Katibu Mkuu Wizara ya Madini Mhandisi Yahya Samamba, ameupokea  ujumbe wa Serikali ya Marekani kupitia Ubalozi wake nchini  na kufanya kikao kifupi cha utambulisho ambapo ujumbe huo umeeleza kusudio la kufika Wizarani.

Akizungumza katika kikao hicho kifupi, kilichofanyika leo Julai 16, 2024, Mhandisi Samamba ameueleza ujumbe huo kuhusu mpango wa Wizara kuhuisha Mpango Mkakati wake ili  kukidhi matakwa kuhusu dhamira yake ya kuendeleza  madini muhimu na  mkakati  pamoja na utayari wa Wizara ya Madini kushirikiana na Marekani katika uendelezaji wa madini hayo na kuongeza  kwamba, Wizara Iko tayari kubadilishana taarifa za msingi zitakazowezesha kusudio la ushirikiano huo.

" Mkitoka hapa mtapata nafasi ya kukutana na taasisi zetu za GST, STAMICO na Tume ya Madini ambao watatoa mawasilisho yatayowasaidia ninyi kupata taarifa muhimu. Pia,  STAMICO  wanayo maeneo ambayo wangependa kushirikiana kuyaendeleza Kwa hivyo mtasikia mengi kutoka kwao," amesema Mhandisi Samamba.

Naye, Meneja  Mipango wa Idara ya Rasilimali Nishati na Madini  kutoka Ubalozi wa Marekani nchini Bw. Evan McGlaughlin

amesema nchi hiyo imelenga kushirikiana na Tanzania katika maeneo kadhaa ikiwemo kuboresha mkakati wa kuendeleza madini mkakati, ushirikiano katika masuala ya jiosayansi na kuwajengea uwezo wataalam wa ndani.

Pia, ameishukuru Wizara kwa kuupokea ujumbe huo na kuukutanisha na taasisi zake utakaowezesha kuanzisha ushirikiano baada ya kuwa na majadiliano kwa takriban kipindi cha mwaka mmoja nyuma 

Itakumbukwa Tanzania inajiandaa vilivyo  katika  uendelezaji wa madini mkakati hususan kupitia Vision 2030: Madini ni Maisha& Utajiri katika kipindi hiki ambacho kuna mahitaji makubwa ya madini hayo duniani. 

Madini mkakati yanayotumika kutengenezea bidhaa mbalimbali za teknolojia ikiwemo za betri za magari ya umeme, betri za simu na vizuia joto.

Madini hayo ni kama kinywe, nikeli, lithium, manganese, kobati na mengine ambayo Tanzania imebarikiwa kuwa nayo.

Share To:

Post A Comment: