Baadhi ya wananchi waliotembelea banda la Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) katika Kliniki maalum ya kutatua kero za wananchi iliyofanyika katika viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma, wameshauri Wakala kuanza kujenga nyumba za makazi kwa ajili ya kupangishwa kwa watu binafsi kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya nyumba za kupanga katika mkoa huo.

Ushauri huo umetolewa wakati wa kliniki hiyo iliyolenga kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali za wananchi, sambamba na kuonesha miradi iliyotekelezwa ndani ya siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu kuingia madarakani.

Wananchi hao wamesema kuwa pamoja na mahitaji ya nyumba za makazi kwa watumishi wa umma, bado kuna uhitaji mkubwa wa nyumba za kupanga kwa wananchi wa kawaida wanaoishi katika Jiji la Dodoma.

Bi. Saada Salum, mkazi wa Nzuguni Boda, amesema kuwa upatikanaji wa nyumba za kupanga bado ni changamoto kwa wakazi wengi wa Dodoma, hivyo TBA inapaswa kufikiria kupanua huduma zake ili kuwahusisha pia watu binafsi.

“Suala la nyumba za kupanga hapa Dodoma ni changamoto. Watu wengi wanahitaji nyumba za kupanga. TBA mnatakiwa kufikiria sasa kuanza kujenga nyumba na kupangisha watu binafsi ili nao waweze kukaa kwenye nyumba zenu, si watumishi wa serikali pekee yao,” amesema Bi. Salum.

Kwa upande wake, Peter Masule, mkazi wa Nzuguni kwa Masista, ameishukuru TBA kwa kutekeleza mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 katika eneo hilo, akisema kuwa mradi huo umechangia kuimarika kwa hali ya usalama tofauti na ilivyokuwa awali.

Amesema kabla ya mradi huo kulikuwa na matukio mengi ya uhalifu katika eneo hilo, ambapo wahalifu walikuwa wakitumia vichaka vilivyokuwepo kujificha baada ya kufanya wizi.

“Mimi nimekuwa mkazi wa Nzuguni kwa muda mrefu. Kabla ya mradi wa nyumba hizi kulikuwa na matukio mengi ya uhalifu, vibaka walikuwa wakija kujificha kwenye vichaka baada ya kufanya wizi. Lakini sasa matukio hayo yamepungua sana,” amesema Masule.

Wananchi hao pia wameeleza kuwa uwepo wa mradi wa nyumba hizo umechangia kuboresha mandhari na kupendezesha eneo la Nzuguni.

Kupitia kliniki hiyo, TBA pia imepata fursa ya kukutana na wadau na wateja wake, wengi wao wakiwa ni wapangaji wa nyumba zake, ambapo baadhi ya changamoto walizowasilisha zimepatiwa ufumbuzi papo hapo.

Kliniki hiyo ya siku tatu ilianza Jumatano, Machi 4, 2026 na kuhitimishwa Ijumaa, Machi 6, 2026 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayofanyika tarehe 08 Machi kila mwaka,Wakala wa huduma za Misitu (TFS) imepokea tuzo ya Shukrani kufuatia udhamini katika hafla ya The citizen rising woman Gala iliyofanyika tarehe 6 Machi Jijini Dar Es Salaam katika ukumbi wa The Super dome.

Tuzo hiyo ambayo ni ishara ya kutambua mchango wa TFS katika kufanikisha hafla hiyo yenye lengo la kutambua na kuthamini mchango wa mwanamke ambao ni chachu katika kuleta maendeleo endelevu nchini imepokelewa na Kaimu Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimali za Misitu TFS Dkt. Zainabu Shabani Bungwa.

Pamoja na wadau mbali mbali wanawake kutoka TFS ni miongoni mwa washiriki waliohudhuria hafla hiyo iliyopabwa na midahalo na burudani.

 

 


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba amesema utafiti unaonesha kuwa kuendesha gari la umeme nchini ni nafuu kwa takribani asilimia 85 kwa kila kilomita ikilinganishwa na gari linalotumia petroli au dizeli.

Mramba ameyasema hayo Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi rasmi wa matumizi ya magari ya umeme nchini kupitia kampuni ya DOW ELEF AUTO EV (ZERA) Limited.

Amesema kwa wastani gari linalotumia mafuta linaweza kugharimu takribani Sh.200 kwa kilomita moja, wakati gari la umeme linatumia karibu Sh.25 pekee kwa kilomita.

“Gharama hii inaonesha wazi kuwa teknolojia ya magari ya umeme ni nafuu zaidi na inaweza kusaidia wananchi kupunguza matumizi katika sekta ya usafiri,” amesema Mramba.

Ameeleza kuwa uzinduzi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya usafiri nchini na unaendana na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan za kukuza uwekezaji na kuhamasisha matumizi ya teknolojia safi ya nishati.

Mramba amesema Serikali tayari imeweka mazingira wezeshi kwa maendeleo ya teknolojia hiyo kwa kupitisha Mfumo wa Kitaifa wa Sera ya Magari ya Umeme (National Electric Vehicles Policy Framework) Desemba 2024.

Amesema sera hiyo inalenga kuhamasisha uzalishaji wa magari ya umeme nchini, kuongeza matumizi yake, kuunganisha sekta hiyo na nishati jadidifu pamoja na kujenga miundombinu ya vituo vya kuchaji magari hayo.

Aidha, amesema Tanzania imeendelea kupiga hatua katika uzalishaji wa umeme ambapo uwezo umeongezeka hadi zaidi ya megawati 4,500, huku upatikanaji wa umeme ukifikia asilimia 85.5 mwaka 2025.

Kwa mujibu wa Mramba, hatua hiyo inalenga kuimarisha sekta mbalimbali za kiuchumi ikiwamo usafiri wa kisasa wenye gharama nafuu na rafiki kwa mazingira.

Kwa sasa Afrika ina zaidi ya magari ya umeme 30,000, huku Afrika Mashariki ikijitokeza kuwa kitovu cha ubunifu katika sekta hiyo.

Nchini Tanzania, inakadiriwa kuwa tayari kuna zaidi ya magari ya umeme 10,000 yakiwemo pikipiki pamoja na vyombo vingine vya usafiri vya magurudumu mawili na matatu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya DOW ELEF AUTO EV (ZERA) Limited, Emmanuel Kazimoto, amesema kampuni hiyo imeanza na mpango wa kuagiza magari kamili ya umeme, kabla ya kuanza kuleta magari ya kuunganishwa hapa nchini.

Ameongeza kuwa lengo la baadaye ni kuanzisha kiwanda cha kuunganisha magari ya umeme nchini, hatua itakayochochea ajira na kuwajengea vijana wa Kitanzania ujuzi katika teknolojia ya kisasa.

 

Na: OWM (KAM) - Mwanza

Serikali imehimiza wananchi kujiunga katika na Hifadhi Skimu ili kujihakikishia usalama wa maisha yao ya sasa na baadaye ikiwemo kunufaika na mafao yanayotolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Akizungumza katika hafla ya uhamasishaji wa kujiunga na hifadhi hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu amewasihi wananchi kutumia fursa hiyo kujiunga kwa wingi na kuchangia kikamilifu ili wanufaike na mafao mbalimbali yakiwemo ya matibabu pamoja na mafao ya uzeeni.
Aidha, amesema kuwa Serikali kupitia Mfuko wa NSSF imeanzisha Skimu ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii kwa wananchi waliojiajiri kwa ajili ya kuhudumia Wananchi waliojiajiri kwenye shughuli za kiuchumi.
Waziri Sangu amebainisha kuwa Hifadhi Skimu ni mpango wa uchangiaji wa hiari unaolenga kuwafikia wananchi waliojiajiri wakiwemo wavuvi, wafanyabiashara, machinga, bodaboda, wakulima, wachimbaji wadogo, wasanii pamoja na makundi mengine  yanayounda sehemu kubwa ya nguvu kazi ya Taifa.
Vilevile, amesema Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kuweka mazingira rafiki ya ajira na kujiajiri sambamba na kuimarisha mifumo ya hifadhi ya jamii ili kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nyuma katika kunufaika na huduma hizo muhimu.
“Hifadhi ya jamii ni haki ya msingi inayosaidia wananchi kuwa na maisha yenye heshima hasa wanapofikia umri wa uzee au wanapokumbana na changamoto zisizotarajiwa kama vile maradhi” amesema.
Awali akizungumza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amewahimiza wananchi wa Mkoa wa huo kuchangamkia fursa ya kujiunga na Hifadhi Skimu, akieleza kuwa ni hatua muhimu ya kuilinda familia dhidi ya majanga ya maisha pamoja na kujihakikishia kipato cha baadaye.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii Masha Mshomba amesema Hifadhi Skimu itawasaidia wananchi kuboresha maisha yao kwa kuondokana na utegemezi, hivyo kuwawezesha kujitegemea kiuchumi na kupata usalama wa maisha yao si tu kwa sasa bali pia wanapofikia umri wa uzee.
 
 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati akizindua Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Na; Mwandishi Wetu,Dar es Salaam.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ametoa maagizo matano kwa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) kilichopo Morogoro mara baada ya kuizindua bodi hiyo.

Waziri Masauni ametoa maagizo hayo Machi 6, 2026 wakati wa uzinduzi wa Bodi hiyo jijini Dar es Salaam akieleza imepaswa kuimarisha mifumo ya kitaifa ya Upimaji, Utoaji Taarifa na Uhakiki wa gesijoto (MRV) ili kuhakikisha kuwa taarifa za kaboni nchini zinakuwa sahihi, za kuaminika na zinazokubalika kimataifa.

Pia ameielekeza Bodi hiyo kuhakikisha Miradi yote ya kaboni inayotekelezwa nchini inasimamiwa kwa ufanisi, uwazi na kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa pamoja na maslahi mapana ya Taifa. 

Mhe. Masauni ameongeza kuwa bodi inapaswa kuweka Mazingira wezeshi yatakayovutia uwekezaji wa ndani wa kimataifa katika Sekta ya Kaboni huku ikihakikisha kuwa uwekezaji huo unalinda rasilimali za Taifa na kuleta manufaa ya kweli kwa wananchi, kuhakikisha kunakuwepo mfumo wa haki na uwazi wa mgawanyiko wa manufaa ili jamii zinazohifadhi rasilimali za asili zinufaike moja kwa moja na Miradi ya Kaboni inayotekelezwa katika maeneo yao.

“Kuimarisha ushiriki wa Tanzania katika mifumo ya kimataifa ya biashara ya Kaboni hususan chini ya Ibara ya 6 ya Mkataba wa Paris, ikiwemo mifumo ya soko la Kaboni ili kuongeza fursa za kiuchumi kwa Taifa letu.

Aidha, ameisisitiza Bodi hiyo kufanya kazi kwa bidii na kuhakikisha Kituo hicho kinaendeshwa kwa uwajibikaji, uadilifu na weledi wa hali ya juu ili kuhakikisha mifumo ya Usimamizi wa Sekta ya Kaboni inalinda kikamilifu maslahi ya Taifa.

"Ni matarajio ya Serikali kuona kituo hiki kinakuwa kitovu cha ubora katika maswala ya ufuatiliaji wa Kaboni, biadhara ya Kaboni na Tafiti za mabadiliko ya tabianchi katika ukanda wa Afrika. Haya ni matarajio makubwa kwa taifa letu na yanahitaji Usimamizi madhubuti wa taasisi, mifumo imara ya ufuatiliaji pamoja na ushirikiano wa wadau wote.” Amesema Mhe. Masauni.

Ameongeza kuwa matarajio ya Serikali yaliyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, na Mpango wa muda mrefu wa Utekelezaji wake, sekta ya Kaboni inauwezo wa kuchangia takribani Dola za kimarekani bilioni mbili kwa Mwaka katika uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi, Dkt. Albina Chuwa amesema ushirikiano ndio jambo la msingi katika kufikisha lengo na ndoto za watanzania, hivyo watajitahidi kutafuta fursa ili kupata matokeo mazuri.

“Ushirikiano wa kutosha ndio naomba kutoka kwa kila mmoja wetu kwani haya yote tunayoyazungumza tutakuwa tunafanya kazi nyepesi katika kuhakikisha kituo chetu cha Kaboni kinafanya vizuri,” amesema Dkt. Albina.

Amesema Uzinduzi wa Bodi unakuja katika kipindi muhimu ambacho sekta ya biashara ya kaboni inaendelea kukua kwa kasi duniani na hapa nchini, NCMC ina jukumu muhimu la kuhakikisha kuwa rasilimali za kaboni za nchi yetu zinasimamiwa kwa uwazi, weledi na kwa kuzingatia mifumo na viwango vinavyokubalika kimataifa.

Wajumbe wanaounda Bodi hiyo ni Bw. Khamis Hamza Khamis, Bi. Amne Sued Kagasheki, Bi. Farhat Mabrouk, Dkt. Ladislaus Kyaruzi, Bw. Rishad Bade pamoja na Dkt.Philipina Fenest Shayo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati akizindua Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya NCMC, Dkt. Albina Chuwa (kushoto kwake), Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt, Festo Dugange, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi (kulia kwake) na Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda, mara baada ya uzinduzi wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akimpongeza Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC, Dkt. Albina Chuwa mara baada ya uzinduzi wa Bodi hiyo, Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam

Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Festo Dugange akizungumza wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), mara baada ya uzinduzi wa Bodi hiyo, Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS

 " NINA IMANI KUBWA NA UTENDAJI KAZI WA OFISI YA MWANDISHI MKUU WA SHERIA".  MWANASHERIA MKUU 



Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza S. Johari amewataka  Watumishi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kufanya kazi kwa Weledi na Ufanisi ili kufikia malengo ya Ofisi kwani ana Imani kubwa na utendaji kazi wa OFISI ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.


Mhe. Johari amesema hayo alipofungua kikao cha kwanza cha Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria tarehe 6 Machi, 2026 jijini Dar es Salaam.


*"Niwaombe muendelee kutekeleza majukumu ya Ofisi hii kwa Weledi na Ufanisi ili kufikia malengo ya Ofisi na nina imani kubwa na utendaji kazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria”* amesema Mhe. Johari 

Aidha Mhe. Johari ameendelea kwa kuwataka watumishi wa  Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kuzingatia kanuni na Sheria za Utumishi wa Umma ili kutoathiri utendaji kazi wa Serikali.


*"Utumishi wa Umma unaongozwa na Sheria pamoja na Kanuni, hivyo natoa rai kwa watumishi wote tuzingatie Miongozo ya Utumishi wa Umma ili tusiathiri utendaji kazi wa Serikali,"* ameongeza Mhe. Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Vilevile Mhe. Johari ameitaka Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kuboresha matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.


*"Naomba nisisitize matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kurahisisha utendaji kazi na kutoa kazi zenye ufanisi kwa matumizi ya Serikali na jamii kwa ujumla,"* ameeleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza Johari.

Awali, akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwandishi Mkuu wa Sheria, Bw. Onorius Njole, amesema Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria imewekeza nguvu kubwa kwenye mifumo ya TEHAMA ili kuendelea kuimarisha utendaji kazi.


*"Katika kuendelea kuimarisha  utekelezaji wa Uandishi wa Sheria tumeamua kuweka nguvu kubwa kwenye mifumo ya Tehama kwa kuanzisha e-drafting, e-translation na e-revision na kwa usaidizi wako Mwanasheria Mkuu wa Serikali tutaweza kufanikisha hili.* amesema.


Pia, Mwandishi Mkuu wa Sheria Bw. Njole amemshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuendelea kuwa kiongozi bora na mwenye msaada mkubwa kwa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.



*"Kwa niaba ya menejimenti ya Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria na Wafanyakazi wote, tunamshukuru Sana Mhe. Johari kwa kuwa kiongozi bora kwa Ofisi yetu, na kutupa ushirikiano kila tunapohitaji”* Amesema.


Miongoni mwa Wageni waalikwa katika Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria ni Mkurugenzi wa Mashtaka, Bw. Sylvester Mwakitalu. 


Baraza la kwanza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria, limefanyika tarehe 6 Machi, 2026 katika ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) jijini, Dar es salaam.

 

Na Mwandishi Wetu

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetangaza kufuta leseni ya rejareja ya bidhaa za mafuta ya petroli ya kampuni ya Iyan Energy Limited na kusitisha kwa muda wa miezi sita leseni ya kampuni ya Crescent Energy Tanzania Limited, baada ya kubaini ukiukwaji wa sheria na masharti ya leseni.

Kwa mujibu wa taarifa ya EWURA, uamuzi huo umefanyika kufuatia maamuzi yaliyotolewa na Bodi ya Wakurugenzi wakati wa vikao vyake vya hivi karibuni.

EWURA imesema leseni iliyofutwa ni Petroleum Retail Licence Na. PRL-2018-269, iliyokuwa ikimilikiwa na Iyan Energy Limited kwa ajili ya kuendesha biashara ya rejareja ya mafuta katika Kiwanja Na. 26 na 27, Barabara ya Pangani, Jiji la Tanga.

Wakati huohuo, Bodi imesitisha kwa muda wa miezi sita leseni ya rejareja ya bidhaa za mafuta ya petroli Namba PRL-2022-296 ya Crescent Energy Tanzania Limited, iliyotolewa kwa ajili ya kuendesha biashara ya rejareja katika Kiwanja Na. 5, Kitalu “N”, Eneo la Chamakweza, Wilaya ya Chalinze, Mkoa wa Pwani.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa maamuzi hayo yamefanyika baada ya EWURA kujiridhisha kuwa kampuni hizo zilikuwa zikijihusisha na shughuli zinazofanana na biashara ya uuzaji wa bidhaa za mafuta kwa jumla, hali ambayo haikuruhusiwa chini ya leseni za rejareja walizokuwa nazo.

EWURA imeeleza kuwa hatua hizo zinakiuka Kifungu Na. 131 cha Sheria ya Petroli, Sura ya 392, pamoja na Kanuni ya 9 na 11 za Kanuni za Mafuta (Biashara ya Jumla, Uhifadhi, Rejareja na Matumizi Binafsi), Tangazo la Serikali Na. 150/2022.

Onyo kwa umma

Katika taarifa yake, EWURA imeutaarifu umma kuwa kujihusisha kwa namna yoyote na kampuni hizo katika biashara ya usambazaji wa bidhaa za mafuta ya petroli kutakuwa kinyume cha sheria, na kwamba hatua stahiki za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watakaokiuka.

Mamlaka hiyo imeongeza kuwa itaendelea kusimamia sekta ya mafuta kwa kuhakikisha kunakuwa na mazingira ya ushindani wa haki na upatikanaji wa uhakika wa bidhaa za mafuta nchini, kwa kudumisha “uwanja ulio sawa” kwa wadau wote.

 

Na Mwandishi Wetu, Handeni

Wanawake katika Halmashauri ya Mji Handeni wametakiwa kutumia simu janja na teknolojia ya kidijitali kwa kuwa ni nyenzo muhimu ya kukuza biashara na kujikwamua kiuchumi kupitia fursa mbalimbali zinazopatikana mtandaoni.

 Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese ameyasema hayo wakati akizindua Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi katika kongamano la wanawake lililofanyika mjini Handeni.

Amesema matumizi sahihi ya simu janja yanaweza kuwasaidia wanawake kupanua masoko ya biashara zao kupitia mitandao ya kijamii pamoja na kupata taarifa muhimu za fursa za kiuchumi zinazotolewa na serikali.

Nyamwese amesema jukwaa hilo limekuja wakati muafaka kutokana na juhudi za serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuwawezesha kiuchumi wanawake na wasichana.

“Jukwaa hili litawawezesha kupata fursa na kujadiliana namna ya kujikwamua. Mtapata mbinu mbalimbali za kuongeza thamani ya biashara zenu na namna ya kuzifikia fursa zinazotolewa na serikali ikiwamo mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri,” amesema.

Aidha, amewasisitiza wanawake kuwa wabunifu katika biashara zao na kutumia kikamilifu teknolojia pamoja na mikopo inayotolewa na halmashauri ili kujiongezea kipato.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju amesema halmashauri imeandaa mkakati wa kusaidia vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kujiunga kwenye mfumo wa ununuzi wa umma wa NeST ili viweze kunufaika na fursa ya asilimia 30 ya zabuni zinazotolewa kwa makundi hayo.

Amesema kupitia mfumo huo vikundi vitapata nafasi ya kushiriki kikamilifu katika zabuni zinazotangazwa na halmashauri na hivyo kuongeza kipato na kukuza uchumi wao.

Akizungumza kuhusu kongamano hilo, Mkurugenzi huyo amesema katika kongamano hilo wanawake walipata elimu mbalimbali ikiwamo masuala ya fedha, msaada wa kisheria, umiliki wa ardhi pamoja na masuala ya ndoa ili kuwajengea uelewa na kuwasaidia kuwa chachu ya maendeleo ya Handeni.

Aliongeza kuwa elimu hiyo pia inalenga kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa yaliyowekwa katika Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Akisoma taarifa ya uendeshaji wa shughuli za majukwaa ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, Mratibu wa majukwaa hayo, Carin Umwambe amesema jukwaa hilo linalenga kuwaunganisha wanawake wajasiriamali na watoa huduma katika sekta za umma na binafsi ili waweze kupata fursa mbalimbali za kiuchumi na kibiashara.

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Dodoma unashiriki katika Kliniki maalum ya kutatua kero na changamoto mbalimbali za wananchi iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, inayofanyika tarehe 3 hadi 6 Machi, 2026 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Kupitia kliniki hiyo, TBA inakutana na wateja wake ambao ni wapangaji wa nyumba zake kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto pamoja na kero mbalimbali zinazojitokeza katika maeneo wanayoishi.

Aidha, kliniki hiyo imekuwa fursa kwa taasisi mbalimbali za Serikali kutoa elimu kwa wananchi pamoja na kueleza mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa majukumu yao ndani ya siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu kuingia madarakani.

Katika kliniki hiyo, TBA kama zilivyo taasisi nyingine za Serikali imeweka banda maalum kwa ajili ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake pamoja na kueleza miradi mbalimbali iliyotekelezwa na wakala huo katika kipindi hicho.

Akitembelea mabanda ya taasisi mbalimbali katika viwanja hivyo leo Machi 5, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameipongeza TBA kwa kutekeleza miradi mikubwa ya Serikali katika mkoa wa Dodoma, ikiwemo ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 za makazi ya watumishi wa umma katika eneo la Nzuguni.

Kwa upande wao, wananchi waliotembelea banda la TBA wamepongeza utekelezaji wa mradi wa nyumba za makazi katika eneo la Nzuguni, wakisema umechangia kusogeza huduma za kijamii na biashara karibu na wananchi pamoja na kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika eneo hilo.

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kupitia Kanda ya Kaskazini, leo tarehe 5 Machi 2026 imetoa elimu kwa viongozi wa Wilaya ya Korogwe katika semina iliyofanyika katika ukumbi wa GMCC.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, George Mhina, alisema lengo ni kuwajengea viongozi uelewa kuhusu majukumu ya EWURA na maeneo inayoyadhibiti ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika semina hiyo, washiriki walipatiwa elimu kuhusu umuhimu wa uvunaji wa maji ya mvua, matumizi ya nishati safi ya kupikia, leseni za mafundi umeme, ujenzi wa vituo vya mafuta vijijini pamoja na namna ya kutatua migogoro katika sekta za maji na nishati.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Mhe. William Mwakilema amewasisitiza viongozi hao kuwa mabalozi wa elimu waliyoipata kwa kuhakikisha wanaifikisha kwa wananchi ili kuongeza uelewa na matumizi sahihi ya huduma za maji na nishati.