Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu soka Tanzania Bara Yanga SC, leo wanashuka dimbani kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam dhidi ya Njombe Mji huku ikiwa inamtegemea mshambuliaji Obrey Chirwa.
Chirwa ambaye aliisaidia Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Lipuli FC wikiendi iliyopita kwa kuhusika kutengeneza mabao yote, leo tena ataendelea kuwa tegemeo kutokana na idadi kubwa ya mejeruhi ndani ya kikosi hicho.
Baadhi ya nyota wa Yanga watakaoukosa mchezo wa leo Youthe Rostand, Juma Abdul, Haji Mwinyi, Andrew Vicent na Ibrahim Ajib. Majeruhi wa muda mrefu ni Thaban Kamusoko, Hamis Tambwe na Donald Ngoma.
Kwasasa Chirwa ndiye anaongoza kwa mabao ndani ya klabu hiyo akiwa na mabao saba na amesaidia mengine manne hivyo umuhimu wake kwenye mchezo wa leo ni mkubwa.
Yanga inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 31 baada ya michezo 16 huku Njombe Mji ikiwa ya mwisho kwenye msimamo ikiwa na alama 13 kwenye mechi 16.
Share To:

Post A Comment: