Na Joel Maduka,Msalala Shinyanga. 

Naibu waziri wa Nishati  Mhe,Stephen Byabato  amewasha umeme kwenye  Kijiji cha Butondolo Kata ya Jana,pamoja na kwenye vijiji vya Mhama ,Igombe vilivyopo Kata ya Ngaya  Halmashauri ya Msalala Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga.

Naibu waziri  wa Nishati Mhe,Byabato ameongozana na Mbunge wa Jimbo la Msalala Iddi Kassim Iddi ,ambapo akiwa kwenye Kata ya Jana kijiji cha Butondo ametumia nafasi kuwaeleza wananchi kiasi cha Shilingi Bilioni 18 ambazo zimetolewa na Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassani kwaajili ya Kusambaza Umeme kwenye vijiji 69 vilivyopo Jimbo la Msalala.

Naibu Waziri wa Nishati Byabato amesema pamoja na kuwasha umeme  kwenye Kijiji cha Butondo  lakini ni vyema wakatambua kuwa ifikapo Mwezi Desemba Mwaka huu watahakikisha vijiji vyote ambavyo havijafikiwa na huduma ya umeme vinafikiwa kwa haraka zaidi  na kwamba wao kama wananchi ni vyema wakaendelea kuwa wavumilivu kwani ni ya Serikali ni kuona wananchi Wote wanafikiwa na Nishati ya umeme.

“Natambua kuna tatizo la Mkandarasi ambaye kwa kiasi kikubwa ameonekana kusuasua kwenye utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme,Sasa nasema hivi mradi wa Msalala kama ulivyokuwa mradi wa Kahama nataka uishe kwa makubaliano  tuliyoelewana tukiwa kwenye kikao cha Mkuu wa WIlaya ya Kahama na kama basi Mkandarasi hataendelea na mwenendo huu hatutamvumilia na hatua zitachukuliwa zidi yake”Stephen Byabato Naibu Waziri wa Nishati.

Hata hivyo kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Msalala Iddi Kassim Iddi  amemshukuru Mhe,Rais Samia Suluhu Hassan kwa kusaidia  kuwafikishia wananchi wa maeneo hayo umeme kutokana na muda mrefu walikuwa na changamoto kubwa ya kukosa umeme ,huku akimuomba Naibu Waziri wa Nishati kuwasaidia kuwaongezea nguzo nyingine kwenye vijiji hivyo kutokana na awamu ya kwanza kila kijiji kilipatiwa nguzo ishirini ambazo zimeshindwa kuenea kwa wananchi.

“Mhe Naibu waziri wa Nishati pamoja na kusema tunashukuru kwa kupatiwa umeme kwenye vijiji vyetu ambavyo leo umewasha umeme lakini tunaomba walau utuongeze nguzo ambazo naamini zitasaidia wananchi ambao awajafikiwa na umeme waweze kufikiwa sasa najua hili lipo ndani ya uwezo wako na unaweza kutusaidia”Iddi Kassim Iddi,Mbunge Jimbo la Msalala.

Kufuatia Maombi hayo Naibu waziri,Mhe Stephen Byabato ameongeza nguzo 40 kwa kila kijiji kwa maana ya kijiji cha Butondolo,Mhama na Igombe ambapo ni sawa na kila kijiji kimeongezewa urefu wa Kilomita 2.

Share To:

Post A Comment: