New York, Marekani


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza hatua zake za kuanza kutekeleza Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, 2026/27–2030/31 (FYDP IV), ambao ni mpango wa kwanza wa muda wa kati wa kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hayo yamelezwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais–Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Mbaga Kida, wakati wa mkutano wa pembezoni mwa Jukwaa la Ngazi ya Juu la Siasa la Umoja wa Mataifa linalosimamia Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (HLPF 2026), uliofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.

Mkutano huo, wenye mada “Driving Industrial and Inclusive Economic Transformation: Financing, Innovation and Sustainable Growth in Agricultural and Blue Economy Value Chains”, uliandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), pamoja na UNDP, UNIDO na washirika wengine.

Dkt. Kida alisema Tanzania inaingia katika awamu mpya ya utekelezaji wa maendeleo inayolenga kubadilisha mafanikio ya ukuaji wa uchumi na uwekezaji katika miundombinu kuwa ongezeko la uzalishaji, ajira zenye tija, mauzo ya nje, ongezeko la thamani ya bidhaa na ustawi mpana wa wananchi.

Dkt. Kida alisema uchumi wa Tanzania kwa sasa unakua kwa asilimia 5.9 na unatarajiwa kufikia asilimia 6.3 ifikapo mwisho wa mwaka huu. Ukuaji huo ulichangiwa na kuimarika kwa shughuli mbalimbali za uzalishaji na huduma, pamoja na kuendelea kwa uwekezaji katika miundombinu na miradi ya kimkakati.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa lengo si kasi ya ukuaji pekee, bali ukuaji unaogusa maisha ya wananchi wote. “Lengo letu si kuongeza ukubwa wa uchumi pekee. Tunataka ukuaji unaoongeza kipato cha wananchi, unaotengeneza ajira, unaopunguza umaskini na unaowezesha wanawake, vijana, wakulima wadogo na wajasiriamali kushiriki kikamilifu katika uchumi,” alisema Dkt. Kida.

Dkt. Kida alibainisha kuwa kilimo, misitu na uvuvi vinaendelea kuwa sehemu muhimu ya uchumi wa Tanzania, vikichangia asilimia 24.3 ya Pato la Taifa mwaka 2025. Alisema mchango wa uvuvi katika Pato la Taifa uliongezeka kutoka asilimia 1.9 mwaka 2020 hadi asilimia 2.2 mwaka 2025, hatua inayoonesha fursa zinazoongezeka katika uchumi wa buluu.

“Tunataka kuondoka katika uchumi unaouza malighafi na kuelekea uchumi unaosindika, unaoongeza thamani, unaotumia teknolojia na unaounganisha wazalishaji wa ndani na masoko ya kitaifa, kikanda na kimataifa,” alisema.

Dkt. Kida pia alisema Tanzania itawasilisha Mapitio ya Tatu ya Hiari ya Nchi ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu tarehe 14 Julai 2026.

Mapitio hayo yanaonesha maendeleo yaliyopatikana katika maji safi, nishati, miundombinu, afya, usafiri, teknolojia ya kidijitali na uimarishaji wa rasilimali za ndani.

Kwa upande wake, Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, New York, Mhe. Togolani Edriss Mavura, alisema mageuzi ya viwanda barani Afrika yanapaswa kuwa jumuishi na kuwanufaisha wakulima wadogo, wanawake, vijana, wavuvi, wafugaji, biashara ndogo na washiriki wa sekta isiyo rasmi.

Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika teknolojia, uwekezaji, masoko, ujuzi, fedha za maendeleo na ujenzi wa minyororo ya thamani inayounganisha nchi za Afrika.

Ofisa Mkuu wa Fedha wa UNCDF, Bw. Karen Vardanyan, aliitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoonesha namna fedha bunifu zinavyoweza kutumika kuharakisha maendeleo katika ngazi ya taifa na mamlaka za serikali za mitaa.

Alieleza kuwa upatikanaji wa nishati safi ya kupikia umeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025. Maendeleo hayo yanaungwa mkono na utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, uwekezaji wa sekta binafsi na juhudi za Serikali za kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa.

Bw. Vardanyan pia alitaja Tanga UWASA Green Revenue Bond, iliyokusanya dola za Marekani milioni 20.8 kwa ajili ya miundombinu ya maji inayohimili mabadiliko ya tabianchi. Hatifungani hiyo ilikuwa ya kwanza ya kijani katika ngazi ya mamlaka ya chini ya kitaifa Afrika Mashariki, huku wawekezaji wa ndani wakichangia asilimia 65 ya uwekezaji wote.

Mifano mingine iliyotajwa ni PesaTech Accelerator, inayosaidia ubunifu wa huduma za kifedha na biashara zinazoongozwa na vijana, pamoja na mfumo wa LoCAL unaowezesha mamlaka za serikali za mitaa kuongeza uwekezaji unaohimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Bw. Vardanyan alitoa wito kwa Serikali, taasisi za fedha, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kubadili ahadi za kimataifa kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na uwekezaji halisi katika kilimo, uchumi wa buluu, viwanda, maji, nishati na miundombinu.

Mkutano huo ulihitimisha kuwa utekelezaji wa Dira 2050 na FYDP IV utahitaji ushirikiano madhubuti kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha, Umoja wa Mataifa, washirika wa maendeleo, asasi za kiraia na jamii.

Dira 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati cha juu, yenye Pato la Taifa la dola za Marekani trilioni moja, pato la wastani kwa mtu linalozidi dola 7,000 na kuondoa umaskini ifikapo mwaka 2050.










Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bw. Emmanuel Tutuba (kulia) akimueleza jambo Afisa Kurugenzi ya Usimamizi wa sarafu BoT, Bw. Shadrack Mapunda, wakati alipotembelea banda la Benki Kuu ya Tanzania (BoT) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu ya "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania", yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

CHAMA cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) kimeipongeza Tume ya Ushindani (FCC) kwa kuendelea kutoa elimu kuhusu utambuzi wa bidhaa bandia na ulinzi wa biashara kwa wajasiriamali, kikisema mafunzo hayo yameongeza uelewa na kusaidia kulinda biashara halali nchini.

Akizungumza baada ya darasa la elimu leo Julai 10, 2026 katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Afisa Ushirikiano wa TWCC, Nelson Clevary, amesema ushirikiano kati ya TWCC na FCC umeendelea kuzaa matunda kwa kuwajengea wajasiriamali uwezo wa kutambua bidhaa bandia pamoja na namna ya kulinda bidhaa na biashara zao dhidi ya vitendo vya udanganyifu.

Alisema mwaka huu ni wa tatu mfululizo kwa TWCC kushirikiana na FCC kuendesha mafunzo hayo, huku matokeo yakionyesha kuwa wajasiriamali wengi wameanza kuelewa athari za bidhaa bandia na umuhimu wa kushirikiana na mamlaka husika zinapotokea changamoto zinazohusiana na bidhaa hizo.

"Leo tumepata darasa zuri ambalo limewasaidia wajasiriamali kutambua bidhaa halisi na bidhaa bandia, lakini pia wamefundishwa namna ya kulinda biashara zao ili zisidhurike kutokana na watu wanaoiga au kutengeneza bidhaa bandia kwa kutumia majina ya biashara zao," amesema Clevary.

Amebainisha kuwa ingawa mafunzo yanayotolewa wakati wa maonesho huwafikia washiriki wachache, bado kuna haja ya kupanua wigo wa elimu hiyo ili kuwafikia wajasiriamali wengi zaidi nchini.

Clevary amesema TWCC ina wanachama zaidi ya 22,000 nchini, hivyo ushirikiano wa karibu na FCC utawezesha elimu hiyo kuwafikia wengi zaidi na kuongeza uwezo wa wafanyabiashara kulinda bidhaa zao na haki za biashara.

Aidha, amewataka wajasiriamali kuendelea kutumia fursa ya mafunzo hayo kujifunza namna ya kutambua bidhaa bandia na kuripoti vitendo vya ukiukwaji vinavyoweza kuhatarisha biashara zao.

Kwa upande wake Mjasiriamali kutoka mkoani Mwanza, Praxeda Mgyabuso, amesema elimu inayotolewa na Tume ya Ushindani (FCC) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) imewasaidia wafanyabiashara na wananchi kutambua tofauti kati ya bidhaa halisi na bidhaa bandia, pamoja na umuhimu wa kulinda biashara zao kupitia usajili wa alama na nembo za biashara.

Amesema awali alikuwa hana uelewa wa kutosha kuhusu madhara ya bidhaa bandia na namna ya kuzitambua, hali iliyowafanya watumiaji wengi kununua bidhaa zisizo halisi bila kufahamu athari zake kwa afya na uchumi.

Amesema elimu hiyo imewafungua macho wafanyabiashara kutambua kuwa pamoja na kuzingatia ubora wa bidhaa, ni muhimu pia kusajili majina na nembo za biashara ili kuzuia watu wengine kuiga bidhaa zao na kutumia utambulisho wao kinyume cha sheria.

"Kwa kweli tumepata elimu kubwa. Wengi wetu tulikuwa tunanunua bidhaa kwa kuangalia bei ya chini bila kujua kuwa baadhi yake ni bandia na zinaweza kuhatarisha afya zetu. Sasa tumeelewa namna ya kutambua bidhaa halisi na umuhimu wa kulinda biashara zetu kupitia usajili wa nembo na majina ya biashara," amesema.

Nae Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma wa FCC, Roberta Feruzi, amesema kuwa maonesho hayo yameipa tume hiyo fursa ya kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha kuhusu haki zao pamoja na huduma zinazotolewa na taasisi hiyo.

Pamoja na hayo amesema mbali na kutoa elimu, FCC pia inatoa huduma za moja kwa moja kwa wananchi wanaotembelea banda lake, ikiwemo kupokea na kushughulikia malalamiko, usajili wa mikataba na huduma nyingine zinazotolewa na tume hiyo.

Na. Mwandishi Wetu

Mwenyekiti wa Tume ya Ushindani (FCC), Dkt. Aggrey Mlimuka, ametembelea banda la FCC katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba 2026), yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.

Maonesho hayo yamewakutanisha washiriki mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi, wakiwemo kampuni binafsi, taasisi na mashirika ya Serikali, yakitoa fursa ya kutangaza bidhaa, huduma na uwekezaji.

Akiwa katika banda la FCC, Dkt. Mlimuka ameipongeza Tume hiyo kwa kazi kubwa inayofanya katika kulinda ushindani wa haki sokoni na kuimarisha mapambano dhidi ya bidhaa bandia, hatua inayochangia kulinda maslahi ya walaji na kukuza mazingira bora ya biashara nchini.

Pia amempongeza Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, Menejimenti pamoja na watumishi wote wa Tume hiyo kwa kujituma, weledi na ufanisi katika kutekeleza majukumu yao na kuhakikisha taasisi hiyo inatimiza malengo yake kwa mafanikio.

FCC ina jukumu la kulinda na kuhimiza ushindani wa haki katika biashara, kulinda maslahi ya walaji, kupokea na kushughulikia malalamiko yanayohusu ukiukwaji wa sheria za ushindani, pamoja na kudhibiti uingizaji, usambazaji na uuzaji wa bidhaa bandia nchini.

Mbali na kutembelea banda la FCC, Dkt. Mlimuka pia alitembelea mabanda ya taasisi mbalimbali zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kujionea shughuli na huduma zinazotolewa kwa wananchi.

Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba 2026), yenye kaulimbiu "Sabasaba Fahari ya Tanzania," yalianza rasmi Juni 28, 2026, na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026 katika Viwanja vya Maonesho vya Julius Nyerere (Sabasaba Grounds), Barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Tume ya Ushindani (FCC) akipata maelezo kutoka kwa Bi. Roberta Feruzi, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano - FCC wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya biashara ya Kimataifa  yanayoendelea viwanja wa Sabasaba jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Tume ya Ushindani (FCC) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa FCC wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya biashara ya Kimataifa  yanayoendelea viwanja wa Sabasaba jijini Dar es Salaam.

Tanzania imepata heshima ya kutunukiwa Tuzo ya Kimataifa ya WSIS Prizes 2026 kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa minara 758 ya mawasiliano ulioongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika maeneo ya vijijini na ambayo hayakuwa na huduma ya mawasiliano nchini.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Kassim Mchatta, amesema chanjo zinazozalishwa na Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) zimeendelea kuthibitisha ubora wake kwa kusaidia kudhibiti magonjwa mbalimbali ya mifugo na kuongeza tija kwa wafugaji nchini.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, akizungumza na Mwenyekiti wa Al Mansour Holding, Mhe. Sheikh Mansour, leo tarehe 10, 2026 jijini Doha, Qatar.

Na: OWM (KAM) – Doha, Qatar

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amekutana na kufanya mazungumzo na Mwenyekiti wa Al Mansour Holding, Mhe. Sheikh Mansour, leo tarehe 10, 2026 jijini Doha, Qatar ambapo wamejadili kuhusu ushirikiano katika maeneo ya uwekezaji, ajira na maendeleo ya ujuzi.

Aidha, katika mazungumzo yao Mhe. Sangu alitumia fursa hiyo kumueleza Mwenyekiti wa Al Mansour Holding dhamira ya Serikali ya Tanzania katika kuendelea kuweka mazingira bora na rafiki kwa wawekezaji pamoja na kuendeleza ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Qatar.

Vilevile, Waziri Sangu ameipongeza kampuni ya Al Mansour Holding kwa kuendelea kuongeza wigo wa uwekezaji katika Mataifa mbalimbali ikiwemo Tanzania Bara na Zanzibar. Pia, amehamasisha kampuni hiyo kutumia wataalamu na nguvu kazi ya Watanzania katika shughuli zake nchini Qatar na katika masoko mengine ya kimataifa.

Kadhalika, ameihakikishia kampuni hiyo ushirikiano katika kukuza maendeleo ya rasilimali watu kupitia mafunzo, uhamishaji wa teknolojia na ujuzi ili kuchochea ajira na ukuaji wa uchumi.

Katika ziara hiyo, Waziri Sangu ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Mhe. Habibu Awesi Mohamed, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Zuhura Yunus, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji Zanzibar, Khalid Masoud Waziri, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kazi na Uwekezaji, Rashid Ali Salim, pamoja na wataalamu wengine kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, akizungumza na Mwenyekiti wa Al Mansour Holding, Mhe. Sheikh Mansour, leo tarehe 10, 2026 jijini Doha, Qatar.