Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula (kulia) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini Dkt. Ladislaus Chang’a (kushoto) wakionyesha hati za makubaliano mara baada ya kusaini Machi 31,2025 jijini Arusha.

.....

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela ( NM-AIST) imesaini makubaliano ya ushirikiano na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika masuala ya utafiti na sayansi kwenye maeneo mbalimbali yanayohusu mabadiliko ya hali ya hewa na tabia ya nchi, ikiwemo namna mabadiliko hayo yanavyoathiri afya ya akili kwa kushirikisha Chuo Kikuu cha Hurbert Kairuki.

Hayo yamesemwa Machi 31, 2025 jijini Arusha na Makamu Mkuu wa Taasisi Prof. Maulilio Kipanyula ambaye ni Mwenyeji wa Warsha ya Jopo la Kimataifa la Sayansi na Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabia ya Nchi kwa uratibu wa Kituo cha Umahiri cha WISE-Future kwa kushirikiana na TMA.

Alieleza kuwa, NM-AIST na TMA imekubaliana kushirikiana katika maeneo makuu matatu ikiwemo utafiti katika masuala ya hali ya hewa na mabadiliko ya tabia ya nchi, kuwajengea uwezo wataalamu wa TMA kupitia mafunzo ya muda mfupi pamoja na kuendeleza Teknolojia na Ubunifu, kupitia matumizi ya teknolojia kidigitali ikiwemo Akili Mnemba ( AI).

“Sisi kama Taasisi ya kikanda tunafurahi sana kuwa sehemu ya tukio hili , ambalo limetupa fursa ya kutoa mchango wetu kwenye taarifa ya tathmini ya hali ya hewa na mabadiliko ya tabia ya nchi duniani” Prof. Maulilio Kipanyula.

Kwa upande wake  Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya hali ya Hewa Nchini (TMA) Dkt. Ladislaus Chang’a,ametoa wito kwa wananchi kuendelea kufuatilia na kuzingatia taarifa zinazotolewa na Mamlaka hiyo hususani tahadhari ya hali mbaya ya hewa.

“Mambo makubwa yaliyofanyika hapa ni kuhakikisha wataalamu kutoka Tanzania, Afrika na ukanda wa nchi zinazoendelea wanashiriki kwa wingi katika kazi za kisayansi katika masuala ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabia ya nchi” alisema Dkt. Ladislaus Chang'a Kaimu Mkurugenzi Mkuu

Dkt. Chang'a alisema kuwa, makubaliano ya ushirikiano na NM-AIST ni kuchagiza na kuongeza ufanisi na tija katika huduma za hali ya hewa kupitia matumizi ya teknolojia ya kisasa ikiwemo akili mnemba ,Sayansi, Teknolojia na ubunifu.

Warsha ya Jopo la Kimataiafa la Sayansi na mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabia ya Nchi , imeshirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wanafunzi wa shahada ya uzamili na uzamivu katika masuala ya mazingira na biolojia, Msalaba Mwekundu na NEMC.

Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula (kulia) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini,Dkt. Ladislaus Chang’a (kushoto) wakionyesha hati za makubaliano mara baada ya kusaini Machi 31,2025 jijini Arusha.

Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula (kulia) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini Dkt. Ladislaus Chang’a (kushoto) wakisaini makubaliano ya mashirikiano Machi 31,2025 jijini Arusha.

Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula (kushoto) akipokea Jarida la Tathmini ya Hali ya Hewa Nchini kwa Mwaka 2024.0 kutoka kwa Mwenyekiti wa Bodi ya TMA Prof. Jaji Mshibe Ali Bakari ( Kulia ) katika Warsha ya Jopo la Kimataifa la Sayansi na Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabia ya Nchi Machi 31,2025.

Wadau waliohudhuria Warsha ya Jopo la Kimataifa la Sayansi na Mabadiliko ya Hali ya Hewa na tabia ya nchi wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwakilishwa na Wataalam Machi 31,2025 Jijini Arusha.

Mwenyekiti wa Bodi ya TMA Prof Jaji Mshibe Ali Bakari ( katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela wakati wa Warsha ya Jopo la Kimataifa la Sayansi na Mabadiliko ya Hali ya Hewa na tabia ya nchi Machi 31,2025.

 

Pichani, Bw Wilfred Mwakalosi (kushoto), Ofisa Mkuu wa Mawasiliano na Uhusiano EWURA akipokea tuzo kutoka kwa Bw. Bakari Machumu, moja ya majaji wa tuzo za PRST kwa mwaka 2024, katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam, tarehe 29 Machi 2025,

......

Kwa mara ya pili, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeshinda tena tuzo ya Uhusiano Mwema na Vyombo vya habari nchini, kwa mwaka 2024 ikidhihirisha namna taasisi hiyo inavyothamini ushirikano na uhuru wa vyombo vya habari katika kuuhabarisha umma kuhusu shughuli za udhibiti wa huduma za nishati na maji.

Tuzo hiyo iliyotolewa jana(29.3.2024) na Chama cha Maofisa Uhusiano Tanzania (PRST), baada ya mchuano mkali uliohusisha taasisi nyingi imeipa EWURA heshima na ari ya kuendelea kudumisha uhusiano wake thabiti na vyombo vya habari pamoja na waandishi wa habari nchini.

Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw. Titus Kaguo alisema ushindi huo kwa mara ya pili mfululizo ni kielelezo cha utawala bora, uwazi, uwajibikaji, na miongozo inayotolewa na Bodi na Menejimenti ya EWURA, chini ya mwemyekiti wake Prof. Mark Mwandosya na Mkurugenzi wake Mkuu, Dkt. James Mwainyekule.

Vigezo vilivyotumika kuipatia EWURA ushindi huo ni kuwa na mpango mkakati bora wa ushirikishwaji wa vyombo vya habari, ubora wa maudhui na uthabiti wa utoaji taarifa pamoja na mtazamo walionao vyombo vya habari kuhusu Mamlaka hiyo.

Wakati huo huo, Bi. Janeth Mesomampya, ambaye ni Ofisa Uhusiano wa EWURA amepokea tuzo ya Ofisa Uhusiano bora kwa mwaka 2024, akiwa mmoja wa washindi watano katika kipengele hicho.

Rais wa PRST Bw. Assah Mwambene, alisema utoaji wa tuzo hizo ni chachu kwa wataalam walioko kwenye kada hiyo kufanya kazi zao kwa ubora zaidi ili kuimarisha huduma katika maeneo yao ya utendaji.

EWURA ilipata tuzo ya aina hiyo pia kwa mwaka 2022, iliyotolewa na PRST kutambua mchango wake katika kushirikiana vyema na vyombo vya habari nchini.

 

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Arusha Simon Maximillian Iranghe amewataka vijana Wilayani Arumeru kugombea nafasi za nyazifa mbalimbali za uongozi ili kuweza kuisemea serikali vyema kupitia miradi mbalimbali ya kimaendeleo iliyotekelezwa na inayotekelezwa katika sehemu mbalimbali za nchi hii.

Simon Iranghe ameyasema hayo katika ziara ya Kamati ya utekelezaji ya Uvccm mkoa wa Arusha iliyofanyika Wilayani humo ya kukagua uhai wa Jumuiya hiyo sambamba na kukutana na makundi mbalimbali ya vijana wakiwemo madereva wa bodaboda,vijana na shirikisho pamoja na wanufaika wa mikopo ya halmashauri ya asilimia 10.

Akizungumza na vijana hao Mwenyekiti huyo amewaonya vijana hao kuacha tabia ya kutengenezeana chuki na ajali katika kipindi hiki ambacho kunatarajiwa kufanyika uchaguzi mkuu.

Ameongeza kuwa kwasasa jamii imeingia katika changamoto kubwa ya kijinsia ya kupotea kwa vijana kutokana na mmomonyoko wa maadili na ukatili wa kijinsia unaoendelea kufanyika kwenye jamii hivyo amewataka vijana hao kutumia nafasi zao kukemea vitendo hivyo viovu.

Sambamba na hilo mwenyekiti huyo amempongeza kada ya chama cha mapinduzi Jonhson Exaud Sarakikya kwa kutoa matofali 1000 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba wa Katibu wa vijana wa Wilaya hiyo kwani kukamilika kwa nyumba ya mtumishi huyo kutasaidia kuondoa changamoto ya makazi.

Naye Mjumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi  (VCCM) Taifa na Mbaraza Mkoa wa Aruasha Tezra Furaha Semuguruka amesema kuwa lengo la ziara hiyo ni kuwahamasisha vijana kushiriki kikamilifu katika uchaguzi wa utakaofanyika oktoba 2025.

"Ila niwaombe Vijana wenzangu mgombea atakayesimamishwa na Chama chetu CCM kupeperusha bendera tuungane kwa pamoja kwenda kuhakikisha anapata ushindi wa kishindo wa CCM,hivyo vijana tusilale mpaka kieleweke" Aliongezea Tezra

Kwa upande wake Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Meru Ombeni Pallangyo amesema kama vijana wa Meru watafanya kazi za chama cha mapinduzi na siyo kubeba mikoba ya watu ili kuhakikisha Chama hicho kinasonga mbele.

Hata hivyo Pallangyo amewataka vijana wa meru kuacha tabia ya kubeba mabegi ya wagombea badala yao nao wajitokezekugombea katika nafasi za udiwani na ubunge ili kuongeza wigo mpana wa vijana kuingia katika vyombo vya maamuzi.















 Na. Peter Haule, WF, Dar es Salaam


Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East, iliyoko chini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira, kuhusu program ya kuongeza ujuzi na kuangalia maeneo mahususi ya kuongeza uwezo.

Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) linaendesha program ya kuongeza ujuzi katika baadhi ya nchi za Afrika, ikiwemo Tanzania, Rwanda, Uganda, Kenya, Eritri na Malawi.

Mkutano huo ulihudhuliwa pia na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bw. Sebastian Acevedo na Kamishna Msaidizi wa Idara ya Sera, Wizara ya Fedha, Dkt. Remidius Ruhinduka.

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akiagana na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East iliyoko chini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira, baada ya mazungumzo yao kuhusu program ya kuongeza ujuzi na kuangalia maeneo mahususi ya kuongeza uwezo, mazungumzo yaliyofanyika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akiteta jambo na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East iliyoko chini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira, baada ya mkutano wao kuhusu program ya kuongeza ujuzi na kuangalia maeneo mahususi ya kuongeza uwezo, mazungumzo yaliyofanyika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.


Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akiongoza mkutano kati yake na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East iliyochini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira (wa pili kushoto), ambapo walijadili kuhusu program ya kuongeza ujuzi na kuangalia maeneo mahususi ya kuongeza uwezo, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.

Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bw. Sebastian Acevedo, akieleza kuhusu program ya kuongeza ujuzi kwa nchi nane za Afrika ikiwemo Tanzania, wakati wa mkutano kati ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, (kulia) na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East iliyochini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira (hayupo pichani), uliofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.

Kamishna Msaidizi wa Idara ya Sera, Wizara ya Fedha, Dkt. Remidius Ruhinduka, akieleza umuhimu wa kuongeza ujuzi kwa watanzania wakati wa mkutano kati ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, (kulia) na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East iliyochini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira (hayupo pichani), uliofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, kushoto ni Mchumi kutoka Idara hiyo, Bi. Neema Mtei.

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akisikiliza maelezo ya Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bw. Sebastian Acevedo (kushoto), kuhusu program ya kuongeza ujuzi kwa nchi za Afrika ikiwemo Tanzania, wakati wa mkutano kati yake na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East iliyochini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira (kulia), uliofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Taasisi ya Afritac East iliyoko chini ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bi. Clara Mira (wa tatu kushoto), Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bw. Sebastian Acevedo (wa pili kulia), na wajumbe wengine kutoka Wizara ya Fedha na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), baada ya mkutano wao kuhusu program ya kuongeza ujuzi kwa watanzania Tanzania, uliofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Dar es Salaam)

 


OR-TAMISEMI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema hataki kusikia tena kuhusu changamoto ya upatikanaji wa dawa katika Hospitali ya Utete na kumtaka Mganga Mkuu wa Wilaya ya Rufiji,  Hamis Abdallah, kuhakikisha anashughulikia tatizo hilo ili wananchi waendelee kupata huduma bora.

Mhe. Mchengerwa ametoa maelekezo hayo kwa Mganga Mkuu wa Wilaya, wakati wa ziara yake ya kikazi ya kuhimiza uwajibikaji katika Hospitali ya Wilaya ya Rufiji, iliyopo Utete.

"Mganga Mkuu, umepata nafasi ya kuja Rufiji, hivyo unapaswa kushirikiana na wasaidizi wako kutatua changamoto ya kutopatikana kwa dawa katika eneo hili, ambalo mimi ni Waziri wa TAMISEMI," Mhe. Mchengerwa amesisitiza.

Waziri Mchengerwa ameeleza kuwa, Rufiji haijawahi kukutana na changamoto hiyo ya ukosefu wa dawa na kutolea mfano kipindi alichokuwepo Dkt. Makenge, ambaye aliwahi kuwa Mganga Mkuu wa Wilaya ya Rufiji.

"Mganga Mkuu, suala hili halifurahishi. Sitaki wananchi walalamike tena kuhusu kukosa dawa. Jipange kuhakikisha kuwa dawa hazipungui, na nitafanya uchunguzi ili kubaini tatizo ni nini, kwani Serikali haina tatizo la fedha za madawa," ameongeza Mhe. Mchengerwa.

Aidha, Mhe. Mchengerwa amewapongeza Waganga Wakuu na watumishi wa kada ya afya kwa juhudi zao katika kupunguza vifo vya mama na mtoto na  kudhibiti vitendo vya rushwa, hususan dhidi ya akina mama wanaofuata huduma ya afya ya uzazi katika hospitali na vituo vya afya nchini.

Naye, Mmoja wa wananchi wa Wilaya ya Rufiji, Mwema Said, ametoa shukrani kwa Waziri Mchengerwa kwa kuboresha miundombinu katika Hospitali hiyo ambayo kwasasa  wananchi kufurahiya wodi zilizojengwa, vifaa tiba vilivyonunuliwa, pamoja na huduma bora zinazotolewa.














Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamadi Yussuf Masauni amesema wakati Tanzania ikiendelea kutatua changamoto za upatikanaji wa Nishati Safi ya Kupikia, Serikali inaongeza juhudi za ushirikiano wa kimataifa na kikanda ili kuondokana na vikwazo katika maeneo mbalimbali kama vile Mipango ya Kujenga Uwezo na Uhamasishaji, Utafiti, Ubunifu, na Maendeleo ya Teknolojia, Msaada wa Kifedha na Kiufundi, Ufuatiliaji, Tathmini, na Tathmini ya Athari.


Ameyasema hayo Machi 28, 2025 jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na balozi wa Finland nchini Tanzania Mhe. Balozi Theresa Zitting, Balozi wa Korea nchini Tanzania Mhe. Balozi Bi. Ahn Eunju pamoja na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania Mhe. Balozi Marianne Young. Mhe. Masauni amekutana na viongozi hao jijini Dar es Salaam Machi 28, 2025 ambapo amesema Ofisi ya Makamu wa Rais (OMR) inakaribisha ushirikiano na wadau katika maeneo muhimu kama vile Mipango ya Mabadiliko ya Tabianchi na Kusaidia Utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa Nishati Safi ya Kupika (2024–2034).


“Ofisi ya Makamu wa Rais inahusika na masuala mawili, moja ni Uratibu wa Mambo ya Muungano, kwani utakumbuka kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Muungano wa nchi mbili (Tanganyika na Zanzibar). Ofisi hii pia ina jukumu la uangalizi wa kuratibu utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Mazingira na sheria, mikakati na vyombo vingine vya sera husika.Chini ya Ofisi hii, tuna taasisi mbili, Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) lenye jukumu la kuhakikisha uzingatiaji na utekelezwaji wa sheria na Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC) ambacho kina jukumu la kupima, kuhakiki na kutoa taarifa kuhusu utoaji wa gesi chafuzi katika viwango,” amesema Waziri Masauni.


Ameongeza Serikali ya Finland imekuwa ikisaidia uhifadhi kupitia Wizara ya Maliasili naUtalii, programu za misitu ya Mashamba; Programu za Kijiji cha Upandaji miti na kusaidia tasnia ya usindikaji wa kuni; Kujenga uwezo wa Kituo cha Kitaifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni.


Mhe Masauni amesema Mkakati wa Kitaifa wa Nishati Safi ya Kupika (2024–2034) unaangazia upatikanaji wa suluhu za Nishati safi kwani bado kuna changamoto, ambapo zaidi ya asilimia 82 ya nishati ya msingi hutoka kwa mimea. Hivi sasa, karibu asilimia 90 ya kaya zinategemea kuni na mkaa kama nishati kuu ya kupikia, huku kuni zikichukua asilimia 63.5 na mkaa kwa asilimia 26.2 ya matumizi.


Pamoja na hayo wamezungumzia kuhusu Muhtasari wa Usimamizi wa Taka, ambapo amesema Tanzania inazalisha takriban tani milioni 14.4 hadi 20.7 za taka ngumu za manispaa kila mwaka, sawa na kilo 0.66 hadi 0.95 kwa kila mtu kwa siku au kilo 241 hadi 347 kwa mwaka.

Inakadiriwa kuwa 70% ya taka hizi zina vifaa vinavyoweza kutumika tena, lakini ni 5-10% tu ndio huchakatwa na sekta isiyo rasmi. Makadirio yanaonyesha kuwa kufikia 2030, karibu hekta 200 za ardhi zitahitajika kila mwaka ili kudhibiti tani milioni 26 za taka zinazozalishwa kila mwaka.


Kwa upande wake, Balozi wa Korea nchini Tanzania Mhe. Balozi Bi. Ahn Eunju amepongeza kwa juhudi zinazofanywa na serikali ya Tanzania katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira.


Naye balozi wa Finland nchini Tanzania Mhe. Balozi Theresa Zitting kwa upande wake alizungumzia suala la Biashara ya Kaboni akieleza jitihada zinapaswa kuwekezwa zaidi eneo hilo, ambayo hapa nchini inaratibiwa na kituo cha NCMC kilichopo mkoani Morogoro.


“Eneo lingine ni kuhusu Uchumi wa Buluu hili pia ni sehemu nzuri ambalo nimeona kuna nguvu inafanywa na serikali kama ilivyo katika udhibiti wa taka na katika Nishati Safi hivyo nipende kuwapongeza,”


Pia Mhe. Masauni amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Shirika la Kimataifa lisilo la kiserikali la Good Neighbors ambapo walizungumzia kuhusu namna ya uboreshwaji wa Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira.