Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezitaka Taasisi zilizochini ya Wizara yake kuwajibika katika nafasi zao za uongozi na siyo kusubiria mpaka kiongozi wa juu aibue changamoto zinazojitokeza katika maeneo ya kazi


Waziri Ndalichako amesema kupitia kikao kazi hicho watendaji wataweza kujifunza na kubaini mapema viashiria ambavyo vitaonekana kukwamisha utekelezaji wa mipango ya wizara.


Amesema lengo  la kikao hicho  ni kuzuia madhara badala ya kusubiri madhara yatokee, hivyo kupitia kikao kazi hicho watendaji watajifunza kwa lengo la kufikia na kutekeleza malengo ya Wizara yaliyokusudiwa


Waziri Ndalichako pia amezitaka Taasisi na Watendaji wa Wizara hiyo kuanzia leo kuacha mara moja kulipana stahili ambazo hazifuati miongozo na nyaraka za serikali.


Profesa Ndalichako ametaja baadhi ya stahili ambazo zimekuwa zikilipwa bila kufuata taratibu na miongozo hiyo kuwa ni pamoja na posho za kujikimu, Nyumba,  umeme na simu.


Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu ,  Sayansi na Teknolojia Dkt.  Leonard Akwilapo amesema mkutano huo umelenga kuondoa viashiria hatarishi ambavyo vimekuwa vikikwamisha ufanisi katika utendaji kazi wa wizara.


 Dkt. Akwilapo amewataka washiriki wa mkutano huo kuandaa mpango mkakati wa kuweza kutambua mapema viashiria hatarishi na kuvifanyia kazi ili kufikia malengo  ya wizara.


Kikao kazi hicho ambacho kimeanza leo kitahusisha pia  Wakurugenzi wasaidizi, waratibu wa miradi na wasaidizi wa miradi,wathibiti ubora na wakuu wa vitengo vya Wizara hiyo.


Imeandaliwa na;


Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,

WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA

Share To:

msumbanews

Post A Comment: