Serikali imeendelea kuimarisha huduma na mazingira katika Makazi ya Wazee na Wasiojiweza kwa lengo la kuhakikisha wazee wanaishi kwa heshima, usalama na kupata huduma stahiki za kijamii na afya.

Hayo yamesema na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi tarehe 20, Februari 2026 wakati alipotembelea Makazi ya wazee Nunge  yaliyopo Kigamboni, mkoani Dar Es Salaam kwa lengo la kujionea hali ya utoaji wa huduma na kusikiliza changamoto zinazowakabili wazee wanaoishi katika kituo hicho. 

Mhandisi Mahundi amesema Serikali inawatambua Wazee kama tunu, hazina ya hekima na msingi wa maadili ya Taifa hivyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha mazingira ya kuishi kwa Wazee, hususan wale walio katika mazingira hatarishi na wasiokuwa na msaada wa familia.

“Ndugu zangu nipende kusema Serikali inawatambua Wazee kama tunu, hazina ya hekima na msingi wa maadili ya Taifa letu, Tunathamini mchango wenu mkubwa walioutoa katika ujenzi wa familia, jamii na Taifa na tutaendelea kuhakikisha wanaishi kwa heshima, usalama na utu wanaostahili ni ukweli usiopingika kuwa kuzeeka ni hatua ya maisha ambayo kila mmoja wetu anaelekea kuifikia na kufikia uzee ni neema kubwa ya Mwenyezi Mungu,” amesema Mhandisi Mahundi. 

Kwa upande wake, Mfawidhi wa Makazi ya Wazee Nunge, Jacklina Kanyamwenge, amesema kituo hicho kinaendelea kutoa huduma mbalimbali kwa wazee ikiwemo malazi, lishe na huduma za afya kwa lengo la kuhakikisha ustawi wao unaimarika.

“Tunawahudumia wazee hawa kwa kuwapatia mahitaji yao muhimu ya kila siku na tunaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali kuboresha zaidi huduma na mazingira ya makazi haya ili yaendane na mahitaji yao,” amesema Jacklina.

Nao Baadhi ya wazee wanaoishi katika makazi hayo wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwapatia matunzo na huduma muhimu, wakisema hatua hiyo imewapa faraja na kuwafanya waishi kwa matumaini na amani.









 


Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya, Mkoa wa Dodoma limewasikiliza wananchi wa jamii ya Kiiraqw waliofika katika Baraza hilo kuwasilisha hoja na ushahidi wao katika mgogoro wa ardhi, wakidai kumiliki kihalali shamba lenye ukubwa wa ekari nane lililopo Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Hatua hiyo imekuja kufuatia maombi ya wadaawa hao ambao ni pande mbili zinazohusika katika shauri hilo, kubainisha kuwa wanakabiliwa na changamoto ya lugha, hali iliyokuwa ikiathiri uwezo wao wa kujitetea na kueleza kwa uwazi hoja zao mbele ya Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Omary Mbega.

Kutokana na hilo, Baraza lilitoa huduma ya ukalimani kupitia mkalimani, Ndg. Simon Tlatlaa Emmay, ambaye alitafsiri maelezo yao na kuwawezesha wadaawa hao kufafanua kwa kina madai yao, kuwasilisha ushahidi pamoja na vielelezo muhimu bila kikwazo cha lugha.

Shauri hilo ni Shauri la Ardhi Na. 92 la mwaka 2025, linalomhusu Ekaristi Ngu’nda kama Mleta Maombi dhidi ya Lolote Nanacha na Martin Lolo Nanacha, ambao ni Wajibu Maombi. Mgogoro huo unahusu umiliki wa shamba lenye ukubwa wa ekari nane lililopo Kitongoji cha Msunjirire, Kijiji cha Zajilwa, Kata ya Zajilwa, Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Katika madai yake, Mleta Maombi anadai kuwa ndiye mmiliki halali wa eneo hilo la ardhi, akieleza kuwa ekari hizo ziliuzwa na Wajibu Maombi kwa utaratibu unaozua mgogoro wa kisheria.

Akizungumza mara baada ya kusikilizwa kwa shauri hilo, mmoja wa Wajibu Maombi, Ndg. Lolo Nanacha, alisema uwepo wa mkalimani umeimarisha imani yake katika mfumo wa utoaji haki.

“Leo nimejisikia huru kueleza ukweli wangu. Nimeeleweka vizuri, na ninaamini haki itatendeka,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Omary Mbega, alisisitiza kuwa huduma ya ukalimani ni sehemu muhimu ya kuhakikisha kila mwananchi anapata haki sawa bila kujali tofauti ya lugha au asili yake.

Shauri hilo limeahirishwa hadi tarehe 15 Aprili 2026, ambapo mashahidi zaidi watasikilizwa kabla ya kutolewa uamuzi wa mwisho.





Katika kipindi hiki cha Ramadhan na Kwaresma kinachosisitiza ibada, mshikamano na kujitafakari, Oryx Gas Tanzania imezindua kampeni ya “Pishi la Kibabe” yenye lengo la kurahisisha upatikanaji wa nishati safi ya kupikia.

Akizungumza leo Februari 20,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi huo Meneja Masoko na Mauzo wa Oryx Gas Tanzania Shaban Fundi amesema huu ni mwezi wa kujitafakari ,kushirikiana ,kujitolea na zaidi ya yote kuunganisha watu wote.

“Ili kuunga mkono wateja wetu katika kipindi hiki maalum tunatoa bei ya promosheni kwenye mitungi yetu mipya ya kilo sita itauzwa kwa Sh.37000 nchi nzima hadi Zanzibar.”amesema Fundi-

Pia amesema mbali ya kupunguza bei katika kipindi hiki cha Ramadhan na Kwaresma wateja wao watakaonunua au kujaza gesi kwenye maduka maalum ya Oryx na Mangi Shop watapokea zawadi ya futari papo kama ishara ya shukrani yao kwao.

Akizungumza kuhusu gharama za mtungi wa kilo sita amesema mpaka unafika nchini Tanzania gharama yake haipungui Sh.80,000 lakini Oryx katika soko mtungi huo unapatikana kwa Sh.40000 na kwa sasa tumetoa promosheni mpaka Sh.37000.

-“Hata hivyo tunaomba Serikali iendelee kuangalia katika maeneo mengine ili kuhakikisha kwamba gesi pamoja na mtungi bei yake inakuwa chini ili wananchi waweze kupata kwa bei nafuu.Kwafanya hivyo Oryx Gas kwa kushirikiana na Serikali tunaweza kufanikisha matumizi ya nishati safi kwa wananchi wengi zaidi.”

“Kuhusu gharama ukilinganisha mkaa na kuni bei yake iko juu zaidi ya nishati safi ya kupikia kwani kwa familia ya kawaida kwa siku moja inatumia kopo moja la mkaa ambalo linauzwa Sh.2000 hivyo kwa mwezi ni Sh.60,000 wakati mtungi wa gesi ya oryx wa kilo 6 ni Sh.40,000.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Benoit Araman amesema lengo la kampeni iliyozinduliwa kwa ajili ya Mfungo wa Mwezi wq Ramadhan na Kwaresma ni muendelezo wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhimiza wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.

“Oryx Gas lengo letu kubwa ni kuendelea kuhamasisha nishati safi ya kupikia na mimi na timu yangu tumejipanga vema kuhakikisha tunaendelea kufanya kampeni za kuwezesha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.Wakati huu wa Ramadhan na Kwaresma tunawatakia mfungo mwema lakini wakati huo huo tukihamasisha matumizi ya nishati safi.”

Wakati huo huo Mkuu wa Idara ya Mauzo ya Gesi kwa Ujumla Carloline Msokwa amesema kipindi hiki Waislamu na Wakristo wanaungana pamoja kuomba toba na ni kipindi ambacho familia zinakaa kufanya ibada na kuomba toba lakini pia ni wakati wa kupika chakula kizuri kwa ajili ya kufuturu.

“Kwahiyo Oryx Gas tumekuja na kampeni ya Pishi la kibabe ambapo familia zitakaa na kupika pamoja lakini pia Oryx tumetoa punguzo la bei ili kuwezesha wananchi kutumia gesi.Pia nitoe rai huu ni wakati wa Watanzania kuwa wamoja na tuliombee taifa letu.”


Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) imekutana na wadau wake wa ndani na nje ya nchi ikiwemo Wizara ya Maji na Benki ya Dunia katika kikao cha kujadili Mpangomkakati wa miaka mitano wa taasisi hiyo unaotoa mwelekeo wa vipaumbele vya kuimarisha huduma endelevu ya Maji safi ya bomba kwa wakazi wa maeneo ya vijijini katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

Akifungua kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Februari 20, 2026, mwakilishi kutoka Wizara ya Maji Mha. Mashaka Sitta ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uendeshaji na Matengenezo alisema mwelekeo wa RUWASA kuelekeza nguvu zaidi katika kuimarisha huduma endelevu ya maji ni jambo muhimu kwa sasa kwani tayari imeshajenga miradi mingi vijijini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu wa RUWASA Titus Mkapa ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu Mha. Wolta Kirita aliwapongeza na kuwashukuru wadau wote wa maendeleo wanaoshirikiana na taasisi hiyo ambapo alisema baadhi ya vipaumbele katika kipindi cha miaka mitano ijayo ni pamoja na kuhakikisha huduma ya maji vijijini inakuwa imara na endelevu pamoja na kuimarisha eneo la data na takwimu.

Akitoa maelezo ya awali, Mkurugenzi wa Mipango wa RUWASA Enock Wagala alisema kuwa, nyaraka hiyo ya Mpangomkakati wa miaka mitano imeshapitia hatua tofauti za maandalizi na sasa inawasilishwa kwa wadau wa maendeleo hususan wa maji vijijini ili watoe maoni na michango yao katika kuboresha na kuwa sehemu muhimu ya mpangomkakati huo wakati wa utekelezaji wake.

Mkurugenzi Wagala alitaja maeneo makuu Matano ambayo yamepewa kipaumbele zaidi katika Mpangomkakati huo kuwa ni pamoja na uendelevu wa huduma ya maji vijijini, kujenga miradi katika vijiji 1575 vilivyobaki, kuimarisha mbinu za upatikanaji wa fedha, kukamilisha ujenzi wa miradi 878, na kujenga na kuimarisha huduma za usafi wa mazingira vijijini.

Takribani taasisi za wadau 40 walihudhuria kikao hicho ambapo baadhi ya wadau hao ni Wizara ya Maji, Benki ya Dunia, AfDB, Oikos ETS, Water Mission Tanzania, Global Water Center, TAWASANET, Water for Pepople, Netherland Development Organization, UNICEF, CRDB, World Vision Tanzania, Benki ya Equity, NMB, Global Water Partnership Tanzania na DPG WASH Secretariet.








 


Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Shinyanga Mabala Mlolwa, amempongeza Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba, kwa kutopandisha mabega kulingana na nafasi yake, na kuhudhuria kikao cha Baraza cha Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Mkoani humo, licha ya kuwa na vikao vingi lakini ametanguliza chama kwanza.

Mabala ametoa pongezi hizo leo Februari 20, 2026, wakati akifungua kikao cha baraza cha UWT CCM mkoani humo.

Amesema, amefarijika kumuona Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba kwenye kikao hicho, pamoja na Mjumbe wa Mkutano wa SADC Mwanahamisi Munkunda, kwa kutanguliza Chama kwanza licha ya kuwa na vikao vingi, na kusema kwamba huo ndiyo uzalendo.

“Nakupongeza Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba kwa kuhuhuria kikao hiki cha baraza la UWT pamoja na mwenzako Mjumbe wa SADC Mwanahamisi, kutokana na nafasi zenu mgeweza kupandisha mabega na kutohudhuria kabisa na kutoa hudhuru kuwa mnavikao vingi, lakini kwa uzalendo wenu mmetanguliza chama kwanza,” amesema Mabala.

“Najua Salome una mkutano mwingine na ulipaswa kuwapo huko, lakini ukasema uhudhurie kwanza kwenye kikao hiki cha UWT hapa Shinyanga, nafasi yako uliyonayo upo kwa ajili ya kumsaidia Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na wanawake wa Shinyanga hongera sana kwa kuaminiwa na Rais na kuonyesha uzalendo,” ameongeza.

Aidha, amemmwagia pia sifa Salome Makamba, kwamba yeye siyo mtu wa maneno maneno wala kuwa na makundi, bali ni mtu wa kuchapa kazi na kutekeleza maagizo ambayo hupewa na kumsihi aendelee hivyo hivyo kukitumikia Chama na Taifa kwa ujumla kwa kuwaletea maendeleo wananchi kupitia Sekta ya Nishati.

Katika hatua nyingine Mabala amewaomba UWT Mkoani humo waendelee kuwa na umoja, mshikamano na upendo na kujiepusha na migogoro ili kuendeleza Jumuiya yao ipate kusongambele, na kuimarika zaidi.

Naye Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba, akizungumza kwenye kikao hicho, amesema amefarijika kuhudhuria kikao hicho, huku akiwashukuru UWT kwa kumpigia kura nyingi za ushindi Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, katika uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 29, 2025, pamoja na kumshukuru Rais kwa kumuamini na kumpatia dhamana ya kuwa Naibu Waziri wa Nishati, kwamba ataitendea haki nafasi hiyo kwa kuchapa kazi, na hatowaangusha wanawake wa Shinyanga.

“kwa mara ya kwanza UWT Mkoa wa Shinyanga imetoa Naibu Waziri wa Nishati kupitia Vitimaalum, hii dhamana ambayo nimepewa na Rais ni kubwa sana, sito waangusha wanawake wa Shinyanga nitachapa kazi kwa bidii zote kumsaidia Rais,” amesema Makamba.












📌Aipongeza TPDC kwa ujenzi wa vituo vya CNG; utekelezaji wa ajenda ya nishati safi ya kupikia

📌Asisitiza kuhusu ushirikishwaji kamilifu wa wazawa katika miradi

Watendaji katika Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) wametakiwa kutekeleza kwa vitendo maelekezo ya Viongozi Wakuu wa Kitaifa yanayolenga kuendeleza sekta ya mafuta na gesi asilia, ikiwemo agizo la kuhakikisha mazungumzo ya Mradi wa Kuchakata Gesi kuwa Kimiminika (LNG) yanakamilika kwa wakati ili utekelezaji wake uanze.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema hayo tarehe 20 Februari, 2026 jijini Mwanza wakati akifunga kikao kazi cha menejimenti ya TPDC kilicholenga kujadili mipango na bajeti ya Shirika kwa mwaka 2026/2027 pamoja na kufanya tathmini ya utendaji kazi wa Shirika.

“Maelekezo mengine yaliyotolewa ni pamoja na kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2030 ujenzi wa Bomba la Kusafirisha Gesi Asilia kutoka Kinyerezi hadi Chalinze unakamilika, pamoja na kuharakisha ujenzi wa vituo vya Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (CNG) katika mikoa ya Morogoro na Dodoma. Haya ni maelekezo ya kimkakati yanayohitaji mshikamano, umakini na kasi ya utekelezaji kutoka TPDC na wadau wake, na utekelezaji wa maelekezo haya utafanyiwa tathmini,” amesema Mhe. Salome.

Aidha, Mhe. Salome amelitaka Shirika hilo kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa mafuta ya kutosha, ikiwemo kwa kujenga miundombinu ya hifadhi ya mafuta, kuimarisha shughuli za utafutaji, uzalishaji na usambazaji wa gesi asilia viwandani, kwenye taasisi, majumbani na kwenye magari, pamoja na kukamilisha miradi ya kimkakati ukiwemo wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Kuhusu utekelezaji wa Ajenda ya Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, Mhe. Salome amepongeza jitihada za TPDC katika miradi ya usambazaji wa gesi asilia kama nishati safi ya kupikia katika mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam, na kulitaka Shirika hilo kuongeza kasi ili kufikia mikoa mingine.

Vilevile ameipongeza TPDC kwa mchango wake katika kuchochea matumizi ya CNG na hivyo kupunguza foleni katika vituo vya kujaza gesi kwenye magari. Amesema juhudi za TPDC pia zimeonekana kupitia ujenzi wa kituo mama cha CNG katika Barabara ya Sam Nujoma, Dar es Salaam, ambacho kinaendelea kuchochea wawekezaji binafsi kuanzisha vituo vyao kutokana na uhakika wa upatikanaji wa gesi. Pia amepongeza utoaji wa idhini kwa kampuni binafsi kuwekeza katika biashara ya CNG.

Katika hatua nyingine, TPDC pia imetakiwa kutokubaki nyuma katika matumizi ya teknolojia na mageuzi ya kidijitali, ikiwemo matumizi ya Akili Mnemba (Artificial Intelligence – AI), mifumo ya kidijitali na uchambuzi wa takwimu kwani Serikali inatarajia TPDC ijipambanue kidijitali ili kurahisisha utoaji wa huduma, kupunguza urasimu, kuongeza uwazi katika manunuzi, kupunguza gharama za uendeshaji na kuongeza faida.

“Jambo jingine kubwa kwenu TPDC, mnapaswa wakati wote mjiridhishe kuhusu ushirikishwaji wa wazawa kwa kuhakiki uhalali wa kampuni za wazawa, si kwa usajili tu hapa nchini bali kwa uhalisia wa umiliki wa kampuni hizo. Nasisitiza pia umuhimu wa uwajibikaji kwa jamii (CSR), kwani miradi ya mafuta na gesi inapaswa kuleta manufaa yanayoonekana kwa jamii zinazozunguka maeneo ya miradi. Tayari mmeanza kufanya vizuri katika eneo hili, lakini mnapaswa kuongeza juhudi,” amesema Mhe. Salome.

Naye, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Mafuta na Gesi Asilia), Mhandisi Antelimi Raphael  ameipongeza TPDC kwa kikao hicho cha kujitathmini, akisema ni hatua muhimu katika kuendeleza Shirika.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame, alisema kikao hicho kililenga kujadili mipango na bajeti ya Shirika kwa mwaka 2026/2027. Pia kililenga kufanya tathmini ya utendaji kazi ili kubaini changamoto na kuzitatua, hivyo kuiwezesha miradi kuendelea kwa kasi iliyokusudiwa.

Kikao hicho pia kilienda sambamba na mafunzo mbalimbali ikiwemo ya uongozi.











 

Wakulima wa zao la pamba mkoa wa Simiyu ambao ni wanachama wa Vyama vya Ushirika wameshauriwa kulima kwa tija kwa kutumia teknolojia ya kisasa na kuepukana kilimo cha mazoea ambacho kinawapa hasara.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha katika Mkutano wa 8 Chama Kikuu Simiyu, SIMCU (2018) LTD, uliofanyika leo Februari 20, 2026 Wilayani Maswa Mkoa wa Simiyu, pia amewaahakikishia wakulima kuwa Serikali itaendelea kuwawezesha kwa kutoa rudhuku za mbolea, viuatilifu na kutafuta masoko ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo.

"Mkulima anapata kilo mia tatu za pamba kwa heka ni hasara na ni upotevu wa muda inabidi tutoke kwenye kilimo cha namna hii..." alisema Mhe. Macha

Akizungumza kwa niaba ya Mrajis wa Vyama vya Ushirika nchini, Consolata Kiluma, ambaye ni Naibu Mrajis - Uhamasishaji, amewasistiza wajumbe wa bodi za vyama vya Ushirika kuwa waadilifu na waaminifu katika kutekeleza majukumu, na kuwa wabunifu kuleta ushindani kwenye biashara kama kauli mbiu isemavyo "Ushirika ni Biashara" ili kuongeza mapato kwa maslahi ya wanaushirika na Wananchi kwa ujumla.

Aidha, Mrajis Msaidizi Mkoa wa Simiyu Godfrey Mpepo amesema Ushirika umeendelea kuimarika tangu kilipoanzishwa chama kikuu SIMCU Ltd mwaka 2018, ambapo awali vyama vya mkoa huo vilikuwa vikisimamiwa na SHIRECU chama kikuu kutoka mkoa wa Shinyanga.

Naye, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Shemsha Mohamed amewataka wajumbe wa Mkutano huo kuepuka na ubadhilifu wa fedha za wanachama jambo ambalo linarudisha Ushirika nyuma kimaendeleo.

Awali, akitoa taarifa ya Utendaji wa SIMCU(2018) LTD, Meneja Mkuu wa chama hicho, Mercy Atanazi alibainisha kuwa mkutano huo umehudhuriwa na wajumbe 625 kati ya wajumbe 675 kutoka vyama wanachama 335.