Na Mwandishi Wetu, WHMTH, Mwanza


Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Moses Nnauye (Mb) amewataka wananchi kutokubali kununua vocha kwa bei tofauti na iliyoandikwa kwenye vocha hizo ambayo zimeelekezwa na Serikali.

Waziri Nape ametoa kauli hiyo tqrehe 18 Julai akiwa katika Kisiwa cha Lyakanyasi Ziwa Viktoria katika Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi wanaouziwa vocha za sh 1,000 kwa sh 1200 na za sh. 500 kwa sh. 600.

"Vocha ya 1,000 nunua kwa 1,000, vocha ya 500 nunua kwa 500 ukinunua kwa bei zaidi unalanguliwa, ni wizi na unatusumbua, kwa sababu muuza vocha ameingia mkataba na mwenye vocha kama kuna mahesabu ya kuongezeka wanajuana wao tunachotaka sisi mwananchi anunue vocha kwa bei iliyoandikwa kwenye vocha," amesema Waziri Nape.

Amewaagiza wauza vocha kwenye kisiwa hicho kuacha mara moja ulanguzi huo kwani Serikali imepeleka mnara ili kuwasaidia wananchi visiwani huko. 

"Nimepanda boti kuja hapa kukagua ujenzi wa mnara huu tuliowaletea, mkiuza zaidi tutawakamata mmoja mmoja kwa sababu huo ni wizi, waambieni na wenzenu huko nimeambiwa yapo maduka wanauza kwa bei tofauti za zilizoelekezwa," amesema. 

Waziri Nape amesema tayari alishatolea ufafanuzi na maelekezo mara kadhaa Bingeni baada ya Wabunge kulalamika hivyo hawezi kuwavumilia wafanyabiashara wachache wanaokiuka.

Amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Said Mtanda kuweka watu wake wa kufuatilia wanaokiuka maagizo wachukuliwe hatua.


Share To:

Post A Comment: