*Ni katika mikakati yake ya kukuza na kuendeleza sekta ya kilimo*
 
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) limeahidi kuunga mkono jitihada za Serikali ya Tanzania katika kukuza na kuendeleza sekta ya kilimo.
 
Amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zina mipango ya kuifanya Tanzania kuwa mzalishaji mkubwa wa chakula ndani ya nchi na ziada kuuza nje ifikapo 2030.
 
Waziri Mkuu ameyasema hayo jana jioni (Jumatatu, Oktoba 16, 2023) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Jukwaa la Kimataifa la Chakula Duniani ulioanza Oktoba 16 hadi  Oktoba 20, 2023. Waziri Mkuu amehutubia mkutano huo kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.
 
Kabla ya ufunguzi wa mkutano huo uliowahusisha Wakuu wa nchi na Serikali, Waziri Mkuu alishiriki katika Maadhimisho ya miaka 78 tangu kuanzishwa kwa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO). 
 
"Pamoja na jitihada ambazo tumeziweka ndani za kushirikisha vijana na wanawake kuhakikisha kwamba tunaongeza teknolojia, kutumia mbolea kwenye kilimo, pamoja na ushirikishaji wa sekta binafsi, tumeamua kuungana na FAO kupitia Mkurugenzi Mkuu  na wameahidi kutuunga mkono kwenye Sekta ya kilimo."
 
Amesema Serikali imeendelea kuimarisha miundombinu mbalimbali ikiwemo ujenzi wa reli ya kisasa, barabara na nishati vijijini ili kurahisisha shughuli za kilimo. “Maboresho mengine ni ujenzi wa viwanda vya kuzalisha pembejeo za kilimo na kuhamasisha wakulima kutumia teknolojia za kisasa katika uzalishaji.”
 
Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa FAO, Dkt. Qu Dongyu amesema Tanzania ina fursa kubwa ya kuendeleza sekta ya kilimo na uchumi wa buluu, hivyo  Shirika lao liko tayari kushirikiana na Tanzania katika kutoa msaada wa kitaalam pamoja na kukuza mifumo ya uzalishaji wa chakula.



 

Share To:

ASHRACK

Post A Comment: