Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akipokea zawadi iliyotolewa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kwaajili ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa kinara wa utunzaji wa mazingira na matumizi ya nishati safi ya kupikia. Zawadi hiyo imetolewa wakati wa Mkutano wa 109 wa Mwaka wa Watayarishaji wa Vipindi vya Elimu kwa Umma uliyofanyika katika Ukumbi wa City Park mkoani Mbeya. Tarehe 21 Februari 2025. (anayekabidhi zawadi hiyo ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Palamagamba Kabudi)
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akihutubia wakati akifunga Mkutano wa 109 wa Mwaka wa Watayarishaji wa Vipindi vya Elimu kwa Umma uliyofanyika katika Ukumbi wa City Park mkoani Mbeya. Tarehe 21 Februari 2025.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akikabidhi majiko ya gesi kwa baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Mbeya yaliyotolewa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) wakati wa Mkutano wa 109 wa Mwaka wa Watayarishaji wa Vipindi vya Elimu kwa Umma uliyofanyika katika Ukumbi wa City Park mkoani Mbeya. Tarehe 21 Februari 2025.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Dkt. Venance Mwasse kuhusu mkaa mbadala wa Rafiki Briquettes wakati wa Mkutano wa 109 wa Mwaka wa Watayarishaji wa Vipindi vya Elimu kwa Umma uliyofanyika katika Ukumbi wa City Park mkoani Mbeya. Tarehe 21 Februari 2025.


Na Mwandishi Wetu, Mbeya 


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa waandaaji wa vipindi vya elimu kwa umma, kulenga zaidi kukuza uelewa na kuhamasisha jamii kushiriki shughuli za uhifadhi na usimamizi wa mazingira kwa kuwakumbusha suala hilo ni wajibu wa kila mmoja.
Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati akifunga Mkutano wa 109 wa Mwaka wa Watayarishaji wa Vipindi vya Elimu kwa Umma uliyofanyika katika Ukumbi wa City Park mkoani Mbeya. Amesema jukumu la kuhamasisha utunzaji wa mazingira na matumizi ya nishati safi ya kupikia ni kubwa na linahitaji nguvu ya pamoja inayojumuisha vyombo vya habari na wadau wote.
 
Amesisitiza umuhimu wa vyombo vya habari kuifanya agenda ya usafi na utunzaji wa mazingira pamoja na matumizi ya nishati safi kuwa sehemu muhimu ya programu zao badala ya kusubiri matukio, kama milipuko ya magonjwa, moto kwenye hifadhi za misitu au mafuriko.
 
Makamu wa Rais amewahimiza watayarishaji wa vipindi vya elimu kwa umma, kujizatiti kujifunza zaidi na kutoa elimu kwa usahihi kuhusu mabadiliko makubwa ya sayansi na teknolojia yanayoendelea duniani na hivyo kuwahamasisha watanzania kuchangamkia teknolojia mbalimbali zinazoibuka, kama vile matumizi ya Akili Mnemba, roboti na matumizi salama ya mitandao.
 
Hali kadhalika, Makamu wa Rais amewasihi watumiaji wa mitandao kuzingatia maadili ya sekta ya habari, sheria, pamoja na mila na desturi za Tanzania zinazolinda heshima na utu. Amesema wapo baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii wanaotoa taarifa bila kujali utu na heshima ya binadamu wengine kwa kutumia kudhalilisha na kuumiza wengine.
 
Pia ametoa rai kwa watayarishaji wote wa vipindi vya elimu kwa umma kuzingatia matumizi sanifu na sahihi ya lugha adhimu ya Kiswahili. Amewataka kuwa mabalozi wa Kiswahili sanifu na fasaha kwenye maeneo ya kazi na kuhakikisha wanakuwa vinara wa kupeleka Kiswahili sanifu na fasaha duniani na kuutangaza Utamaduni wa Mtanzania Kimataifa kupitia lugha na fasaha ya Kiswahili.
 
Makamu wa Rais amewaasa washiriki wa Mkutano huo kujiepusha na habari zitakazoibua taharuki na migogoro isiyo na tija kwa Taifa. Amewasihi kutoa taarifa zinazogusa maslahi ya wananchi ikiwemo elimu ya uraia na uchaguzi katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, Oktoba 2025 na hasa kuwakumbusha watanzania kuhusu umuhimu wa kutunza amani na utulivu katika nchi.
 
 
 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi amesema kutokana na juhudi zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita usikivu wa redio ya Taifa umeongezeka kutoka asilimia 54 mwaka 2016 hadi asilimia 87 mwaka 2024. Ametoa wito kwa wadau wa elimu kwa umma kutumia usikivu wa redio kutangaza shughuli mbalimbali zinazofanywa na serikali ikiwemo miradi ya kimkakati na miradi ya huduma za jamii hususani maeneo ya vijijini ili kuwapa wananchi uelewa wa kutosha namna serikali inavyowahudumia.
 
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania Dkt. Ayub Rioba amesema kauli mbiu ya mwaka huu ambayo ni “Tumia nishati safi na Tunza mazingira” inaenda sambamba na vipaumbele vinavyosimamiwa na Serikali. Amesema TBC imechukua suala la nishati safi na usafi wa mazingira kwa umuhimu mkubwa kwa kutambua suala hilo lina maslahi kwa Taifa.
 
Mkutano wa Wadau wa Elimu kwa Umma unaondaliwa na Shirika la Utangazaji Tanzania hufanyika kila mwaka kwa lengo la kuwajengea uwezo maafisa uhusiano na mawasiliano ili waweze kuwahabarisha wananchi kwa weledi zaidi kuhusu shughuli na miradi mbalimbali inayotekelezwa na serikali. Mkutano huo wa 109 umehudhuriwa na washiriki zaidi ya 280 wakiwemo watendaji wakuu wa taasisi, mashirika, wakala na idara za serikali pamoja na maafisa mahusiano na mawasiliano.


 Wadaia kugawa hongo kati ya Sh.5000 na Sh.50,000 ,Mbunge mwenyewe atoa majibu


Na Shomari Binda,Rorya

WAKATI joto la uchaguzi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), likianza kupanda kwa baadhi ya majimbo imeelezwa katika Jimbo la Rorya

mkoani Mara wajumbe waliokuwa wakipatiwa mafunzo ya utendaji ndani ya Chama hicho wamedaiwa kupewa fedha kati ya Sh.5000 hadi Sh.50,000 kama sehemu ya kuwashawishi wajumbe hao kuelekea uchaguzi mkuu.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopo zinaeleza kwamba juzi katika mafunzo ya watendaji ndani ya Chama Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Rorya, Ongujo Wakibara kwa kushirikiana na mbunge wa Jimbo hilo, Jafari Chege wanadaiwa kuyavuruga kwa kumwaga hongo kwa wajumbe wa mafunzo hayo.

Wakati wa mafunzo hayo inadaiwa Mbunge Chege na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Rorya, Ongujo Wakibara waliingilia katika semina ya makatibu wa matawi na kata iliyofanyika Februari 20, 2025 ambapo wanadaiwa kugawa posho kiasi cha Shilingi 50,000 kwa kila katibu aliyehudhuria mafunzo hayo.

Tuko hilo ambalo liliibua mjadala katika makundi sogozi ya ya WhatsApp ya CCM Mkoa wa Mara ambapo yameeleza utaratibu huo unakiuka maelekezo kutoka makao makuu ya CCM Taifa.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa mafunzo hayo ya watendaji yasiingiliwe na viongozi au wanasiasa kwa sababu ni mafunzo ya kiutendaji na chama kilisema kitagharamia kila kitu ikiwemo chakula na posho.

“Lengo la chama kufanya hivyo ilikuwa ni kuondoa urasimu wa wagombea kutumia nafasi hiyo kutoa rushwa kinyume chake Mwenyekiti wa chama na mgombea wake ambaye ndiye mbunge kwa sasa wamevamia ukumbi na kutoa posho hizo.

“Jambo hili halijawafurahisha hata wakufunzi haswa kauli za Mwenyekiti na Mbunge baada ya kuzuiwa na wakalazimisha kufanya kwa nguvu,” imesema sehemu ya taarifa katika makundi hayo sogezi ya WhatsApp

Hata kupitia Gazeti tando la George Marato Tv, imefatilia taarifa hiyo na kuzungumza na Mbunge wa Jimbo la Rorya, Jafar Chege kwa njia ya simu na kudai yupo msibani toka asubuhi na hajaudhuria kikao hicho na kushangazwa na taarifa hiyo.

Hata hivyo Chege alikiri kuiona taarifa hiyo kwenye makundi sogozi ya CCM lakini hajui lengo lake.”Nimeshangazwa na taarifa hiyo,nipo msibani na nimeambiwa kikao hicho kimeenda vizuri na kimalizika salama hizo taarifa ni za uongo,” amejibu Chege alipokuwa akielezea taarifa hiyo.

Alipotafutwa Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Rorya, Ongujo Wakibara hakupatikana kwenye simu yake ya mkono hivyo jitihada za kumtafuta kuzungumzia jambo hili zinaendelea ili kupata ukweli wa madai ya taarifa hizo.

Hata hivyo pamoja na hali Mwenyekiti huyo wa CCM anadaiwa kuwa amekuwa akiwasimamisha viongozi hovyo hovyo na hivi karibuni katika Kata za Mkoma, Kirogo, Kinyenche, Nyathorogo, Goribe na Tai aliwasimamisha vongozi wa matawi bila kuihusisha kamati ya siasa.

Wakati kwa Mbunge Chege amekuwa akizunguka katika baadhi ya kata na matawi na kukutana na wajumbe moja kwa moja na kugawa fedha kiasi cha Shilingi 5,000 hadi Sh.50,000 kulingana na uwezo na hadhi ya mjumbe.



 Na. Farida Ramadhani na Joseph Mahumi, WF, Dodoma


Washirika wa Maendeleo nchini wameipongeza Serikali ya Tanzania kwa maendeleo mbalimbali hususan katika maeneo ya ukuaji wa uchumi, maendeleo ya rasilimali watu, mifumo ya chakula na miundombinu. 

Pongezi hizo zimetolewa jijini Dodoma katika Mkutano wa Majadiliano ya Kimkakati Ngazi ya Wataalamu kati ya Serikali (Makatibu Wakuu SMT na SMZ) na Washirika wa Maendeleo (Heads of Development Cooperation) ambayo yanalenga kujadili mbinu za kuongeza ustahimilivu wa kiuchumi na maendeleo jumuishi katika kipindi cha mabadiliko na changamoto za kiuchumia katika kipindi kisichotabirika.

Mwenyekiti Mwenza anayewakilisha Washirika wa Maendeleo, Bi. Sisan Ngongi Namondo alisema kuwa Tanzania imepiga hatua katika sekta za afya, miundombinu, na mageuzi ya sera, huku akibainisha maeneo matatu muhimu ambayo yatajadiliwa katika mkutanao huo kuwa ni utulivu wa uchumi wa taifa, ukuaji shirikishi, na uthabiti wa mabadiliko ya tabianchi. 

Bi. Namondo alisema kuwa Tanzania imeonyesha uimara mkubwa wa kiuchumi na usimamizi thabiti wa sera za fedha, lakini maendeleo ya haraka yanahitaji ushiriki mkubwa wa sekta binafsi, mageuzi ya kifedha, na mikakati madhubuti ya kupunguza umasikini.

Kwenye eneo la mabadiliko ya tabianchi na nishati, Mwenyekiti Mwenza huyo alisema kuwa juhudi za Tanzania kama vile Mkakati wa Kitaifa wa Nishati Safi ya Kupikia na Mkakati wa Nishati Jadidifu ni hatua muhimu, lakini uwekezaji zaidi unahitajika ili kuimarisha ujumuishaji wa nishati mbadala na kuongeza uthabiti wa mabadiliko ya tabianchi.

Bi. Sisan Ngongi Namondo aliahidi kuwa Washirka wa Maendeleo wataendelea kushirikiana na Tanzania katika kuhakikisha nchi inapata maendeleo zaidi ya kiuchumi na kijamii.

Akizungumza wakati wa kufungua mkutano huo, kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu Elmaamry Mwamba ambaye ni Mwenyekiti wa Mkutano huo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango -Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil, alisema mafanikio hayo yanatokana na kuimarika kwa ushirikiano kati ya Serikali na Washirika la Maendeleo.

Alisema katika maendeleo ya rasilimali watu, Serikali imeandaa Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana (2007), ili kuendana na mabadiliko yanayoendelea ya kiuchumi, kiteknolojia, kisiasa na kijamii yanayotokea ndani na nje ya nchi. 

“Wizara yenye dhamana ya Maendeleo ya Vijana imeandaa Mkakati wa Utekelezaji wa Sera kwa kipindi cha miaka kumi (2024 – 2034) ikiwa ni nyenzo muhimu ya kufikia malengo yaliyoainishwa katika sera hiyo; inayolenga kukuza jamii ya vijana walio na ujuzi, ubunifu, ujuzi na uwezo wa kutumia teknolojia ipasavyo, waliowezeshwa na wanaolelewa ipasavyo, wazalendo, na wanaowajibika”, alibainisha Dkt. Akil..

Aliongeza kuwa Serikali inaendelea kutekeleza Sera ya Elimu na Mafunzo (2014) ambayo inasisitiza ujumuishaji wa elimu ya ufundi na ufundi katika mfumo rasmi wa elimu na kukuza sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM) ili kukidhi mahitaji ya viwanda, na Sera ya Taifa ya Ajira (2008) ambayo inalenga katika kutengeneza ajira kwa vijana na kuboresha uwezo wa kuajiriwa kupitia mafunzo ya ufundi stadi na kuhamasisha uundaji wa ajira katika sekta binafsi.

Dkt. Akil alisisitiza juu ya uimarishaji wa mifumo ya chakula, Serikali imeboresha kilimo kupitia Teknolojia za Kilimo Hai (Climate-Smart Agriculture), ikiwemo matumizi ya mbegu zinazostahimili ukame, teknolojia za umwagiliaji pamoja na mradi wa Building a Better Tomorrow (BBT) ambao umewawezesha vijana kumiliki mashamba kwa kilimo cha kisasa.

“Juhudi hizi zinalenga kuongeza uzalishaji wa kilimo kupitia mbinu za kisasa za kilimo cha biashara, huku ikipunguza utegemezi wa mazao kutoka nje ya nchi na kukuza usalama wa chakula”, alisema Mwenyekiti, Dkt. Akil.

Kwenye suala la miundombinu, alisema Serikali imeendelea kuboresha miundombinu kupitia mradi wa Reli ya Kisasa (SGR), upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam na upanuzi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano (NICTBB), ambao sasa umeunganisha nchi saba jirani.

Naye, Kaimu Mtendaji Mkuu wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Mursali Milanzi alisema katika mkutano huo, Tume imeelezea muelekeo wa Dira mpya ya maendeleo kwa kuwa sasa wapo katika hatua za mwisho za kutekeleza dira iliyopo.

Alisema pia wameelezea kuhusu miradi ya kipaumbele ambayo itatekelezwa kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo.

Mkutano huo ulihudhuriwa na  Washirika mbalimbali wa Maendeleo kutoka nchi mbalimbali, Asasi zisizo za Kiserikali, pamoja na viongozi waandamizi wa Serikali kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.

Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), kimesaini mkataba na kampuni ya kandarasi ya Arm-Strong International Ltd ya jijini Mwanza kuanza ujenzi wa maabara tatu za sayansi katika kipindi cha miezi nane ikiwa ni muendelezo wa utekelezaji wa Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) katika chuo hiki.


Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), Dkt. Anthony Diallo, amezihimiza taasisi za kilimo nchini kubadili mbinu za utendaji kwa kuachana na mazoea na badala yake kuimarisha matumizi ya utaalamu katika kuwawezesha wakulima kuongeza tija na kuendesha kilimo cha biashara.

Dkt. Diallo alitoa wito huo tarehe 19 Februari 2025, katika siku ya pili ya ziara ya Bodi na Menejimenti ya TFRA walipotembelea taasisi mbalimbali za Wizara ya Kilimo, ikiwemo Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI – Maruku), Kituo cha Uhaulishaji Teknolojia za Kilimo (MATI – Maruku), na Taasisi ya Utafiti wa Kahawa (TaCRI). Ziara hiyo inalenga kuelewa majukumu ya taasisi hizo na kuimarisha ushirikiano katika kuhamasisha matumizi sahihi ya mbolea miongoni mwa wakulima.

Akizungumza katika ziara hiyo, Dkt. Diallo amesisitiza kuwa ili kufanikisha malengo ya serikali kupitia kauli mbiu ya Agenda 10/30: Kilimo ni Biashara, wataalamu wa kilimo wanapaswa kuongeza jitihada katika kutoa elimu na ushauri kwa wakulima ili kubadili mitazamo hasi kuhusu matumizi ya mbolea na kuchochea uzalishaji wenye tija kwa ajili ya soko la ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TFRA, Bw. Joel Laurent, ameeleza kuwa, ziara hiyo imetoa fursa kwa TFRA kufahamu kwa undani zaidi shughuli za taasisi hizo na kutathmini maeneo ya ushirikiano ili kuongeza ufanisi katika uhamasishaji wa matumizi sahihi ya mbolea. 

Amebainisha kuwa TFRA inajumuisha wakufunzi wa MATI katika programu zake za mafunzo kwa wakulima, ili kuwawezesha wakufunzi hao kuendeleza utoaji wa elimu kwa wakulima kwa ufanisi pindi mafunzo yanapohitajika.

Katika wasilisho lake, Meneja wa TARI – Maruku, Dkt. Mpoki Shimwela, ameeleza kuwa, matumizi duni ya mbolea katika kilimo cha migomba yamesababisha upungufu wa virutubisho kwenye udongo, hali inayochangia kuzalisha ndizi kilo chache na zisizo na ubora unaokidhi mahitaji ya masoko ya kimataifa

Alibainisha kuwa, TARI imeanzisha miradi mbalimbali ya kuhamasisha matumizi ya mbolea, ikiwa ni pamoja na vipimo vya afya ya udongo kwa wakulima ili kuwasaidia kuelewa mahitaji halisi ya udongo wao.

Shaban Mkulila, mkulima wa kahawa kutoka Kijiji cha Maruku, baada ya kutembelewa na Bodi na menejimenti ya TFRA shambani kwake Maruku ameeleza kuwa, tangu aanze kutumia mbolea katika kilimo cha kahawa mwaka 2019, ameshuhudia ongezeko kubwa la mavuno. 

Ameishauri TFRA kuanzisha mashamba darasa ili wakulima wapate mafunzo kwa vitendo na kuwasaidia kuondokana na dhana potofu kwamba mbolea inaharibu udongo.

Naye, Bw. Siraji Amri, mkulima wa kahawa kutoka Kijiji cha Mulata, Kata ya Katerero, amethibitisha kuwa matumizi ya mbolea za viwandani yamemwezesha kuongeza uzalishaji hadi kufikia wastani wa kilo sita za kahawa kwa kila mti mmoja, hali inayothibitisha mchango wa mbolea katika kuimarisha tija ya kilimo.

Ziara hiyo imetoa mwangaza kuhusu umuhimu wa ushirikiano kati ya TFRA na taasisi za kilimo katika kuhakikisha wakulima wanapata elimu sahihi kuhusu matumizi ya mbolea kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na kufanikisha azma ya kilimo biashara nchini.

Oparesheni maalumu ya kuwadhibiti wanyamapori wakali na waharibifu aina ya fisi waliokuwa wanaleta taharuki na madhara Kwa jamii inayoendelea Mkoani Simiyu imeonesha mafanikio makubwa baada ya fisi 16 kuvunwa ikiwa ni hatua muhimu iliyochukuliwa na Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii ya kuhakikisha usalama na utulivu Kwa wananchi vinarejea.

Hayo yamesemwa leo Februari 19, 2025 na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Kenani Kihongosi alipokuwa akiongea na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari.

Mhe. Kihongosi amesema kufuatia changamoto hiyo,  Serikali ilichukua jukumu kubwa la kuhakikisha inalinda wananchi wake ikiwemo kuanzisha oparesheni maalumu inayohusisha Jeshi la Uhifadhi Kwa Taasisi za TAWA, TANAPA na TFS Kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi pamoja na wananchi, oparesheni inayotajwa kuanza  Januari 25, 2025.

"Tarehe 20/12/2024 baada ya fisi kuvamia wananchi Serikali ilichukua hatua kubwa ya kushirikisha vyombo vyake (TAWA na Jeshi la Polisi) na kuanza Oparesheni, lakini ilipofika tarehe 25/01/2025 oparesheni ya mkoa mzima ilifanyika Kwa ukubwa kuhakikisha inakabiliana na fisi wote waliokuwa wanasumbua wananchi" amesema Mhe. Kihongosi 

"Na Kwa taarifa njema ni kwamba tangu kuanza Kwa oparesheni hii vyombo vyetu vimeweza kudhibiti na kuua fisi 16 na ndio maana kwasasa mnaweza kuona hali imetulia" ameongeza Mkuu huyo wa mkoa wa Simiyu.

Aidha Mhe. Kihongosi ameendelea kuwatoa hofu wananchi wa mkoa huo akisisitiza kuwa hali ni shwari na kuwataka waendelee na shughuli zao kama kawaida huku akikemea vikali imani za kishirikina kuhusiana na mnyamapori aina ya fisi kwa baadhi ya wakazi wa Simiyu na kuwataka wote wanaofuga wanyamapori pori hao kuacha mara moja kwani ni kosa kisheria kumiliki nyara za Serikali bila Kibali.

Kwa upande wake Afisa Habari wa TAWA Beatus Maganja amewaomba wananchi wa Mkoa wa Simiyu hususani wilaya ya Itilima kuacha tabia ya kutembea  nyakati za usiku na alfajiri kwani ni nyakati ambazo wanyama fisi huwa katika mawindo yao.

Vilevile amewasisitiza wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Maofisa wa Jeshi la Uhifadhi waliopo uwandani ili kuongeza ufanisi wa zoezi hilo huku akiwahakikishia  kuwa Serikali imedhamiria kulinda wananchi wake na kwamba Askari wapo uwandani wanafanya Kazi usiku na mchana kuwahakikishia usalama wao.

Kwa upande wao wananchi wa Simiyu hususani wilaya ya Itilima wameshukuru Kwa juhudi zinazofanywa na Serikali katika kukabiliana na changamoto hiyo, wakisema kuwa hatua hiyo imeweza kuwarejeshea matumaini, utulivu na amani.

"Kwakweli tulikuwa tunasumbuliwa sana na haya mafisi ambayo yalikuwa yanauma watu, baada ya Serikali kusikia ikaweka ulinzi, kwakweli imetufanyia vizuri sana mpaka leo hatujawasikia tena tangu Askari waanze kuwashambulia hao fisi, mpaka leo hii tuna utulivu sana kwakweli tunashukuru sana"   amesema Mozo Mabula  mkazi wa Kijiji cha Mwamunhu kilichopo wilaya ya Itilima.

 

▪️Yatenga Trilioni 3 kwa ajili ya miradi vya kuongeza thamani madini

▪️Viwanda vya uongezaji thamani madini kupewa kipaumbele

▪️Waziri Mavunde asisitiza madini kuongezwa thamani ndani ya nchi

▪️Serikali yatenga eneo maalum Kahama-Shinyanga

📍 Dar es salaam


Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mh.Lord Collins amevutiwa na mpango wa nchi ya Tanzania kuandaa mkakati maalum wa uongezaji thamani madini nchini Tanzania na kuahidi kwamba Uingereza itatoa ushirikiano katika kusaidia eneo la uongezaji thamani madini hayo ndani ya nchi.

Hayo yamesemwa leo wakati wa kikao kati ya Mh. Lord Collins na Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde kilichofanyika leo Jijini Dar es salaam.

“Tanzania na Uingereza zina ushirikiano wa muda mrefu katika maeneo mengi ya kiuchumi ikiwemo sekta ya Madini.

Nimevutiwa na mkakati wa Tanzania wa kuongeza thamani ndani ya nchi, mkakati ambao Uingereza tunauunga mkono na tupo tayari kuwezesha utekelezaji wake kupitia Mradi wa “Manufacturing Africa“ ambapo ya pauni 2.1 bilioni zimetengwa kusaidia nchi 6 za Afrika,ikiwemo Tanzania,kutengeneza bidhaa za kati na za mwisho kupitia madini“ Alisema Lord Collins

Akizungumza katika Kikao hicho,Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde amesema Tanzania inayo mkakati wake maalum wa uongezwaji thamani madini ili kuongeza manufaa makubwa zaidi kwa nchi kupitia sekta ya madini,ambapo kwa sasa madini yanapaswa kuchakatwa na kuongezwa thamani nchini.

Serikali imetenga eneo maalum la ujenzi wa viwanda vyakuongeza thamani wilayani Kahama,Mkoani Shinyanga kwa lengo la kuvutia uwekezaji katika eneo hili.

“Mradi wa “Manufacturing Africa“ utasaidia kufanikisha azma ya Tanzania kwa kuwezesha uanzishwaji wa viwanda vya kuchakata,kusafisha na kutengeneza bidhaa zitokanazo na madini“ Alisema Mavunde

Kikao hicho pia kimehudhuriwa na Balozi wa Tanzania-Uingereza Mh. Mbelwa Kairuki na Balozi wa Uingereza-Tanzania Mh. Marianne Young





Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi,Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete, ameitaka  Tume ya Usuluhishi na Uamuzi kuwaTaasisi ya kimkakati katika utatuzi wa migogoro ya kikazi nchini ikiwa na lengo la kuchochea ukuaji wa kiuchumi na kuhakikisha mahala pa kazi panakuwa na amani ili kuwafanya  wafanyakazi na waajiri watumie muda mwingi kufanya uzalishaji Wenye Tija.

Ameyasema hayo wakati akifungua kikao kazi cha Tathmini ya Utendaji Kazi na mafunzo kwa watumishi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi Tanzania bara, kilichofanyika Leo tarehe 19 Februari, 2025 Mkoani Morogoro.

Aidha, Mhe. Kikwete ameitaka Tume hiyo kushughulikia migogoro kwa haraka, ufanisi na weledi ili kuweza kutimiza matarajio ya wadaawa na wadau ambao wengi wao ni wawekezaji, hivyo kusaidia kukuza Uchumi wa nchi.

“Serikali iliongeza bajeti ya Tume kiasi cha zaidi ya Shilingi Milioni mia tisa (900,000,000+) bila shaka mmeona ongezeko hilo limeleta mabadiliko siyo tu kwenye maslahi ya wafanyakazi lakini pia kuiwezesha Tume kutekeleza majukumu yake ya msingi” amesema Mhe. Kikwete

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Dkt. Yose Mlyambina amewakumbusha wasuluhishi na waamuzi kutilia mkazo suala la matumizi ya mfumo wa kielekroniki na hususani kuangalia namna bora ya kupokea  vielelezo ili kuwasilisha jalada kamilifu pindi litakapoitishwa mahakamani.

Awali akiongea katika kikao hicho Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) Usekelege Mpulla amemhakikishia Waziri  Kikwete kuwa Tume hiyo ya itaendelea kuwa Taasisi ya kimkakati katika kukuza uchumi nchini kwa kuimarisha utatuzi wa migogoro ya kikazi nchini ili kuweza  kuhakikisha mahala pa kazi panakuwa na amani na kuwafanya  wafanyakazi na waajiri watumie muda mwingi kufanya uzalishaji Wenye Tija.








Kaimu katibu tawala wa Mkoa wa Lindi Natalis Linuma akizungumza na wataalamu mbili mbali katika kikao kazi cha mafunzo kuelekea kwenye uzinduzi wa kampeni ya msaada wa kisheria ya Mama Samia legal Aid kikao kilichokufanya Ruangwa wilayani lindi na kuhudhuriwa na wataalamu kutoka katika Halmashauri zote za Mkoa wa Lindi
Wataalamu mbili mbali katika kikao kazi cha mafunzo kuelekea kwenye uzinduzi wa kampeni ya msaada wa kisheria ya Mama Samia legal Aid kikao kilichokufanya Ruangwa wilayani lindi na kuhudhuriwa na wataalamu kutoka katika Halmashauri zote za Mkoa wa Lindi
Wataalamu mbili mbali katika kikao kazi cha mafunzo kuelekea kwenye uzinduzi wa kampeni ya msaada wa kisheria ya Mama Samia legal Aid kikao kilichokufanya Ruangwa wilayani lindi na kuhudhuriwa na wataalamu kutoka katika Halmashauri zote za Mkoa wa Lindi


Mama Samia legal Aid yafanya mafunzo ya kikao kazi cha usaidizi kwa wataalamu na watakao shiriki katika kutoa huduma ya msaada wa kisheria kutoka wilaya zote za Mkoa wa Lindi ambapo kesho ufunguzi rasmi wa kampeni  katika Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa Mkoani Lindi Na kufunguliwa na Waziri Mkuu wa jamuhuri ya Tanzania.


Tayari mikoa 17 ya Tanzania bara tayari imesha fanyaka uzinduzi wa kampeni na Leo tarehe 18 Februari usinduzi unafanyika katika Mkoa wa Mwanza n lengo Hadi kufikia mwisho wa mwezi huu iwetayari wamesha fikia mikoa 22.


Natalis Linuma kwa niaba ya katibu tawala wa Mkoa wa Lindi Amesema mafunzo hayo ya kikao kazi Amesema anamshukuru sana Rais Samia kwa kutoa kuweza kutoa malekezo kwa wizaran ya katiba na sheria kwakuhakikisha kunakua na program ya kutoa elimu kwa wanainchi kwa kuweza kupata msaada wa kisheria katika kutatua changamoto mbali mbali za kisheria.


Aitha Linuma ametoa wito kwa wataalamu hao waweze kuelewa namna ya kuweza kuwasaidia na  kuwaelewesha wanainchi kwenye maeneo watakayo kwendaa.kwasababu wanainchi hao wanahitaji haki za binaadam na utawala Bora.


Pia Linuma amewataka wataalamu mufunzo hayo yakawe chachu na mwangaza Ili kwenda kupunguza migogoro kwenye maeneo mbali mbali ya Mkoa wa Lindi.


"Kwa hawa ambao wanapata mafunzo leo waweze kujifunza na kuelewa jinsi ya kuwaelewesha na kuwasaidia wanainchi kule wanakoenda Mkoa wetu wa Lindi ni miongoni mwa mikoa ambayo tunazo changamoto za kawaida na kisheria katika sehemu mbali mbali, kuhusu migogoro ya ardhi, Migogoro ya mirathi pamoja na maswala ya ndoa."


Nae Ester Msambazi Mkurugenzi huduma za msaada wa kisheria wizaran ya katiba na sheria Amesema kwa kushirikiana na wadau wanatekeleza kampeni yenyejina la mama Samia legal Aid kampeni ambayo inatekelezwa katka ngazi ya kijiji n jamii kwa lengo kuwafikia wanainchi walio maeneo ya pembezoni ambao hawapati huduma za kisheria.


Aitha Ester Msambazi Amesema kampeni imetokana na ombwe kubwa kwakua wanainchi wengi hawana uelewa juu ya msaada wa kisheria hata wanapokua wamepata changamoto wanakua hawajui wapi kwa kukimbilia na kutatua changamoto zao.


"Lengo la kwanza kabisaa tunataka wanainchi wapate  uelewa kuhusuana na masuala ya kisheria na upatikanaji wa haki za kwa wanainchi kwa kupitia huduma za msaada wa kisheria mwanainchi yeyote ambae anahitaji msaada wa kisheria na anashindwa kwenda mahakamani kwasababutu hana muwakilishi Wala wakili basi atapata huduma hizo kwa kupitia msaada wa kisheria"Amesema Ester Msambazi 


Andrew Munisi afisa aridhi mteule manispaa ya Lindi amesema kampeni hizo za msaada wa huduma za kisheria ya mama Samia itaenda kuondoa changamoto za kisheria pamoja na kutoa elimu kwa wananchi.



"Tunamatarajiao makubwa kama idara ya aridhi kunachangamoto nyingi sana kama migogoro ya wakulima na wafugaji,migogoro ya kifamilia kama watu wa aridhi tunamatarajiao ya kutoa msaada wa kisheria sekta ya aridhi"amesema Munisi


Munisi ameongeza kwakusema kwakiasi kikubwa wanaenda kutatua hizo changamoto watakapoenda kutoa msaada wakisheria.


"Kwakiasi kikubwa tunaenda kutatua hizo changamoto tutakapotoa msaada wakisheria wananchi wataelewa nini chakufanya lakini kama kunamtu anataka ushauri wakisheria hivyo itamsaidia kuondoa hizo changamoto.Hii kampeni itaenda kuleta usawa,utulivu,haki  na maendeleo"amesema Munisi.


Waziri mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa majaliwa akizindua kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya mama Samia mkoani Lindi 
Wananchi waliojitokeza 


Na Fredy Mgunda, Lindi.


Kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya mama Samia imezinduliwa rasmi katika mkoa wa Lindi kwa kuhakikisha wananchi wananufaika kwa kupata haki zao ambazo awali walikuwa wamenyang'anywa.


Akizungumza kampeni hiyo waziri mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa majaliwa alisema kuwa kampeni hiyo imefanikiwa kutatua migogoro mingi iliyodumu kwa muda mrefu hadi hivi sasa.



Waziri mkuu alisema kuwa Kampeni hiyo imeongeza wigo wa utoaji haki kwa wananchi ambao walikuwa hawana uwezo wa kupata haki kwa kukosa fedha hivyo sasa kila mwananchi anapata haki bure.


Alisema kuwa huduma hiyo ya kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya mama Samia inatolewa bure bila malipo yoyote yale kwa kuwa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suhulu Hassan.


Majaliwa alisema kuwa zaidi ya wananchi milioni 1.3  hadi sasa wamefikiwa na huduma hiyo huku wanaume wakiongoza kufika kupata huduma hiyo kuliko wanawake.


Aliwasisitiza wananchi wa mkoa wa Lindi kujitokeza kwa wiki kupata huduma ya kisheria kwa siku 9 kwenye kila wilaya na kufanikisha wananchi kupata haki zao.

  


Na Josephine Maxime- Dar es Salaam       

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko ameagiza Mwanafunzi Mirabelle Msukari na Wenzake wa Shule ya Msingi Sun Rise iliyopo Wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam kupelekwa katika Mradi wa kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) ili kujifunza zaidi kwa Vitendo namna mradi huo unavyozalisha Umeme.

Mheshimiwa Biteko amesema  hayo leo Februari 18 kwa njia ya simu baada ya Naibu Waziri wa Nishati Mheshimiwa Judith Kapinga  kutembelea shule hiyo kwa lengo la kumpongeza mwanafunzi huyo ambaye video yake ilijizolea umaarufu kupitia mitandao ya kijamii ambapo  Mirabelle alielezea kwa ufanisi juu ya miradi mbalimbali ya umeme inayotekelezwa nchini ukiwemo mradi wa Julius Nyerere.

‘’Sisi tukupongeze na tumefurahi kwa umri wako unafuatilia masuala ya Nishati, sasa tutakupeleka kuliona Bwawa la Julius Nyerere uone Umeme unavyozalishwa ili uendelee kujifunza zaidi. Sisi tunatamani kukuona ukifanikiwa zaidi,” amesema Mhe. Biteko

Kwa Upande wake Naibu Waziri wa Nishati Mheshimiwa Judith Kapinga amesema Miradi hii ya kimkakati ambayo inatekelezwa nchini ni jitihada za Serikali chini ya  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dokta Samia Suluhu Hassan ambaye ameonesha dhamira ya dhati  kuendeleza miradi ya umeme nchini ukiwemo mradi wa JNHPP ambao kwa sasa umefikia asilimia 99.8.

“Wakati Mheshimiwa Rais anaingia madarakani, Mradi wa Julius Nyerere ulikuwa asilimia 33, leo tunavyozungumza umefikia zaidi ya asilimia 99 na mashine nane tayari zimeingizwa kwenye gridi ya Taifa. Imebaki mashine moja pekee ambapo mradi uko mbioni kukamilika,” amesisitiza mheshimiwa Kapinga

Nae Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa wateja Bi. Irene Gowelle akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) , amesema wamepokea kwa vitendo agizo la Mheshimiwa Dkt. Biteko la kuhakikisha mwanafunzi huyo anafanya ziara katika Mradi wa Julius Nyerere ambapo pia amefafanua kuwa elimu na taarifa zinazotolewa na TANESCO zinawafikia walengwa kwa usahihi.

“Hatua hii inatupa nafasi ya kuona kwamba elimu na taarifa mbalimbali tunazozitoa zinawafikia moja kwa moja makundi mbalimbali i?wakiwemo  watoto na ndio maana mmeweza kuona Mirabelle akizungumza kwa ufasaha.

Sisi kama Shirika la Umeme tutaendelea kufanya hivyo” amefafanua Bi. Gowele

Mwanafunzi huyo  licha ya pongezi ,amepewa zawadi mbalimbali ikiwemo Komputa Mpakato (Laptop) pamoja na fedha kiasi cha Shilingi Milioni Mbili.















Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini Mhe. Mrisho Gambo, Leo Jumatano Februari 19, 2025 wakati akizungumza na na Wazee wa Wilaya ya Arusha amehimiza wananchi wa Mkoa wa Arusha kumchagua kwa kishindo Rais Samia Suluhu Hassan kwenye uchaguzi Mkuu ujao, akisema Mkutano Mkuu wa CCM haukukosea kumpitisha kuwa Mgombea pekee kwenye uchaguzi huo.

Mhe. Gambo ambaye amekutana na Wazee hao kama sehemu ya utaratibu wake wa kukutana na makundi mbalimbali ya kijamii katika kuwapatia elimu kuhusu matumizi ya nishati safi ambapo pia amegawa majiko ya gesi kwa wazee 182 waliohudhuria Mkutano huo, amesema ndani ya Miaka minne ya utawala wa Rais Samia Mkoa wa Arusha na hususan Jimbo la Arusha mjini wamekuwa wanufaika wakubwa wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Akiitaja baadhi ya miradi hiyo, Gambo amesema kata ya Sombetini, Osunyai na Ungalimited ni miongoni mwa wanufaika wa miradi mikubwa ya barabara ikiwemo barabara ya Mbauda- Simanjiro, ambayo itajengwa kwa kiwango cha Lami kwa njia nne, suala ambalo litaondoa changamoto ya usafiri na usafirishaji hasa nyakati za mvua.

Ameizungumzia pia barabara ya Kilombero mpaka uwanja wa ndege wa Arusha (Kisongo) ambayo ujenzi wake ulikuwa ukisuasua tangu mwaka 2020, na Rais Samia alipoingia madarakani tayari usanifu umefanyika, fidia ya Bilioni 10 imeshaanza kulipwa kwa wananchi na tayari mchakato wa ujenzi wake umeanza katika jitihada za kuondoa msongamano wa magari kwenye Jiji hilo la Arusha sambamba na kuondoa usumbufu kwa wanaofika Jijini Arusha kwa kutumia uwanja wa ndege wa Arusha wakiwemo watalii.

Mhe. Gambo ameeleza pia kuwa Rais Samia ndani ya miaka minne ya Uongozi wake amefanikisha kuupeleka mradi wa TACTICS jijini humo, mradi ambao utajenga Kituo kikubwa cha kisasa cha mabasi Jijini Arusha, soko la Kilombero pamoja na ujenzi wa soko la Morombo ambapo kufikia mwezi wa sita mwaka huu, mkandarasi atakuwa amepatikana na kuanza kazi mara moja.

viongozi na washirika wakiwa  katika zoezi la uzinduzi wa Mradi wa jamii shirikishi Kanda ya kusini

Shirika la Kimataifa lisilo la Kiserikali linalofanya kazi ya kuhamasisha amani,umoja na maendeleo endelevu kupitia miradi mbalimbali (Global PeaceFoundation )limezindua mradi wa jamii shirikishi katika uzalendo kwa kanda ya kusini.


Mradi huo ulio chini ya udhamini wa ubalozi wa Netherlands umezinduliwa Februari 18,2025 Mkoani Lindi ambapo utatekelezwa kwa kipindi cha mwaka mmoja ukijikita kuboresha ushirikiano baina ya vyombo vya ulinzi katika Mkoa wa Lindi hasa kwenye Wilaya ya Nachingwea na Ruvuma kwa Wilaya ya Nyasa.


Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania Wiebe de Boer amesema inatia moyo kuona kila chombo kinafanya kazi na shirika hilo ili kuileta jamii karibu na kushiriki katika masuala ya ulinzi na usalama kwenye maeneo yao.


Mkurugenzi mtendaji wa shirika hilo la Global Peace Foundation Tanzania (GPF)Hussein Sengu (Wakili)amesema malengo makubwa ya mradi huo ni kuboresha masuala ya ulinzi na usalama kwa kushirikisha polisi jamaii na wanajamii wakiwemo wanawake na vijana ili waweze kushiriki katika masuala hayo kwenye jamii zinazowazunguka.


Aidha,ameeleza kwamba kupitia mradi huo wanakwenda kuboresha mbinu na ujuzi wa kiutendaji miongoni mwa maofisa wa polisi kuhusu ulinzi shirikishi kwa kutoa mafunzo maalum kwa maofisa hao.



Akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Lindi,Mkuu wa Wilaya ya Lindi Victoria Mwanziva amesema zipo dhana mbalimbali ikiwemo ya kufumbia macho matukio ya uhalifu na kuyamaliza nyumbani kimya kimya hali inayosababisha kuendelea kushamiri kwa matukio hayo na uwepo wa mradi huo wenye lengo la kuongeza ushirikiano kati ya polisi na wanajamii wanaenda kutatua hilo.


Nae,Naibu Kamisha wa Jeshi la Polisi na Mkuu wa dawati la ushirikishwaji Kamisheni ya Polisi jamii kutoka Makao Makuu ya jeshi hilo Dodoma Henry Mwaibambe,amesema wamepokea mradi huo ikiwa ni mwendelezo wa miradi walionao kwani unakwenda kufanya kazi kwenye kata ambayo tayari askari wao wapo hivyo amewahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na jeshi la polisi kuibua changamoto mbalimbali kwenye jamii ambazo zimekuwa na sura ya uhalifu ili ziweze kutafutiwa ufumbuzi.


Kwa upande wa wakuu wa Wilaya ya Nchingwea Mohamed Moyo na Nyasa Peres Magiri ambazo mradi huo unakwenda kutekelezwa,wameshukuru serikali ya Uholanzi wakishirikiana na Shirika la Global Peace Foundation kwa kuwapelekea mradi huo wakiamini utakwenda kuongeza uelewa na uzalendo kwa jamii na hivyo kupunguza changamoto za uhalifu katika maeneo yao.


Moyo Amesema anamshukuru kupelekwa mradi huo wilaya Nachingwea na kuahikutoa ushirikiano na jeshi la polisi katika utekelezaji wa miradi huo.

 


🎈🎈Waziri Ridhiwani Kikwete aihakikishia uwekezaji endelevu


Kamati ya Bunge ya Uwekezaji na mitaji ya Umma (PIC) imepongeza serikali ya Awamu ya sita chini Dkt Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uwekezaji wenye tija na manufaa kwa maendeleo ya nchi katika kiwanda cha uzalishaji wa bidhaa za ngozi Kilimanjaro International Leather Industries Co Ltd.

Akiongea mara baada ya kutembelea kiwanda hicho mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Agustine Holle amesema kuwa kutokana na uwekezaji wenye tija waliouona utaiwezesha serikali kuongeza mapato. Vile vile kiwanda hicho kitaunufaisha mkoa wa Kilimanjaro pamoja na mikoa ya jirani kwa kuboresha mfumo wa maisha na kuongeza kipato kwa wakazi hao.

Mwenyekiti amebainisha kuwa wameridhika na uendeshaji wa Kiwanda hicho ambapo kitakapokamilika kwa asilimia 100 kinakwenda kutoa ajira 3,000 kwa ajira za moja kwa moja na ajira nyingine zisizo za moja kwa moja ni 4,000.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Ridhiwani Kikwete ameihakikishia kamati hiyo kuwa ataendelea kusimamia maono ya Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamuhuri ya Muingano Tanzania kwa kuufanya uwekezaji huo wenye tija unakuwa endelevu kwa manufaa ya watanzania na nchi.