Mkuu wa  Wilaya ya Temeke,  Mobhare Matinyi ] kushoto ], akimkabidhi bendera ya Taifa, Abiudi Maugo kwa niaba ya  vijana wenzake wanaokwenda kutembea kwa  miguu mikoa 16 nchini kwa lengo ya kutangaza kazi zinazofanywa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika hafla iliyofanyika leo ofisini kwake. Vijana hao pia katika matembezi hayo ya kizalendo watafanyakazi ya kuwahamasisha vijana kufanyakazi kwa bidii ikiwa ni kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali kwa ajili ya kuliletea Taifa maendeleo.

 ...............................................

Na Mwandishi Wetu

MKUU wa Wilaya ya Temeke,  Mobhare Matinyi, amewaagiza vijana saba wazalendo waliondoka Dar es Salaam leo asubuhi kuanza matembezi ya mikoa 16 kuzitangaza kazi zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akiwakabidhi bendera ofisini kwake, DC Matinyi alizitaja baadhi ya kazi zilizofanywa wilayani Temeke mwaka 2022/23 na thamani ya fedha zilizotolewa na Rais Samia kuwa ni pamoja na miradi ya afya sh. bilioni6.1, elimu ya msingi sh. bilioni 7.6, elimu ya sekondari sh. bilioni 10, maji sh. bilioni 15.5, umeme sh. bilioni 61.6 na barabara sh. bilioni 43.7.

Alisema kwa ujumla wilaya ya Temeke ilipatiwa na Rais Samia zaidi sh. bilioni 152 katika kipindi hicho kutokana na wingi wa wakaazi wake ambao wanafikia milioni 1.35 na nia yake ya kuleta maendeleo kwa Watanzania. Aliwaambia vijana hao kuwa katika kilomita 3,624 wanazotarajia kutembea kwa miguu watakutana na ushahidi lukuki wa kazi za Rais Samia.

Vijana hao saba wanaoongozwa na Abiudi Maugo wanatarajiwa kuhitimisha matembezi yao mkoani Manyara wakati wa sherehe za kuuzima mwenge hapo Oktoba 14, 2023.

Vijana wengine ni Sophia Kooni, Beatrice Masanja, Shabani Juma, Jesca Giribert, Flora Erenest na Paul Mkinga. Hii ni mara ya nane kwa vijana wa Temeke kufanya matembezi nchini kuunga mkono matukio au dhima tofauti.

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: