📌Vijiji vyote 246 na Vitongoji 479 Kahama vimefikiwa
📌Shughuli za kiuchumi na kijamii zimeimarika
📌Naibu Waziri Salome awahakikishia vitongoji vyote vilivyobakia vitafikiwa
📌Awasisitiza kutunza na kulinda miundombinu ya umeme
Wananchi Kata za Wendele na Mwendakulima Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kubadilisha maisha yao kupitia mradi wa umeme uliotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Wametoa shukrani hizo kwa Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba kwa nyakati tofauti leo Januari 10, 2026 wakati wa hafla ya kuwasha umeme kwenye kitongoji cha Majengo Kata ya Wendele na Kitongoji cha Chapulwa Kata ya Mwendakulima.
"Ni neema kubwa kupata umeme, tunaishukuru Serikali kwa kutufikishia umeme, maisha yetu yanabadilika," alisema Mariam Manyesha Mkazi wa Kitongoji cha Majengo.
Mara baada ya kuwasha umeme, Naibu Waziri Mhe. Salome alizungumza na wananchi na kuwaeleza namna ambavyo Serikali imejipanga kuhakikisha kila mwananchi anafikiwa ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi - CCM (2025-2030).
Mhe. Salome alibainisha kuwa Rais Samia ameelekeza ndani ya mwaka huu wananchi 1,700,000 nchini wawe wameunganishwa na huduma ya umeme na kwamba tayari utekelezaji wa maelekezo hayo unaendelea.
"Niwahakikishie tunaendelea kutekeleza maelekezo ya Rais, umeme ni kichocheo cha uchumi tumeshuhudia mabadiliko makubwa kwenye maeneo yaliyofikishiwa umeme na kipaumbele chetu ni kuwasha umeme," amesema Mhe. Salome.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mha. Jones Olotu akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, alieleza namna ambavyo REA imejipanga kufikisha umeme kwenye vitongoji vyote nchini.
Alisema REA inaendelea kutekeleza miradi ya kusambaza umeme vitongojini na kwamba hivi karibuni itasainiwa mikataba ya kusambaza umeme katika vitongoji 9009 kote nchini.








































