Mwenyekiti wa madiwani viti maalum Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ambaye ni diwani wa viti maalum kata ya Lyabukande Mhe. Zawadi Lufungulo Mwasha akizungumza katika ziara yao kata ya Nyamalogo leo Ijumaa Julai 12, 2024.


Na Mapuli Kitina Misalaba

Madiwani wa viti maalum wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wamewakumbusha watendaji, wenyeviti wa vijiji na vitongoji katika Halmashauri hiyo kusoma taarifa za mapato na matumizi ili wananchi waweze kufahamu hatua za maendeleo katika maeneo yao.

Wameyasema hayo leo Ijumaa  Julai 12,2024 katika ziara yao kata ya Nyamalogo na kwamba  wameendelea na ziara yao kwa lengo la kuhamasisha wanawake na wanachama wa CCM na jumuiya zake kujitokeza kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura, kuhamasisha wanawake kujitokeza kuchukua fomu za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi, Usajili wa wanachama wa CCM na jumuiya zake pamoja na na kukemea Ukatili wa kijinsia.

Madiwani wa viti maalum Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wakiongozwa na Mwenyekiti wao Mhe. Zawadi Lufungulo pamoja na mambo mengine wamewasisitiza watendaji, wenyeviti wa vijiji na vitongoji kusoma taarifa za mapato na matumizi katika mikutano ya hadhara kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa.

Wamesema hatua hiyo itawasaidia wananchi kutambua miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo imetekelezwa, inatekelezwa na miradi inayotarajiwa kutekelezwa katika maeneo yao.

Pia wamesema zoezi la kusoma taarifa za mapato na matumizi litasaidia kupunguza au kumaliza kabisa kero na malalamiko mbalimbali kwa wananchi.

Wamesema serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika kila sekta ikiwemo sekta ya Elimu, Afya, Maji pamoja na miundombinu ambapo wamesema ni vema kila mwananchi kuifahamu miradi hiyo kupitia taarifa za watendaji, wenyeviti wa vijiji pamoja na vitongoji.

Katika hatua nyingine wamaendelea kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwajali wananchi wake katika nyanja mbalimbali huku wakiwaomba wananchi kuendelea kuiunga mkono serikali katika hatua za kuwaletea maendeleo.

Wamempongeza mbunge wa jimbo hilo kwa jitihana mbalimbali anazozifanya katika kuwaleta maendeleo wakazi wa jimbo hilo ambapo wamesema yapo mabadiliko makubwa ya maendeleo yamefanyika katika kipindi chake ambayo yalikuwa ni kero na changamoto kwa wananchi.

Madiwani wa viti maalum hao wamesema badae Mwaka huu 2024 taifa la Tanzania linatarajia kufanya uchaguzi wa serikali za mitaa katika nafasi mbalimbali za uongozi ikiwemo wenyeviti wa mitaa, vijiji na vitongoji ambapo wameendelea kuwasisitiza wanawake kujitokeza kwa wingi kuchukua fomu ili waweze kuwatumikia wananchi kwa mujibu wa katiba ya nchi ambayo kwa sasa inatekelezwa kupitia ilani ya Chama cha Mapinduzi CCM.

Pia wameendelea kuiomba jamii kuungana pamoja katika mapambano ya kutokomoza  vitendo vya ukatili vinavyoendelea ikiwemo ubakaji, ulawiti, ndoa za utotoni pamoja na ushoga unaosababishwa na mmomonyoko wa maadili hasa kwa vijana.

Wametumia nafasi hiyo kuwahimiza wazazi, walezi na jamii kuwalea watoto katika maadili mema na misingi inayozingatia mila na desturi za eneo husika ili kuepukana na vitendo vya ukatili ikiwemo ubakaji na ulawiti unaoendelea kwa watoto.

Kwa upande wake katibu wa umoja  wa wanawake UWT Wilaya ya Shinyanga vijijini Bi. Magdalena Dodoma pamoja na mambo mengine ameendelea kuhamasisha uhai wa chama ikiwemo wanachama wa CCM na jumuia zake kujisajili katika mfumo wa kielekroniki.

Pia wamewakumbusha wanawake wa UWT kwenye kata, matawi na mashina yote Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga vijijini kuhakikisha wanashiriki katika vikao vyao vya ndani na kwamba hatua hiyo itasaidia kuwatambua wenye sifa za kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa serikali za mitaa Mwaka huu 2024 pamoja na uchaguzi mkuu 2025.

Baadhi ya wananchi wakiwemo wanachama wa CCM na jumuiya zake wamewapongeza madiwani wa viti maalum kwa kufanya ziara hiyo ambapo wamesema imewasaidia kutambua umuhimu wa wajibu wao katika hatua zote za kuwapata viongozi wa vijiji na vitongoji  ikiwemo kujiandikisha mapema katika daftari la mpiga kura pamoja na daftari la balozi.Burudani ya wimbo maalum wa Chama cha Mapinduzi CCM. baada ya viongozi kuwasili katika mkutano huo kata ya Nyamalogo tarafa ya Nindo.





 

Share To:

Misalaba

Post A Comment: