Na.Ashura Mohamed– ARUSHA
Wananchi zaidi 1,000 wa Jiji la Arusha na maeneo ya jirani wamenufaika na huduma za upimaji na uchunguzi wa afya bure, hususan magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo, kupitia Mpango wa Tiba Mkoba wa Dkt. Samia Suluhu Hassan (Outreach Program).
Akizungumza wakati wa zoezi hilo leo Jan 3,2025, Dkt. Kisenge amesema kambi hiyo imelenga kuwafikia wananchi wengi zaidi kwa kuwapatia huduma muhimu za uchunguzi wa afya mapema,hatua ambayo itasaidia kuzuia madhara makubwa ya kiafya yanayotokana na kuchelewa kugundua magonjwa.
Huduma hizo zimetolewa na timu ya madaktari bingwa wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ikiongozwa na Mkurugenzi wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge, ambaye ni bingwa wa magonjwa ya moyo, ambapo zoezi hilo litafanyika mkoani Arusha kwa kipindi cha siku kadhaa kuanzia tarehe 3 hadi 7.
Dkt.Kisenge amesema huduma zilizotolewa ni pamoja na vipimo vya moyo vya Echo na ECG, pamoja na vipimo vingine muhimu, vyote vikifanyika bila malipo yoyote, ikiwa ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya kwa wakati na kwa usawa.
“Upimaji wa mapema humsaidia mtu kugundua tatizo kabla halijawa kubwa na kuepusha madhara makubwa kama kushindwa kwa moyo, figo au kupata kiharusi,” alisema Dkt. Kisenge.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wananchi kadhaa wamebainika kuwa na matatizo mbalimbali ya moyo, ambapo wagonjwa 36 wamepatiwa rufaa ya kwenda Hospitali ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu ya kibingwa zaidi.
Alisema baadhi yao wanahitaji kufanyiwa uchunguzi maalum wa mishipa ya damu ya moyo kwa kutumia mtambo wa Cath Lab, huku wengine wakihitaji upasuaji wa kuziba matundu ya moyo au kuanza matibabu ya shinikizo la damu.
Aidha, wananchi waliogundulika kuwa na shinikizo la damu bila wao kufahamu wamepatiwa elimu ya lishe bora, ushauri wa kitaalamu na kuanzishiwa dawa, hatua inayolenga kuwakinga dhidi ya madhara makubwa ya baadaye kama figo kushindwa kufanya kazi au moyo kuchoka.
Dkt. Kisenge amewahimiza wananchi wa Jiji la Arusha na mikoa ya pembezoni katika Kanda ya Kaskazini kuendelea kujitokeza kupata huduma za uchunguzi wa afya katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC),na vituo vingine vilivyobainishwa, akisisitiza umuhimu wa kupima afya mara kwa mara hata pale mtu anapoonekana kuwa mzima.
Katika hatua nyingine muhimu, Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imeingia makubaliano na Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre, ambapo hospitali hiyo itatoa huduma za magonjwa ya moyo chini ya usimamizi wa JKCI kwa kipindi cha miaka 20, huku huduma zote za upasuaji wa kibingwa zikiendelea kusimamiwa na JKCI.
Uamuzi huo umetokana na umuhimu wa Mkoa wa Arusha kama kitovu cha utalii pamoja na maandalizi ya mashindano ya AFCON, hatua itakayosaidia kusogeza huduma za kibingwa karibu na wananchi bila ulazima wa kusafiri umbali mrefu.
Kwa sasa, wananchi wote wenye matatizo ya moyo na magonjwa mengine yasiyoambukiza wanahimizwa kufika katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre, ambayo sasa inatoa huduma hizo chini ya usimamizi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete.