Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Februari 12, 2026 amekagua na kuweka jiwe la msingi la Mradi wa ujenzi kituo cha kupokea na kupoza umeme cha MVA 60 Mkatata Tanga na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovolti 33.
Akiweka jiwe la msingi mradi huo, Dkt. Mwigulu amesema kutekelezwa kwa mradi huo ni jitihada za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika.
"Nitoe rai kwa Wizara ya Nishati kuhakikisha kasi ya ukamilishwaji wa mradi huo na unakamilika kwa wakati ". Amesisitiza Mhe. Waziri Mkuu.
Katika hatua nyingine ameiagiza Wizara ya Nishati kuwasiliana na Wizara ya Fedha ili kukamilisha malipo ya fidia kwa Wananchi takribani shilingi bilioni moja.
Ujennzi wa mradi huo ni shilingi bilioni 44 na unahusisha ujenzi wa vituo viwili vya kupokea, kupoza na kusambaza umeme vyenye uwezo wa MVA 60 huku kila kimoja kikiwa na MVA 30, pamoja na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 33 kutoka kituo cha Mkata hadi kwa Msisi.
Kwa upande wake Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amemshukuru Mhe. Rais kwa kuwezisha upatikanaji wa fedha zitakazo tumika katika utekelezaji wa mradi huo.
“Utekelezaji wa mradi huu unakwenda kuondoa changamoto za umeme katika Wilaya za Handeni na Kilindi ambazo zinapata umeme kutokea Tanga mjiani ambapo ni umbali mrefu". Amesema Mhe. Ndejembi.
Amefafanua kuwa kupitia miundombinu hiyo mipya, umeme utasafirishwa kutoka Mkata kwenda Msisi kwa umbali wa kilomita 45, hatua itakayoongeza uwezo wa usambazaji na kuimarisha huduma katika maeneo hayo.
Kuimalika kwa huduma ya umeme Wilaya za Handeni na Kilindi kutachochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi na kijamii.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb), akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Dhahabu Duniani (WGC), Bw. David Tait, pamoja na Waheshimiwa Mawaziri baada ya mazungumzo ya kimkakati.
Majadiliano hayo yamelenga kuboresha mnyororo wa thamani wa sekta ya dhahabu nchini, hususani katika kuwajengea uwezo wachimbaji wadogo ili kukuza mchango wao katika uchumi wa taifa.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Katika kutekeleza sera ya kutosafirisha madini bila kuongeza thamani, serikali imekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Dhahabu Duniani (World Gold Concil) Bw. David Tait juu ya kuendeleza sekta ya dhahabu nchini.

Mazungumzo hayo yamefanyika leo Februari 13, 2026 jijini Dar es Salaam ambapo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb.) ameongoza Mawaziri wanne, Mawaziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Maendeleo ya Vijana Mhe. Joel Nanauka, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima katika mazungumzo hayo.
Mazungumzo hayo yameangazia namna ya kuirasimisha sekta ya wachimbaji wa dhahabu wadogo ili kuhakikisha wanafanya uchimbaji wenye faida bila kuathiri mazingira.
Aidha, wamejadili namna ambavyo baraza hilo litashiriki kuiwezesha Tanzania kuvutia wawekezaji zaidi katika kuongeza thamani ya madini yanayozalishwa nchini ikiwa ni utekelezaji wa sera na sheria za sasa ambazo haziruhusu kuuza na kusafirisha madini bila kuongeza thamani.

Waziri wa Madini Mhe. Antony Mavunde amesema kuwa Baraza la madini duniani limevutiwa na namana serikali invyojenga mfumo mzuri wa kuwawezesha wachimbaji wadogo ambao huchangia uzalishaji wa madini kwa asilimia 40, huvyo kulifanya baraza hilo kuiona Tanzania ikiwa ni sehemu salama ya kufanya ushirikiano katika kukuza sekta hiyo.

Kwa upande wake Bw. Tait Amesema kuwa Baraza la Dhahabu duniani linavutiwa na namna serikali ya Tanzania inavyowawezesha wachimbaji wadogo, na hivyo ushirikia baina ya shirika hilo utakuwa ni kitovu na kielelezo cha namna sekta ya inavyoweza kukua na kuongeza tija.




Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) Bw. Abdul-Razaq Badru ameongoza kikao cha kimkakati kilichojumuisha waheshimiwa Madiwani, Viongozi wa Mila, watendaji wa kata, wenyeviti wa Vijiji na watendaji wa vijiji kwa lengo la kudumisha mahusiano na uboreshaji wa huduma za kijamii na uboreshaji wa shughuli za Uhifadhi shirikishi.
Kamishna Abdul-Razaq Badru ameeleza kuwa kikao hicho ni sehemu ya mkakati wa Mamlaka hiyo kukutana na makundi mbalimbali kujadili uboreshaji wa shughuli za kijamii na huduma za wananchi kama Maji, shule, Malisho, barabara, mawasiliano, afya na mengineyo.
"Viongozi na Wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro ni wadau muhimu katika hifadhi, tunakutana nao kama sehemu ya kuboresha uhusiano na kuwaeleza mikakati ya Serikali dhidi yao.
kwa sasa tunaboresha miundombinu ya huduma za maji, ujenzi wa Barabara kwa tabaka gumu kutoka Loduare hadi Golini, kujenga minara mipya ya mawasiliano 9 ndani ya hifadhi ili kufikisha huduma kwa wananchi na wadau mbalimbali" amefafanua Kamishna Badru.
Kwa upande wa Viongozi waheshimiwa Madiwani, viongozi wa Mila wameiomba Serikali kupitia Mamlaka hiyo kuendelea kuboresha mahusiano, huduma za kijamii kama miundombinu ya Maji, barabara, ukarabati wa vituo vya afya na shule, mahitaji ya baraza la wafugaji, chunvi za mifugo na mpango wa malisho ya mifugo hawa wakati wa kiangazi.
Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (wapili kushoto) akiwasili katika katika hafla ya uzinduzi wa programu ya Go Green Na IMBEJU inayolenga kuwezesha biashara na bunifu za kijani za vijana kama sehemu ya kuchochea uchumi wa kijani kuelekea Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050. Alioongozana nao ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, (katikati), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori (wapili kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (wakwanza kushoto), na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa.
Na Munir Shemweta, WANMM
Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani mwaka huu, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi itaendesha Kliniki Maalum ya Ardhi kwa ajili ya wanawake itakayojulikana kwa jina la "Samia Ardhi Week."
Kiniki hiyo itashughulikia changamoto za ardhi kwa wanawake na itafanyika kuanzia tarehe 2 hadi 7 Machi 2026 katika mikoa yote ya Tanzania Bara ikiwa ni kuelekea maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake ambayo huadhimishwa tarehe 8 Machi kila mwaka ambapo kwa mwaka huu inaongozwa na Kaulimbiu "Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050"
Akizungumza jijini Dodoma tarehe 12 Februari 2026 wakati wa kuahirisha Kliniki Maalum ya Maombi ya Hati, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo amesema, wanawake wote wenye changamoto za ardhi wanatakiwa kujitokeza kwa wingi katika maeneo ambayo kliniki hizo zitafanyika.
"Wanawake wote wenye shida za masuala ya ardhi wanatakiwa kujitokeza katika mikoa ya Tanzania Bara ambayo kliniki hizo zitafanyika" amesema Mhe Dkt. Akwilapo.
Kwa mujibu wa Waziri huyo wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, nia ya wizara yake kuanzisha kliniki za ardhi katika maeneo mbalimbali nchini ni kuwafikia wananchi wenye shida zinazohusiana masuala ya ardhi.
Akizungumzia Kliniki Maalum ya Maombi ya Hati aliyoiahirisha, Mhe. Dkt Akwilapo amesema, kliniki hiyo imekuwa na mafanikio makubwa ambapo hadi kufikia tarehe 12 Februari 2026 wananchi 4,597 wamehudumiwa huku Hatimilki 3,878 zikiwa zimeandaliwa.
"Kumbe kupata hati inawezekana, katika hati 3,878 zilizoandaliwa jumla ya hati 1,508 zimechukuliwa na wahusika huku hati 2,370 zikiwa bado hazijachukuliwa", amesema Dkt. Akwilapo.
Ametoa rai kwa wananchi ambao wamepata huduma na hati zao zimekamilika wafike ofisi za ardhi kwa ajili ya kuzichukua kwa kuwa hati hizo za ardhi ni mali yao.
Kliniki Maalum ya Maombi ya hati ilianza januari 28, 2026 katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dodoma na kuhitimishwa tarehe 12 Februari 2026.
Na Mwandishi Wetu Morogoro
Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa, imefanya kikao kazi kinacholenga kuimarisha ushirikiano kati ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Taasisi za Elimu ya Juu na Taasisi za Utafiti katika eneo la usimamizi wa maafa leo tarehe 12 februari, 2026 Mkoani Morogoro.
Akifungua Kikao hicho Dkt. James Henry Kilabuko Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa niaba ya Dkt. Jim Yonazi Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo amesema;
Lengo kuu la kikao kazi hiki ni kuandaa Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano na Mpango Kazi wa kuimarisha matumizi ya Sayansi, Teknolojia, Utafiti na Ubunifu katika usimamizi wa maafa kwa pamoja nchini ili kuweza kuwasaidia Wananchi katika kujiandaa, kuzuia na kukabiliana na maafa kipindi yanapotokea.
Aidha ameeleza kwamba, Serikali inadhamira ya kuimarisha mfumo wa taifa wa usimamizi wa maafa kwa kuzingatia mzingo mzima wa maafa unaojumuisha kuzuia na kupunguza madhara, kujiandaa, kukabiliana na maafa yanapotokea pamoja na kurejesha hali baada ya maafa.
Amesema Mwelekeo huu, umeainishwa wazi katika Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya mwaka 2004, (Toleo la Mwaka 2025) inayosisitiza matumizi ya sayansi, teknolojia na tafiti katika kufanya maamuzi na utendaji wenye ufanisi.
"Katika utekelezaji wa sera na sheria, Ofisi ya Waziri Mkuu imeona umuhimu wa kuimarisha ushirikiano na Vyuo vya Elimu ya Juu na Taasisi za Utafiti nchini, Ushirikiano huu unalenga kuhakikisha kuwa tafiti, mafunzo na teknolojia zinajibu changamoto zinazokabili taifa letu" amesema Dkt. Kilabuko
Pamoja na hayo, Dkt. Kilabuko amesisitiza uunganishaji wa nguvu, maarifa na rasilimali tulizonazo, utajenga Taifa lenye ustahimilivu dhidi ya maafa na lenye uwezo wa kufikia malengo ya maendeleo yaliyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Awali Mkurugenzi wa Idara ya Menejimentu ya Maafa Brg. Jenerali Hosea M. Ndagala alisema, kikao hiki kinatoa fursa ya kujenga uelewa wa pamoja kati ya wahadhiri, wataalamu wa kitaaluma na watendaji wa Serikali kuhusu mahitaji halisi ya shughuli za usimamizi wa maafa katika ngazi ya kitaifa, mkoa hadi wilaya kwa lengo la kuongeza ufanisi wa majibu wakati wa maafa na kuboresha mikakati ya kurejesha hali baada ya maafa.















































