Na Mwandishi Wetu - Dodoma


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepokea ugeni wa viongozi wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomu Duniani (IAEA) ukiongozwa na Bwana Gashaw Gebeyehu Wolde, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kiufundi kwa Afrika, pamoja na Bi. Azza Kashlan, Afisa wa Usimamizi wa Programu.

Ziara hiyo inalenga kufuatilia utekelezaji wa miradi mbalimbali inayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Tanzania na IAEA katika sekta za viwanda, afya, elimu, kilimo na chakula.

Ugeni huo, ukiwa na mwenyeji wake Profesa Najat Kassim Mohammed, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), ulianza ziara yake jijini Dodoma kwa kutembelea Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ambapo walikutana na Katibu Mkuu, Mhe. Balozi Dkt. Samweli William Shelukindo.

Mazungumzo hayo yalihusu nafasi ya Tanzania katika ushirikiano wa kimataifa wa nyuklia kwa maendeleo endelevu.


Baadaye, viongozi hao walitembelea Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na kufanya mazungumzo na Naibu Katibu Mkuu, Profesa Daniel Mushi, kuhusu mafanikio ya miradi inayotumia teknolojia ya nyuklia nchini.


Aidha, walijadili maendeleo ya programu za elimu zilizoanzishwa kwa msaada wa IAEA, ambazo zinalenga kuongeza idadi ya wataalamu wa fizikia ya tiba ili kuimarisha huduma za saratani nchini.


Naibu Katibu Mkuu alibainisha kuwa ushirikiano wa Tanzania na IAEA ni wa muda mrefu na umeleta matokeo ya vitendo kupitia Programu ya Ushirikiano wa Kiufundi. Kikao hicho kilikumbusha mafanikio ya hivi karibuni, yakiwemo miradi ya kitaifa ya TC inayoendelea katika awamu ya mwaka 2025–2026 na kiwango cha juu cha maendeleo kilichoripotiwa kufikia mwisho wa Desemba 2025.


Miradi hiyo inahusu sekta za viwanda, afya, kilimo na usalama wa chakula, ikiwemo; Mradi wa kituo cha mionzi cha matumizi mbalimbali (multipurpose irradiator facility), Upanuzi wa huduma za tiba ya nyuklia na radiotherapy, Uzalishaji wa mbegu kwa njia ya mionzi (mutation breeding) kwa pamba na maharage ya kawaida, Kuimarisha uwezo wa maabara ya usalama wa chakula Zanzibar.


Katika kikao hicho, Profesa Mushi aliwasilisha mapendekezo kwa awamu ijayo ya ushirikiano, ikiwemo; Kusaidia Tanzania katika matumizi ya teknolojia za nyuklia na atomu kama sehemu ya mpango wa muda mrefu wa usambazaji wa umeme, Kuimarisha na kusasisha mitaala ya shule na elimu ya juu katika sayansi ya nyuklia na fani zinazohusiana, Kuendeleza na kuimarisha miundombinu ya maabara na uwezo wa kiufundi, Kupanua vyanzo vya nishati ili kuendana na mahitaji ya ukuaji wa taifa, Kuendelea kutoa mwongozo wa kiufundi kwa matumizi salama na yenye uwajibikaji ya teknolojia ya nyuklia.




Naibu Katibu Mkuu alisisitiza Kuimarisha ushirikiano kwenye mifumo na miundombinu, hususan katika: Uchambuzi wa uwezekano wa utekelezaji wa Mitambo Midogo ya Nyuklia (Small Modular Reactors – SMRs), Kupanua huduma za tiba ya mionzi ya saratani (radiotherapy) kwenda katika mikoa mingine, Matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika chakula na kilimo, na Usalama na ulinzi, ikijumuisha uboreshaji wa miundombinu ya usimamizi wa taka za mionzi (radioactive waste management facilities).




Naye Mkurugenzi Gashaw kutoka Wakala wa Nguvu za Atomu Duniani alipongeza mapendekezo hayo na kuthibitisha kuendelea kwa ushirikiano. Walisisitiza kuwa Tanzania imekuwa na uhusiano wa muda mrefu na shirika hilo, na sasa imefikia hatua ya ukomavu katika programu zake, huku ikichukua nafasi ya kuwa kitovu cha kikanda katika kujenga uwezo wa kitaalamu.


Mambo muhimu yaliyosisitizwa ni pamoja na; Kuendelea kuunga mkono vipaumbele vya kitaifa kupitia Programu ya Ushirikiano wa Kiufundi, Hatua za awali katika mchakato wa kuanzisha mradi wa nyuklia, ikiwemo kuimarisha taasisi, mifumo na rasilimali watu, Kutambua uongozi wa Tanzania na mchango wake katika kujenga uwezo wa kikanda, Kuendeleza matumizi ya kituo cha mionzi cha matumizi mbalimbali, Kupanua matumizi ya nishati ya nyuklia kwa maendeleo ya taifa, Kuweka usalama na ulinzi kama msingi wa matumizi ya nyuklia, Kuendeleza rasilimali watu kupitia mafunzo ya muda mrefu katika tiba ya nyuklia na fani nyingine maalumu, huku wakihimiza wataalamu wa Kitanzania kuchangamkia nafasi zinazotolewa na IAEA.




Ugeni huo pia ulitembelea Wizara ya Nishati, ambapo ulipokelewa na Katibu Mkuu Mhandisi Felichism Mramba. Mazungumzo yalihusu hatua zilizofikiwa katika mchakato wa Tanzania kuelekea kuanzisha mradi wa umeme wa nyuklia, hatua inayolenga kuongeza vyanzo vya nishati safi na salama kwa maendeleo ya uchumi wa taifa.


Mnamo tarehe 4 Februari 2026, ugeni huo utatembelea Chuo cha Nelson Mandela cha Sayansi na Teknolojia Afrika (NM-AIST) Jijini Arusha, ambapo watajionea maendeleo ya mradi wa Green House for Beans (RAF5059). Mradi huo unatumia mbinu za nyuklia kuboresha uzalishaji wa mazao ya jamii ya kunde, ukilenga kuongeza usalama wa chakula na kipato kwa wakulima wadogo.


Ziara ya viongozi wa IAEA nchini Tanzania inaendelea kuthibitisha dhamira ya serikali ya kuendeleza ushirikiano wa kimataifa katika matumizi salama na endelevu ya teknolojia ya nyuklia. Kupitia miradi hii, Tanzania inalenga kuimarisha huduma za afya, kuongeza rasilimali watu wenye ujuzi wa kisayansi, kukuza kilimo, na kuandaa mazingira ya kuanzisha nishati ya nyuklia kwa maendeleo ya taifa.







Jijini Dodoma📍

Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule ametoa wito kwa Wananchi wa vitongoji vitakavyonufaika na Mradi wa Kusambaza Umeme katika vitongoji 379 kujiandaa kwa kutandaza nyaya majumbani (Wiring) mapema ili kuunganishwa na huduma hiyo mara Mradi utakapokamilika.

Akizungumza wakati wa hafla ya kumtambulisha mkandarasi huyo (Kampuni ya Giza Cable Industries S.A.E) kutoka Misri ambaye anatekeleza Mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 379 vya mkoa wa Dodoma; Mhe. Senyamule alisema ni muhimu Wananchi kuwekeza mapema katika miundombinu ya ndani ya majengo yao ili kuepuka kuchelewa kupata huduma hiyo.

Mkuu huyo wa mkoa alitoa rai kwa mkandarasi huyo kuhakikisha kazi hiyo ya kusambaza umeme katika vitongoji 379 inakamilika sawa sawa na mkataba au ikiwezekana kabla ya muda uliopangwa.

Aidha, Mkuu wa mkoa Senyamule alionya vikali dhidi ya vishoka; wanaopita kwa Wananchi wa maeneo mbalimba ya mkoa huo akisema kuwa Serikali ya mkoa imejipanga ili kuhakikisha jambo hilo halitokei tena na kutoa wito kwa Wananchi wanawatumia mafundi wenye ujuzi na wanaotambulika kisheria katika kufanya ‘wiring’ ya umeme kwenye nyumba zao.

Kwa upande wake; Mhandisi Msimamizi wa Miradi ya REA Kanda ya Kati, Aneth Malingumu alisema hafla hiyo imelenga kumtambulisha rasmi mkandarasi ili aanze kazi ya kusambaza umeme katika vitongoji vya mkoa wa Dodoma ambapo Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 43.9 kwa ajili ya Mradi huo wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 379 katika wilaya ya Chamwino; Kongwa; Mpwapwa; Kondoa na Chemba.

Alisema mradi huo utawezesha Wateja wa awali (Wananchi 12,256) kupata huduma ya umeme na kuongeza kuwa huduma ya umeme ikitumiwa vizuri, itasaidia kuinua uchumi wao pamoja na kuboresha utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya na elimu.

Mhandisi Malingumu aliwahimiza Wananchi kuhakikisha wanafanya ‘wiring’ ya ndani ya nyumba mapema ili wawe tayari kuunganishwa na umeme mara miundombinu itakapokamilika na aliongeza kuwa REA itaendelea kushirikiana na mkandarasi ili kutatua changamoto katika maeneo ya kazi na kumlipa kwa wakati ili mradi ukamilike ndani ya muda wa mkataba wa miaka mitatu.

Naye Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, Mhandisi, Donasia Shamba, alisema TANESCO ambaye ndiye Mtaalam Elekezi (Consultant) watahakikisha vifaa pamoja ujenzi wa Mradi huo unazingatia ubora unahitajika ili malengo ya Serikali kupitia REA yafanikiwe.

Kwa upande wake, Mhandisi, Almas Msuya; Mwakilishi wa kampuni ya Giza Cable alisema kampuni hiyo iko tayari kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Serikali ili kuhakikisha mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 379 unakamilika kwa wakati kulingana na masharti ya mkataba.

 


Na OWM - TAMISEMI, Dodoma

Bibi Clotilda Isidory Kokupima, mkazi wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, amemtembelea Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, na kumuomba awasilishe shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa msaada alioutoa wa   Shilingi Milioni 20 kugharamia matibabu ya ugonjwa wa kansa ya utumbo uliokuwa ukimsumbua kwa muda mrefu.

Akizungumza na Prof. Shemdoe ofisini kwake, Bibi Clotilda amesema alifika ofisini hapo mahsusi kuomba shukrani zake ziwasilishwe kwa Mheshimiwa Rais, ambaye msaada wake ulimwezesha kupata matibabu katika Hospitali ya Ocean Road jijini Dar es Salaam, hatua iliyookoa maisha yake.

“Ninamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuokoa maisha yangu. Nilikuwa nikisumbuliwa na ugonjwa wa kansa ya utumbo kwa kipindi cha miaka sita, na matibabu yalisimama baada ya familia yangu kushindwa kumudu gharama. Hata hivyo, baada ya kupata msaada wa Shilingi Milioni 20 kutoka kwa Mheshimiwa Rais, niliweza kuendelea na matibabu,” amesema Bibi Clotilda.

Ameongeza kuwa aliwasilisha barua za maombi ya msaada wa fedha za matibabu kwa wadau wasiopungua kumi, akiwemo Mhe. Rais na ndani ya kipindi cha mwezi mmoja tangu kuwasilisha ombi lake, alipatiwa msaada huo uliomuwezesha kuendelea na matibabu.

Bibi Clotilda amesema fedha hizo zilimwezesha kukamilisha matibabu katika Hospitali ya Ocean Road na baada ya kumaliza dozi ya mwisho, vipimo vilionesha kuwa hana tena ugonjwa wa kansa uliokuwa ukimsumbua. 

Ameeleza kuwa ameruhusiwa kuendelea na shughuli zake za kila siku, huku akitakiwa kufanyiwa uchunguzi wa afya kila baada ya miezi mitatu.

Aidha, amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kukubali kuwasilisha shukrani zake kwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, akieleza kuwa huruma na upendo wake umeokoa uhai wake, na kumuomba aendelee kuwa msaada kwa wananchi wengine wenye uhitaji.

Katika jitihada za kuboresha sekta ya elimu nchini Tanzania, ADEM na Taasisi ya Project Zawadi wameingia makubaliano ya ushirikiano utakaowezesha kuendesha mafunzo ya muda mfupi kuhusu uongozi, usimamizi na uendeshaji wa elimu kwa viongozi wa Mkoani Mara. 

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Mahakama ya Wilaya ya Handeni leo Februari 2,2026.

Na Augusta Njoji

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, ametoa rai kwa Mahakama ya Wilaya ya Handeni kutoa kipaumbele katika usikilizwaji wa mashauri yanayohusu ardhi ili yahitimishwe kwa wakati na kuchochea maendeleo ya wananchi.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Mahakama ya Wilaya ya Handeni, Mhe. Nyamwese amesema migogoro ya ardhi imekuwa ikichukua muda mrefu kusikilizwa pindi inapofikishwa mahakamani, hali inayosababisha kucheleweshwa kwa utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Amesema ardhi ni rasilimali muhimu katika Wilaya ya Handeni, lakini imeendelea kukumbwa na migogoro mingi, ambayo baadhi yake haina tija kwa maendeleo ya jamii.

Amesisitiza kuwa haki inapocheleweshwa, maendeleo nayo hucheleweshwa, hususan pale wananchi wanapokusudia kutumia ardhi kwa uwekezaji au shughuli za uzalishaji.

“Sisi kama Wilaya tumekuwa na migogoro ya ardhi, lakini inapofika mahakamani mashauri haya huchukua muda mrefu kusikilizwa. Hali hii inawaathiri wananchi na kudumaza maendeleo kwa ujumla,” amesema Mhe. Nyamwese.

Aidha, amepongeza hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha utendaji wa Mahakama, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya mahakama karibu na wananchi pamoja na matumizi ya teknolojia, hatua zinazoongeza imani ya wananchi katika mfumo wa utoaji haki.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Handeni, Joseph Waruku, amesema Mahakama imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kuanzisha Mahakama za Mwanzo 12 mwaka 2025 katika maeneo yenye msongamano wa mashauri, ikiwemo Mahakama ya Mwanzo Msomera.

Naye, Mwakilishi wa Mwanasheria wa Halmashauri ya Mji Handeni, Regina Pangah, amesema Mahakama zina mchango mkubwa katika ustawi wa jamii na ukuaji wa uchumi kwa kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati, huku akiahidi kuendeleza ushirikiano katika kutoa elimu ya sheria kwa wananchi.

Ndani ya kipindi kifupi cha siku 100 za uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sekta ya Madini imeendelea kujiimarisha kama moja ya vielelezo bora vya mageuzi ya kiuchumi yanayoongozwa na maono, Sera thabiti na utekelezaji wenye mwelekeo wa kimataifa. Sekta ya Madini imepiga hatua kubwa si tu katika ukusanyaji wa mapato, bali pia katika uongezaji thamani wa madini, ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content) maendeleo ya teknolojia na nafasi ya Tanzania katika ramani ya madini duniani.

Ukuaji wa Mapato na Mchango kwenye Uchumi wa Taifa

Takwimu zinaonesha mabadiliko Chanya na ya msingi, ndani ya miezi mitatu pekee (Novemba 2025 hadi Januari 25, 2026), Sekta ya Madini imekusanya kiasi cha Shilingi bilioni 311, sawa na asilimia 103 ya lengo ndani ya kipindi hicho, mwenendo huo unaakisi mageuzi ya mifumo ya usimamizi, udhibiti na uwazi katika shughuli za madini. Kwa ujumla, mapato ya Serikali kutoka sekta hiyo yameongezeka kutoka shilingi bilioni 526 Mwaka wa Fedha wa 2020/2021 hadi zaidi ya shilingi trilioni 1.071 mwaka 2024/2025, huku mwaka wa fedha uliopo wa 2025/2026 sekta ikiwekewa lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.2.

Mafanikio haya yamechochea mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa (GDP) kuongezeka kutoka asilimia 10.1 hadi asilimia 12 ndani ya siku 100 pekee. Hatua hii inaipa Tanzania nafasi ya kipekee miongoni mwa nchi za Afrika zinazotumia rasilimali zao za madini kama kichocheo cha ukuaji wa uchumi jumuishi.

Local Content: Watanzania Kuwekwa Kwenye Moyo wa Sekta

Moja ya mafanikio makubwa yenye athari chanya ya kijamii na kiuchumi ni utekelezaji wa Sera na Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content), kupitia marekebisho ya Kanuni za mwaka 2018, Serikali imeweka mfumo unaohakikisha ajira, manunuzi na huduma migodini zinawanufaisha Watanzania moja kwa moja. Matokeo yake, ajira za Watanzania migodini zimeongezeka kutoka 6,668 mwaka 2018 hadi kufikia zaidi ya 18,800 mwaka 2024, sawa na zaidi ya asilimia 97 ya ajira zote migodini.

Kwa upande wa manunuzi, mageuzi haya yamepunguza utegemezi wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi ambapo manunuzi ya ndani yameongezeka hadi asilimia 88 ya manunuzi yote ya migodini kufikia mwaka 2024, ikilinganishwa na asilimia 62 mwaka 2018. Hatua hiyo imesaidia kubakiza mzunguko mkubwa wa fedha ndani ya nchi na uchumi wa Taifa, kukuza viwanda vya ndani na kuongeza ajira katika sekta shirikishi kama ujenzi, usafirishaji, nishati na huduma za kitaalamu.

Uongezaji Thamani na Viwanda: Kuondoka kwenye Uchimbaji wa Malighafi

Katika utekelezaji wa Sera ya Madini ya mwaka 2009, Serikali imeongeza kasi ya ujenzi wa viwanda vya kusafisha na kuongeza thamani ya madini ambako Mkoa wa Dodoma umeibuka kama kitovu kipya cha uongezaji thamani, ukiwa na viwanda 9 vya uongezaji thamani wa madini pamoja na viwanda 4 vya madini ya metali kama shaba na nikeli. Aidha, kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), kiwanda cha kusafisha chumvi kwa ajili ya mikoa ya Lindi na Mtwara kimekamilika kwa asilimia 99, hatua inayoongeza thamani ya rasilimali kabla ya kuingia sokoni.

Uwezeshaji wa Wachimbaji Wadogo: Mageuzi ya Uchumi wa Wananchi

Wachimbaji wadogo, wanaohusisha zaidi ya Watanzania milioni 6 kwenye mnyororo wa thamani wa madini, wamekuwa kitovu cha mageuzi ya kijamii. Ndani ya siku 100, Serikali imenunua mitambo 15 ya uchorongaji miamba, kutoa leseni 511 kwa vikundi vya wachimbaji wadogo Geita na Shinyanga, na kuwezesha mkopo wa Shilingi bilioni 30 kupitia taasisi za fedha. Sambamba na hilo, mpango wa kununua mitambo mikubwa ya CIP yenye uwezo wa kuchenjua tani 120 kwa saa, pamoja na kuanzishwa kwa mfuko wa dhamana, umefungua ukurasa mpya wa uchimbaji wa kisasa, salama na wenye tija.

Miradi Mikubwa na Hadhi ya Kimataifa

Katika hatua ya kihistoria, Tanzania inajiandaa kuingia rasmi kwenye uzalishaji wa Madini ya Ferro-Niobium kupitia mradi wa Songwe, Panda Hill, Mbeya, unaotarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi trilioni 1. Mradi huo utaifanya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakuu wa kimataifa wa madini haya muhimu kwa viwanda vya chuma na teknolojia ya juu. Sambamba na hilo, maandalizi ya utafiti wa kina wa dhahabu (High Resolution Airborne Geo-Physical Survey) na kampuni ya kimataifa ya Barrick Gold katika Nzega na Kahama yanaashiria uwekezaji mpya wa kiwango kikubwa mara baada ya Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde kuzindua urushwaji wa helkopta kwa ajili wa utafiti huo.

Dhahabu, Nishati Safi na Masoko ya Ndani

Kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ununuzi wa zaidi ya tani 17 za dhahabu umeiweka Tanzania miongoni mwa nchi 10 bora barani Afrika kwa hifadhi ya dhahabu, jambo linaloongeza uthabiti wa uchumi na heshima ya kifedha kimataifa. Wakati huohuo, uzalishaji wa nishati safi ya kupikia ya ‘Rafiki Briquettes’ unaotokana na makaa ya mawe kupitia STAMICO unaunga mkono ajenda ya nishati safi, ukipunguza utegemezi wa kuni na mkaa ili kulinda mazingira.

Hitimisho

Kwa mtazamo wa kimkakati, siku 100 za uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia zimeifanya Sekta ya Madini kuwa chombo cha mageuzi ya uchumi, ajira na hadhi ya Taifa kimataifa. Tanzania inaendelea kujizatiti na kujiimarisha kuelekea kwenye uchumi wa uongezaji thamani, teknolojia na ushiriki mpana wa wananchi. Hayo si mafanikio ya kawaida, bali ni mapinduzi ya kimuundo yenye athari chanya za kudumu kwa vizazi vilivyopo na vijavyo.














Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi,akizungumza na wadau leo Februari 02, 2026 jijini Dodoma.

....

Serikali imeelekeza wadau kuhakikisha uwekezaji unaofanyika karibu na kampasi mpya 16 za vyuo vikuu unazingatia mpangilio wa miji, usalama na viwango vya kitaifa ili kuzuia ujenzi holela na kuhakikisha huduma zinazotolewa zinakidhi mahitaji ya wanafunzi, watumishi na jamii jirani.

Akizungumza Februari 02, 2026 jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi,amesema kuwa halmashauri na serikali za mitaa zinapaswa kutenga ardhi na kuandaa mpango wa matumizi ya ardhi kwa kushirikiana na vyuo husika.

Prof. Mushi amesisitiza kuwa mipango hiyo lazima izingatie viwango vya kitaifa vya upangaji miji na kuondoa migongano ya matumizi ya ardhi.

Profesa Mushi pia amevielekeza vyuo vikuu kufungua milango ya ushirikiano na sekta binafsi kupitia ubia rasmi (PPP) katika ujenzi wa hosteli, vituo vya biashara na miundombinu maalum.

Amesema mashauriano ya mara kwa mara kati ya vyuo na serikali za mitaa ni muhimu ili kuoanisha mipango ya maendeleo na kuimarisha mazingira rafiki kwa uwekezaji.

Aidha, sekta binafsi imetakiwa kuhakikisha huduma wanazotoa zinajibu mahitaji halisi ya jamii kwa kuzingatia usalama, ubora na uwajibikaji wa kijamii.

Mratibu wa Mradi wa HEET Taifa, Dkt. Kenneth Hosea, amesema kuwa mbali na kutoa mafunzo ya programu za Shahada ya Kwanza na Shahada ya Pili, kampasi mpya pia zitalenga kutoa ujuzi wa vitendo kwa vijana, wanawake na makundi maalum. Hatua hii inalenga kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo ya pembezoni kupitia ujenzi wa miundombinu, upatikanaji wa huduma za msingi pamoja na fursa za ajira.

Aidha, Dkt. Hosea ameongeza kuwa kila kampasi inatarajiwa kudahili zaidi ya wanafunzi 1,000 mwanzoni, na idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka hadi kufikia takribani wanafunzi 7,000 kadri muda unavyosonga.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga, Rashid Karim Gembe, amesema kuwa kuanzishwa kwa kampasi mpya za elimu ya juu katika maeneo ya pembezoni kumeleta manufaa makubwa ya kiuchumi na kijamii

Amesema kuwa kutachochea ujenzi wa miundombinu kama barabara, maji na umeme, kuongeza upatikanaji wa huduma za msingi, pamoja na kutoa fursa za ajira kwa wananchi kupitia mahitaji ya walimu, wanafunzi na sekta binafsi, hivyo kuchangia kwa kiasi kikubwa ustawi wa jamii na maendeleo ya uchumi wa eneo husika.