Na Tumaini Mafie, Arusha 

Takribani wanawake 603 wamefariki dunia kwa kipindi Cha miaka miwili  2022/2023 huku Chanzo kikitajwa kuwa ni ukatili wa kijinsia.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Mkutano wa Asasi za Kiraia unaoendelea mkoani Arusha Kamishina Msaidizi wa Jeshi la Polisi nchini ambaye ni mkuu wa kitengo Cha Ulinzi wa mtoto dhidi ya biashara  haramu ya  usafirishaji wa Binadamu  kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Tulibake Kasongwa  amesema Idadi ya mauaji kwa wanawake bado ni kubwa.

Aidha Kamishna Kasongwa  amesema chanzo kikuu cha mauaji ni mapenzi  na idadi ndogo hutokana na ndugu pale wanapotaka kugombea mirathi ambapo amewataka  wananchi kutoa taarifa Kwa Jeshi la Polisi endapo watabaini migogoro yenye viashiria vya mauaji.

"Mwaka Jana Takwimu za idadi ya wanawake waliofariki  dunia ni  jumla ya wanawake 305 huku mwaka huu ikiwa ni 298 ambapo imepungua  kwa wanawake 7  sawa na asilimia 2. Amesema  

Naye Mkurugenzi wa Kituo Cha Sheria na Haki za binadamu Dk. Anna Henga amewataka wananchi kutoa Ushirikiano Kwa Jeshi la Polisi hususani yanapotokea mauaji  Kama hayo na lengo likiwa ni kupunguza idadi ya Vifo vitokanavyo na ukatili.

"Rai yangu wanajamii  tusikumbatie ukatili ,toa taarifa kituo Cha Polisi unapoona unyanyasaji, ripoti Serikali za Mitaa, ustawi wa Jamii au Polisi katika madawati ya jinsia , Ili kuweza kutokomeza haya majanga ,Takwimu za mauaji ya wanawake ziko juu kiukweli ni wanawake wengi walioripotiwa kufariki 300 siyo kidogo" amesema Henga.

Kwa Upande wake Mdau mwingine ambaye pia ni mtoa mada katika Mkutano huo akiwakilisha Taasisi za Dini Mch. Richard Hananja amesema ukatili unasababishwa na watu ambao hawana hofu ya Mungu.

"Watu hawataki kumcha Mungu na ndio hao wanasababisha ukatili katika Jamii , mgeukieni Mungu muache ubaya, Mke na mume wanaishi kama maadui ambapo siyo sahihi" amesema Hananja.








Share To:

Post A Comment: