Mgombea wa Chadema katika uchaguzi mdogo kata ya Isamilo jijini Mwanza, John Kiseri leo amesota kutwa nzima kupata fomu ya kuomba uteuzi kutoka ofisi ya mtendaji wa kata hiyo, Dickson Mapunda kutokuwa ofisini tangu saa 4:30 asubuhi hadi aliprejea saa 11:15 jioni.
Katibu wa Chadema Wilaya ya Nyamagana, Andrew Kaniki aliyekuwa miongoni mwa viongozi na wanachama waliomsindikiza mgombea huyo aliiambia Mwananchi kwa njia ya simu kuwa walifanikiwa kupata famu hiyo saa 11:30 jioni kwa maelekezo ya mkurugenzi wa jiji, Kiomoni Kibamba.
“Tangu saa 4:30 asubuhi tulipomkosa mtendaji ofisini tulikuwa tukiwasiliana naye kwa njia ya simu akituahidi kuja kutoa fomu bila mafanikio na ilipofika mchana, simu yake ya mkononi ikawa imezimwa; tuliwasiliana na uongozi wa kitaifa ambao nao uliwasiliana na NEC, kuhusu suala hilo,” amesema Kaniki na kuongeza
“Ilipofika saa 11:15 jioni mtendaji alifika ofisini lakini akagoma kutoa fomu akidai tayari kuna mtu aliyemtaja kwa jina la Isac Joseph Mwenda alishachukua fomu akijitambulisha kuwa ndiye mgombea aliyeteuliwa na Chadema,”
Amesema walimtaka mtendaji huyo kuonyeshe alipomsainisha mtu huyo lakini alishindwa akidai hakumsainisha kwa sababu alimwamini kutokana na kuwa na barua zilizoonyesha kutolewa na kusainiwa na viongozi wa Chadema wa kata ya isamilo.
“Baada ya malumbano ya muda mrefu na mawasiliano na mamlaka za juu, mgombea wetu (wa Chadema) alipata fomu baada ya mkurugenzi wa jiji kuelekeza tuandike barua ya kumkana mtu aliyepewa fomu ya awali,” amesema Kaniki
Juhudi za kuwapata Kibamba na Mapunda kuzungumzia suala hilo hazikufanikiwa baada ya simu zao za kiganjani kuita muda mrefu bila kupokelewa na baadaye kufungwa.
Mgombea Chadema alichukua fomu dakika za mwisho kabla ya zoezi gilo kufungwa leo kutokana na msimamo wa awali chama hicho na vingine vya upinzani kutangaza kususia chaguzi ndogo kushinikiza kikao cha majadiliano kati ya wadau wa siasa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuhusu kasoro zilizojitokeza katika chaguzi ndogo za kata 43 Novemba 26 mwaka jana.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: