Na Oscar Assenga,Muheza, Tanga

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka amesema serikali itaendelea kuvipa kipaumbele vikundi vya vijana vinavyoonyesha uwajibikaji kwa kurejesha mikopo wanayopewa ili viweze kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Nanauka aliyasema hayo leo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyotembelea kikundi cha Vijana cha Mali Hai kilichopo wilayani Muheza mkoani Tanga kwa lengo la kukagua shughuli zao za uzalishaji pamoja na miradi iliyopata fedha kupitia mikopo ya halmashauri.

Akiwa kwenye kikundi hicho alionyesha kuridhishwa na juhudi na nidhamu ya kikundio hicho kurejesha mikopo baada ya kufanikiwa kukuza mtaji wake kutoka shilingi milioni 20 hadi kufikia zaidi ya shilingi milioni 50, hatua inayotajwa kuwa mfano bora kwa vikundi vingine vya vijana nchini.

Nanauka alisema kikundi cha Mali Hali ni miongoni mwa vikundi vichache nchini vilivyofanikiwa kurejesha mikopo kwa wakati, jambo ambalo limekifanya kupata nafasi ya kuangaliwa kwa karibu zaidi katika mipango ya kusaidiwa kuongeza mtaji na kupanua shughuli zake.

Alisema katika mchakato unaoendelea wa kusaidia wajasiriamali wadogo na kurasimisha shughuli zao, serikali itaangalia namna ya kukiweka kikundi hicho kwenye orodha ya vikundi vitakavyosaidiwa ili kuimarisha shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, alieleza kuwa serikali inatekeleza maelekezo ya Rais ya kuhakikisha vijana wanaochukua hatua ya kufanya kazi na kuonyesha juhudi wanapatiwa mikopo na serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi na pia kutoa ajira kwa wengine.

“Vijana hawa wameonyesha mfano mzuri kwa watanzania wengine wameanza na mtaji mdogo mwaka 2008,wakapata msaada wa shilingi milioni tano mwaka 2018 na baadaye mkopo wa shilingi milioni 20 mwaka wa fedha 2020/2021. Leo hii wameongeza mtaji wao hadi kufikia zaidi ya milioni 50. Huu ni ushahidi kwamba ndoto kubwa zinaweza kuanza na mwanzo mdogo,” alisema Nanauka.

Aliongeza kuwa serikali itahakikisha vijana wenye juhudi kama hao wanapata fursa zaidi, ikiwemo mikopo mingine, pamoja na kushirikishwa katika zabuni za serikali ili waweze kukuza biashara zao.

Nanauka pia aliwashauri vijana nchini kutokudharau mwanzo mdogo na kuwa na uvumilivu wanapotekeleza ndoto zao za kimaendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Hawa Mchafu, alisema kamati hiyo ipo katika ziara ya kawaida ya kukagua miradi ya maendeleo kabla ya kuanza kwa Bunge la Bajeti, ambapo wamepita katika maeneo mbalimbali kutathmini miradi iliyopata fedha za serikali.

Alisema kamati hiyo imevutiwa na kazi nzuri inayofanywa na kikundi hicho cha vijana, lakini imebaini changamoto ya eneo la uzalishaji kuwa dogo na huenda lisiweze kukidhi mahitaji yao iwapo wataongeza mtaji zaidi.

Kutokana na hali hiyo, kamati imeitaka wizara husika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuhakikisha vijana hao wanapatiwa eneo kubwa zaidi la kufanyia shughuli zao za uzalishaji ili waweze kupanua biashara zao.

“Eneo walilonalo sasa ni dogo ukilinganisha na malengo yao ya kupanua uzalishaji hivyo tunashauri wapatiwe eneo kubwa zaidi na lililopo sasa likibaki kama sehemu ya maonesho ya bidhaa wanazozalisha,” alisema Mchafu.

Pia aliishauri serikali kuangalia uwezekano wa kukipa kikundi hicho mkopo mwingine wa kifedha ili kiweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokikabili, ikiwemo kununua gari kwa ajili ya shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha vijana nchini kutumia fursa zilizotolewa na serikali kupitia mifuko mbalimbali ya maendeleo ya vijana badala ya kujikita kwenye mfuko mmoja pekee.

Mchafu alisema kuwa Rais ametoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vijana kupitia wizara na taasisi mbalimbali, hivyo vijana wanapaswa kuzitumia fursa hizo kujikwamua kiuchumi.

Kamati hiyo pia imeishauri serikali kuhakikisha sheria ya manunuzi ya umma inayotaka asilimia 30 ya zabuni za serikali zitolewe kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu inatekelezwa kikamilifu ili kuwapatia vijana nafasi ya kukua kiuchumi.

Kwa sasa kikundi cha Mali Hali kinadaiwa kuajiri vijana zaidi ya 20 katika shughuli zake za uzalishaji, jambo ambalo limeelezwa kuwa linaunga mkono dhamira ya serikali ya kukuza ajira kwa vijana na kuimarisha uchumi wa wananchi.

Vijana wa kikundi hicho pia wamemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fursa na kuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kufikia ndoto zao za kuanzisha kampuni kubwa inayoweza kutoa ajira kwa vijana wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini.

Mwisho.

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya kupitia kundi la wanawake, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amewataka wanawake kuchangamkia fursa za mikopo inayotolewa na Serikali ili kujiinua kiuchumi na kujenga jamii imara yenye wanawake wanaojitegemea.

Akizungumza akiwa mgeni rasmi katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Mwanamke Shujaa mkoa wa Mbeya, Mhe. Mahundi amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya upatikanaji wa mikopo kwa makundi mbalimbali hususan wanawake wanaojishughulisha na biashara ndogo ndogo, ili kuwafikia wanawake wengi zaidi na kuwasaidia kujenga uchumi imara. 

 “Serikali imeweka utaratibu wa mikopo kwa ajili ya kuwainua wanawake kiuchumi. Nawahimiza wanawake kuitumia ipasavyo ili kujenga uchumi imara na kuondokana na utegemezi  Wanawake tukisimama kiuchumi tutaimarisha familia zetu na kuchangia maendeleo ya Taifa kwa ujumla, hivyo ni muhimu kila mwanamke kuona fursa hizi na kuzitumia kwa bidii na uaminifu,” amesema Mahundi.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase, amewataka wanawake kuzingatia malezi bora ya watoto, kusimamia haki za watoto pamoja na kushirikiana kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii ambapo jukumu la malezi na ulinzi wa watoto linahitaji mshikamano wa jamii nzima hususan wanawake ambao mara nyingi ndio walezi wakuu katika familia.

 “Wanawake tunapaswa kushirikiana na kupeana fursa badala ya kubaguana tukishikamana ndipo uimara wa mwanamke utaonekana na hapo tutakuwa na nguvu kubwa ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii ili kujenga nguvu ya pamoja katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi na tukiwa na Uchumi imara hata malezi ya familia zetu yanakuwa bora kwa kuwa tunakuwa na uimara wa akili hivyo na wasihi tuzingatie malezi bora ” amesema Josephine.

Naye mwanzilishi wa tuzo hizo, Sara Nyambura Ndambo, amewashukuru wanawake wote waliojitokeza kushiriki na kuunga mkono shughuli mbalimbali za kijamii pamoja na kuwapongeza wanawake waliotunukiwa tuzo hizo kwa juhudi zao katika jamii.

“Lengo la tuzo za Mwanamke Shujaa ni kutoa motisha kwa wanawake wanaojitoa katika shughuli za kijamii na maendeleo ili waendelee kufanya kazi zao kwa bidii zaidi huku wakihamasisha wengine kufuata nyayo zao na tutaendelea kuboresha tuzo hizi kila mwaka ili ziwe chachu ya kuwahamasisha wanawake wengi zaidi kufanya mambo makubwa katika jamii” amesema Sara.

Hafla hiyo ya utoaji wa Tuzo za Mwanamke Shujaa imewakutanisha wanawake kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya na imekuwa jukwaa la kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika shughuli za maendeleo, kuimarisha mshikamano wao pamoja na kutambua mchango wa wanawake wanaofanya kazi kubwa katika jamii.

Maafisa wa kulinda walaji kutoka Tume ya Ushindani (FCC) wametoa elimu kwa wananchi wa Halmashauri ya Chalinze mkoani Pwani kuhusu haki na wajibu wa mlaji, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Kumlinda Mlaji duniani yanayotarajiwa kufanyika Machi 31, 2026.
Elimu hiyo imelenga kuwajengea wananchi uelewa kuhusu namna ya kutambua bidhaa na huduma zenye ubora, pamoja na hatua wanazopaswa kuchukua pale wanapokutana na udanganyifu au ukiukwaji wa haki zao kama walaji. Wananchi pia wamehimizwa kuhifadhi risiti za manunuzi na kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapobaini vitendo vya biashara visivyozingatia sheria.
Maafisa hao wameeleza kuwa lengo la utoaji wa elimu hiyo ni kuhakikisha walaji wanakuwa na uelewa wa kutosha ili kujilinda dhidi ya bidhaa bandia, bei zisizo halali na huduma zisizokidhi viwango. Aidha, wamesisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda maslahi yao kwa kufahamu haki na wajibu wao wanapofanya manunuzi au kutumia huduma mbalimbali.
Maadhimisho ya Siku ya Kumlinda Mlaji hufanyika kila mwaka duniani kote kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu haki za walaji na kuhamasisha biashara kufuata misingi ya haki, uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa bidhaa na huduma. Serikali na taasisi mbalimbali nchini huendelea kutumia maadhimisho hayo kutoa elimu kwa jamii ili kujenga mazingira salama na yenye ushindani wa haki sokoni.
 
 
 



Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya kupitia kundi la wanawake, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ametembelea ofisi za BAKWATA Mkoa wa Mbeya na kukabidhi shilingi milioni tano, kuchangia ujenzi wa Shule ya Sekondari ya BAKWATA Mkoani humo.

Kati ya fedha hizo, shilingi milioni mbili zimetolewa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya ujenzi ikiwemo nondo na saruji, huku shilingi milioni tatu zikitolewa taslimu kusaidia kuendeleza ujenzi wa shule hiyo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Mhe. Mahundi amesema ataendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutafuta rasilimali zaidi ili kuharakisha ujenzi wa shule hiyo muhimu kwa jamii.

“Elimu ni msingi wa maendeleo ya jamii. Nitaendelea kutafuta wadau na washirika ili tuongeze nguvu katika kukamilisha ujenzi wa shule hii ambayo itawanufaisha vijana wengi wa Mkoa wa Mbeya,” amesema Mhe. Mahundi.

Kwa upande wake, Sheikh Mkuu wa BAKWATA Mkoa wa Mbeya Ndg.Ayas Njalambaah  amesema shule hiyo haitawahudumia Waislamu pekee bali itakuwa wazi kwa wanafunzi wa dini zote, kwa lengo la kuimarisha elimu na mshikamano wa jamii.

Aidha, amempongeza Mhe. Mahundi kwa moyo wake wa kujitolea katika maendeleo ya taasisi hiyo, akibainisha kuwa hata katika ujenzi wa ofisi za BAKWATA mkoa wa Mbeya, fedha za kuweka jiwe la kwanza zilitolewa na Mhe. Mahundi mwenyewe.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mahundi kwa moyo wake wa kujitoa. Ameendelea kuwa sehemu ya maendeleo ya taasisi yetu tangu mwanzo, ikiwemo kufanikisha hatua za awali za ujenzi wa ofisi hizi,” amesema Sheikh huyo.

Ujenzi wa Shule ya Sekondari ya BAKWATA Mkoa wa Mbeya unatarajiwa kusaidia kuongeza fursa za elimu kwa vijana na kuchochea maendeleo ya elimu katika eneo hilo.

 


๐Ÿ“Œ Yasema utekelezaji wa mradi huo umeboresha upatikanaji wa umeme vijijini.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeipongeza Wizara ya Nishati kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kasi ya utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 15 kwa kila jimbo nchini ili kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi wa maeneo ya vijijini.

 Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe.Subira Mgalu ametoa kauli hiyo katika ziara ya Kamati hiyo walioambatana na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme katika vitongoji vya Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mhe. Mgalu amesema kuwa Bunge liliidhinisha bajeti ya Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji 15 kwa kila jimbo Tanzania Bara kupitia REA, mpango ambao umeanza kuonyesha matokeo chanya katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Amesema katika Mkoa wa Shinyanga pekee, umeme tayari umefika katika vitongoji 90, jambo linaloonyesha juhudi kubwa za Serikali katika kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma muhimu ya nishati.

“Tunaipongeza Wizara ya Nishati kwa kazi nzuri ya kusimamia mradi huu kupitia REA. Kasi ya usambazaji wa umeme vitongojini inaendelea kuleta matumaini makubwa kwa wananchi na kuboresha maisha yao,” amesema Mhe. Mgalu.

Aidha, ameihimiza REA kuendelea kuongeza juhudi katika kupeleka umeme kwenye taasisi muhimu za umma kama zahanati, vituo vya afya, shule za msingi na sekondari, miradi ya maji pamoja na taasisi za dini ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wananufaika na huduma hiyo.

Amesisitiza Wizara hiyo kusimamia wananchi kuunganishiwa huduma ya umeme katika vitongoji kwa gharama ya Sh.27,000 ili kutimiza maono ya Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha umeme unafika katika vitongoji vyote nchini ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome amesema utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme katika vitongoji mkoani Shinyanga unaendelea vizuri na tayari umeanza kuleta manufaa kwa wananchi, hususan katika shughuli za uzalishaji na huduma za kijamii, hali inayoleta tabasamu kwa wananchi.

Amesema ataendelea kushirikiana na Waziri wa Nishati, Mhe.Deogratius Ndejembi, kusimamia maelekezo ya Rais kuhakikisha umeme unawashwa katika vitongoji vyote, sambamba na kauli mbiu ya wananchi wa Mkoa wa Shinyanga ya 'Salome Makamba, Washa umeme'.

Katika ziara hiyo, Kamati ya Bunge pia ilikagua na kuwasha umeme katika Zahanati ya Mine iliyopo Jimbo la Msalala, pamoja na kuwasha huduma ya umeme katika mashine ya kusaga na kukoboa katika Jimbo la Kahama Mjini, huduma zilizopatikana kupitia mradi wa kusambaza umeme vitongoji 15 kwa kila jimbo (HEP IIA).

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeiagiza Wakala wa Vipimo (WMA) kuhakikisha mita za umeme zinahakikiwa kikamilifu kabla ya kufungwa kwa ajili ya matumizi, kwa kuzingatia sheria zilizopo ili kulinda haki za watumiaji.

Aidha, Kamati hiyo imeipongeza WMA kwa jitihada za uhakiki na ukaguzi wa vipimo mbalimbali, ikiwemo mita za maji, huku ikiitaka Wakala hiyo kuendelea kusimamia kwa ukaribu vipimo katika sekta ya ujenzi ili kupunguza malalamiko ya wananchi yanayotokana na bidhaa hizo.

Hayo yameelezwa leo Machi 14, 2026, na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Deodatus Mwanyika, wakati wa ziara ya kikazi katika Kituo cha WMA cha Uhakiki wa Vipimo Misugusugu mkoani Pwani kwa lengo la kukagua miradi ya maendeleo na kujionea shughuli za uhakiki wa vipimo zinavyotekelezwa kituoni hapo.

Akizungumza katika ziara hiyo, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, aliihakikishia Kamati kuwa wizara itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa.

Alisisitiza kuwa azma ya Serikali ni kuhakikisha WMA inasimamia matumizi ya vipimo sahihi katika uzalishaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali, pamoja na Uhakiki wa mita za umeme na maji, ili kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson Simon, akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, alibainisha kuwa uhakiki wa vipimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa mkoa huo. Alieleza kuwa kwa sasa Mkoa wa Pwani una jumla ya viwanda 1,688, vikiwemo viwanda vikubwa 199 na vidogo sana 1,017, hivyo uhakiki wa usahihi wa Vipimo ni nyenzo muhimu katika kuvutia uwekezaji zaidi.

Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Bw. Alban Kihulla, alisema kuwa ukaguzi na uhakiki wa vipimo una nafasi kubwa katika kuhakikisha haki na usawa baina ya pande mbili zinazofanya biashara.

Pia, aliwahimiza wananchi kuhakikisha wanatumia vipimo vilivyohakikiwa, huku akiwasihi watoa huduma kuzingatia uadilifu kwa kutoa huduma kupitia vipimo sahihi ili kuleta usawa na kuhakikisha bidhaa zinazonunuliwa zinaendana na thamani halisi ya fedha.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefungua kikao kazi cha Chama cha Kulinda na Kutetea Haki za Walimu (CHAKUHAWATA) kinachofanyika jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wadau mbalimbali wa sekta ya elimu ili kuimarisha uongozi, utawala bora na udhibiti wa ubora wa elimu nchini.

 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya imetembelea na kukagua Makazi ya Wazee yanayomilikiwa na Serikali yaliyopo Njiro Mkoani Kilimanjaro, kwa lengo la kuona hali ya huduma zinazotolewa kwa wazee wanaoishi katika kituo hicho.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Hawa Mchafu ameipongeza Wizara  ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa juhudi inazozifanya kuhakikisha wazee wanapata huduma katika vituo mbalimbali nchini.  

“Tunawapongeza Wizara kwa hatua hii ya kuwahudumia wazee katika makazi maalum ni jambo la muhimu kwa ustawi wa jamii, hasa kwa wazee wasiokuwa na msaada wa familia hivyo ni jukumu letu kuendelea kulisemea bungeni kwaajili ya kuendelea kuboresha maisha ya wazee wote Nchini. Ni jambo jema na baraka kutoka kwa Mungu hivyo tutaendelea kuliwekea mkazo suala hili la wazee na kuja kuwaona  na ikiwezekana tuwaalike na wadau waweze kuongeza kunguvu ili mahitaji muhimu yaweyanapatikana kwa wakati." amesema Mhe. Mchafu.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Maryprisca Mahundi, amesema Wizara inaendelea kusisitiza umuhimu wa familia kutunza na kuwalea wazee wao kama sehemu ya maadili ya jamii ya Kitanzania ambapo Serikali inaendelea kutimiza wajibu wake wa kuwalea wazee wanaokosa msaada wa familia pale inapobidi.

“Tunasisitiza jamii na familia kufanya malezi sahihi kwa wazee wao Serikali inatimiza wajibu wake kwa kuwalea wazee hawa, pale ambapo kila kitu kimeshindikana lakini pia tumepokea pia maelekezo ya Kamati kuhusu maboresho ya kituo hiki na tutayafanyia kazi,” amesema Mhe. Mahundi.

Nao baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo wameitaka Wizara kuendelea kusimamia malezi na huduma zinazotolewa kwa wazee katika vituo hivyo pamoja na kuongeza vifaa na kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wanaowahudumia wazee, ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.


 


Kamati ya kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imempongeza Afisa Uhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Dkt. Agnes Gidna kutokana na umahiri, umakini, kujiamini na uchambuzi wake mkubwa wa masuala ya mambo kale na jiolojia.

Wakiongozwa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Timotheo Mnzava wabunge hao wametoa pongezi hizo baada ya kukagua na kupata maelezo ya mradi wa makumbusho ya _Urithi Geopark Museum._ 

Wabunge wamepongeza kazi kubwa iliyofanywa na serikali ya Tanzania na China ambapo hawakusita kuelezea hisia zao kutokana na mtaalam huyo  alivyowakonga nyoyo kwa kuelezea historia kuhusa kutokea kwa kreta ya Ngorongoro, milpuko ya volkano, maumbile ya dunia, chanzo cha binadamu wa kale na masuala mengine.

Kamati ya Bunge imeielekeza wizara ya Maliasili na Utalii kuitumia makumbusho hiyo kama bidhaa ya utalii na kitovu cha elimu kwa vijana wa kitanzania na kimataifa.

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt.Ashatu Kijaji aliwashukuru wabunge kwa pongezi hizo na kuwahakikishia kuwa wizara yake itasimamia kwa karibu maendeleo ya Urithi Geopark Museum.

Dkt.Agnes Gidna, mtaalam wa makumbusho, mambo kale na urithi wa utamaduni amekuwa kiungo muhimu  katika makumbusho hayo kutokana na umahiri wake wa kitaaluma na kitaalam kuihadithia yaliyopo kwenye makumbusho hiyo.

 



๐Ÿ“Œ Watembelea mradi kuona ufanisi wake

๐Ÿ“Œ Shilingi bilioni 118 zatumika kutekeleza mradi

๐Ÿ“Œ Watoa rai awamu ya pili kuanza kwa kasi


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa usimamizi na utekelezaji mzuri wa Mradi wa Uzalishaji Umeme kwa nguvu ya Jua wa Kishapu wenye uwezo wa Megawati 50 unaotekelezwa katika Mkoa wa Shinyanga.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgallu, mara baada ya Kamati kutembelea mradi huo tarehe 13 Machi, 2026 kwa lengo la kujionea maendeleo ya utekelezaji wake pamoja na ufanisi wa matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mhe. Mgallu alisema mradi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya nishati nchini kutokana na matumizi ya teknolojia ya nishati jadidifu.

“Tumetembelea mradi huu wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia teknolojia ya jua na tunaona ni mapinduzi makubwa katika sekta ya nishati nchini. Hii ni hatua muhimu kwani kwa mara ya kwanza Tanzania inapata Megawati 50 za umeme kutoka kwenye nishati ya jua,” alisema Mhe. Mgallu.

Alisema Kamati imeridhishwa na namna fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo zimetumika ipasavyo na kufanikisha utekelezaji wa mradi huo kwa ufanisi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, tumeridhishwa na matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya mradi huu. Tunaona wazi kuwa fedha hizo zimetumika vizuri katika utekelezaji wa mradi huu wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 118,” alieleza.

Aidha, alisema mradi huo tayari umeanza kuchangia Megawati 50 katika Mfumo wa Gridi ya Taifa, hatua inayochangia kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini pamoja na kuimarisha vyanzo mseto vya nishati.

“Utekelezaji wa mradi huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kunakuwa na vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme. Hii inaongeza uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme nchini,” alisema.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema mradi wa Kishapu unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme katika Gridi ya Taifa.

“Mradi huu una awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme kwenye Gridi ya Taifa. Awamu ya pili itahusisha uzalishaji wa Megawati 100 zaidi na kufanya jumla ya Megawati 150 kutoka katika mradi huu,” alisema Mhe. Ndejembi.

Kamati hiyo imetoa Rai kwa Wizara ya Nishati na TANESCO  inaendelea kuendelea na  mikakati ya kuanza utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo ili kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.

 


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, ameitaka Menejimenti ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuhakikisha kuwa miradi ya mafuta na gesi asilia inayoendelea nchini inatekelezwa na kukamilika kwa wakati ili iweze kuendelea kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Dkt. Mataragio ametoa maelekezo hayo leo wakati alipokutana na menejimenti ya TPDC  kwa lengo la kujadili fursa zilizopo katika sekta ya Mafuta  na Gesi Asilia, changamoto pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha sekta.

Aidha, Dkt. Mataragio ameiagiza TPDC, kuongeza vitalu vipya vya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia.

“Ni muhimu TPDC ikaendelea kupanua maeneo ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia kama mnavyofahamu rasilimali hii ni muhimu katika kutoa uhakika wa nishati nchini mfano kwenye  uzalishaji wa umeme na kukuza uchumi wa viwanda." Amesisitiza Dkt.Mataragio

Kwa upande wake, Kamishna wa Petroli, Goodluck Shirima, amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia ili kuongeza matumizi yake katika sekta mbalimbali ikiwemo majumbani, viwandani na katika uzalishaji wa umeme.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutenga na kuandaa maeneo kwa ajili ya ushiriki wa sekta binafsi kwenye miradi ya usambazaji wa gesi, akibainisha kuwa miradi hiyo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati (flagship projects) inayolenga kuongeza matumizi ya gesi asilia.

Naye,  Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame amesema Shirika hilo litaendelea kutekeleza maagizo  yanayotolewa na viongozi wa Wizara kwa lengo la kuzidi kuiimarisha sekta ya Mafuta na Gesi Asilia.

“TPDC itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha miradi ya gesi asilia na mafuta inatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya Watanzania wote."  Amesema Makame

Ziara ya Dkt. Mataragio TPDC ni muendelezo wa ziara zake katika Taasisi zinazosimamia Sekta ya Mafuta na Gesi Asilia ikiwa ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Nishati kuimarisha usimamizi wa taasisi zake ili ziendelee kutekeleza majukumu kwa ufanisi lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wananufaika  na rasilimali zilizopo nchini.

 


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imedhamiria kujenga barabara zote zinazounganisha mkoa wa Katavi kwa lami ili kuufanya mkoa wa kimkakati na kibiashara.

Amesema hayo leo mkoani Katavi alipoweka jiwe la msingi ujenzi wa barabara ya Kagwira-Ikola- Karema yenye urefu wa km 112.

Dkt. Nchema amesema barabara hiyo inaunganisha mji wa Mpanda na ziwa Tanganyika kwenye bandari ya Karema itachochea huduma za bandari na shughuli za kiuchumi itakapokamilika.

" Tumedhamiria kuunganisha barabara zenu za Rukwa- Mpanda na Mpanda -Kigoma kwa lami ili kuifanya Katavi mkoa wa kimkakati na kiuchumi", amesisitiza Dkt. Nchemba.

Nae Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amesema Serikali imeipandisha hadhi barabara ya Kagwira- Karema kutoka kuwa barabara ya mkoa kuwa barabara Kuu hivyo ujenzi wake utakuwa wa viwango vya juu ili kuwezesha magari makubwa kupeleka na kuchukua mizigo katika bandari ya Karema ambayo ujenzi wake umekamilika.

" Katika kuhakikisha ujenzi wa barabara hii unakamilika kwa wakati na ubora tumeugawa sehemu mbili ambazo ni Kagwira-Kasekese km 54.1 na Kasekese- Karema km 56", amesema Eng. Kasekenya.

Barabara hiyo yenye madaraja makubwa 7 na madogo 88 inatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 219 itakapokamilika.

Naibu Waziri Kasekenya amesema Serikali inaendelea kuzijenga kwa kiwango cha lami barabara za Kibaoni-Sitalike km 72 na Vikonge- Mishamo hadi Uvinza km 156 ili kuunganisha mkoa wa Rukwa, Katavi na Kigoma kwa lami na hivyo kuufungua ushoroba wote wa mwambao wa ziwa Tanganyika na hivyo kuchochea uchumi wa mikoa hiyo.



Wakala wa Nishati Vijijini (REA), umeendelea kutekeleza miradi ya kupeleka huduma ya umeme katika maeneo ya vitongoji ili kuwawezesha wananchi waliopo maeneo hayo kupata huduma bora ya nishati ya umeme kwa ajili  ya Maendeleo yao na Taifa kwa ujumla. 

Hayo yamebainishwa na Msimamizi wa Miradi ya REA, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Mha. Danstan Kalugira wakati akizungumza  na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) kuhusu miradi inayotekelezwa na REA katika wilaya ya Ludewa mkoani Njombe.

Mha. Kalugira amesema kuwa, kiasi cha fedha takribani shilingi bilioni 3.1 tayari zimetolewa na Serikali kupitia REA ili kutekeleza mradi huo wa kupeleka umeme kwenye vitongoji takribani 6 vya wilaya ya Ludewa ili wananchi wanufaike na huduma ya umeme.

"Katika mradi huu hapa wilayani Ludewa, mkandarasi kampuni ya SUMA JKT ndiye anayetekeleza mradi huu mkubwa ambao unatarajiwa kuunganishia wateja wapatao 160 wa awali mara baada ya mradi kuwa umekamilika, " Amesema Mha. Kalugira

Ameongeza kuwa, japokuwa kipindi hichi ni cha masika mvua nyingi zinanyesha  ila mkandarasi huyo anaendelea kutekeleza mradi kwa kasi, weledi na ni matarajio kuwa atakwenda kumaliza mradi huo kwa wakati katika muda uliopangwa ili wananchi watakaounganishwa na nishati ya umeme waweze kunufaika.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (TEF), Bw. Deodatus Balile ameishukuru Serikali kwa kutoa fedha ya utekelezaji wa miradi hiyo inayoendelea katika mkoa wa Njombe na maeneo mengine nchini.

"Tumejionea kwa macho yetu namna fedha hizi zinazotolewa na Serikali na  jinsi zinavyotekeleza miradi ya kupeleka huduma ya umeme katika wilaya hii ya Ludewa ili wananchi wapate nishati bora ya uhakika, " Amesisitiza Bw. Balile.

Ziara ya TEF imelenga kutembelea miradi ya kimkakati inayotekelezwa na REA katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo miradi ya Awamu ya Pili B (HEP 2B) ya kupeleka umeme kwenye vitongoji vipatavyo 9,009.

  



Na OWM – TAMISEMI, Ufaransa


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amekutana na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe.Ali Mwadini, kujadili mikakati ya kuvutia na kutafuta wawekezaji katika eneo la Bonde  la Msimbazi lililopo jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kuwa na mpango madhubuti wa kutafuta wawekezaji wa kimataifa watakaoshiriki kuwekeza katika maendeleo ya bonde hilo, ambalo Serikali imeanza kulijenga ili kupunguza athari za mafuriko na wakati huo huo kufungua fursa mpya za uwekezaji na biashara.

Utekelezaji wa mpango huo unatarajiwa kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuboresha huduma za kijamii pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi wa jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani, huku pia ukivutia wafanyabiashara na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Prof. Shemdoe amefanya ziara katika ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa jana Machi 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha uwekezaji unaofanyika katika Bonde la Msimbazi unaleta manufaa makubwa kwa uchumi wa taifa na kuwawezesha wajasiriamali na wafanyabiashara wa jijini Dar es Salaam.

Uwekezaji unaotarajiwa katika bonde hilo ni sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuendeleza miundombinu ya kisasa mijini, kudhibiti mafuriko na kuifanya Dar es Salaam kuwa kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.


Wananchi na wakazi wa Hydom wilayani Mbulu mkoa wa Manyara wamemshukuru Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia Wizara ya Maji kupitia RUWASA kutekeleza mradi mkubwa wa Majisafi ya bomba wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 41 na tayari vijiji vinne vimeshaanza kunufaika na mradi huo.

Wametoa pongezi hizo wakati wa ziara ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira alipotembelea na kukagua mradi huo ikiongozwa na Mwemyekiti wake Mhe. Jackson Kiswaga (Mb) katika eneo la Hydom lilipo tangi kubwa la ujazo wa lita 2,000,000 la mradi huo.

Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA Mha. Wolta Kirita aliieleza Kamati hiyo kuwa tayari wananchi zaidi 800 wameshasajiliwa na kupatiwa kadi za malipo kabla ya matumizi kwani mradi huo unaenda sambamba na ufungaji wa dira za maji za malipo ya kabla, ambapo mwananchi anaweza kuchota maji kwenye kituo muda wowote anapokuwa anahitaji huduma hiyo.

Mkurugenzi Mkuu Kirita alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika Novemba 2027.

Kwa mujibu wa Meneja wa RUWASA mkoa wa Manyara Mha. James Kionaumela alisema mradi huo umeshaanza kutoa huduma katika vijiji vinne na ukikamilika utahudumia zaidi ya wakazi 100,000 wa eneo hilo.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbulu Mhe. Michael Semindu akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga alisema kwa sasa wananchi wa wilaya hiyo wanapata maji kwa saa 12 kwa siku huku akiipongeza RUWASA kwa kazi nzuri katika kutekeleza mradi huo.








Na. Joyce Ndunguru, Dodoma.

Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mlage Yussuf Kabange amefungua rasmi kikao kazi cha maandalizi ya bajeti ya TAWA kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi kilichofanyika Machi 13,2026, Jijini Dodoma, Kamishna Kabange amesema Bajeti ya mwaka 2026/27 ni ya kipekee kwa kuzingatia kuwa ni bajeti ya kwanza katika kuchangia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025 pamoja na Dira ya maendeleo ya Taifa 2050.

“Pia bajeti hii imezingatia kutafsiri Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan wakati wa kuzindua Bunge la 13, Mkakati wa kuongeza mapato wa TAWA na ni bajeti ya kwanza tangu Bodi ya Nne ya Wakurugenzi ya TAWA iteuliwe”, amesema Kamishna Kabange.

Kamishna Kabange ameongeza kuwa katika bajeti hii TAWA itajielekeza katika vipaumbele mbalimbali ikiwemo kuimarisha ulinzi na usimamizi wa Rasilimali wanyamapori na malikale.

Pia, Kuimarisha shughuli za utalii pamoja na kuongeza idadi ya watalii kwa kuboresha miundombinu ya utalii pamoja na kuongeza vyanzo vipya vya mapato.

Kadhalika, Utatuzi wa migogoro ya mipaka na udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu pamoja na Kuimarisha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi na uwezo wa Mamlaka katika kutoa huduma.

Vilevile , Kamishna Kabange amewapongeza Makamanda na Askari ambao wamekuwa mstari wa mbele kusimamia utekelezaji wa malengo ya Mamlaka. Aidha, amewaelekeza Makamanda wa vituo kuhakikisha Usimamizi madhubuti wa vitendea kazi yakiwemo magari.

Aidha, Kamishna Kabange amewaelekeza Makamanda kuendelea na utangazaji wa vivutio vya utalii pamoja na kubuni mazao mapya ya utalii.

“Nitoe rai kwenu kuendelea kuwa wabunifu na kutangaza maeneo mnayoyasimamia,” amesema Kamishna Kabange 

Sambamba na hilo, Kamishna Kabange amewaelekeza Makamanda kuendelea kusimamia askari kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kwa kuzingatia haki, sheria na miongozo iliyowekwa.

Kikao kazi cha maandalizi ya bajeti kimehudhuriwa na viongozi wa TAWA kwa ngazi ya Makao Makuu, Kanda na Vituo.