Kesi ya Jinai namba 1883/2024  inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Dk.Yahaya Nawanda imeanza kupokea na kusikiliza mashahidi katika Mahakama ya Hakimu Mfawidhi Mkoa wa Mwanza.

Licha ya shauri hilo kutakiwa kuwa la wazi kwa mujibu wa sheria za Mwenendo wa Makosa ya Jinai namba 20 kifungu namba 186, lilionesha kuwa na vizuizi kwa waandishi wa habari pamoja na wananchi waliofika mahakamani hapo kulisikiliza.

Awali shauri hilo litakuwa kusikizwa katika ukumbi mkubwa wa Mahakama ya Hakimu Mfawidhi Mkoa lakini bila taarifa yoyote kama ulivyo utaratibu wa kutangaza mienendo ya Mashtaka katika kituo hicho jumuishi, washtakiwa walipelekwa katika chemba ya Hakimu huyo na kuanza kusikizwa kuanzia majira ya saa tatu Asubuhi.

Baada ya waandishi pamoja na wananchi waliofika mahakamani hapo kusikiliza shauri hilo kusubiri bila mafanikio ilibidi kudadisi kwa baadhi ya wahudumu wa mahakamani hapo ambao alieleza kuwa tayari shauri hilo linaendelea ndani ya chemba.

Kufuatia hali hiyo waandishi walielekea katika mlango wa chemba hiyo ambapo hata hivyo kilikuwa kinafika kipindi cha mapumziko ambako zilitolewa dakika 35 kisha warejee kusikiliza mashahidi.

Baada ya muda mfupi Hakimu Mfawidhi Mkuu wa Mahakama hiyo, Erick Marley alimtuma mmoja wa wasaidizi wake kueleza waandishi kuwa hawatoruhusiwa kuingia katika chemba hiyo mpaka pale itakapotoka idhini ya Mshtakiwa pamoja na shahidi kuruhusu kuwepo kwa waandishi pamoja na wasilikizaji wengine.

Kufuatia hali hiyo Waandishi wa habari walimfuata Msajili katika Kituo hicho jumuishi ili kujua chanzo cha shauri hilo kuitwa na kuhamishwa ukumbi bila taarifa sambamba na kutakiwa kusikilizwa bila kuwepo kwa waandishi wa habari wala wasilikizaji.

Msajili aliwasiliana na Hakimu Mfawidhi Mkuu, Erick Marley na kumtaka kuongea na waandishi juu ya maswali yao ambapo Hakimu alikubali na kuwaita katika chemba yake na kutaja hatua hiyo kuwa ni takwa la kisheria na haki ya mtoa ushahidi katika makosa ya namna hiyo.

Alipohojiwa kuhusu kifungu cha kisheria kinachosimamia takwa hilo, Hakimu Erick Marley alisema ni Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai namba 20 iliyofanyiwa marejeo mwaka 2022 Kifungu namba 186(3).

"Kufuatia takwa hilo Mahakama itawahiji na kupata ridhaa yao baada ya mapumziko, na endapo wakikubali tutawaita waandishi na wale wanaohitaji kusikiliza shauri hili lakini pia wasiporidhia pasi hamtoruhusiwa."

Majira ya saa 11:23 washtakiwa pamoja na mashahidi walirejea katika chemba hiyo ambapo waandishi waliendelea kukaa nje kwa muda bila kupata mrejesho hivyo kuthibitika juu ya walengwa kutokukubali wao kusikiliza shauri hilo.


KISEMAVYO KIFUNGO NAMBA 186(3).

Kwa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai namba 20 iliyorejelewa mwaka 2022, kifungu hicho namba 186 (3) kinasema,

"Bila ya kujali masharti ya Sheria nyingine yoyote, ushahidi wa watu wote katika kesi zote zinazohusu makosa ya kingono yatapokelewa na Mahakama kwa kamera (ikimaanisha bila kurekodiwa) ushahidi na mashahidi wanaohusika katika makosa ya kesi za namna hii haitachapishwa na au katika gazeti lolote au vyombo vingine vya habari.

Lakini kifungu hiki hakitapiga marufuku uchapishaji au usambazaji wa jambo lolote kama hilo kwa uaminifu mfululizo wa ripoti za kisheria au katika gazeti au majarida kwa nia njema inayokusudiwa kusambazwa miongoni mwa wanachama wataaluma ya sheria au matibabu." mwisho wa kunikuu.

Hata hivyo, Hakimu Mfawidhi Mkuu wa Mahakama hiyo, Erick Marley aliahirisha shauri hilo ambapo kwa mujibu wa Hakimu huyo Mashahidi wawili kati ya 15  walisikilizwa kwa zaidi ya saa tatu na nusu.

Mashahidi hao ni pamoja na Mama Mzazi wa binti anayedaiwa kulawitiwa pamoja na Binti mwenyewe. Ambapo kesi hiyo imeahirishwa mpaka Agosti 13 itakapo sikilizwa kwa siku tatu mfululizo.

Kadhalika Mahakama hiyo itapokea vielelezo 18 na mashahidi 13 kutoka upande wa Jamhuri.


CREDIT : NIPASHE

Share To:

Post A Comment: