MBUNGE wa Jimbo la Mlimba Godwin Kunambi amekagua ujenzi wa miradi miwili ya Barabara kiwango cha lami ya Mlimba/Matangini katika Kata ya Mlimba yenye urefu wa km 1 utakaogharimu zaidi ya Sh Milioni 700 pamoja na km 1 nyingine ya Barabara ya Itongoa iliyopo Kata ya Mngeta itakayogharimu Sh Milioni 500.


Akizungumza mara baada ya ukaguzi wa barabara hizo, Kunambi amemshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa ela katika Jimbo la Mlimba kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimaendeleo kwa wananchi wa Jimbo hilo.

" Kwa kweli wananchi wa Mlimba tuna kila sababu ya kumshukuru sana Rais wetu Dkt Samia. Hapa Kata ya Mlimba mtandao wa lami utazidi kuenea, tumepata Milioni 700 ambazo sasa zinatekeleza ujenzi wa km 1 ya Barabara ya Mlimba/Matangini kiwango cha lami na pia itakua na Taa za barabarani 35 zinazotumia umeme wa Jua.

Huu ni muendelezo wa kuweka lami kwenye Kata ya Mlimba ambapo hapo awali tayari tulishaweka km 1.2 zingine pamoja na taa zake. Uwepo wa barabara hizi na taa pia utaongeza chachu za maendeleo na kukuza uchumi wetu ndani ya kata yetu hii," Amesema Kunambi.

Mbunge Kunambi pia alizungumzia Barabara ya Itongoa iliyopo katika Kata ya Mngeta ambayo nayo inagharimu kiasi cha Sh Milioni 500 na inajengwa kuelekea ilipo Hospitali ya Wilaya pamoja na Ofisi za Halmashauri.

" Kama hiyo haitoshi Rais Dkt Samia pia alitupatia Sh Milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii ya Itongoa kwenda Hospitali ya Wilaya ambayo pia ni ya kiwango cha lami. Uwepo wa barabara hii utasaidia ndugu zetu wanaofuata huduma za kiafya katika Hospitali yetu ya Wilaya pamoja na wanaokwenda katika ofisi za Halmashauri yetu kufuata pia huduma. Kazi kubwa inaendelea ya kuzidi kupanua maendeleo katika Jimbo letu," Amesema Kunambi.

Amewataka wakandarasi wanaotekeleza miradi hiyo miwili kujitahidi kukamilisha kwa wakati uliopangwa ili kuweza kutimiza azma ya Serikali ya kupeleka huduma kwa wananchi wa maeneo hayo.



Share To:

Post A Comment: