Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema ujenzi wa Daraja la Muhoro utaleta ukombozi kwa wananchi wa Kata ya Muhoro, ambao kwa muda mrefu wamekumbwa na changamoto za usafiri na hata kupoteza maisha wanapovuka Mto Rufiji.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo, Mhe. Mchengerwa amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanikisha mradi huo wa kisasa wenye thamani ya zaidi ya Sh.Bilioni 17.

“Nimeridhishwa na kasi ya ujenzi, lakini nataka mkandarasi aongeze juhudi ili daraja likamilike ifikapo Julai 2025,” amesisitiza Waziri Mchengerwa.

Kwa mujibu wa Meneja wa Wakala qa Barabara Mijini na Vijijiji (TARURA) Mkoa wa Pwani, Mhandisi Leopold Runji, ujenzi umefikia asilimia 40, tayari nguzo nne kati ya sita zimekamilika na lina urefu wa mita tisa, hivyo litasaidia kuzuia mafuriko.

Nao, Wakazi wa Muhoro, Pili Lwambo na Mikidadi Omary, wameeleza furaha yao, wakisema daraja hilo litaepusha vifo vinavyosababishwa na mamba, kusaidia kina mama kujifungua hospitalini, na kurahisisha usafiri wa watoto kwenda shule.











 


📍 Seoul, Korea Kusini

Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa amesema kuwa kutokana na kuongezeka kwa mahitaji na matumizi ya Madini Muhimu duniani, Tanzania ina dhamira ya dhati ya kuendeleza Sekta ya Madini ikiwa ni pamoja na Madini Mkakati hapa nchini kwa kuimarisha ushirikiano na Nchi ya Korea ya Kusini kwa lengo la kuleta mageuzi yenye kuleta tija zaidi kupitia sekta hiyo.

Ameyasema hayo leo Machi 25, 2025 jijini Seoul, Korea Kusini wakati akizungumza katika Mkutano wa Madini Muhimu kati ya Tanzania na Korea yaliyoandaliwa jijini humo. 

Dkt. Kiruswa amesema kuwa, kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Kimataifa la Nishati (IEA) ya mwaka 2023, matumizi ya lithiamu yameongezeka kwa asilimia 30, huku mahitaji ya nikeli, kobalti, kinyewe (graphite), na madini adimu yakiongezeka kati ya asilimia 8 hadi 15  na kwamba hali hiyo inatoa fursa kubwa kwa Tanzania kushirikiana na mataifa yenye teknolojia za kisasa kama Korea katika uchimbaji, uongezaji thamani, na biashara ya madini haya.

Aidha, Dkt. Kiruswa amesisitiza kuwa, Tanzania ni nchi yenye utajiri mkubwa wa madini yanayohitajika kwa teknolojia za kisasa, hususan nishati mbadala.

“Tanzania ina hifadhi kubwa ya madini kama vile grafiti, nikeli, kobolti, lithiamu, madini adimu (REE), shaba, manganese, zinc, dhahabu, na vito vya thamani, ambavyo vinahitajika kwa maendeleo ya viwanda vya teknolojia na nishati safi,” amesema Dkt. Kiruswa.

Sambamba na hilo , Dkt. Kiruswa amebainisha kuwa, katika jitihada za kuhakikisha sekta ya madini inawanufaisha Watanzania, Tanzania inalenga kuongeza thamani ya madini yake ndani ya nchi kabla ya kuuza nje. “Tunatambua uwezo mkubwa wa Korea katika teknolojia za uchimbaji, utafiti, na uchenjuaji wa madini. Ushirikiano wetu utaleta manufaa kwa pande zote mbili,” ameongeza Naibu Waziri.

Katika hatua nyingine, Dkt. Kiruswa amepongeza Kampuni za Kikorea kama POSCO International, inayoshiriki katika mradi wa Mahenge Graphite, na Yulho, ambayo imewekeza katika uchimbaji wa nikeli kusini mwa Tanzania na kwamba uwepo wa Kampuni hizo hapa nchini ni ushahidi kwamba Tanzania ni mahali salama na sahihi kwa uwekezaji wa madini.

Katika mkutano huo, Ujumbe wa Tanzania umesheheni wadau muhimu wa Sekta ya Madini, ikiwa ni pamoja na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Tume ya Madini, Kampuni za uchimbaji na usafirishaji wa madini, mabenki, na wataalam wa sheria ili kutoa taarifa na kujibu maswali ya wawekezaji wa Kikorea.

“Tupo hapa kuhakikisha kuwa kila mwekezaji anapata majibu sahihi na kuelewa fursa zilizopo Tanzania. Tuko tayari kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi ya Korea ili kufanikisha uwekezaji wa muda mrefu wenye tija kwa nchi zetu zote mbili,” amesisitiza Dkt. Kiruswa.

Naibu Waziri Dkt. Kiruswa amesisitiza umuhimu wa utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa katika Mkutano wa Korea-Afrika, akisema kuwa Tanzania iko tayari kuchukua hatua madhubuti ili kuhakikisha kuwa sekta ya madini inachangia kikamilifu maendeleo ya kiuchumi.

































 



Na. Josephine Majura, WF, Mwanza

Watumishi wa Umma na Sekta Binafsi wameshauriwa kujifunza kuhusu uwekezaji mapema ili kuhakikisha kuwa baada ya kustaafu wanaendelea kuishi maisha mazuri, kama walivyokuwa kazini.

Ushauri huo umetolewa na Afisa Masoko Mwandamizi, Kampuni ya Uwekezaji ya UTT – AMIS, Bw. Rahim Mwanga, wakati wa mafunzo ya elimu ya fedha yaliyotolewa kwa watumishi wa Halmashauri hiyo na Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha na Taasisi zake.

Aliongeza kuwa kustaafu hakupaswi kuwa chanzo cha matatizo ya kifedha, kwa mfanyakazi yoyote aliyekuwa analipwa mshahara bali iwe fursa ya kufurahia matunda ya kazi ya muda mrefu.

“Tukijijengea utamaduni wa kuwekeza mapema kutatusaidia sisi wafanyakazi kuepuka changamoto za kifedha baada ya kustaafu na kuwa na maisha ya uhakika”, alisema Bw. Mwanga.

Aidha aliwasisitiza wafanyakazi wote nchini kuhakikisha michango yao inalipwa kwa wakati na waajiri wao lakini pia watumie Mifuko ya Hifadhi ya Jamii inayotoa faida kubwa.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Bw. Erick Mvati, aliipongeza Wizara ya Fedha kwa kufika katika Mkoa wa Mwanza kutoa elimu ya fedha ambayo ni muhimu kwa wananchi ili waweze kujikwamua kiuchumi.

Aliongeza kuwa elimu hiyo ikifika kwa wananchi wote katika makundi mbalimbali itasaida kupunguza matatizo katika jamii kwa kuwa wananchi wataelewa haki zao lakini pia watajua sheria mbalimbali zitakazowaongoza na kujiepusha na migogoro ya mikopo.

Naye Afisa Usimamizi wa Fedha, Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Bw. Santley Kibakaya, alisema kuwa Wizara inaendelea na zoezi la utoaji elimu ya fedha kwa wananchi ili wafahamu fursa mbalimbali zinazopatikana katika Sekta ya Fedha.

Aliongeza kuwa Sekta ya Fedha imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali, kupitia elimu hiyo inayoendelea kutolewa, wataalamu hao wanapata fursa ya kusikiliza changamoto, ushauri na maoni yanayotolewa na wananchi kwa ajili ya kufanyiwa utatuzi zile ambazo zinatakiwa kufanyiwa utatuzi, ushauri na maoni kwa ajili ya kuboresha zoezi hilo kwa mikoa ambayo haijafikiwa.




Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Bw. Erick Mvati, akikabidhiwa vipeperushi na Afisa Usimamizi wa Fedha, Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bw. Santley Kibakaya, vyenye mada mbalimbali ikiwemo akiba, mikopo na uwekezaji ambazo zitafundishwa kwa wananchi wa Halmashauri hiyo.




Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Bw. Erick Mvati, akiwasikiliza Timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Fedha na Taasisi zake, ambao walifika ofisini kwake kujitambulisha ili kuanza kutoa elimu ya fedha kwa wananchi katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri hiyo.







Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Bw. Erick Mvati, akizungumza alipokutana na Timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Fedha na Taasisi zake ambao walifika ofisini kwake kujitambulisha ili kuanza kutoa elimu ya fedha kwa wananchi katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri hiyo.




Afisa Masoko Mwandamizi, Kampuni ya Uwekezaji ya UTT – AMIS, Bw. Rahim Mwanga, akiwafungulia akaunti ya uwekezaji watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza baada ya mafunzo ya elimu ya fedha yaliyotolewa na Wizara ya Fedha na Taasisi zake.




Baadhi ya watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, wakifuatilia mada mbalimbali ikiwemo akiba, mikopo, uwekezaji, bima, kujiandaa kustaafu wakati wa mafunzo ya elimu ya fedha yaliyotolewa na Wizara ya Fedha na Taasisi zake.




Afisa Usimamizi wa Fedha, Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Bi. Elizabeth Mnzava, akiteta jambo na baadhi ya watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, baada ya kumalizika kwa mafunzo ya elimu ya fedha kwa watumishi hao yaliyotolewa na Wizara ya Fedha na Taasisi zake.




Afisa Sheria Mwandamizi, Idara ya Ustawi na Huduma Jumuishi za Fedha, Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bw. Ramadhani Myonga, akitoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, yaliyotolewa na Wizara ya Fedha na Taasisi zake

 Kamati ya ushauri ya mkoa wa Njombe ( RCC ) ikiongozwa na mkuu wa mkoa huo Anthony Mtaka kimepokea na kupitisha pendekezo la kuligawa Jimbo la Ludewa na kuruhusu mchakato huo kuendelea kwa hatua zinazofuata


Awali akiwasilisha taarifa ya kuligawa Jimbo hilo mwanasheria wa halmashauri hiyo Mathani Chalamila amesema kwa asilimia kubwa wamekidhi vigezo vya kuligawa Jimbo hilo ikiwemo ukubwa na jiografia yake kuwa ngumu.

"Mheshiwa mwenyekiti moja kati ya vigezo vya kugawa majimbo ni ukubwa wa eneo wa Jimbo husika ambapo ludewa ina eneo la kilometa za mraba takribani 8,000". Alisema Chalamila.

Akichangia hoja hiyo mwenyekiti wa CCM mkoa wa Njombe ambaye pia ni mbunge wa Jimbo la Makambako Deo Sanga amesema ni kweli Jimbo la Ludewa linastahili kugawanywa kutokana na ukubwa wa eneo na jiografia yake.

" Chama Cha Mapinduzi huwa tunafanya ziara kule Ludewa, Mheshimiwa mwenyekiti nilikuwa na ombi kwenye kikao chako kuwe na ombi maalum kupitia kikao hiki, hata kama baadhi ya vigezo havikidhi lakini jiografia ya Jimbo hili ni ngumu sana". Amesema Sanga.

Kupitia kikao hicho Deo Sanga ameomba ombi la kuligawa Jimbo la Ludewa likubaliwe ili waendane na Ilani ya CCM ya kusogeza huduma kwa wananchi.

"Imani yangu Jimbo lile likigawanyika jinsi lilivyo litakuwa limesogeza huduma sana kwa wananchi, yani katika Jimbo kwenye mkoa huu lenye jiografia ngumu ya namna ya kuwahudumia na kuwafikia wananchi ni Jimbo la Ludewa". Ameongeza Sanga.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Ludewa Mheshimiwa Wise Mgina sambamba na katibu tarafa wa tarafa ya Liganga Edward Wayotile kwa pamoja wameomba Jimbo la ludewa ligawanywe kutokana na ukubwa wa Jimbo kwani unaweza kutumia muda mwingi kutoka kata moja hadi nyingine kutokana na jografia pamoja na umbali.


Hata hivyo kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Njombe Anthony Mtaka amesema mbali na kuligawa Jimbo kuna haja ya kuanza kufikiria namna ya kuongeza halmashauri katika wilaya hiyo kwani halmashauri ndiyo zinasogeza huduma kwa wananchi kwa ukaribu zaidi.

"Kwahiyo kwangu Mimi tungeiomba serikali iiangalie Ludewa kwa jicho la pili tuombe kupata halmashauri nyingine huko mbeleni". Amesema Mtaka

Ikumbukwe hatua hiyo imeefikiwa baada ya hivi karibuni Baraza maalum la madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Ludewa pamoja na kamati ya ushauri ya wilaya hiyo kwa pamoja kulidhia kugawanywa kwa Jimbo hili.