DAR ES SALAAM: Nyumba mbili za aliyekuwa mmiliki wa Kampuni ya Lugumi Enterprises, Said Lugumi, zilizopo maeneo ya Mbweni- JKT zimepigwa mnada leo, Alhamisi, Novemba 9, 2017.

Katika mnada huo ulioanza majira ya saa 5 za asubuhi na kudumu kwa dakika tano kwa kila nyumba, Dk Louis Shika ndiye aliyenunua nyumba hizo zenye kila kitu ndani huku zikiwa umbali wa takribani mita100 kutoka moja hadi nyingine.

Hata hivyo baada ya mnada huo, Dk Louis aliyeuziwa kwa shilingi milioni 900 na nyingine bilioni 1.1, alidakwa na polisi kwa madai ya kuharibu mnada baada ya kushindwa kutoa asilimia 25 ya fedha inayohitajika.

Mnada huo umeendeshwa na kampuni ya udalali ya Yono, baada ya mnada wa mara ya kwanza uliofanyika Septemba 7, 2017 kukwama kutokana na wateja waliojitokeza kutofikia bei iliyohitajika.

Akizungumza na Gazeti la Ijumaa, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Yono, Scholastica Kevela alisema lengo la mnada ni kufidia Sh14 bilioni ambazo mfanyabiashara Lugumi anadaiwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Nyumba hizo mbili ni kati ya tatu ambazo zitapigwa mnada. Nyingine ikiwemo nyumba iliyopo Upanga,  jijini hapa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: