Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki na wajibu wao katika sekta za nishati na maji, sambamba na kuhamasisha uwekezaji wa vituo vya mafuta vijijini ili kuongeza upatikanaji wa huduma salama na kukomesha biashara holela ya mafuta.

Hatua hiyo ni sehemu ya mafanikio ya ushiriki wa EWURA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma, ambapo maelfu ya wananchi wamefika katika banda la mamlaka hiyo kupata elimu na ufafanuzi kuhusu huduma mbalimbali zinazodhibitiwa na EWURA.

Akizungumza katika maonesho hayo, Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesema kwa siku nane mfululizo mamlaka hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi kuhusu sekta za mafuta, umeme, gesi asilia na maji, pamoja na kupokea na kushughulikia maswali na changamoto mbalimbali zinazowakabili watumiaji wa huduma hizo.

Amesema wananchi wengi walitumia fursa hiyo kupata ufahamu kuhusu namna ya kuwasilisha malalamiko wanapokumbana na changamoto za huduma, huku mada ya uwekezaji katika vituo vya mafuta vijijini ikiwa miongoni mwa masuala yaliyoibua maswali mengi zaidi.

“Wananchi wengi walitaka kufahamu taratibu na fursa zilizopo za kuanzisha vituo vya kisasa vya mafuta vijijini ili kuondokana na biashara ya mafuta inayofanyika kwa kutumia chupa, ndoo na magaloni, ambayo mara nyingi huhatarisha usalama wa watu na mali,” amesema Mwakalosi.

Ameeleza kuwa Serikali kupitia EWURA imeweka mazingira rafiki ya uwekezaji kwa kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za vibali na leseni kwa wawekezaji wa vituo vya mafuta vijijini.

Kwa mujibu wa EWURA, ada ya kibali cha ujenzi wa kituo cha mafuta katika maeneo ya vijijini imepunguzwa kutoka Shilingi 500,000 zinazotozwa maeneo ya mijini hadi Shilingi 50,000, huku ada ya leseni ikishushwa kutoka Shilingi milioni moja hadi Shilingi 100,000.

Mbali na punguzo hilo, EWURA imepunguza baadhi ya masharti ya uwekezaji kwa kuruhusu matumizi ya nyaraka za uthibitisho wa umiliki wa ardhi zinazotolewa na serikali za vijiji badala ya hati kamili za ardhi zinazohitajika katika maeneo ya mijini.

Hatua hiyo inalenga kuvutia wawekezaji wengi zaidi katika maeneo ya vijijini na kuongeza upatikanaji wa mafuta kwa njia salama, nafuu na inayozingatia viwango vya usalama.

Katika maonesho hayo, wananchi pia walipata ufafanuzi kuhusu namna EWURA inavyosimamia ukokotoaji wa bei za mafuta, viwango vya huduma za maji na umeme, pamoja na taratibu za kuwasilisha malalamiko pale wanaporidhika au kutoridhika na huduma zinazotolewa na watoa huduma.

Aidha, Mwakalosi amewahimiza wananchi kusoma na kuelewa mikataba ya huduma kwa wateja inayotolewa na taasisi za maji, umeme na nishati, akieleza kuwa mikataba hiyo inaainisha kwa uwazi haki, wajibu na viwango vya huduma vinavyopaswa kutolewa kwa mteja.

Amesisitiza kuwa wananchi wenye uelewa wa mikataba hiyo wanakuwa na uwezo mkubwa wa kudai huduma bora, kufuatilia utekelezaji wa haki zao na hata kudai fidia pale ambapo watoa huduma watashindwa kutekeleza viwango walivyoahidi.

Vilevile, EWURA imewahakikishia wananchi kuwa nchi inaendelea kuwa na hali nzuri ya upatikanaji wa umeme, gesi na maji kutokana na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta hizo.

Mwakalosi ametaja ongezeko la uzalishaji wa umeme kupitia Bwawa la Mwalimu Nyerere kuwa miongoni mwa hatua zilizochangia kuimarika kwa huduma za nishati nchini, huku EWURA ikiendelea kusimamia upatikanaji endelevu wa huduma za maji na nishati kwa manufaa ya wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.




Na Mwandishi Wetu - Dodoma


Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imehitimisha kwa mafanikio ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, ambapo ilitoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya mionzi na mchango wa teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Katika kipindi chote cha maonesho hayo, banda la TAEC lilitembelewa na wananchi, wanafunzi, wataalamu na wadau mbalimbali waliopata fursa ya kujifunza kuhusu majukumu ya Tume katika kusimamia matumizi ya mionzi nchini pamoja na kuhakikisha teknolojia ya nyuklia inatumika kwa kuzingatia viwango vya usalama vinavyolinda afya za binadamu na mazingira.

Wataalamu wa TAEC walitoa elimu kuhusu usimamizi na udhibiti wa matumizi ya vyanzo vya mionzi, utoaji wa vibali kwa watumiaji wa teknolojia hiyo pamoja na ukaguzi wa mara kwa mara unaofanyika katika taasisi na maeneo mbalimbali yanayotumia vifaa vya mionzi ili kuhakikisha usalama unaendelea kuzingatiwa wakati wote.

Aidha, wananchi walipata uelewa kuhusu matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, viwanda, migodi, maji na utafiti wa kisayansi. Elimu hiyo ilibainisha mchango mkubwa wa teknolojia hiyo katika kuboresha huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa, kuongeza uzalishaji katika sekta za uzalishaji na kusaidia matumizi endelevu ya rasilimali za taifa.

Vilevile, TAEC ilitoa ufafanuzi kuhusu nafasi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati ya umeme, ikieleza namna teknolojia hiyo inavyoweza kuchangia upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa ajili ya kuendeleza shughuli za viwanda, biashara na ukuaji wa uchumi wa taifa.

Katika sekta ya afya, wananchi walielimishwa kuhusu matumizi ya mionzi katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali, huku katika sekta ya chakula wakipata maelezo kuhusu matumizi ya teknolojia ya mionzi katika uhifadhi wa mazao na bidhaa za chakula kwa kuzuia uharibifu unaosababishwa na wadudu na vimelea, hivyo kuongeza muda wa matumizi na kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvunwa.

Mbali na kupata elimu, washiriki wa maonesho hayo walipata fursa ya kuuliza maswali na kufanya majadiliano ya moja kwa moja na wataalamu wa TAEC kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu usalama wa mionzi, hatua za tahadhari zinazopaswa kuzingatiwa pamoja na mchango wa Tume katika kulinda jamii dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na matumizi yasiyo salama ya mionzi.

TAEC imeeleza kuwa ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi, kutoa taarifa sahihi kuhusu huduma zake na kuongeza uelewa wa umma kuhusu matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyohitimishwa leo yameendelea kutoa fursa kwa taasisi za umma kuwasilisha huduma zao kwa wananchi, kuimarisha uwajibikaji, kujenga imani ya umma na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu mchango wa taasisi hizo katika maendeleo ya Tanzania.











 

Dodoma

Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, amepongeza matumizi ya mfumo wa kisasa wa Supervisory Control and Data Acquisition (SCADA) unaotumiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), akisema umeongeza uwazi na ufanisi katika usimamizi wa mafuta nchini.

Dkt. Nguvila alitoa pongezi hizo Juni 23, 2026, alipotembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma na kupata maelezo kuhusu namna mfumo huo unavyofanya kazi.

Alisema matumizi ya teknolojia za kisasa katika sekta ya mafuta yanaisaidia Serikali kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mafuta yanayoingia nchini na kuhifadhiwa katika maghala mbalimbali, hivyo kudhibiti upotevu na kuongeza uwajibikaji.

“Ni jambo la kutia moyo kuona taasisi za umma zinatumia teknolojia za kisasa katika kuboresha usimamizi wa rasilimali za taifa. Mfumo huu unasaidia kuongeza uwazi na kuhakikisha mafuta yanayopokelewa yanafika katika maeneo yaliyokusudiwa,” alisema Dkt. Nguvila.

Akitoa maelezo kwa mgeni huyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Khamis Mwitazy, alisema mfumo wa SCADA umechangia kwa kiasi kikubwa kudhibiti upotevu wa mafuta ambao kwa muda mrefu ulikuwa changamoto katika sekta hiyo.

Bw. Mwitazy alisema mfumo huo hulinganisha kiwango cha mafuta kilichopokelewa kutoka melini na kiwango kilichofika kwenye maghala, ambapo taarifa hutolewa mara moja endapo kutabainika tofauti yoyote ili hatua za haraka zichukuliwe.

Aidha, alisema mfumo huo unasoma na kufuatilia kwa wakati halisi ujazo wa mafuta kupitia mita za Serikali zilizopo katika bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, pamoja na kusoma kiwango cha mafuta kilichopo katika maghala ya kampuni za mafuta.

Kwa mujibu wa PBPA, matumizi ya mfumo wa SCADA ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha usimamizi wa mafuta nchini na kuhakikisha sekta hiyo inaendeshwa kwa uwazi, ufanisi na tija zaidi.

 

Wataalamu wa afya, watafiti, viongozi wa vijana na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya Afrika wamekutana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha huduma na sera za afya kwa vijana balehe barani Afrika.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtandao wa ARISE kupitia Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Afya ya Umma, Dkt. Mary Mwanyika Sando, Juni 22, 2026, inaeleza kuwa Mkutano wa 2026 wa Afya ya Vijana Balehe Kusini mwa Jangwa la Sahara (CAH-SSA) pamoja na Mikutano ya Mwaka ya Mtandao wa Utafiti, Sayansi ya Utekelezaji na Elimu Afrika (ARISE), unafanyika kuanzia Juni 22 hadi 25, 2026 Jijini Dar es Salaam.


Mkutano huo unafanyika chini ya kaulimbiu “Kuonesha Mafanikio ya Afua Endelevu za Afya ya Vijana Balehe Zinazoongozwa na Jamii”, ukiwa na lengo la kuonesha matokeo ya tafiti na kujadili mbinu bora za kuboresha afya ya vijana.

Mgeni rasmi katika mkutano huo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Tanzania, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe, ambaye amezungumzia namna matokeo ya tafiti yanavyoweza kutumika kuboresha sera za afya, kuimarisha huduma kwa vijana na kuongeza ushiriki wa vijana katika ubunifu na utekelezaji wa afua zinazowahusu.

Mkutano huo umewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo Serikali, washirika wa maendeleo, viongozi wa vijana, watafiti, taasisi za utafiti na sekta binafsi kwa lengo la kujenga ushirikiano wa kuongeza matokeo chanya katika afya ya vijana barani Afrika.

Katika mkutano huo, vijana pia wamepewa nafasi kupitia Wawakilishi wa Bodi ya Ushauri ya Vijana Balehe na Vijana kwa ujumla (AYAB), akiwemo Mtanzania Bi. Mariam Surve na Bi. Mariam Yusuff kutoka Nigeria, ambao wanawakilisha sauti na mahitaji ya vijana katika uundaji na utekelezaji wa programu za afya.

Miongoni mwa maeneo yatakayojadiliwa ni matokeo ya miradi ya DASH na ARISE-NUTRINT inayolenga kuboresha afya ya vijana katika maeneo ya lishe, mazoezi, afya ya uzazi na afya ya akili. Miradi hiyo imefadhiliwa na Serikali ya Ujerumani pamoja na Umoja wa Ulaya.

Aidha, mkutano huo unalenga kuimarisha mipango ya Mtandao wa ARISE kwa kipindi cha mwaka 2026–2027 kwa kuweka mikakati itakayowezesha afua za afya kwa vijana kuwa endelevu kifedha na kutekelezwa kwa upana katika ngazi za jamii, kitaifa na kikanda.

Wakizungumza kuhusu umuhimu wa mkutano huo, viongozi wa ARISE wamesema jukwaa hilo ni muhimu katika kuunganisha tafiti, matokeo yake, sera na utekelezaji wa programu zinazolenga kuboresha maisha ya vijana barani Afrika.

Mtandao wa ARISE ni ushirikiano wa taasisi za Afrika na mabara mengine unaolenga kuimarisha uwezo wa utafiti wa afya ya umma na kuendeleza utekelezaji wa afua zenye msingi wa ushahidi, ukiwa na zaidi ya taasisi 22 kutoka nchi mbalimbali Kusini mwa Jangwa la Sahara.








 


Na Oscar Assenga, Muheza

WANANCHI 6,258 wa Kijiji cha Muungano, Wilaya ya Muheza, wanatarajiwa kunufaika na huduma bora za afya kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa Zahanati ya Muungano, mradi ambao umepokelewa na kuridhiwa na Mwenge wa Uhuru 2026 baada ya kukaguliwa na kupokea taarifa ya utekelezaji wake.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 alisema kukamilika kwa zahanati hiyo kutasaidia kusogeza huduma za matibabu karibu na wananchi na kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya.

Alisema Serikali tayari imepeleka vifaa tiba pamoja na watumishi wa afya watakaotoa huduma katika zahanati hiyo, hatua inayoonesha dhamira ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya, hususan katika maeneo ya vijijini.

“Mradi huu ni muhimu kwa wananchi wa Muungano na maeneo jirani kwa sababu unasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuongeza ustawi wa jamii,” alisema.

Kiongozi huyo aliongeza kuwa mafanikio ya mradi huo yametokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, hususan Taasisi ya Islamic Help, iliyochangia ujenzi wa zahanati hiyo, huku Serikali ikigharamia vifaa tiba na watumishi wa afya.

Aliwashukuru wadau wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kijamii, na kuwataka kuendeleza ushirikiano huo ili kusaidia kuboresha huduma muhimu kwa wananchi.

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi, akisema kuwa mazingira hayo yanawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuvutia wadau zaidi kushirikiana na Serikali.

Kwa upande wake, akitoa taarifa ya mradi huo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk. Fani Mussa, alisema ujenzi wa Zahanati ya Muungano ulianza Machi 2, 2025 na kukamilika kwa gharama ya Shilingi milioni 165.94.

Alieleza kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 141.55 zilitumika kwa ujenzi, huku Shilingi milioni 24.39 zikitumika kununua vifaa tiba.

Kwa mujibu wa Dk. Mussa, zahanati hiyo itahudumia wakazi 6,258 wa Kijiji cha Muungano, wakiwemo wanaume 3,089 na wanawake 3,169, na inatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya katika eneo hilo.

Baada ya ukaguzi huo, Mwenge wa Uhuru 2026 ulieleza kuridhishwa na ubora wa utekelezaji wa mradi huo, ukibainisha kuwa ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya afya nchini.



Meneja wa Shirika  la Viwango Tanzania (TBS) Kanda ya Kati, Hamisi Sudi Mwanasala,akizungumza na waandishi wa habari katika banda la TBS wakati wa  Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwenye Viwanja vya Chinangali  jijini Dodoma,

....

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kuonesha ubora wa huduma zake kwa wananchi kupitia ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, huku mamia ya wananchi na wafanyabiashara wakifurika katika banda la taasisi hiyo kupata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa kwa njia ya kisasa.

Hayo yamesemwa leo Juni 23,2026 na Meneja wa TBS Kanda ya Kati, Hamisi Sudi Mwanasala, amesema mwitikio wa wananchi katika maonesho hayo umekuwa mkubwa kutokana na hamu ya kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu viwango, ubora wa bidhaa na taratibu za usajili.

Amesema TBS imetumia maonesho hayo kama jukwaa la kuwasogezea wananchi huduma muhimu zikiwemo utoaji wa vibali, usajili wa bidhaa na majengo ya biashara ya chakula na vipodozi pamoja na kupokea maombi ya leseni ya kutumia Nembo ya Ubora ya TBS.

"Tumeshuhudia mwamko mkubwa wa wananchi. Wengi wamekuja na maswali mbalimbali kuhusu huduma zetu na wamepata majibu ya kina. Kiu yao ya kupata taarifa sahihi imeweza kutimizwa kupitia wataalamu waliopo katika banda letu," amesema Mwanasala.

Amefafanua kuwa pamoja na kutoa huduma, TBS imeendelea kutoa elimu kwa wazalishaji, wafanyabiashara na waingizaji wa bidhaa kuhusu taratibu zinazopaswa kufuatwa ili kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa, kuingizwa au kuuzwa zinakidhi viwango vinavyotakiwa ndani na nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Mwanasala, maonesho ya mwaka huu yamekuwa na umuhimu wa kipekee kwa TBS kwani yanafanyika wakati Shirika hilo likiadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, safari ambayo imeambatana na mafanikio makubwa katika kuimarisha ubora wa bidhaa na huduma nchini.

Amesema maadhimisho hayo yamekuwa fursa ya kukutana na wadau mbalimbali wakiwemo wafanyabiashara, wajasiriamali, taasisi za umma na wananchi wa kawaida ambao wametoa maoni na mapendekezo yatakayosaidia kuboresha zaidi huduma za Shirika hilo.

Katika hatua nyingine, Mwanasala amesema TBS imepiga hatua kubwa katika matumizi ya teknolojia ya kidijitali kwa kuweka mifumo inayorahisisha upatikanaji wa huduma bila wananchi kusafiri umbali mrefu kufika kwenye ofisi za Shirika hilo.

Ametaja mifumo hiyo kuwa ni Online Application System (OAS) pamoja na Integrated Standardization, Quality Assurance, Metrology and Testing System (ISQMT), ambayo inamwezesha mteja kufanya maombi ya usajili wa bidhaa, usajili wa maeneo ya biashara ya vipodozi na chakula na kupata leseni ya kutumia Nembo ya Ubora kwa njia ya mtandao.

"Leo hii mteja anaweza kuwasilisha maombi yake akiwa mahali popote alipo na kufuatilia hatua zote za maombi yake kidijitali hadi anapopata huduma anayohitaji. Hii imepunguza gharama, muda na usumbufu kwa wananchi," amesema 

Aidha, amebainisha kuwa jitihada za TBS katika kuboresha utendaji na utoaji wa huduma zimeendelea kutambuliwa kitaifa, baada ya Shirika hilo kushika nafasi ya tatu kati ya taasisi 47 za umma zilizoshindanishwa katika eneo la utawala bora kwenye utumishi wa umma mwaka huu, taasisi ya kwanza mwaka 2025 katika masuala ya udhibiti nchini na taasisi ya kwanza kwa mwaka 2023 Afrika.

Mwanasala amesema kuwa mafanikio hayo ni ishara ya dhamira ya TBS katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, huku akisisitiza kuwa Shirika hilo halitaridhika na mafanikio yaliyopatikana bali litaendelea kuboresha mifumo na huduma zake ili kukidhi mahitaji ya wananchi na wadau wa maendeleo.

Amewataka wananchi, wafanyabiashara na wazalishaji ambao hawajafika katika banda la TBS kutumia siku zilizobaki za maonesho hayo kutembelea banda hilo ili kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali zinazohusu ubora na usalama wa bidhaa.

"Tunawakaribisha wananchi wote kufika katika banda la TBS. Tunayo elimu, tunayo huduma na tunayo suluhisho la changamoto mbalimbali zinazohusu viwango. Lengo letu ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata bidhaa zenye ubora na salama," amesema

 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mhe. Paschale Katambi Patrobas (Mb), aliyewakilishwa na Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Afande Jeremiah Katungu Amewatunuku wafungwa 173 kati yao wanawake 6 na wanaume 167 vyeti vya mafunzo ya ujasiriamali na stadi za biashara katika hafla ya mafunzo ya ujasiriamali na stadi za biashara kwa ushirikiano wa Chuo Cha Uhasibu Arusha yaliyofanyika leo tarehe 22/June/2026 katika viwanja vya magereza kisongo mkoani Arusha.

Wakati wa utoaji wa vyeti hivyo Mhe. Katungu amesema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya marekebisho ya wafungwa kwa kuwekeza katika elimu na ujuzi unaowawezesha kuwa wananchi wenye tija wanaporejea katika jamii na kuongeza kuwa  mafunzo hayo yamekuwa nyenzo muhimu ya kuibua vipaji, kuongeza uwezo wa kujiajiri na kupunguza uwezekano wa kurudia vitendo vya uhalifu, huku akipongeza ushirikiano uliopo kati ya Jeshi la Magereza na Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) katika kufanikisha programu hiyo yenye manufaa makubwa kwa taifa.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Mhe. Joseph Mkude, amesema uwekezaji katika elimu ya ujasiriamali na stadi za biashara kwa wafungwa ni hatua muhimu ya kuwawezesha kujijengea maisha mapya yenye heshima na mchango chanya kwa jamii. 

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Profesa Eliamani Sedoyeka, amesema chuo hicho kinaendelea kutekeleza wajibu wake wa kijamii kwa kutoa elimu na mafunzo yanayolenga kuleta mabadiliko chanya kwa makundi mbalimbali ya jamii,na kuongeza kuwa mafunzo ya ujasiriamali na stadi za biashara yaliyotolewa kwa wafungwa yamewajengea uwezo wa kubuni, kuanzisha na kusimamia shughuli mbalimbali za kiuchumi, hatua ambayo itawawezesha kujitegemea na kuwa sehemu ya nguvu kazi ya taifa baada ya kumaliza vifungo vyao. Profesa Sedoyeka ameongeza kuwa IAA itaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali katika kutoa elimu inayojenga jamii jumuishi na yenye ustawi endelevu.

Utekelezaji wa mafunzo hayo kwa ushirikiano kati ya Jeshi la Magereza na Chuo cha Uhasibu Arusha unakwenda sambamba na azma ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi shindani.










 


Wizara ya Nishati imesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kufanikisha lengo la Taifa la kufikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Wito huo umetolewa na Mjiolojia Mkuu wa Wizara ya Nishati, Bw. Ngereja Mgejwa, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, wakati akifungua Maonesho na Kongamano la Nishati Safi ya Kupikia 2026 (Clean Cooking Expo 2026), Juni 23, 2026 katika Ukumbi wa EACLC jijini Dar es salaam.

Akizungumza katika kongamano hilo, Bw. Mgejwa amesema nishati safi ya kupikia ni ajenda muhimu ya kitaifa inayohitaji ushirikiano wa wadau wote ili kuleta mabadiliko ya kudumu katika sekta ya nishati. Amesema matumizi ya nishati safi yana mchango mkubwa katika kulinda afya za wananchi, hususan wanawake na watoto, kuhifadhi mazingira, kuinua elimu kwa watoto wa kike na kuongeza tija ya kiuchumi.

Ameeleza kuwa kazi iliyopo mbele ni kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi ya kupikia iliyo nafuu, salama na endelevu ikiwemo gesi oevu (LPG), majiko banifu, gesi asilia, umeme, bayogesi na bayoethanoli.

 Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya nishati safi pamoja na kutoa elimu kwa umma ili kubadili matumizi ya nishati za jadi kwenda kwenye nishati safi.

Bw. Mgejwa amepongeza Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TABWA) kwa kuandaa kongamano hilo, akisema majadiliano yatakayofanyika yataibua suluhisho na mapendekezo yatakayochochea ongezeko la matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

 Ameongeza kuwa kongamano hilo litahitimishwa kwa Mbio za Nishati Safi ya Kupikia zitakazotumika kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi kwa afya na uhifadhi wa mazingira.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa ya Wafanyabiashara Wanawake Tanzania(TABWA) Bi. Noreen Mawalla amesema maonesho hayo yameandaliwa chini ya kaulimbiu ya "Linda Afya, Hifadhi Mazingira, Okoa Muda kwa Uchumi Endelevu" kwa lengo la kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuunga mkono utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia.

Amebainisha kuwa Clean Cooking Expo 2026 itafanyika kwa siku tatu na itajumuisha mafunzo, mijadala na maonesho ya teknolojia mbalimbali za nishati safi zitakazowakutanisha wadau kutoka sekta ya umma na binafsi. 

Amewakaribisha wananchi kutembelea mabanda ya maonesho ili kupata elimu na taarifa sahihi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia, huku akieleza kuwa Mbio za Nishati Safi ya Kupikia zitafanyika Jumamosi na zinatarajiwa kuongozwa na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi.