Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dk. Toba Alnason Nguvila, amewasistiza watumishi wa Umma kufanya kazi kwa kufuata Sheria, taratibu na kanuni kwa kuzingatia kiwango cha juu cha Maadili ya Utumishi wa Umma, ili kufikia lengo la Serikali la kuwahudumia wananchi.

Dkt.Nguvila ametoa wito huo, wakati akizungumza na baadhi ya watumishi wa Umma mkoa wa Arusha, kwenye hafla fupi ya mapokezi yake, iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, leo Februari 10, 2026, muda mfupi baada ya kupokelewa ofisini hapo, tayari kwa kuanza kutekeleza majukumu yake kwa washifa huo.

Amewasisitiza watumishi hao, kila mmoja kwa nafasi yake kuzingatia kuwa, mkoa huo ni mkoa wa Utalii hivyo wanalo jukumu la kuhakikisha wadau wa utalii wanafanya kazi kwenye mazingira rafiki, yasiyo na vikwazo vya aina yoyote huku akisisitiza kuto kuvumilia vikwazo vya kiutendaji wala urasimu unaokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii. 

"Sisi watalamu tunapaswa kuwa kichocheo cha kuiimarisha sekta ya utalii, kwa kuwa kila wilaya ina vivutio vyake, hivyo si busara kwa baadhi ya watendaji kuweka urasimu usio wa lazima unaoweza kudhoofisha sekta hiyo, sitavumilia urasimu wala migogoro inayokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii". Amesema Dkt.Nguvila

Aidha, amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri zote, kutenga bajeti ya kutekeleza shughuli za utalii kwenye maeneo yao, kubuni vyanzo vya mapato pamoja na kusimamia ukusanyaji wa mapato, ikiwa ni pamoja na kutoka maofisini na kuwafuata wananchi ili kubaini changamoto zao na kuzitatua kwa haraka.

Katika kutekeleza maelekezo ya Serikali, Dkt.Nguvila ameataka viongozi hao, kuwa na kampeni maalumu ya kutoa elimu na usajili sambamba na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa wote, ili ili kufikia lengo la Serikali ya awamu ya sita ya kila mwananchi kujiunga na Bima hiyo, itakayowawezesha kupata huduma za matibabu wanapougua.

Awali, Dkt.Nguvila amemshukuru Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kumuanini na kumteua kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha na ameahidi kushirikiana na watalamu wa ngazi zote katika kuwahudumi wananchi.

















Na Oscar Assenga,MUHEZA

MKURUGENZI Bonde la Maji la Pangani Segule Segule amewaonya watu ambao wanao kuchukua maji chini ya ardhi,juu ya ardhi bila kufuata utaratibu uliowekwa kisheria ikiwemo kuwa vibali kuacha mara moja kwani wakiwafikia watawakamata.

Segule aliyasema hayo wakati wa Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Jumuiya ya Maji Mto Zigi uliofanyika mjini Muheza ambapo alisema iwe mtu binafasi au taasisi huku akiwashauri wafuate utaratibu na kuchukua vibali na vibali vyao vinawaeleza kitu gani wanapaswa kufanya.

Aliwaeleza wadau wa Jumuiya hiyo kuwa Bonde la Mto Pangani linasimamia vyanzo vilivyopo chini ya ardhi kupitia visima na katika eneo hilo watu wengi hawana ufahamu au wengine wanaelewa lakini hawafuati utaratibu uliowekwa

Aidha alisema watu hawana ufahamu wa kutosha katika eneo la visima kwamba ukipewa ridhaa na Mkurugenzi wa Halmshauri ukipewa hatia na Wizara ya Ardhi juu ya kutumia ardhi na unaporaka kutumia rasilimali maji lazima upate kibali kutoka kwenye Bonde husika na katika Kanda ya Kaskazini anayetaka kutimia maji kutoka chini ya ardhi lazima apate kibali kuyoka Bonde la Pangani.

Aidha alisema kwamba Serikali imefanya kwa nia njema na sio kuweka ugumu watu wasitumie lakini wasiposimamiana katika hilo ipo siku maji yote yatachafuliwa na yanaweza yasiwepo.

Alieleza kwamba wao hawatoi vibali pekee bali wanaratibu wachimbaji kujua wana utaalamu wa kutosha wanaanza kuratibu kwenye utafiti huyo anayefanya utafiti je ana taaluma hiyo mpaka wanapotoa kibali cha kuchimbiwa visima wanauhakika wanakuwa ni watu sahihi wanaotumia utaalamu sahihi hivyo uchimbahji wake hauwezi kuleta madhara kwenye jmii husika,

Awali akizungumza wakati akifungua mkutano huo kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Muheza, Katibu Tawala wa wilaya hiyo serikali inatambua ushirikishwaji wa wadau mbalimbali katika usimamizi na uhifadhi na uendelezaji wa rasimali za maji na mazingira.

Alisema lengo kuu katika juhudi hizo ni kuhakikisha rasilimali za maji zinazopatikana kwa wingi ikiwemo ubora unaokubalika na kwa uendelevu wa matumizi ya maji kwa sasa na vizazi vijavyo.

“Niwapongeze viongozi mliomaliza muda wenu kwa kazi nzuri na kubwa mlioifanya na kusimamia uendeshaji wa jumuiya ikiwemo usimamizi wa vyanzo vya maji”Alisema

Aliongeza kwa athari za mabadiliko ya tabia ya nchi na hali ya hewa hapa nchini ikiwemo Muheza joto kali mvua hazinyeshi hayo yote yamebadilika kutokana na uharibifu wa mazingira unaoendelea.

Alisisitiza utunzaji wa mazingira ni jambo muhimu ambalo limeendelewa kupewa kipaumbele na Rais na hata alipoazimisha siku ya kuzaliwa alipanda miti hivyo kupitia jumuya hiyo waendelee kuwahamasisha watu wapande miti katika kila sikukuu zao muhimu ikiwemo kuzaliwa.

Hata hivyo alieleza kwamba kuna umuhimu wa Jumuiya hizo kuendelea kujengewa uwezo ili kuweza kutunza mazingira ikiwemo mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kuendana na kazi na mazingira kipindi cha sasa.









 

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tanga(TangaUWASA) imeingia makubaliano maalum na taasisi ya ROTARY inayofanya kazi kwa kushirikiana na Mamlaka za Maji Nchini Uholanzi (VEi) ya kutekeleza mradi wa kuwezesha huduma za kijamii mashuleni kupitia ujenzi wa vyoo (SCHOOL WaSH) kwa shule za msingi katika Jiji la Tanga.

Akizungumza kwa niaba ya uwakilishi wa ROTARY Bi.Emma Lesterhuis ameainisha kuwa mradi huo utatekelezwa na TangaUWASA kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Tanga na utajikita zaidi katika ujenzi wa vyoo kwa baadhi ya shule zenye idadi kubwa ya wanafunzi na uhaba wa matundu ya vyoo.

Nae kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TangaUWASA, Mha. Geofrey Hilly amewashukuru ROTARY kwa kutambulisha mradi huo ambao unaenda kuwezesha jamii hususani wanafunzi kupata huduma muhimu na kuahidi kutoa ushirikiano wa kutosha wakati wote wa utekelezaji wa mradi na usimamizi wake.



Tanga unakuwa Mkoa wa tatu nchini kunufaika na mradi wa "SCHOOL WaSH" ukiungana na Mikoa ya Arusha na Mwanza ambayo utekelezaji wake unaendelea.

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Maendeleo ya Usimamizi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, anashiriki warsha ya uthibitishaji iliyoandaliwa na Kituo cha Afrika cha Uongozi wa Shule (ACSL) jijini Nairobi, Kenya, kuanzia tarehe 10 hadi 13 Februari 2026.

 


Na OWM - TAMISEMI, Dodoma

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, Mhe Cecilia Daniel Paresso amesisitiza ushirikishwaji wa wananchi wakati wa utungaji na uhuishaji wa Sheria Ndogo za Mamlaka za Serikali za Mitaa, ili kuwajengea wananchi uelewa wa sheria hizo ambao utawezesha utekelezaji wake katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mhe. Paresso ametoa wito huo wa ushirikishwaji wa wananchi katika utungaji wa sheria ndogo leo  Februari 10, 2026 Jijini Dodoma, wakati akiongoza Kikao cha Mafunzo kwa kamati yake kuhusu Sheria Tatu za Mamlaka ya Serikali za Mitaa na uhusiano wake na sheria ndogo za Mamlaka hizo.

Mhe. Paresso na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo wameishauri Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI kufanya mapitio ya Sheria Ndogo ambazo zimepitwa na wakati ili kuzihuisha au kuziondoa sheria zitakazobainika kutotekelezeka.

Akimwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe katika kikao hicho, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya amesema Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI itawashirikisha wananchi wakati wa kutunga Sheria Ndogo za Mamlaka za Serikali za Mitaa kama kamati ilivyoelekeza, lengo likiwa ni kuwajengea uelewa wananchi na kuwezesha utekelezaji wake.

Aidha, Mhe. Mmuya ameiahidi kamati hiyo kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI itafanya mapitio ya Sheria Ndogo za Mamlaka za Mitaa ili kujiridhisha kama zinakwenda na wakati, na kuongeza kuwa itazihuisha na kuziondoa sheria ambazo zitakazobainika kupitwa na wakati.

Katika kikao kazi hicho cha mafunzo, wajumbe wa Kamati hiyo ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo wamepata fursa ya kupitia Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura ya 288, Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura ya 287, na Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290.












Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo, 10 Februari 2026, imetoa msaada wa mashuka 455 katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa ili kuboresha huduma za kimatibabu hospitalini hapo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka hiyo, lililofanyika mkoani humo tarehe 9 hadi 10 Februari 2026.

Kaimu Katibu Tawala mkoa wa Iringa, Bi. Nuru Siyovelwa, alipokea msaada huo kwa niaba ya Katibu Tawala Mkoa, na kueleza kuwa, mashuka yamekuwa hayatoshelezi katika hospitali za mkoa huo, hivyo ameishukuru EWURA kwa kuguswa kwani yatasaidia kutoa huduma bora kwa wananchi.

Naye Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. Alfred Mwakalebela, alieleza kuwa mashuka hayo yatapunguza changamoto iliyokuwepo ya upungufu wa mashuka, kwani kwa siku, kila mgonjwa anatakiwa kutumia mashuka 6, ilhali kwa sasa huduma hiyo haitoshelezi kwa kila mgonjwa.

Akiwasilisha msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Meneja wa EWURA Kanda ya Kati, Mha. Hawa Lweno, alisema kuwa EWURA itaendelea na utaratibu wa kutoa mchango kwa jamii katika masuala mbalimbali ikiwemo afya.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa, amekagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Wagonjwa Mahututi (ICU) katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji Handeni, mradi unaolenga kuondoa changamoto ya muda mrefu ya upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi.

Mhe. Kwagilwa amefanya ukaguzi huo leo Februari 10, 2026, wakati wa ziara yake ya kikazi hospitalini hapo, ambapo alipata fursa ya kujionea hatua mbalimbali za utekelezaji wa mradi huo pamoja na maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa.

Katika ziara hiyo, alipokea maelezo ya kitaalamu kutoka kwa wataalamu wa Halmashauri kuhusu maendeleo ya ujenzi, hali ya utekelezaji wa mradi pamoja na matarajio ya kukamilika kwake.

Ujenzi wa jengo hilo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuboresha miundombinu ya sekta ya afya, kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi pamoja na kuongeza uwezo wa hospitali kutoa huduma za dharura na kuokoa maisha ya wagonjwa.

Jengo hilo la kisasa linatarajiwa kuwa na mfumo wa hewa tiba (Oxygen) pamoja na vifaa maalum vya ufuatiliaji wa wagonjwa mahututi vitakavyowezesha uangalizi wa karibu wa hali zao.