Na Karama Kenyunko Michuzi TV

MAHAKAMA YA Hakimu Mkazi Kisutu imeshindwa kumuunganisha Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe na wenzake watatu wanaokabiliwa kwa tuhuma za kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka ya ugaidi kutokana na mawasiliano mabaya kwenye Ukumbi wa mahakama ya mtandao ( Video Conference) kati ya Kisutu na Gerezani Ukonga walipo Washtakiwa.

Mapema leo Agosti 5, mwaka 2021, kesi hiyo ambayo imepangwa kusikilizwa kwa ajili ya mtandao ilikuja kwa ajili ya kutajwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba na  kumuunganisha Mbowe na wenzake baada ya yeye kusomewa mashtaka peke yake, lakini ilishindikana baada ya Mbowe na wenzake kushindwa kupata mawasiliano mazuri kutoka mahakamani.

Katika kesi hiyo, upande wa mashtaka unawakilishwa na Wakili wa Serikali Pius Hilla, Christopher Msigwa na Grace Mwanga huku upande wa utetezi ukiwakilishwa na Wakili wa utetezi Peter Kibatala, Jonathan Mndeme, John Malya na Frederick Kihwelo.

Wakati Mahakama inaendelea, washtakiwa Mbowe na wenzake walikuwa wakionekana kwenye video ya ukumbini hapo lakini wao walikuwa hawaoni kitu ndipo Mbowe akalalamika kuwa,  kuwa haoni picha ya mahakamani."Mheshimiwa hatuwaoni, tunawasikia sauti tu lakini hatuwaoni," amedai Mbowe

Wakati marekebisho yakiendelea kufanyika wakili Simba alishauri kuahirishwa kwa kesi iwapo mawasiliano yatashindikana kutengemaa ushauri ambao ulikubaliwa na pande zote mbili.

Baada ya dakika kadhaa za juhudi za wataalamu wa teknolojia ya mawasiliano kushindikana, washtakiwa waliulizwa kama wako tayari kuendelea kusomewa mashtaka katika hali hiyo lakini Mbowe alikataa na hivyo pande hizo mbili zikakubaliana kurudi mahakamani kesho, kwa makubaliano ya washtakiwa wawepo mahakamani.

Nje ya mahakama kabla ya kuanza kwa kesi, hali ya ulinzi iliimarishwa na kuonekana kuwa shwari bila vurugu zozote ambapo wafuasi wa Chadema walionekana katika maeneo ya nje ya mahakama wakitaka kuingia mahakamani hapo lakini wafuasi wachache asilimia kubwa wakiwa ni viongozi ndiyo walipata nafasi ya kuingia ndani ya ukumbi wa mahakama mtandao.

Hata hivyo baada ya kutoka nje ya ukumbi huo baadhi ya wafuasi waliopata fursa ya kuingia ndani walianza kuimba kuelekea getini wimbo uliosikika kwa maneno 'Mbowe siyo gaidi' lakini askari walifanikiwa kuwanyamazisha huku wale walio nje wakijaribu kuonesha mabango na kuimba wimbo huo hali iliyolazimisha askari wa  Jeshi la Polisi kuingilia kati na kuwakamata baadhi ya wafuasi hao.

Mbali na Mbowe washtakiwa wengine ni  Halfan Hassan, Adam Kasekwa na Mohamed Lingwenya.Katika shtaka la kwanza la kuongoza genge la uhalifu, washtakiwa wote wanadaiwa kati ya Mei Mosi na Agosti Mosi 2020 katika hoteli ya Aishi iliyopo Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro na katika maeneo mengine ya Dar es Salaam,  Morogoro na Arusha kwa pamoja.

Na wengine ambao hawakuwepo mahakamani kwa makusudi walitengeneza mikakati ya kigaidi ambayo ni kufanya milipuko katika vituo vya mafuta na mikutano ya hadhara kwa lengo la kuharibu misingi ya kisiasa, katiba, uchumi na sifa ya jamuhuri ya muungano wa Tanzania

Shtaka la pili la kufadhili vitendo vya ugaidi imedaiwa, katika siku na mahali hapo Mbowe Mbowe aliwasaidia washtakiwa hao kutekeleza mpango wa kigaidi.

Pia washtakiwa,  Hassan, Kasekwa na Lingwenya wanadaiwa katika tarehe na maeneo hayo washtakiwa hao watatu walipokea msaada kutoka kwa Mbowe kwa ajili ya kutekeleza vitendo vya ugaidi ambavyo ni kulipua vituo vya mafuta na mikutano ya hadhara.

Aidha mshtakiwa Kasekwa anadaiwa Agosti 5, 2020 katika eneo la Rau Madukani alikutwa na silaha aina ya pistol yenye namba A 5340 aina ya Luger na risasi tatu bila ya kuwa na kibali.

Katika shtaka la tano mshtakiwa Hassan anadaiwa Agosti 10, 2020 katika Manispaa ya Temeke jijini Dar es Salaam,  kwa lengo la kuhatarisha usalama wa nchi alitumia sare za jeshi la wananchi JWTZ na Jeshi la kujenga Taifa  JKT.

Sare hizo zilkuwa ni suruali moja ya JKT, suruali nne, fulana moja, Koti la mvua moja, jacket moja, kofia tano, overall tano, begi la kubebea vifaa vya lijulikanalo kwa jina la ponjoo,  vyeo vinne vya koplo, mikanda minne, soksi pea moja, sweta, beji ya mafunzo ya parachuti, kibuyu cha kunywea maji vyote vikiwa ni mali ya JWTZ pamoja na kisu aina ya AK 47 CCCP.











 

 

Share To:

Post A Comment: