📌Vijiji vyote 246 na Vitongoji 479 Kahama vimefikiwa

📌Shughuli za kiuchumi na kijamii zimeimarika

📌Naibu Waziri Salome awahakikishia vitongoji vyote vilivyobakia vitafikiwa

📌Awasisitiza kutunza na kulinda miundombinu ya umeme


Wananchi Kata za Wendele na Mwendakulima Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kubadilisha maisha yao kupitia mradi wa umeme uliotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

Wametoa shukrani hizo kwa Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba kwa nyakati tofauti leo Januari 10, 2026 wakati wa hafla ya kuwasha umeme kwenye kitongoji cha Majengo Kata ya Wendele na Kitongoji cha Chapulwa Kata ya Mwendakulima.

"Ni neema kubwa kupata umeme, tunaishukuru Serikali kwa kutufikishia umeme, maisha yetu yanabadilika," alisema Mariam Manyesha Mkazi wa Kitongoji cha Majengo.

Mara baada ya kuwasha umeme, Naibu Waziri Mhe. Salome alizungumza na wananchi na kuwaeleza namna ambavyo Serikali imejipanga kuhakikisha kila mwananchi anafikiwa ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi - CCM (2025-2030).

Mhe. Salome alibainisha kuwa Rais Samia ameelekeza ndani ya mwaka huu  wananchi 1,700,000 nchini wawe wameunganishwa na huduma ya umeme na kwamba tayari utekelezaji wa maelekezo hayo unaendelea. 

"Niwahakikishie tunaendelea kutekeleza maelekezo ya Rais, umeme ni kichocheo cha uchumi tumeshuhudia mabadiliko makubwa kwenye maeneo yaliyofikishiwa umeme na kipaumbele chetu ni kuwasha umeme," amesema Mhe. Salome.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mha. Jones Olotu akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, alieleza namna ambavyo REA imejipanga kufikisha umeme kwenye vitongoji vyote nchini.

Alisema REA inaendelea kutekeleza miradi ya kusambaza umeme vitongojini na kwamba hivi karibuni itasainiwa mikataba ya kusambaza umeme katika vitongoji 9009 kote nchini.














 


📌 Ni katika kuongeza tija ya upatikanaji wa umeme wa kutosha kwenye gridi ya Taifa

📌Asema huu ni muendelezo wa juhudi za Serikali kuhakikisha umeme unapatikana kwa wingi na kuwanufaisha wananchi

📌Akagua mradi wa upanuzi wa kituo cha kupoza umeme cha Ibadakuli na njia ya kusafirisha umeme Ibadakuli-Simiyu

📌Mradi wafikia zaidi ya asilimia 89, Majaribio ya baadhi ya mitambo yaanza rasmi

Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba, amesema mradi wa umemejua unaotekelezwa wilayani kishapu mkoani Shinyanga utaleta mapinduzi makubwa kwenye sekta ya nishati na kiuchumi kutokana na kutoa mchango mkubwa wa upatikanaji wa umeme wa uhakika utakaoingizwa kwenye gridi ya Taifa.

Mhe Salome ameyasema hayo leo tarehe 9 Januari,2026 akiwa mkoani Shinyanga mara baada ya kutembelea mradi wa umemejua wa kishapu pamoja na ule wa upanuzi wa kituo cha kupoza umeme cha  Ibadakuli sambamba na njia ya kusafirisha umeme kutoka Ibadakuli-Simiyu.

Amesema huu ni muendelezo wa jitihada za Serikali kupitia Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuhakikisha wananchi wananufaika na miradi inayotekelezwa na Serikali hususani ya umeme.

Kuhusu mradi wa upanuzi wa kituo cha kupoza umeme cha Ibadakuli na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme Mhe.Salome amesema umeme utakaozalishwa utawanufaisha wananchi wote wa Tanzania na kuleta mapinduzi kwani sekta ya umeme inawagusa mwananchi mmojammoja.

Akizungumzia maendeleo ya mradi huo, Meneja mradi wa Kishapu Mha.Emanuel Anderson amesema, mpaka sasa mradi umefikia zaidi ya asilimia 89 na unahusisha ujenzi wa paneli elfu 82 zenye uwezo wa Wati 605 kika moja zitakazozalisha megawati 50 za awali kwa awamu ya kwanza

Amesema mradi wa umemejua kishapu utakuwa wa manufaa makubwa kutokana na umuhimu wake kwenye utunzaji wa mazingira unaoepuka uzalishaji wa hewa ya ukaa na umeajiri Watanzania wengi kwa kipindi chote cha utekelezaji wake.

Akitoa tathmini ya ujenzi wa upanuzi wa kituo cha kupoza umeme Kaimu Mkurugenzi wa Miradi ya umeme TANESCO makao Makuu Mha. Frank Mashalo amesema miradi hiyo inahusisha uongezaji na uwekaji wa Transfoma yenye uwezo wa MVA 780 ili kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme kwa wananchi wa Mkoa wa Shinyanga na Mikoa jirani.

Aidha ameeleza kuwa miradi hiyo inatekelezwa na  Mkandarasi Sieyuan Electric kutoka China na Kalpataru kutoka India  anayetekeleza mradi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Shinyanga hadi Simiyu.

Awali kabla ya kuanza ziara yake Mhe Salome na ujumbe wake walipata fursa ya kumtembelea Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe.Mboni Mhita ambaye alimshukuru Mhe.Salome kwa kazi nzuri anayoifanya kutembelea miradi inayotekelezwa na Wizara ya nishati chini ya taasisi zake.

Miradi yote ya upanuzi wa kituo cha kupoza umeme njia ya kusafirisha umeme kutoka Shinyanga hadi Simiyu na ule wa umemejua wa kishapu imegharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa asilimia mia moja.










Na Mwandishi Wetu

Halmashauri ya Mji Handeni imetoa mafunzo maalum ya Mfumo wa Kidigitali wa Taarifa za Shule (School Information System – SIS) kwa Walimu Wakuu wa Shule za Msingi, Wakuu wa Shule za Sekondari pamoja na baadhi ya walimu, huku ikielezwa kuwa mfumo huo utasaidia kuongeza uwajibikaji kwa walimu na kudhibiti tatizo la utoro shuleni.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika Januari 9, 2026, mjini Handeni, Kaimu Afisa Elimu Idara ya Sekondari ambaye pia ni Afisa Elimu Vifaa na Takwimu wa Halmashauri ya Mji Handeni, Montan Mathew, amesema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo Walimu Wakuu wa Shule za Msingi, Wakuu wa Shule za Sekondari pamoja na mwalimu mmoja kutoka kila shule ili waweze kutumia mfumo huo kwa ufanisi.

Amesema mfumo wa SIS utatumika kukusanya, kuhifadhi na kuchambua taarifa zote muhimu za shule na kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI imeelekeza mfumo huo kuanza kutumika rasmi mara shule zitakapofunguliwa Januari 13, 2026.

“Walimu hawa wanapaswa kuanza kutumia mfumo huu mara moja ili kuweka taarifa za shule zao. Sisi kama Halmashauri ya Mji Handeni tuna wajibu wa kuhakikisha mfumo unatumika kama ilivyoelekezwa, na tutafanya ufuatiliaji wa mara kwa mara,” amesema Mathew.

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mshikamano, Beatrice Chaeka, amesema mfumo huo utasaidia kuwa na takwimu zenye mpangilio mzuri ikilinganishwa na awali walipokuwa wakitumia karatasi ambazo wakati mwingine zilipotea au kuharibika.

Ameongeza kuwa mfumo wa SIS utakuwa suluhisho la changamoto mbalimbali ikiwemo utoro wa wanafunzi na walimu.

“Katika mfumo huu, mwanafunzi anapowekewa alama ya hayupo mara tatu mfululizo, ujumbe hutumwa moja kwa moja kwa mzazi. Hii itawasaidia wazazi kufuatilia mahudhurio na maendeleo ya watoto wao, kwani kuna baadhi ya wanafunzi wanatoka nyumbani lakini hawafiki shuleni,” amesema Chaika.

Naye, Mkuu wa Shule ya Sekondari Kwenjugo, John Rajabu, amesema hapo awali kulikuwa na changamoto katika mipangilio ya taarifa za shule, lakini ujio wa mfumo wa SIS utaboresha usimamizi wa shule kwa ujumla.

Amesema mfumo huo utaongeza uwajibikaji kwa walimu katika ufundishaji pamoja na kuwahusisha wazazi kikamilifu katika kufuatilia maendeleo ya watoto wao kielimu.

Na Mwandishi Wetu, Handeni

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, ametoa wiki tatu kwa Halmashauri ya Mji Handeni kufanya maboresho mbalimbali katika Soko la Chogo, ikiwamo kurekebisha mageti ya kuingilia sokoni, ili kudhibiti tatizo la wizi wa bidhaa za wafanyabiashara.

Mhe. Nyamwese ametoa agizo hilo Januari 9, 2026, baada ya kufanya ziara ya kushtukiza katika soko hilo na kusikiliza changamoto zinazowakabili wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo.

Amesema dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wafanyabiashara wanafanya shughuli zao katika mazingira safi, salama na rafiki, ili waweze kutoa huduma bora kwa wananchi bila hofu ya usalama wa mali zao.

Aidha, katika ziara hiyo, Mhe. Nyamwese ameelekeza Halmashauri ya Mji Handeni kufanya marekebisho ya haraka ya mageti ya kuingilia sokoni hapo ili kudhibiti wizi wa mara kwa mara wa bidhaa za wafanyabiashara, jambo ambalo limekuwa likisababisha hasara kwao.

“Hali ya usafi katika lile dampo hairidhishi. Mrundikano wa taka uliopo unahatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara. Naiagiza Halmashauri kwa kushirikiana na viongozi wa soko kuangalia namna bora ya kuhakikisha taka zinaondolewa kwa haraka pindi zinapokusanywa,” ameagiza.

Naye, Afisa Biashara wa Halmashauri wa Mji Handeni, Paul Lusinde, ameahidi kufanyia kazi maagizo ya Mkuu huyo.

Na.Mwandishi Wetu-DAR ES SALAAM

Taasisi ya Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) imesema imeendelea kuhimiza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za nchi, ili kuhakikisha wananchi wananufaika na shughuli za uchimbaji na utafutaji.

Akizungumza jijini Dar es salam jana katika mahojiano maalum,Katibu Mtendaji wa TEITI, Bi. Mariam Mgaya, amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi 57 zinazotekeleza viwango vya kimataifa vya uwazi na uwajibikaji vinavyosimamiwa na EITI.

Amesema Tanzania ilijiunga na EITI mwaka 2009, hatua iliyolenga kuimarisha usimamizi bora wa rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia kwa maslahi ya maendeleo endelevu.

“Asasi hii inahamasisha wananchi kuelewa hatua zote za mnyororo wa thamani wa rasilimali hizi, ikiwemo ukusanyaji na ufuatiliaji wa mapato,” amesema Bi.Mgaya

Bi. Mgaya amebainisha kuwa utekelezaji wa majukumu ya TEITI unasimamiwa na Sheria ya TEITA ya mwaka 2015 ambayo imeainisha jukumu la kuboresha uwazi na uwajibikaji, hasa katika uvunaji wa rasilimali hizo.

Aidha, ameeleza kuwa mpaka sasa TEITI imechapisha ripoti 15 zinazolinganishwa kati ya malipo ya kampuni za madini, mafuta na gesi na mapato ya Serikali, kuanzia Julai 1, 2008 hadi Juni 30, 2023.

“Uwekaji wazi wa ripoti hizi ni sehemu ya utekelezaji wa viwango vya kimataifa ambapo nchi wanachama hutakiwa kufichua takwimu zote za mnyororo wa thamani,” ameongeza.

Hata hivyo Bi. Mgaya ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kuendelea kuiwezesha TEITI kifedha na kimiongozo ili kuhakikisha rasilimali za madini, mafuta na gesi zinaendelea kunufaisha wananchi na kukuza uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Uwazi na Uwajibikaji, Bw. Erick Ketagory, amesema TEITI inaendelea kutoa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa kuhusu taarifa zinazochapishwa kwenye ripoti hizo na namna zinavyoweza kutumika kuibua mijadala kuhusu manufaa ya rasilimali za nchi.

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Madini imeweka wazi huduma 20 muhimu zinazotakiwa kutolewa na kampuni zinazomilikiwa na Watanzania kwa asilimia 100 katika migodi, akitoa wito kwa Watanzania kuchangamkia fursa hizo.

Ketagory ameongeza kuwa TEITI ina wajibu wa kuhakikisha kampuni za uchimbaji na utafutaji zinatoa taarifa za shughuli zao kwa mujibu wa sheria, sambamba na kujenga uwezo wa wananchi kutumia takwimu hizo kuhoji na kufuatilia uwajibikaji.

“Ripoti za TEITI ni nyaraka muhimu sana kwa sababu zinaweka wazi malipo ya kodi na tozo mbalimbali zinazolipwa serikalini,” amesisitiza.

KITUO cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi ( PPP Centre), kimeendesha mafunzo kwa wafanyabiashara, wawekezaji na maafisa kutoka taasisi za kiserikali katika Halmashauri za Mkoa wa Tanga, kikielimisha juu ya kazi zinazofanywa na kituo hicho.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akizungumza na watumishi Umma wa Halmashauri ya Mji na babati vijijini wakati akiwa wa ziara yake ya kikazi Mkoani Manyara, tarehe 8 January, 2026.

Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) wakati wa kikao na watumishi hao, tarehe 8 Januari, 2026 katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Ayalagaya.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akisaini kitabu cha wageni baada ya kuwasili katika Ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Babati Mhe. Emmanuela Kaganda kwa ziara ya kikazi.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akiwasili katika Ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Babati wakati wa ziara yake ya kikazi Mkoani Manyara, tarehe 8 Januari, 2026.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (wa pili kulia) akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Babati Mhe. Emmanuela Kaganda baada ya kuwasili katika Ofisi hiyo iliyopo Mkoani Manyara, tarehe 8 Januari, 2026

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Babati Mhe. Emmanuela

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (watatu kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali mara baada ya kikao na watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, tarehe 8 Januari, 2026. Wa pili kutoka kulia ni Katibu Tawala Mkoa wa Manyara Bi. Maryam Muhaji.


Na Antonia Mbwambo - Manyara


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray amewataka watumishi wa Umma kutambua wajibu wao katika kutekeleza majukumu ya kila siku ili kufanya kazi kwa uwezo, maarifa na ujuzi walio nao kwa lengo la kuboresha huduma ikiwa ni mojawapo ya njia ya kuwatumikia wananchi kwa ustawi wa Taifa.

Mhe. Qwaray ameyasema hayo tarehe 8 Januari, 2026 Mkoani Manyara wakati akizungumza na watumishi wa umma ngazi ya Mkoa, Halmashauri ya Mji wa Babati na Hamashauri ya Wilaya ya Babati wakati alipokuwa katika ziara yake ya kikazi ambapo ni ziara ya kwanza Mkoani hapo tangu alipoteuliwa tarehe 17 Novemba, 2025 na Mhe Raisi wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Amesema Waajiri wote wa Taasisi za Umma lazima waweke kipaumbele katika kushugulikia changamoto zinazowakumba watumishi waliopo chini yao ikiwemo madai ya kupandishwa vyeo na malimbikizo ya mishahara ili kuongeza dhana ya uwajibikaji na kupunguza malalamiko ya watumishi hao.

“Ukiona mtumishi wa umma anakuja hadi Wizarani kwa ajili ya kufuatilia utatuzi wa changamoto zake za kiutumishi, ujue wewe kama msimamizi hujawajibika ipasavyo”,Mhe. Qwaray alisema.

Pia Mhe. Qwaray amewataka watumishi kuzingatia Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma ambazo zinaelekeza tabia na mienendo ambayo mtumishi anapaswa kuwa nayo anapokuwa anatoa huduma katika eneo lake la kazi.

“Mtumishi anapokuwa eneo la kazi hana budi kuachana na masuala binafsi na kujikita katika utoaji wa huduma kwa mwananchi ili kutumia vizuri rasilimali za Serikali katika kuhakikisha kila anayefika kupata huduma anaipata kwa wakati”, Mhe. Qwaray alisema.

Aidha amesisitiza matumizi ya mifumo iliyopo na inayotumika katika kushughulikia masuala mbalimbali ya kiutumishi ikiwemo maombi ya uhamisho na likizo ili kuendana na teknolojia iliyopo kwa lengo la kuwa na utendaji unaozingatia muda na usawa.

Mhe. Qwaray alihitimisha kwa kutoa wito kwa watumishi wa umma kuwa wazalendo na wenye kutanguliza Maslahi ya Taifa mbele katika kulinda na kuimarisha Amani ya nchi kwa kutoa huduma bora, kuzingatia maadili ya kazi na kuepuka vitendo vinavyoweza kuleta mgawanyiko katika jamii.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kushoto) akimsikiliza Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein (kulia) wakati akizungumza nae alipomtembelea kumjulia hali nyumbani kwake Kibele, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini, Zanzibar tarehe 08 Januari, 2026

Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohamed Gharib Bilal (kulia) akisisitiza jambo kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kushoto) wakati Waziri huyo alipomtembelea nyumbani kwake Mbweni, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini, Zanzibar tarehe 08 Januari, 2026.

Mama Sitti Mwinyi, mke wa Hayati Ali Hassan Mwinyi (kushoto) akifafanua jambo kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kulia) alipomtembelea nyumbani kwake Nyamanzi, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini, Zanzibar kumjulia hali ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake.

Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein (wa kwanza kulia) akisisitiza jambo kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (wa pili kutoka kulia) wakati Waziri huyo alipomtembelea nyumbani kwake Nyamanzi, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini, Zanzibar kumjulia hali ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kulia) akifurahia jambo na Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohamed Gharib Bilal (kushoto) baada ya kuzungumza nae nyumbani kwake Mbweni, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini, Zanzibar tarehe 08 Januari, 2026.

Mkurugenzi Msaidizi Utawala na Dawati la Viongozi wa Kitaifa Wastaafu, Bi. Nyasinde Mukono (wa kwanza kushoto) akizungumza jambo wakati Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) alipomtembelea Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohamed Gharib Bilal (hayupo pichani). Wengine ni wake wa Dkt. Bilal

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein (katikati) baada ya kuzungumza nae nyumbani kwake Nyamanzi, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini, Zanzibar alipomtembelea kumjulia hali ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Utawala na Dawati la Viongozi wa Kitaifa Wastaafu, Bi. Nyasinde Mukono.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (wa pili kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohamed Gharib Bilal (watatu kutoka kulia). Wengine ni Wakurugenzi na Maafisa kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kulia) akifurahia jambo na Mama Sitti Mwinyi, mke wa Hayati Ali Hassan Mwinyi (kushoto) baada ya kuzungumza nae alipomtembelea nyumbani kwake Nyamanzi, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini, Zanzibar kumjulia hali ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (wa tatu kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein (watatu kutoka kulia). Wengine ni Wakurugenzi na Maafisa kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (wa tatu kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mama Sitti Mwinyi (wa tatu kutoka kushoto), mke wa Hayati Ali Hassan Mwinyi wakati Waziri huyo alipomtembelea nyumbani kwake Nyamanzi, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini, Zanzibar kumjulia hali ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake. Wengine ni Wakurugenzi na Maafisa kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI.


Na. Veronica Mwafisi-Zanzibar


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amefikisha salamu za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Viongozi Wakuu wa Kitaifa Wastaafu ambaye ameahidi kuendelea kuwatunza Viongozi na Wenza wao kwa kuzingatia Katiba, Sheria na Kanuni zilizopo.

Salamu hizo zimefikishwa Januari 8, 2026 kwa nyakati tofauti alipomtembelea Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein nyumbani kwake Kibele Mkoa wa Kusini Unguja, Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohamed Gharib Bilal nyumbani kwake Mbweni, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini na Mwenza wa Hayati Ali Hassan Mwinyi-Mama Sitti Mwinyi nyumbani kwake Nyamanzi, Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini.

Mhe. Kikwete amesema, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ina jukumu la kutunza Viongozi Wakuu Wastaafu Kitaifa na Wenza wao, hivyo yuko tayari kuendelea kutekeleza jukumu hilo alilopewa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein amemshukuru Rais Mhe. Dkt. Samia kwa salaamu na kumpongeza Mhe. Kikwete kwa kupanga ziara ya kuwatembelea Viongozi Wakuu wa Kitaifa Wastaafu. Ziara hiyo inawapa faraja, heshima na inaonesha thamani ya mchango wao kwa taifa.

Aidha, Dkt. Shein ametumia fursa hiyo kutoa rai kwa watumishi wa umma kufanya kazi kwa kupendana, ushirikiano na kuzingatia mipaka ya kazi zao kwa kuwa watumishi hao wanamsaidia Rais ambaye anawajibika kwa wananchi.

Naye, Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mohamed Gharib Bilal ameishukuru Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora kwa kuwajali na kuwahudumia vyema kwa mujibu wa taratibu


Kwa upande wake, Mama Sitti Mwinyi amemshukuru Rais. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali wenza wa Viongozi Wastaafu na ameomba moyo huo uendelee.