Mkuu wa mkoa wa Njombe Anthony Mtaka, amewaagiza Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira (RUWASA) mkoani humo kufundisha wananchi nidhamu ya kutumia maji ili yasiotee.

Mtaka ametoa agizo hilo wakati wa kufunga kikao cha kuunganisha Jumuia za CBWSO za mkoa wa Njombe kwenye mfumo wa kieletroniki wa ukusanyaji mapato ambapo amesema ni lazima wananchi wakumbushwe juu ya kuwa na nidhamu ya kutumia maji.

“Kwa sababu kuna mtu anafungua maji ananawa huku anaongea na simu huku wenzake wanasubiria mpaka aje kumaliza kuongea kamaliza lita tatu hao watu wapo mfundishe namna ya utumiaji wa maji,” amesema Mtaka.

Pia amesema elimu juu ya mfumo huo wa Tehama inapaswa kuwa endelevu kwa wananchi ili wapate uelewa wa kutosha.

Aida Mtaka ametoa rai kwa jumuia hizo za watumia maji kuzingatia uadilifu katika kutoa huduma ili wasidondokee kwenye vyombo vya dola.

“Zingatieni uadilifu mkikuta mtu kaingia TAKUKURU kwa kula hela ya sh. 50,000, impeleke Takukuru sh.15,000 impeleke lockup, zambi za namna hiyo zipunguze mwenyewe,” amesema Mtaka.

Awali Mratibu wa Mfumo wa Maji IS kutoka Wizara ya Maji, Injinia Masoud Almasi alisema hadi kufikia juni mwaka huu jumuiya zote zinapaswa kuwa zimejiunga na mfumo huo.

“Vyombo vyote 36 kutoka wilaya zote zimechatoa ankra ya kwanza kupitia mifumo, kwa hiyo wananchi wa sasa hivi wamepokea sms na ile sms inacotrol namba ikionyesha kiwango kila mtu anachodaiwa na inawezesha sasa kulipa kwa utaratibu kupitia mitandao ya simu na benki,” amesema Almasi.

Nao viongozi wa jumuiya za watumia maji, akiwemo Magreti Maulaga alisema mfumo huo wameuelewa lakini katika maeneo ya vijijini bado kuna changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama pamoja na kukosekana kwa ajira kwa ajira za uhakika.

“Pia tunapata changamoto ya usafiri kwa sababu unakuta kama mimi nahudumia vijiji vitano natoka kata ya Mdandu naenda kuhudumia kata ya Itulaumba tunapata changamoto ya usafiri,” amesema Maulaga.

Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira RUWASA Mkoa wa Njombe, Sadick Chaka alisema kwa mujibu wa utaratibu ajira zao zinatokana na jumuiya zao hivyo waongeze juhudi kwenye ukusanyaji wa mapato.

Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira (RUWASA) wilaya ya Njombe, Elikalia Malisa alisema mfumo huo utasaidia kuleta tija kwa serikali hasa kwenye suala la ukusanyaji wa mapato.

Share To:

Post A Comment: