Watoto 22 na Mwalimu wao wa Madrasa Watiwa Mbaroni Kwa Madai ya Kujifunza UGAIDI.

 

JESHI la polisi mkoani Pwani ,limewakamata watoto 22 wa madrasa ya Arahma pamoja na mwalimu wa madrasa hiyo Ashura Said(47) ambae alikuwa akiendesha mafunzo ya kigaidi kwa watoto hao,huko Kimarang’ombe ,kata ya Nianjema ,Bagamoyo.

Aidha jeshi hilo limefanikiwa kukuta bomu moja la moshi lenye namba G2020c.SS-STCS katika makazi anayoishi mwalimu huyo .

Akizungumzia tukio hilo,kamanda wa polisi mkoani Pwani,Boniventure Mushongi,alisema Ashura anashikiliwa na polisi kwa mahojiano zaidi kuhusiana na kuhusika kuendesha mafunzo ya kigaidi kinyume na sheria.

Alieleza kuwa taarifa hiyo ilitolewa na raia wema juu ya mwenendo wa mwalimu huyo wa madrasa na baada ya kumfanyia upekuzi polisi walifanikiwa kukuta na bomu moja la moshi.

Kamanda Mushongi,alisema uchunguzi wa awali ulibaini makazi hayo yanamilikiwa na taasisi ya kiislamu iitwayo Akha Laagul Islam,iliyosajiliwa kwa lengo la utoaji huduma kwa watoto yatima kutoka maeneo mbalimbali ikiwemo Dar es saalam ,Tanga,Handeni,Mlandizi na Bagamoyo kwa mkoa wa Pwani.

“Badala yake watoto hao wamekuwa wakitumika kwa mafunzo yasiyofaa kwa watoto wa kituo hicho”alisema kamanda Mushongi.

Hata hivyo alisema jeshi la polisi limewamakata watoto 22 ambao walikuwa wakijaribu kukimbia ambao kati yao 16 ni wakike na 6 ni wa kiume kwa ajili ya uchunguzi wa tukio.

Katika tukio jingine ,Bakari Saidi (45)mkazi wa Kimanzichana Kusini ,wilayani Mkuranga, ameuwawa kwa kupigwa risasi kifuani upande wa kulia na kutokea chini ya bega la kushoto ,mgongoni na watu wasiofahamika.

Katika tukio hilo,Omar Ally (55)ambae ni afisa mtendaji wa kijiji cha Kimanzichana Kusini,alijeruhiwa kwa kupigwa risasi kwenye mkono wake wa kushoto na amelazwa katika hospitali ya wilaya hiyo kwa matibabu.

Kadhalika katika eneo la tukio kumekutwa maganda mawili ya risasi yanayotumika kwenye silaha ya SAR/SMG .

Kamanda Mushongi alisema watu hao walivamia katika ofisi ya serikali ya kijiji cha Kimanzichana Kusini na kufanya mauaji hayo ambapo  mtu huyo alifariki dunia  na mwingine mmoja kujeruhiwa.

Anasema tukio hilo limetokea octaba 5 mwaka huu katika kitongoji cha Ukwama kata ya Kimanzichana tarafa ya Mkamba wilayani hapo.

“Wakati marehemu akiwa anajaza fomu za mkopo wa benki ya  akiba  Commerce bank(ACB),ghafla walitokea watu wawili wakiwa na silaha mbili na kuanza kuwafyatulia risasi na kutoweka kusikojulika wakitumia usafiri wa pikipiki"alisema kamanda Mushongi.

Kamanda huyo alifafanua kuwa mwili wake umehifadhiwa katika hospitali ya wilaya ya Mkuranga na utakabidhiwa kwa ndugu zake kwa ajili ya mazishi mara baada ya uchunguzi kukamilika.

Jeshi hilo limewahakikishia wananachi wote usalama wao na kwamba linapambana kwa nguvu na wale wenye nia ya kuwatia hofu wananchi,kwani hawataweza kufanikiwa katika mipango yao .

Limewaasa wananchi kuwafichua wahalifu ambao ni sehemu ya jamii wanapoishi badala ya kuoneana muhali pamoja na kutoa taarifa pale wanapobaini kuna watu ama raia asiyemwema
Share To:

msumbanews

Post A Comment: