Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, leo Juni 27, 2026 ameshiriki Mbio za Nishati Safi ya Kupikia (Clean Cooking Marathon) zilizofanyika katika Viwanja vya St. Peters Oysterbay jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kitaifa ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.
Akizungumza wakati wa kufungua mbio hizo, Mhe. Salome amesema pamoja na hatua nzuri iliyofikiwa, matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini bado yako katika kiwango cha asilimia 28.6, hali inayoonesha kuwa bado kuna kazi kubwa ya kufanya ili kufikia lengo la asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Amesema mbio hizo si mashindano ya kawaida ya kutafuta medali au vikombe, bali ni chachu ya mabadiliko ya kifikra na kijamii yanayolenga kulinda afya za wananchi, kuhifadhi mazingira na kuwawezesha wananchi kiuchumi, huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024–2034 unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Ameongeza kuwa mafanikio ya lengo hilo yanahitaji ushiriki wa Serikali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo na wananchi kwa ujumla, huku akisisitiza kuwa Tanzania ina kila sababu ya kuwa mfano wa kuigwa barani Afrika katika matumizi ya nishati safi ya kupikia iwapo ushirikiano utaendelea kuimarishwa.
Aidha, amebainisha kuwa tukio hilo ni sehemu ya kuthamini na kuunga mkono juhudi kubwa zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.
Mhe. Salome ameeleza kufurahishwa na mwitikio mkubwa wa wananchi wa Dar es Salaam katika marathon hiyo, pia amewashukuru Jumuiya ya Wafanyabiashara Wanawake Tanzania (TABWA) kwa kuandaa tukio hilo muhimu na wadau mbalimbali waliofanikisha tukio hilo wakiwemo Taasisi za Serikali, kampuni
za nishati safi ya kupikia, vyombo vya habari pamoja na wanamichezo walioshiriki mbio hizo.
Kupitia marathon hiyo ametoa wito kwa wananchi kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia, vijana kuwa mabalozi wa mabadiliko hayo kupitia teknolojia na mitandao ya kijamii, na pia amewahamasisha Mama Lishe na Baba Lishe kutumia nishati safi ili kulinda afya zao, afya za wateja wao na kupunguza gharama za uendeshaji.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, Wizara ya Nishati, Mjiolojia Mkuu, Bw. Ngereja Mgejwa, amesema marathoni hiyo ni moja ya mbinu zinazotumiwa kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia, kwani matumizi ya michezo yamekuwa njia bora ya kuwafikia wananchi wengi kwa wakati mmoja na kuwawezesha kuelewa faida za nishati safi katika kulinda afya, mazingira na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Naye, Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Wanawake Tanzania (TABWA), Bi. Noreen Mawalla, amewashukuru wadhamini, washiriki na wadau wote waliofanikisha Nishati Safi Expo 2026 pamoja na Clean Cooking Marathon, akisema lengo la kampeni hiyo ni kufikisha elimu na uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa wananchi katika mikoa mbalimbali nchini.
Amebainisha kuwa kampeni hiyo imefikia mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Kilimanjaro na Arusha.
Amesema kampeni inaendelea kuifikia mikoa mingine sita katika kila kanda ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata uelewa kuhusu manufaa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Washindi wa Mbio za Kitaifa za Nishati Safi ya Kupikia walizawadiwa mitungi ya gesi na majiko banifu kama sehemu ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akizungumza wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania waliopata fursa za ajira nje ya nchi iliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akizungumza wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania waliopata fursa za ajira nje ya nchi iliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam.

Sehemu ya Vijana walionufaika na fursa za ajira katika nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Saudi Arabia, Qatar, Kuwait, Bosnia na Ujerumani wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (hayupo pichani), wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania iliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam.

Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Ajira, Jane Sorogo akieleza jambo wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania waliopata fursa za ajira nje ya nchi iliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Masha Mshomba akizungumza wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania waliopata fursa za ajira nje ya nchi iliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam.

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mawakala Binafsi wa Huduma za Ajira, Rashid Millao akieleza jambo wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania waliopata fursa za ajira nje ya nchi iliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, akiwa pamoja na Viongozi wengine wakifuatilia igizo maalumu lililoandaliwa na Kikundi cha Maigizo cha COMHESWA kuhusu manufaa ya kufuata taratibu sahihi za kuomba nafasi za ajira nje ya nchi.
Na: OWM – KAM, Dar es Salaam Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kuongeza fursa za ajira ndani na nje ya nchi kwa Watanzania kupitia maboresho ya Sera, Sheria, Kanuni na Miongozo. Aidha, alibainisha kuwa kupitia juhudi za kidiplomasia za Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan zimeendelea kuzaa matunda, ambapo ndani ya kipindi kifupi cha awamu yake ya pili, vijana 8,408 wameweza kuunganishwa na fursa za ajira nje ya nchi, idadi ambayo ni kubwa kuwahi kufikiwa nchini. Mhe. Sangu amesema hayo wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania waliopata fursa za ajira nje ya nchi iliyofanyika Juni 25, 2026 katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam, amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua kuwa ajira ni nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, kwani huchangia kuongeza kipato cha wananchi, kupunguza umasikini, kuimarisha ustawi wa jamii na kukuza uchumi wa taifa. Amesema, Serikali pia inatambua ajira za nje ya nchi kama mkakati muhimu wa kupanua fursa za ajira kwa vijana wa Kitanzania, huku zikiwapa nafasi ya kupata kipato, kujenga taaluma, kuongeza ujuzi na uzoefu wa kazi pamoja na kujifunza teknolojia na mbinu bora zinazotumika katika masoko ya kimataifa. Vile vile, Waziri Sangu ametoa wito kwa vijana hao kutumia vyema kipato watakachopata kwa kujifunza elimu ya fedha na kushirikiana na taasisi za kifedha ili kujiwekea akiba kwa ajili ya maendeleo yao ya baadaye. Pia aliwahimiza kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kupitia mpango wa Hifadhi Scheme ili kujijengea usalama wa maisha baada. Kadhalika, amewahamasisha vijana hao kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania katika nchi wanazokwenda kufanya kazi, hivyo wanapaswa kuzingatia maadili, uadilifu, bidii katika kazi, kuheshimu sheria, tamaduni na mila za nchi hizo, huku wakidumisha utamaduni na maadili mema ya Kitanzania. Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Ajira, Jane Sorogo, amesema vijana hao wanaliopata nafasi za ajira katika nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Saudi Arabia, Qatar, Kuwait, Bosnia na Ujerumani wameweza kupatiwa mafunzo maalumu kabla ya kuondoka nchini ili kuwajengea uelewa kuhusu haki na wajibu wao, pamoja na kutambua mila na desturi za nchi wanazokwenda kufanya kazi. Akizungumza kwa niaba ya vijana wenzake, Husna Seif aliyepata fursa ya kwenda kufanya kazi nchini Saudi Arabia kama Mhudumu wa Usafi katika hoteli, ameishukuru Serikali kwa watafutia fursa za ajira na amesema ajira hizo zitawawezesha kupata ujuzi, kukua kiuchumi na kuboresha hali ya maisha ya familia zao. Naye kijana Ally Mwajei, ameshukuru Serikali kwa kumwezesha kupata fursa ya kwenda kufanya kazi nchini kama dereva teksi, amesema anafurahia kupata nafasi hiyo kwa kuwa itampa fursa ya kutimiza malengo yake ya maisha, kujifunza mazingira mapya pamoja na mila na tamaduni tofauti. Amesema anaamini uzoefu atakaoupata nje ya nchi utamjengea uwezo na kumuinua kimaendeleo. Pia amewashauri vijana wenzake wasiache kuomba nafasi za ajira kila zinapotangazwa, kwani zinaweza kuwa mwanzo wa mafanikio yao.
Serikali ya Tanzania imeingia makubaliano na kampuni mbili kutoka Japan kwa ajili ya kufungua fursa za soko la biashara ya kaboni kupitia mpango wa Uratibu wa Pamoja wa Mikopo (JCM), hatua inayolenga kuongeza mchango wa sekta binafsi katika kufanikisha dira ya taifa ya maendeleo ya mwaka 2050.
Akizungumza katika warsha ya kusaini Hati ya makubaliano hayo, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Dkt. Richard Mayungi, alisema serikali ina jukumu la kuhakikisha dira ya 2050 inafikiwa kupitia uwekezaji katika nishati safi, biashara ya kaboni na udhibiti wa taka.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara ya Kaboni (NCMC), Ngenda Kigaraba, alibainisha kuwa utoaji wa mikopo kwa pamoja utasaidia kulinda mazingira, kukuza biashara na kuongeza mapato ya Serikali.
Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya 3T kutoka Japan, Kan Shimizu, alisema Tanzania itanufaika kwa kiasi kikubwa kupitia ushirikiano huu, hususani katika sekta ya utunzaji wa mazingira na biashara ya kaboni
Makubaliano haya ya ushirikiano kati ya NCMC na kampuni za Japan yanalenga kuchochea mchango wa sekta binafsi katika kufanikisha malengo ya Dira ya taifa ya mwaka 2050, ambapo nguzo ya tatu ya Dira hiyo inasisitiza ukuaji wa uchumi wa Taifa na maendeleo endelevu yanayozingatia mazingira endelevu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amesema Bodi inatarajia kuongeza bidhaa nyingine tano katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuendelea kuwanufaisha watanzania katika sekta mbalimbali.
Akifungua kikao cha wadau cha kujadili na kupitisha Rasimu ya Mpango Mkakati wa WRRB wa miaka mitano (2026/27–2030/31) pamoja na kupokea maoni kuhusu maboresho ya Kanuni za Stakabadhi za Ghala, kilichofanyika Juni 26, 2026, mjini Morogoro, Bw. Bangu amesema mfumo huo umeendelea kukua kwa kasi na kuleta mafanikio makubwa.
Amesema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita mfumo huo ulikuwa unahusisha bidhaa mbili pekee, lakini kwa sasa unahusisha bidhaa 18, huku maandalizi yakiendelea kuongeza bidhaa nyingine tano ili kuimarisha uwazi, ushindani wa bei na kuongeza fursa za biashara ya mazao.
Bw. Bangu amebainisha kuwa pamoja na kuwanufaisha wakulima kwa kuwawezesha kuuza mazao yao kwa bei yenye ushindani, mfumo huo umechangia kuongeza mapato ya Serikali na kurahisisha Halmashauri kukusanya mapato yatokanayo na biashara ya mazao.
Aidha, amesema WRRB inaendelea na mazungumzo na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) pamoja na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB) ili kuwezesha biashara ya mazao kufanyika kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, hatua itakayoongeza ufanisi na uwazi katika biashara hiyo.
Ameongeza kuwa Bodi itaendelea kuhamasisha matumizi ya mfumo huo kwa kuanzisha njia bunifu zitakazowasaidia wakulima kuepuka kuuza mazao yao mara tu baada ya mavuno, wakati bei zikiwa chini.











