Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 22 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kuimarisha usimamizi na udhibiti wa shughuli za gesi asilia katika mkondo wa kati na chini, hatua inayolenga kuhakikisha usalama wa miundombinu, upatikanaji wa huduma bora pamoja na kukuza matumizi ya nishati safi nchini.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, wakati akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa fedha 2026/2027 leo Aprili 22,2026 bungeni Dodoma.
Amesema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, EWURA ilifanya kaguzi 68 katika miundombinu ya gesi asilia iliyopo katika mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam. Miundombinu hiyo inahusisha mitambo minne ya uchakataji, miwili ya usafirishaji, mtandao wa usambazaji wenye urefu wa kilomita 243 pamoja na vituo 18 vya kujazia gesi asilia iliyoshindiliwa (CNG) kwa magari. Taarifa zinaonesha kuwa miundombinu yote iliyokaguliwa ilikidhi viwango vya ubora vinavyotakiwa.
Katika kuendeleza sekta hiyo, EWURA ilitoa vibali tisa vya ujenzi wa vituo vya CNG katika mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro na Ruvuma. Maeneo yaliyopata vibali katika mkoa wa Dar es Salaam ni pamoja na Mbezi Beach, Mbagala, Kigamboni, Buguruni, Mwenge, Kinyerezi na Gongolamboto, huku Morogoro (Msamvu) na Ruvuma (Tunduru) kila mmoja ukipata kibali kimoja.
Aidha, vibali viwili vilitolewa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya kupokelea gesi asilia iliyoshindiliwa kwa matumizi ya viwanda vilivyopo Kibaha mkoani Pwani, hatua inayotarajiwa kuongeza matumizi ya nishati hiyo katika uzalishaji wa viwandani.
Katika sekta ya usafirishaji na usambazaji, EWURA ilitoa vibali saba vya ujenzi wa mabomba ya gesi asilia, ikiwemo mabomba ya kuunganisha gesi kwenye viwanda, taasisi, migahawa na majumbani, pamoja na mabomba ya kuhudumia vituo vya CNG. Kibali kingine kilihusu ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kutoka Ntorya hadi Madimba mkoani Mtwara.
Sambamba na hilo, jumla ya leseni 17 zilitolewa kwa ajili ya uendeshaji na usafirishaji wa gesi asilia, zikiwemo leseni za vituo vya CNG na usambazaji wa gesi katika mkoa wa Pwani. Ongezeko la utoaji wa vibali na leseni linaonesha mwitikio mkubwa wa sekta binafsi kushiriki katika mnyororo wa thamani wa gesi asilia.
Serikali imeeleza kuwa itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika sekta hiyo, hasa katika mikoa ya kimkakati kama Morogoro, Dodoma, Mbeya na Tanga. Wito umetolewa kwa sekta binafsi kuchangamkia fursa zilizopo, kufuatia ongezeko la matumizi ya gesi asilia katika usafiri, viwandani na matumizi ya majumbani.
Hatua hizi zinaakisi dhamira ya Serikali ya kuhakikisha gesi asilia inakuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi, huku ikichangia upatikanaji wa nishati safi, nafuu na salama kwa wananchi.
Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Bw. Wilfred Mwakalosi,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kwenye banda la EWURA wakati wa maonesho ya Wiki ya Nishati yanayoendelea katika viwanja vya bunge jijini Dodoma.
























