MBUNGE wa Jimbo la Chamwino, Dodoma na Naibu Waziri Tamisemi, Deo Ndejembi amesema Serikali imetenga kiasi cha Sh Bilioni 1.1 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kuunganisha Kata ya Ikoa na Kata ya Manchali ambapo kinachosubiriwa ni kupatikana kwa mkandarasi ambaye atatekeleza ujenzi huo.

Ndejembi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza kwenye mikutano ya hadhara na wananchi wa Kata hizo mbili katika muendelezo wa ziara yake ya kuzungumza na wananchi wa Jimbo hilo ambapo amefanya mikutano katika kata tatu za Msamalo, Ikoa na Manchali.

" Wananchi wa Kata ya Manchali tuna kila sababu ya kumshukuru sana Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia Sh Bilioni 1.1 kwa ajili ya kuifungua barabara hii ya Ikoa-Manchali. Mkandarasi tayari kashapatikana na muda siyo mrefu ataanza kazi. Kufunguliwa kwa barabara hii ambayo imekua kilio chetu cha muda mrefu kutawezesha kunyanyua shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa kata hizi mbili.

Siyo kwenye miundombinu tu, pia tumepokea Sh Milioni 544 za ujenzi wa shule ya pili ya Sekondari kwenye kata yetu na kama hiyo haitoshi, Rais Dkt Samia ametupatia tena Sh Bilioni 3 kwa ajili ya ujenzi wa Shule kubwa ya Wasichana kuanzia kidato cha kwanza hadi cha Sita ya Mkoa wetu wa Dodoma ambayo itajengwa hapa Manchali. Haya ni maendeleo makubwa sana kwenye kata yetu hii," Amesema Ndejembi.

Akiwa katika kijiji cha Mnase kata ya Msamalo, Ndejembi amemuagiza Meneja wa Ruwasa Wilaya ya Chamwino kuhakikisha ndani ya saa 24 anatengeneza mashine ya kuvuta maji kwenye kisima ili wananchi wa kijiji hicho waendelee kunywa maji safi na salama.

" Huu mradi hapa unasaidia wananchi wa kijiji cha Mnase na ulijengwa kwa gharama kubwa Sh Milioni 38, haiwezekani mashine tu iharibike iwe chanzo cha wananchi wetu kukaa bila maji, Meneja wa Ruwasa nakupa saa 24 uwe umefika hapa na timu yako muweze kutatua changamoto hii wananchi wetu wanywe maji, Amesema Ndejembi.

Aidha akiwa katika kijiji cha Makoja kata ya Ikoa, Ndejembi amewatoa hofu wananchi wa kijiji hicho kuhusu changamoto ya maji ambapo amewaeleza tayari zishapatikana Sh Milioni 30 za ujenzi wa kisima ambacho kitakua ni muarobaini wa changamoto hiyo ikiwa ni lengo la Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kumtua Mama Ndoo kichwani.

Share To:

Post A Comment: