Belem, Brazil

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor Seff amesema Serikali ya Tanzania imefanya jitihada kubwa ambayo imeweza kukamilisha miundombinu iliyoathiriwa na mabadiliko ya tabianchi katika maeneo mengi.

Mhandisi Seff ameeleza hayo wakati akiwasilisha mada kwenye Mkutano wa Mkutano wa 30 wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP 30) unaoendelea katika Jiji la  Belem nchini Brazil.

Aidha, katika wasilisho lake Mtendaji Mkuu huyo aliweza kuonesha Makala fupi ya namna Wakala huo ulivyofanikiwa kurudisha mawasiliano ya miundombinu ya barabara iliyoharibika kwa kujenga miundombinu himilivu ‘resilient’ kwa athari za mabadiliko ya tabianchi na zenye uwezo wa kupitika mwaka mzima.

Amesema kupitia programu ya uondoaji vikwazo katika barabara (bottleneck), wameweza kujenga madaraja na barabara na hivyo kufungua mawasiliano katika vijiji na hivyo kuweza kuwasaidia wananchi kusafirisha mazao yao pia kuwarahisishia kupata huduma za kijamii zikiwemo huduma za afya.

Akichangia kwenye mradi wa Scale unaosimamiwa na TAMISEMI, amesema  TARURA ni mdau mkubwa kwenye mradi huo.

 



▪️Agawa Photocopier Machines kubwa kwa kata 20


▪️Alenga kuwapunguzia michango ya mitihani wazazi wa Mtumba


▪️Maafisa Elimu Kata,Walimu wakuu na Wakuu wa Sekondari wote wapewa Kompyuta Mpakato(𝙇𝙖𝙥𝙩𝙤𝙥𝙨) 110


▪️Aahidi kuanzisha SACCOS ya Walimu Mtumba na kuchangia 20m


▪️Wadau wa Elimu wampongeza Rais Samia kwa miundombinu bora ya Shule Dodoma Jiji


*Mtumba,Dodoma*


Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mh. Anthony Mavunde leo ametimiza ahadi yake ya kugawa Photocopier Machines 20 kwa kila kata,Kompyuta Mpakato(𝙇𝙖𝙥𝙩𝙤𝙥𝙨) 110 kwa Maafisa Elimu Kata,Walimu wakuu na Wakuu wa Shule zote za Msingi na Sekondari za Jimbo la Mtumba.


Mh. Mavunde amesema dhamira kuu ya zoezi hilo ni kuboresha sekta ya elimu Jimbo la Mtumba kidijitali kwa kurahisisha ufundishaji na pia kupunguza adha ya michango ya mitihani kwa wazazi.


Na pia ametumia fursa hiyo kuwataka walimu wote wa Jimbo la Mtumba kuunda umoja wao na kutengeneza SACCOS ambayo ameahidi kuchangia kiasi cha *Tsh 20,000,000* kutunisha mfuko wa walimu wa Jimbo la Mtumba.


Akizungumza katika hafla hiyo,Afisa TEHAMA Mkuu Ndg. David Nyangaka amesema vifaa hivyo vimewekwa;


▪️Mitihani yote ya kitaifa kuanzia mwaka 1988-2024 kwa Kidato cha II, IV,VI

▪️Vitabu vya ziada na kiada

▪️Simulation za masomo ya Sayansi

▪️Video tutorials za masomo mbalimbali

▪️Notes za masomo yote.


Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji,Afisa Elimu Sekondari-Takwimu Ndg. Fred Mwakisambwe amempongeza Rais Dkt. Samia S. Hassan kwa maboresho makubwa ya sekta ya Elimu na hasa katika ujenzi wa Shule mpya na uboreshaji wa miundombinu ndani ya Jiji la Dodoma na hivyo kuwataka wadau wote kuvitunza na kuvitumia ipasavyo vifaa vilivyotolewa na Mbunge Mavunde kwa manufaa ya sekta ya Elimu.

 


Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro Dkt. Mussa Ali Mussa amewataka waratibu na watalaam kutoka katika Halmashauri zinazotekeleza Mradi wa Kukuza Usawa wa Kijinsia Tanzania Bara (PAMOJA) kuhakikisha wanakwenda kutafuta masoko ya bidhaa za walengwa wa mradi huo ili kuwawezesha kupata kipato kitakachoinua uchumi wao.

Dkt. Mussa ametoa wito huo mjini Morogogoro katika Ukumbi wa Chuo Kikuu cha Jordan, wakati akifunga mafunzo ya kuzijengea uelewa timu za utekelezaji wa mradi ili ziweze kutekeleza kikamilifu jukumu la kuimarisha fursa za kiuchumi kwa wanawake wa vijijini, kuzuia ukatili pamoja na kutoa huduma kwa manusura wa vitendo vya ukatili wa kijinsia.

“Kama ni kweli mmedhamiria kuwawezesha walengwa wa mradi wa PAMOJA kupiga hatua kimaendeleo, ni lazima kuwatafutia masoko ya bidhaa zao wanazozizalisha,” Dkt. Mussa amesisitiza.

Dkt. Mussa ameongeza kuwa, waratibu na watalaam hao wa mradi wa PAMOJA wanapaswa kuziongezea thamani shughuli za walengwa wa mradi na kuhakikisha wanafanya kazi kwa ushirikiano, ili kupanua wigo wa ajira kwa walengwa wengine pamoja na kuleta matokeo chanya kama ilivyokusudiwa na Serikali.

Mmoja wa waratibu wa mradi wa PAMOJA, ambaye ni Afisa Maendeleo Mkoa wa Geita Bi. Marth Kaloso ameahidi kuwa watahakikisha utekelezaji wa mradi unazingatia thamani ya fedha iliyotolewa, watatoa elimu ya ukuzaji wa miradi pamoja na kuhakikisha kuna ulinzi na usalama kwa watoto.

Kwa upande wake, Bw. Wanchoke Chichibela ambaye ni Mratibu wa Mradi wa Pamoja Mkoa wa Mara amesema kuwa wataenda kutoa elimu ya ujasiriamali, elimu ya kuweka akiba na kukopa ili mikopo itakayotolewa kupitia Mradi wa Pamoja iwawezeshe akina mama kujikomboa kiuchumi.

Kwa upande wake, Meneja Mahusiano Dhamana za Wateja kutoka Benki ya NMB Bi. Monica George amesema watawezesha ufunguaji wa akaunti ya mradi, ufunguaji wa akaunti za walengwa wa mradi, kutoa elimu ya fedha na mikopo ili walengwa waweze kufanya shughuli walizokusudia pamoja na kufanya marejesho kwa wakati ili fedha za mradi wa PAMOJA ziwasaidie pia walengwa wengine.

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais-TAMISEMI zimeweza kutoa mafunzo kwa waratibu na wataalam kutoka katika halmashauri  40 zinazonufaika na Mradi wa PAMOJA, waratibu na wataalam hao wanatoka katika Mikoa 10 ya Tanzania Bara ambayo ni Mwanza, Kagera, Mara, Shinyanga, Simiyu, Geita, Singida, Tabora, Rukwa na Arusha.









Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala amewataka washiriki wa Jukwaa la  Wadau wa Usimamizi wa Maafa kushiriki kikamilifu kutoa maoni kuhusu rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura wa kukabiliana na ukame, mafuriko na majanga mengine ili kuwa na mpango thabiti wa kuwezesha Serikali na wadau kuchukua hatua stahiki za kuzuia au kupunguza madhara, kujiandaa, kukabili na kurejesha hali kutokana na maafa yanayoweza kusababishwa na mwelekeo wa mvua za msimu.

Brigedia Jenerali Ndagala ameyasema hayo  wakati akifungua Mkutano wa  Jukwaa la  Wadau wa Usimamizi wa Maafa leo tarehe 14 Novemba,2025 Jijini Dodoma.

“Kama mtakumbuka tarehe 17 Oktoba, 2025 Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ilitoa taarifa ya mwelekeo wa mvua za msimu kwa kipindi cha mwezi Novemba 2025 hadi Aprili 2026, kufuatia utabiri huo, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, na Uratibu imeandaa Rasimu ya Mpango wa Dharura wa Kukabiliana na Ukame, Mafuriko na Majanga mengine” 

“Rasimu hii itawasilishwa katika jukwaa hili la wadau wa Usimamizi wa mafaa kwa ajili ya kujadili na kutoa maoni kwa kuzingatia utabiri wa msimu uliotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania” ameeleza Brigedia Jenerali Ndagala.

Aidha, amebainisha kuwa, jukwaa hilo ni muhimu ili kuweka mikakati ya pamoja kwa ajili ya maandalizi ya msimu, hivyo, kuwataka Wadau hao kushiriki kikamilifu na kutoa maoni  huku wakijielekeza kwenye athari tarajiwa na hatua zitakazochukuliwa.

Vilevile, Brigedia Jenerali Ndagala ameongeza kuwa pamoja na Rasimu ya Mpango wa dharura ulioandaliwa, Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa miongozo ya Uanzishaji na Uendeshaji wa Vituo vya Operesheni za dharura na Timu za Kukabiliana na dharua ngazi za Mikoa ambayo pia itawasilishwa  kwa ajili ya kupata maoni.














Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii, imeandaa Kongamano la 15 la Kimataifa la Kisayansi, litakalowakutanisha wanasayansi zaidi ya 500 litakalofanyika tarehe 3-5 Desemba 2025, katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC), hapa jijini Arusha.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo Dkt. Eblate Mjingo, ofisini kwake Jijini Arusha, alipokuwa akizungumza na Wanahabari. 

Dkt. Mjingo amebainisha  lengo la Kongamano hilo ni kurejesha matokeo ya tafiti zinazofanywa na TAWIRI pamoja na wadau wake kwa Serikali, Mamlaka za Uhifadhi, Wadau wa Uhifadhi, na watanzania wote. 

"Matokeo haya yatatumiwa na watunga sera na wafanya maamuzi kwa ajili ya kuhakikisha uhifadhi na utalii endelevu nchini Tanzania, na duniani kwa ujumla". Alisema Dkt. Mjingo.

Aidha ameongeza kuwa mada kuu ya kongamano hilo ni ‘Ubunifu katika uhifadhi wa wanyamapori na Utalii endelevu: Kutafuta mustakabali katika ulimwengu unaobadilika’ au “Innovations in Wildlife Conservation and Sustainable Tourism: Navigating the Future in a Changing World”.

Naye Mkurugenzi wa Utafiti TAWIRI Dkt. Julius Keyyu amesema kuwa, nchi zaidi ya 20 zinatarajiwa kushiriki kongamano hilo huku huku mawasilisho 248 kuwasilishwa pamoja na  kuwa na maonesho ya matokeo ya tafiti mbalimbali.

 


Imeelezwa kuwa Mkakati wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia ni dira muhimu ya kufanikisha malengo ya Taifa ya kuhakikisha wananchi  wanatumia nishati salama, rafiki wa mazingira na yenye gharama nafuu hadi kufikia mwaka 2034.

Hayo yameelezwa na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia Wizara ya Nishati, Mhandisi Banezeth Kabunduguru wakati wa kuhitimisha mafunzo kwa Maafisa Dawati na Waratibu wa Nishati Safi ya Kupikia wa Kanda ya Ziwa, yaliyofanyika jijini Mwanza tarehe 14 Novemba, 2025.

Mha. Kabunduguru amefafanua kuwa, mkakati huo umekusudiwa kuwa mwongozo wa kitaifa utakaowaongoza wadau wote katika kutoa elimu sahihi, iitayofika kwa urahisi kwa wananchi wa  makundi mbalimbali, ili kuongeza kasi ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kama vile gesi (LPG), umeme, biogas na majiko banifu.

“Kwa kutumia mkakati huu, tunatarajia kuongeza uelewa wa wananchi kwa kiwango kikubwa na hivyo kupunguza utegemezi wa nishati isiyosafi unaochangia uharibifu wa mazingira na madhara ya kiafya. Huu ni mkakati wa mabadiliko na ninyi Maafisa Dawati ni nguvu ya mabadiliko hayo”. Amesema Mha. Kabunduguru.

Ameongeza kuwa Serikali imejipanga kufanya kazi kwa karibu na Halmashauri, sekta binafsi, asasi za kiraia na wadau wa maendeleo kuhakikisha taarifa sahihi kuhusu nishati safi zinawafikia wananchi kwa wakati na kwa lugha inayowafaa.

Kwa upande wa Maafisa Dawati, washiriki wa mafunzo hayo akiwemo Dotto Masanja kutoka Karagwe na Christopher Kyamalesi kutoka Shinyanga, wameipongeza Serikali kwa kuandaa mkakati huo wakisema kuwa umetoa mwelekeo wa pamoja katika utoaji wa elimu kwa jamii.

Wameongeza kuwa, mkakati huo utawawezesha kuzungumza kwa sauti moja na kushirikiana kwa ufanisi na Viongozi wa vijiji, taasisi na wanajamii katika kuhamasisha matumizi ya nishati salama na kuondokana na matumizi ya kuni na mkaa.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Aron Kalondwa amewataka Maafisa Dawati kutumia vyema mafunzo waliyopata na kuendelea kuwafikia wananchi wote kwa ubunifu na kujituma.

“Nishati safi ya kupikia si suala la Wizara pekee. Ni ajenda ya maendeleo ya Taifa. Elimu mliyopata leo inaweza kubadilisha maisha ya wananchi wetu na kupunguza Athari  za kiafya na kimazingira”, Amesema Kalondwa.

 Elimu hiyo imetolewa na Wizara Nishati kwa kushirikiana na Taasisi zilizo chini ya Wizara ambazo ni Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambazo zilieleza namna zinavyotekeleza mkakati wa Taifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Aidha, Maafisa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira na Ofisi ya Waziri Mkuu walitoa mawasilisho.

 Mafunzo hayo yamehitimishwa leo Jijini Mwanza ambapo Mikoa iliyoshiriki mafunzo hayo ni Mwanza, Geita, Kigoma, Kagera, Shinyanga, Mara na Simiyu, ikiwa ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuongeza kasi ya uelimishaji kuhusu nishati safi ya kupikia katika mikoa yote nchini.











 


Mkurugenzi Msaidizi, Idara ya Serikali za Mitaa, Ofisi ya Rais-TAMISEMI Bw. Stephen Motambi amewataka waratibu na watalaam kutoka katika Halmashauri zinazotekeleza Mradi wa kukuza Usawa wa Kijinsia Tanzania Bara (PAMOJA) kwenda kutekeleza kikamilifu mradi huo, ili kutatua changamoto ya umaskini kwa wanawake, kuzuia ukatili wa kijinsia pamoja na kuwahudumia manusura wa vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Bw. Motambi ametoa wito huo mjini Morogogoro katika Ukumbi wa Chuo Kikuu cha Jordan, wakati akifungua mafunzo ya kuzijengea uelewa timu za utekelezaji wa mradi ili ziweze kutekeleza kikamilifu jukumu la kuimarisha fursa za kiuchumi kwa wanawake wa vijijini, kuzuia ukatili pamoja na kutoa huduma kwa manusura wa vitendo vya ukatili wa kijinsia.

“Nendeni mkatekeleze mradi wa PAMOJA kwa ufanisi ili mziwezeshe jamii kuondokana na changamoto za umaskini na ukatili wa kijinsia, itakuwa ni ajabu mpatiwe mafunzo alafu halmashauri zenu zidiwe na halmashauri ambazo waratibu wao hawajapatiwa mafunzo”, Bw. Motambi amesisitiza.

Aidha, Bw. Motambi amewataka waratibu na wataalam hao kuhakikisha wanazingatia mpango kazi ili kufikia malengo ya mradi, ikiwa ni pamoja na kuzingatia muda uwasilishaji wa taarifa za utekelezaji wa mradi.

Sanjali na hilo, amewataka waratibu na wataalam hao kujitoa kikamilifu katika kuwasaidia wanawake kujinasua katika lindi la umaskini ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyejitoa kutafuta fedha za utekelezaji wa mradi wa PAMOJA ili ziwanufaishe walengwa.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Jinsia Bw. Josiah Saoke amesema waratibu na wataalam hao wanaopatiwa mafunzo wanalo jukumu kubwa la kuhakikisha jamii wanayoenda kuisimamia inawezeshwa kiuchumi na inaondokana na vitendo vya ukatili wa kijinsia ambavyo vimekua ni kikwazo kwa wananchi kupiga hatua katika maendeleo.

Naye, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Afya, Ustawi wa Jamiii na Lishe wa Ofisi ya Rais-TAMISEMI Bi. Subisya Kabuje, ametoa wito kwa waratibu na wataalam hao kuhakikisha wanafanya kazi kwa ushirikiano na uadilifu pamoja na kuishirikisha jamii katika kuianisha matatizo yanayowakabili ili kuyapatia ufumbuzi, ikiwemo suala la ubainishaji wa maeneo ambayo vituo vya kulelea watoto mchana vinapaswa kujengwa.

Washiriki wa mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoandaliwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais-TAMISEMI wanatoka kwenye Mikoa 10 ya Tanzania Bara ikiwemo, Mwanza, Kagera, Mara, Shinyanga, Simiyu, Geita, Singida, Tabora, Rukwa na Arusha, ambapo jumla ya Halmashauri 40 zinanufaika na mradi huo wa PAMOJA kwa kipindi cha miaka 5 (2024/25 hadi 2028/29).














 


Mbunge wa Jimbo la Mtumba Anthony Mavunde leo ameshiriki na mamia ya wananchi wa Mtaa wa Maseya-Kata ya Hombolo Makulu kuanzisha ujenzi wa Zahanati katika mtaa huo ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa Uchaguzi Mkuu 2025.

“Nawashukuru wananchi wa Maseya kwa kumchagua Rais Samia,mimi na Diwani wa kata yetu kwa kura nyingi sana kwenye uchaguzi mkuu uliomalizika.

Kazi yetu sasa ni kufanya kazi na kutatua changamoto za wananchi,nawapongeza kwa kuitikia wito wa ujenzi wa zahanati yetu ambayo itasaidia kusogeza karibu huduma ya Afya kwa wananchi wetu.

Nitakabidhi matofali 2000 na saruji mifuko 100 ili kulifikisha juu jengo letu mpaka hatua ya upauaji,ni imani yangu kwamba serikali yetu sikivu itatuunga mkono ukamilishaji wa zahanati hii”Alisema Mavunde

Akitoa salamu za wananchi,Mwenyekiti wa Mtaa wa Maseya Ndg. Alexander Fwalu amemshukuru Rais Samia S. Hassan kwa utekelezaji wa haraka wa ahadi ya  usambazaji umeme pamoja na uchimbaji wa visima vya umwagiliaji kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ambapo wananchi wengi wakulima watanufaika na kupata maji ya uhakika kwa ajili kilimo cha umwagiliaji.

Aidha pia Mwenyekiti Fwalu amemshukuru Mbunge Mavunde kwa kutimiza ahadi yake ya kuanzisha ujenzi wa zahanati ya Maseya kwa uharaka na kuahidi kwamba wananchi wa Maseya watatoa ushirikiano wa kutosha kuhakikisha ujenzi wa zahanati hiyo inakamilika kwa wakati na hivyo kusogeza huduma ya Afya kwa wananchi.