambao umefanywa katika kiwanda hiki cha Mkulazi, tunaendelea kumpongeza sana Mhe. Rais Dkt. Samia kwa kazi kubwa anazofanya ikiwemo ya kuzindua kiwanda hiki ambacho kinaenda kupunguza nakisi ya sukari nchini," amesema Mhe. Fatma.

Amesema katika kiwanda hicho ambacho kimeanza uzalishaji wa sukari ya majumbani, wamejionea mitambo ikiendelea kufanya kazi ya uzalishaji.

Naye, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe.Patrobas Katambi, amesema ajira zaidi ya 2500 zinatarajiwa kuzalishwa na kwamba hadi sasa tangu kiwanda kianze uzalishaji tani 12000 za sukari zimezalishwa.

Pia amesema kiwanda hicho kinazalisha umeme megawati 15 ambapo kati ya hizo nane zinatumika kiwandani na saba zimeingizwa kwenye gridi ya taifa

Mhe. Katambi amesema miongoni mwa faida za kiwanda hicho ni pamoja na kutoa ajira kwa vijana pamoja na uhakika wa soko la miwa kwa wakulima wa maeneo jirani na mradi huo.

Baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo, wameonesha matumaini makubwa na uwepo wa mradi huo kwa sababu umegusa maisha ya Watanzania moja kwa moja ikiwemo kupata ajira pamoja na wakulima kupata soko la uhakika la miwa na hivyo kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja.
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Masha Mshomba akifafanua jambo mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, ilipotembelea na kukagua mradi wa uzalishaji Sukari wa Mkulazi Holding  Company, uliopo Mbigiri Mkoani Morogoro.
Share To:

Post A Comment: