Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira imewataka wadau wote wa Sekta ya Maji kushirikiana ili kuhakikisha vyanzo vya maji vinalindwa, vinatunzwa na kuendelezwa. 

Wito huo umetolewa na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Felix Kavejuru (Mb) wakati wa ziara ya kikazi ya  kukagua bwawa la Mindu linalotarajiwa kuboreshwa ili kuwa na uwezo wa kuhifadhi maji zaidi na kuwezesha upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama yenye kutoshekeza kwa wakazi wa Manispaa ya  Morogoro.

Amesema uhai wa binadamu kwa kiasi kikubwa unategemea maji na ili maji yapatikane kwa uhakika lazima sekta zote zishirikiane. 

Amezitaja miongoni mwa   sekta hizo kuwa ni pamoja na sekta ya ardhi, misitu, mazingira, sekta ya kilimo na sekta nyingine mtambuka  ambazo kwa njia moja au nyingine zinahusika moja kwa moja nab huduma ya maji.

Kwa upande wa jamii inayozunguka vyanzo vya maji amesisitiza utoaji wa elimu itakayowezesha wananchi kutambua umuhimu wa vyanzo vya maji na hivyo kushiriki katika kuvilinda na kuviendeleza kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Naibu Waziri wa Maji Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb) amesema Wizara ya Maji imejipanga kuhakikisha vyanzo vyote vya maji nchini vinalindwa ili kuwezesha upatikaji wa huduma ya maji kwa kila Mtanzania.

 Amekiri kuwepo na changamoto ya uvamizi wa vyanzo vya maji sehemu mbalimbali ikiwemo vyanzo vya bwawa la Mindu hali ambayo imepekekea kina cha maji kupungua na hivyo kutishia uendelevu wa Bwawa hilo, na kusisitiza jamii inashirikishwa ili maji yaendelee kuwepo kwa kuepuka uharibifu. Amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu fedha itolewe kwa ajili ya ukarabati wa bwawa hilo.

Awali akitoa taarifa ya ukarabati wa Bwawa hilo Mkurugenzi wa  Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA) Mhandisi Tamimu Katakweba amesema serikali inatarajia kutumia kiasi cha Bilioni 225 za kuboresha huduma ya Majisafi na usafi WA mazingira katika mji morogoro ikiwamo   ukarabati wa tuta la bwawa hilo ambalo ni chanzo pekee cha uhakika kwa huduma ya maji kwa wakazi wa Manispaa ya Morogoro.





Share To:

Post A Comment: