Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) wakiongozwa na Mwenyekiti Dkt. Anthony Diallo (wa 6 kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Bi. Mwamvua Mrindoko (kulia kwa Mwenyekiti) mara baada ya kumaliza kikao kilichofanyika ofisini kwa mkuu wa Mkoa wa Katavi.

 Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) wakiongozwa na Mwenyekiti wa bodi hiyo, Dkt. Anthony Diallo wameanza ziara ya kikazi mkoani Katavi.


Akieleza kwa nyakati tofauti lengo la ziara hiyo iliyoanza tarehe 14 Oktoba, 2023, Dkt. Diallo amesema, imelenga katika kujifunza namna tasnia ya mbolea inavyosimamiwa, kusikiliza na kutafutia ufumbuzi changamoto mbalimbali wanazokutana nazo wadau wa tasnia ya mbolea nchini.

"Bodi hii ni mpya hivyo tumeona kuliko kutegemea taarifa zinazotolewa na menejimenti ni vyema tukawatembelea na kuwasikiliza wadau wetu ili tunapojadili mada tuwe na uelewa wa yale yanayotendeka katika maeneo mbalimbali nchini" Dkt. Diallo alisema.

Akizungumza wakati wa kikao baina ya wajumbe wa bodi hiyo na Uongozi wa Mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwamvua Hoza Mrindoko ameiomba mamlaka kufikisha elimu ya matumizi sahihi ya mbolea kutokana na imani ya wananchi wa mkoa huo kuwa ardhi yao inarutuba.

Aidha, ameishukuru Bodi hiyo kwa kuona umuhimu wa kuwatembelea na kupokea maoni na changamoto wanazokutana nazo wakati wakitekeleza majukumu yao kwa wananchi.

Kwa upande wake Afisa Kilimo wa Mkoa wa Katavi, Faridu Mtiru akiwasilisha taarifa ya Mkoa, amesema changamoto wanayokutana nayo ni uchache wa Mawakala wa mbolea na kueleza waliosajiliwa ni mawakala 25 lakini wanaofanya kazi ni 10 pekee na kuiomba Mamlaka kuongeza idadi ya mawakala ili kuwafikia wakulima karibu na maeneo yao.

Akieleza juhudi za Mamlaka katika kutatua changamoto ya uchache wa mawakala, Meneja wa TFRA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Michael Sanga amesema changamoto hiyo imetafutiwa ufumbuzi kwa kushirikisha vyama vya ushirika na tayari mafunzo yamekwisha tolewa utekelezaji utaanza punje.

Ziara hiyo imelenga kutembelea mikoa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkoa wa Katavi.


Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania Patric Mwalunenge (kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina ya wajumbe wa bodi hiyo, Menejimenti ya TFRA, Wakuu wa Wilaya zilizo ndani ya mkoa huo na watendaji wake kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwamvua H. Mrindoko (hayupo pichani) tarehe 14 Oktoba, 2023. Katikati ni mjumbe wa bodi Dkt. Catherine Senkoro

Share To:

Post A Comment: