Na Oscar Assenga, Tanga

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Balozi Batilda Burian, amesema mkoa huo umeanza mkakati maalum wa kukuza na kutangaza utalii wa fukwe pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo, ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

Akizungumza leo, amesema ameita wadau mbalimbali kwa ajili ya kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuitangaza Tanga, akibainisha kuwa mkoa huo umejaliwa kuwa katika ukanda wa Bahari ya Hindi wenye maeneo mengi yenye fursa za kiuchumi na utalii.

Ametaja baadhi ya maeneo hayo kuwa ni pamoja na Kipumbwi (Pangani), Ushongo, Kwale (Mkinga) na maeneo ya Raskazone jijini Tanga, ambapo kuna mradi wa kuboresha fukwe unaofadhiliwa na Benki ya Dunia. 

Amesema mradi huo utakapokamilika utafungua fursa za michezo ya maji, matembezi ya boti, kuogelea pamoja na shughuli za kijamii kama harusi.

Aidha, amesema mkoa umeanza kushirikiana na Kampuni ya Makazi Solution pamoja na wadau wa Zanzibar ili kujifunza na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza utalii wa fukwe.

 Timu ya wataalamu inatarajiwa kwenda Zanzibar kukutana na Wizara ya Utalii na wadau wengine ili kuimarisha ushirikiano huo.

“Tunajifunza kutoka Zanzibar, ambako maeneo kama Nungwi na Paje yalianza kidogo lakini sasa yamekua vituo vikubwa vya utalii. Sasa ni wakati wa Tanga kuchukua nafasi hiyo,” amesema.

Kwa upande wa uwekezaji, Dkt. Burian ameeleza kuwa mradi wa Kipumbwi Satellite City, unaotekelezwa kwa ushirikiano na Halmashauri ya Pangani na Makazi Solution, unalenga kutoa fursa kwa wananchi na wawekezaji kupata viwanja na kuendeleza eneo hilo.

Amesema eneo la Kipumbwi lina umuhimu mkubwa kimkakati, likiwa kilomita 3 kutoka bandari ya Kipumbwi, kilomita 80 kutoka Tanga, kilomita 60 kutoka Zanzibar kwa njia ya bahari, na kilomita 180 kutoka Dar es Salaam. Pia ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani–Saadani–Bagamoyo unatarajiwa kufungua zaidi ukanda huo wa pwani.

Mbali na fukwe, mkoa wa Tanga una vivutio vingi vya utalii ikiwemo Mapango ya Amboni, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Milima ya Usambara (Lushoto), pamoja na urithi wa kihistoria kama makaburi ya vita ya kwanza ya dunia na Kisiwa cha Toten.

Ameongeza kuwa Tanga pia ni kitovu cha utamaduni wa Kiswahili, likiwa na historia ya muziki wa taarab, vyakula vya asili, pamoja na kuwa chimbuko la lugha ya Kiswahili, ambapo mwanazuoni mashuhuri Sheikh Shaban Robert alizaliwa katika eneo hilo.

Kwa sasa, amesema mkoa unapokea wageni kutoka ndani na nje ya nchi, hususan kutoka Kenya, Ujerumani, Uholanzi na Uswisi, wanaovutiwa na historia, mazingira asilia na utamaduni wa Tanga.

Dkt. Burian amesema jitihada hizo zinaunga mkono azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuitangaza Tanzania kupitia kampeni ya Royal Tour na kuongeza idadi ya watalii.

Kwa upande wa uchumi, amesema mkoa wa Tanga kwa sasa unachangia takribani shilingi trilioni 9.8 katika pato la taifa, na una mpango wa kuongeza mchango huo na kufikia nafasi ya pili kitaifa baada ya Dar es Salaam ifikapo mwaka 2028.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanga ni eneo sahihi kwa uwekezaji na utalii, akiwakaribisha wawekezaji na watalii kutoka ndani na nje ya nchi kuja kutumia fursa zilizopo.




Na, Mwandishi Wetu, Muleba – Kagera

KAIMU Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Bw. Salum Kimbau amesema maandalizi ya Mpango wa Afya Moja kwa mkoa wa Kagera utaunufaisha mkoa huo kwa kuzingatia malengo yake ya kuboresha uratibu na utekelezaji wa Dhana ya Afya ya Moja na kuendelea kutatua changamoto zilizopo na zenye mwingiliano kati ya binadamu, wanyama na mazingira


Amezungumza hayo wakati akifungua kikao kazi cha wataalamu wa masuala ya Afya Moja kutoka sekta mbalimbali zikiwemo za afya, mifugo, mazingira, wanyamapori na kilimo ambao wamekutana katika Halmashauri ya Wilaya ya Muleba mkoani Kagera kwa siku tano kuanzia tarehe 27 Aprili hadi 01 Mei, 2026 ili kuandaa Mpango huo utakaotumika kubaini rasilimali zitakazosaidia kutatua changamoto na vihatarishi vya afya ya binadamu, wanyama na mazingira.





Bw. Kimbau amesema kuwa, mkoa utanufaika kwa uwepo wa Mpango huo kwani utaongeza tija katika kutatua changamoto zinazokabili sekta hizo hususan katika kuendelea kutatua changamoto za mwingiliano wa magonjwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na binadamu kwenda kwa wanyama.


“Tunashukuru kuufikia mkoa wetu wa Kagera, tunajua kuwa asilimia 75 ya magonjwa yanatokana na mwingiliano ulipo kati ya wanyama na binadamu, hivyo kuandaliwa kwa mpango kutasaidia utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja kwa kushirikiana pamoja, hivyo utatusaidia kutatua changamoto zilizopo na kuwa na jamii salama,” alisema Bw. Kimbau



Aliongezea kuwa ufanisi wa mpango huu unategemea ushirikishwaji wa sekta zote zinazohusika ili kuleta matokeo chanya.


Naye Mratibu wa Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa sehemu ya Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Valentina Sanga amesema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani imeratibu maandalizi ya uwepo wa mpango huo huku akisihi kuunganisha nguvu ya pamoja katika kuhakikisha utekelezaji wake unaleta matunda yanayotarajiwa.

Aidha, aliwasihi wataalamu wa Masuala ya Afya Moja kutumia fursa hiyo kuja na Mpango utakaoinufaisha Kagera, kwa kuzingatia ni miongoni mwa Mikoa inayokumbwa na majanga ya mlipuko mengine yakichangiwa na mwingiliano wa wanyama na binadamu.

“Dhana ya Afya Moja (One Health) inatoa fursa ya kutambua uhusiano wa karibu kati ya afya ya binadamu, wanyama, na mazingira. Inasisitizwa kuendelea kujifunza zaidi dhana hii ili kutatua changamoto zilizopo zikiwemo za milipuko ya magonjwa na kuweza kuyakabili endapo yanatokea katika maeneo yetu,” alisisitiza Bi. Valentina

Aliongezea kuwa, Mpango huo utasaidia kutatua changamoto za masuala ya kiafya zinazotokea katika Halmashauri za mkoa wa Kagera, kujiandaa na kukabili majanga hayo ili kuwa na jamii salama kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Shirika la CIHEB Tanzania, Bw. Mark Lwakatare alisema mradi wa Usalama wa Afya Duniani utaendelea kushirikiana na mikoa husika katika kuimairisha utekelezaji wa dhana ya Afya Moja ili nchi iweze kukabiliana na vihatarishi vya majanga mbalimbali.



“Mradi huu unashirikiana na Serikali kuboresha na kuimarisha utekelezaji wa afua mbalimbali kupitia dhana ya Afya Moja nchini, hivyo mradi utaendelea kushirikiana katika kujiandaa na kukabili athari katika afya ya binadamu, manyama na mazingira,” alisisitiza Lwakatare.


Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe,Kamati ya Michezo ya Meimosi, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeshiriki zoezi la upandaji miti lililofanyika  katika eneo la Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe.

Katika zoezi hilo Mkuu wa mkoa wa Njombe Mhe. Anthony Mtaka awewahimiza Wafanyakazi na wananchi kuhakikisha kuwa wanapanda miti yenye kuleta faida hususan miti ya matunda ili kusaidia upatikanaji wa kipato cha mtu mmojammoja na Taifa kwa ujumla.

" Kumekuwa na tabia ya watu wengi kupanda miti kwaajili ya kivuli tu, pasipo faida yoyote, vi vizuri sasa tukapanda miti yenye kuleta faida kubwa kama vile miti ya matunda, amesema Mtaka.

Zoezi hilo lilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Katibu Tawala wa mkoa wa Njombe, Rais wa Shirikisho la Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Mwenyekiti wa Kamati ya Meimosi na Watumishi wa Serikali kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali.

 


Na. Josephine Majura na Saidina Msangi, WF, Dodoma.


Serikali imeeleza kuwa iko tayari kushirikiana na Hispania katika maeneo ya kipaumbele ikiwemo kukuza uchumi endelevu, ujenzi wa miundombinu, mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, na kuendeleza rasilimali watu, kwa lengo la kuchochea maendeleo jumuishi nchini.

Hayo yalielezwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Hispania chini, Mhe. Paloma Serra Robles, aliyefika kwa ajili kujitambulisha na kuwasilisha masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania na Hispania, katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, Dodoma.

Mhe. Balozi Omar alisema dhamira ya Serikali ni kuendelea kushirikiana na Hispania katika kutafuta rasilimali za kifedha kwa ajili ya miradi mingine ya maendeleo yenye maslahi mapana kwa Taifa, lengo likiwa ni kuchochea ukuaji wa uchumi na huduma bora kwa jamii.

‘‘Uhusiano uliopo kati ya Tanzania na Hispania ni wa muda mrefu, ambapo kampuni za Hispania zimekuwa zikiwekeza nchini katika sekta mbalimbali, ikiwemo utalii, pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo na zitaendelea kuja kuwekeza nchini kwa kuwa mwelekeo wa Serikali ya Hispania ni kuongeza ushirikiano wa pamoja wenye mandeleo endelevu ikiwemo kuunganisha kampuni za Tanzania na kampuni za Hispania’’, alisema Mhe. Balozi Omar.

Pia Mhe. Omar alitoa wito kwa kampuni na wawekezaji kutoka Hispania kuja kuwekeza nchini Tanzania na kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufanya biashara na kutoa vivutio mbalimbali vya kikodi na uwekezaji vinavyoendana na ukubwa wa miradi, ikilenga kukuza ushirikiano.

Aliishukuru Hispania kwa kufadhili utekelezaji wa miradi mbalimbali nchini, ikiwemo kutoa mkopo wa masharti nafuu wa Dola za Marekani milioni 30 kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Uendelezaji wa Bonde la Msimbazi, jijini Dar es Salaam ambao unatarajiwa kuleta mabadiliko katika kukabiliana na changamoto za mafuriko, kuimarisha hifadhi ya mazingira, na kukuza ustahimilivu wa miundombinu ya jiji hilo dhidi ya majanga ya asili.

Akizungumza kuhusu uchumi wa Tanzania Mhe. Omar alisema kuwa uchumi umeendelea kuimarika kwa kasi baada ya Pato la Taifa (GDP) kukua hadi kufikia asilimia 6.4 katika robo ya tatu ya mwaka 2025, ikilinganishwa na asilimia 6.1 katika kipindi kama hicho mwaka uliopita.

Aliongeza kuwa mfumuko wa bei umesalia kuwa tulivu kwa wastani wa asilimia 3.5 hadi kufikia Desemba 2025, ndani ya malengo ya kitaifa ya kati ya asilimia 3 na 5, huku kikiwa chini ya viwango vya ukomo vilivyowekwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Utulivu huo wa bei za bidhaa na huduma unatajwa kuwa kigezo muhimu kinachojenga imani kwa wawekezaji na kutoa fursa pana kwa washirika wa maendeleo kuendelea kuwekeza nchini kutokana na mazingira tabiri ya uchumi mkuu.

Alisisitiza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kuimarisha ushirikiano wa pande hizo mbili kwa ajili ya maendeleo na ustawi wananchi na kumpongeza kwa kuteuliwa kwake kuwa Balozi wa nchi hiyo.

Kwa upande wake Balozi wa Hispania nchini, Mhe. Paloma Serra Robles, ameeleza dhamira ya nchi yake kuendelea kuisaidia Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta tofauti zikiwemo miundombinu ya usafirishaji na miradi ya kijamii yenye tija kwa wananchi.

Alisema nchi hiyo imesaidia katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo wa uendelezaji wa bonde la msimbazi ambao kukamilika kwake kutaleta tija kwa wakazi wa Dar es Salaam.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El -maamry Mwamba, Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Madeni,  Bw. Omary Khama, Kamishna Msaidizi Idara ya Fedha za Nje, Bw. James Msina pamoja na Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano Wa Afrika Mashariki.



Taasisi kongwe ya dini ya kiislamu ya Twariqa Tulqadirya Arazakia Jailania Tanzania yenye makao yake makuu mkoani Arusha, imedhamiria kufanya sensa ya watu  na mali za taasisi hiyo ili kupata Idadi sahihi ya waumini wake.

Lengo la  zoezi hilo ni kuweza kufanya kazi kwa Ufanisi na kuyafahamu makundi  mbali mbali yaliyomo katika taasisi hiyo yakiwemo  makundi ya Viongozi Vijana,Wanawake,Walemavu,Yatima,Wajane na Wagane ili waweze kupatiwa huduma stahiki katika Mikoa yote ya Tanzania .

Akizungumza na Vyombo vya Habari mkoani Arusha Mwenyekiti wa Twariqa Taifa Shekhe  Mubaraka Salim Gahran amesema kuwa taasisi hiyo  ilifanya sensa ya kitwariqa  mnamo mwaka 1932,ambapo imepita kipindi kirefu bila zoezi hilo kufanyika hali ambayo inapelekea tasisi kushindwa kuwa na Idadi kamili ya watu  pamoja na mali zilizopo sasa.

Shekhe  Gahrani amesema kuwa  pia Ofisi yake imeona  ni vema kufanya uhakiki wa mali zilizopp kwa kuwa tangu kiongozi wao  Daruweshi Mti Mkavu alipofariki takribani mwaka mmoja na nusu  kuna baadhi ya vitu wanapaswa kuviweka sawa ili kuhakiki mali zote na kuepusha migogoro isiyo ya lazima ndani yao ikiwa ni pamoja na watu binafsi kujimilikisha mali za taasisi hiyo nchini.

"Hii ni sensa ya kawaida ya kitwariqa na inawahusu wanatwariqa wa Daraweshi Mti Mkavu na tunataka kuhakiki  kila kitu kuanzia Idadi ya Waridi wetu waliopata Ijaza,Elimu zao za kawaida,kufahamu haya yote itatuwezesha sisi  Viongozi kujua mahitaji yao na tuna watu wa aina gani na tunawahudumiaje na kwa namna gani bila kusahau migogoro isiyo ya lazima  na isielewele vinginevyo.Alisisitiza Shekhe Gahran 

Nae katibu mkuu wa twariqa Taifa shekhe  Haruna Hussein Lotha ameiomba serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuwapa Ushirikiano wakati wa zoezi hilo ili kufanya zoezi hilo kutekelezwa kwa utulivu na kwa kufuata taratibu.

Shekhe Haruna Hussein amesema kuwa tangu wameingia madarakani hawajui idadi ya waumini wao,majengo wala mali walizonazo ili kuwasaidia kujua mapungufu yaliyopo na kisha kuboresha kwa kuwa kazi ya dini ni kujenga Imani za watu na kuwahudumia kiroho.

"Taasisi  yetu imekuwa ikishirikiana  na serikali yetu kila eneo hivyo tunatazamia kuwa mashirikiano haya  yatakuwa endelevu na  pia tumetumia vyombo vya habari ni kuhakikisha jamii inaendelea  kupata taarifa kwa wakati na zoezi litakapoanza katika mikoa yote ya Tanzania,liwe rahisi "Amesisitiza Katibu Lotha


Na Mwandishi wetu- DODOMA



Katibu Tawala  Mkoa wa Dodoma, Dkt. Khatibu Kazungu, amesema Ofisi yake ikishirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Idara ya Menejimenti ya Maafa ipo katika hatua ya kuanzisha Kituo cha Operasheni ya Dharura katika Mkoa ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya mwaka 2004.

Dkt. Kazungu ameyasema hayo leo tarehe 27 Aprili,2026 jijini Dodoma kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma wakati akifungua  mafunzo ya siku nne ya  kujiandaa na kukabiliana na maafa kwa Timu ya kukabiliana na dharura ya Mkoa ambayo yameandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa pamoja na  uanzishaji wa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa.

Aidha, Dkt. Kazungu ameshukuru ujio wa elimu hiyo ndani ya Mkoa wa  Dodoma  akisema  itasaidia kuwajenga kielimu Maafisa wa Mkoa ili waweze kupeleka elimu katika ngazi za Wilaya.

"Elimu hii itasaidia kuongeza ujuzi na weledi kwa Maafisa wa Mkoa kwani majanga haya yamekuwa na madhara mengi kwa jamii," alisema Dkt. Kazungu.

Pia, alisisitiza  ukusanyaji wa taarifa kwa wakati na kabla ya majanga ili kurahihisisha  kuyakabili pamoja na kuboresha mawasiliano ya karibu baina ya wananchi na Maafisa wa Mkoa.

"Lazima kuwepo ushirikiano baina yetu na Wananchi ili tuweze kupambana na maafa ndani ya Mkoa wetu wa Dodoma," alisisitiza.


Awali Kaimu Mkurugezi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Selestine Masalamadu aliupongeza Mkoa wa Dodoma kwa kuwa tayari kupokea elimu ya maafa na majanga na kusema kuwa  Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara hiyo ina jukumu la kuratibu shughuli za Kuzuia, Kupunguza Athari, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa.

Vilvile, alisema kuwa Ofisi inaendelea kuratibu uanzishaji na uendeshaji wa Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura vya Mikoa  pamoja na Timu za kukabiliana na  dharura , ikiwa ni utekelezaji wa  Sera ya Taifa ya Usimamaizi wa Maafa ya Mwaka 2004, Sheria ya Usimamaizi wa maafa Na. 6 ya mwaka 2022 na kanuni zake.

“Lengo la mafunzo haya ni kuimarisha uwezo wa Mkoa kuratibu shughuli za usimamaizi wa maafa ili kupunguza madhara wakati wa dharura. Mafunzo haya yatawajengea uwezo washiriki katika maandalizi, uratibu wa taarifa, mwitikio wa haraka, usimamizi rasilimali na utoaji wa huduma kwa waathirika,” alifafanua Kanali Masalamadu.

Aidha, alibainisha kwamba kila Mkoa unatakiwa kuwa na chumba maalum kwa ajili ya kuratibu shughuli za maafa na dharura huku akihimiza kuharakishwa kwa upatikanaji wa chumba chenye sifa stahiki kuwezesha uanzishwaji kamili wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Dodoma.




MWISHO

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) wamekutana Aprili 27,2026 katika ziara ya mafunzo, kwa lengo la kubadilishana uzoefu katika utekelezaji wa majukumu ya kimazingira, hasa mchakato wa ufanyaji wa Tathmini ya Athari kwa Mazingira na jamii katika miradi mikubwa na mchakato wa kupata vyeti vya kimazingira ili kuhakikisha maendeleo yanaendana na uhifadhi wa mazingira.

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (NEC), Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), Ndugu Rabia Abdalla Hamid akiwa kwenye kikao kazi na Kansela wa Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) wa Ubalozi wa China nchini Tanzania, Ndugu Xu Sujiang, leo Jumatatu tarehe 27 Aprili 2026, Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, jijini Dar Es Salaam, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea ugeni wa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CPC na Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mhe. Liu Haixing, anayetarajiwa kufanya ziara rasmi nchini Tanzania, mwezi Mei 2026.

#KazinaUtuTunasongaMbele





Wananchi wametakiwa kupanda miti na kutunza Misitu nchini kwa maslahi mapana ya Taifa na mtu mmoja mmoja.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhe. Antony Mtaka, Mkoani Njombe, kwenye zoezi la upandaji wa miti katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kama sehemu ya maadhimisho ya Mei Mosi 2026

Mhe. Mtaka amesema kuwa, Misitu ni nguzo muhimu kwa uchumi wa nchi hivyo nivyema ikalindwa kwa wivu mkubwa na kutoichoma moto.

 Amesisitiza kuwa zoezi la upandaji miti liendane sambamba na upandaji wa miti ya matunda hususani Miparachichi ambayo inasoko kubwa ndani na nje ya nchi. 

Zoezi hilo la upandaji miti linalojulikana kwa Jina la "27 ya KIJANI, MTI WA MAMA" pamoja na viongozi wengine limeudhuriwa na rais wa Shirikisho la vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Cde. Tumaini Nyamhokya, Mkurugenzi Msaidizi Utawala Bi. Violeth Mlinga kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii na watumimishi mbalimbali wa serikali.


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Imeelezwa kuwa usawa wa kijinsia unaendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha maendeleo endelevu, kuchochea ukuaji wa uchumi na kuimarisha utawala bora katika jamii na taifa kwa ujumla.
Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Antony Mtaka akizungumza na Wanamichezo wanaoshiriki Mashindano ya Mei Mosi, 2026 Mkoani humo wakati waliofika katika Ofisiza Mkoa huo Aprili 27, 2026 kwa ajili ya zoezi la upandaji Miti kupitia kampeni ya 27 ya kijani, Mti wa Mama inayofanyika tarehe ya Kila mwezi.

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Kikundi cha We Are Family kinachowahusisha wenza wa majaji nchini, kimetembelea wagonjwa wa saratani katika Ocean Road Cancer Institute jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira yao ya kufanya matendo ya huruma kwa jamii.

 

Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amemshukuru  Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kuadhimisha miaka 62 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukagua ujenzi wa miradi ya maendeleo ya daraja jipya la Mkwajuni, daraja jipya la Kigogo ikiwa ni pamoja na kutatua kero za wananchi wa jiji la Dar es Salaam.

Prof. Shemdoe ametoa shukurani hizo leo Aprili 26, 2026 jijini Dar es Salaam       wakati akizungumza na wananchi wa jiji la Dar es Salaam katika Uwanja wa Shule ya Msingi Msimbazi mara baada ya Mhe. Waziri Mkuu kukagua miradi hiyo ya maendeleo, ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 62 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Mhe. Waziri Mkuu nakushukuru sana kwa uamuzi wako wa kuadhimisha miaka 62 ya Muungano kwa kukagua miradi ya maendeleo na kutatua kero za wananchi wa Dar es Salaam tena siku ya Jumapili,” Prof. Shemdoe amesisitiza.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, uwanja umefurika idadi kubwa ya wananchi licha kuwa ni siku ya jumapili kwasababu wana Imani na wanafahamu kuwa Mhe. Waziri Mkuu utawasikiliza kero zao na kuzitatua hivyo watarejea kwenye makazi yao na tabasamu la kudumu.

Akizungumzia mwendelezo wa Serikali kutatua kero za wananchi, Prof. Shemdoe amesema siku chache zilizopita Mhe. Waziri Mkuu alimtuma kuja jijini Dar es Salaam kushuhudia utiaji wa saini wa Mradi wa Uendelezaji wa Bonde la Mto Msimbazi utakaogharimu zaidi ya  Shilingi Bilioni 190, fedha ambazo ziliidhinishwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuongeza kuwa   mradi huo ni sehemu muhimu kwa uchumi na mazingira mkoani Dar es Salaam.

“Nichukue fursa hii kumshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kuletwa kwa fedha za kutekeleza Mradi wa Uendelezaji wa Bonde la Mto Msimbazi, lakini pia nikushukuru wewe Mhe. Waziri Mkuu kwani nikiwa Katibu Mkuu TAMISEMI nakumbuka ulikuwa ukiongoza vikao vya Serikali na wadau wa Maendeleo vilivyowezesha kupatikana kwa fedha hizo ,” amesema Prof. Shemdoe.


Katika kuadhimisha miaka 62 ya Muungano wa Tanzania, Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPPC), David Kafulila, amesema mafanikio ya Muungano huo yanatokana zaidi na mshikamano wa watu kuliko mifumo ya kiserikali.




Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya Taifa Gas imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi na salama ya gesi, sambamba na kuhamasisha usalama mahali pa kazi katika maadhimisho ya Wiki ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi Duniani.

Akizungumza katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema, Njombe, Mtaalamu wa Masuala ya Afya, Mazingira, Usalama na Ulinzi Mahali pa Kazi kutoka Taifa Gas, Aurelius Marcus Mdemu, alisema kampuni hiyo imeshiriki maadhimisho hayo yanayoanza Aprili 24 hadi 29, 2026 kwa lengo la kutoa elimu kwa wateja na jamii kwa ujumla.

 
Alisema kupitia banda lao, wanaonesha vifaa mbalimbali vinavyotumika kazini ili kuimarisha usalama wa wafanyakazi, pamoja na kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya gesi na faida zake. Aidha, alieleza kuwa wanajitahidi kuondoa hofu na dhana potofu zilizopo miongoni mwa watumiaji wa gesi.

“Tunawaonesha wananchi namna Taifa Gas inavyoweka kipaumbele kwenye usalama wa wafanyakazi, ikiwa ni pamoja na matumizi ya vifaa kinga vinavyotakiwa kutumika muda wote wakiwa kazini,” alisema Mdemu.



 

Kwa upande wake, Afisa Masoko wa Chapa wa Taifa Gas, Santina Ngaponda, alisema maonyesho hayo yameandaliwa na OSHA, yalianza Aprili 24 na yanatarajiwa kufikia kilele chake Aprili 29 mwaka huu.

Ngaponda aliwahimiza wakazi wa Njombe na maeneo ya jirani kutembelea banda la Taifa Gas ili kupata elimu kutoka kwa wataalamu wa usalama, kujifunza matumizi sahihi ya gesi, pamoja na kuona vifaa vya usalama vinavyotumika kazini na umuhimu wake.
 

Aidha, aliongeza kuwa kampuni hiyo inatoa punguzo maalum la bei ya gesi na vifaa vyake, pamoja na zawadi mbalimbali kwa wateja watakaotembelea banda hilo.
 

Naye Meneja Mauzo wa Kanda ya Nyasa wa Taifa Gas, Arnold Salewa, alisema wanaendelea kutumia maonyesho hayo kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya nishati safi pamoja na kuuza bidhaa zao kwa bei ya promosheni.

Alisema kanda hiyo inajumuisha mikoa ya Njombe, Iringa na Ruvuma, na kwamba pia wanatoa fursa kwa wananchi wanaotaka kuwa mawakala wao, kwa kuwapatia elimu ya biashara na usimamizi salama wa mitungi ya gesi.

Salewa alisisitiza kuwa Taifa Gas ipo mstari wa mbele kuhakikisha kaya, migahawa na taasisi mbalimbali zinaanza kutumia nishati safi ya kupikia kwa gharama nafuu, ili kupunguza athari za matumizi ya mkaa na kuni kwa mazingira na afya za Watanzania.

Aliongeza kuwa mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa, huku Taifa Gas ikiendelea kuwa chaguo sahihi kwa watumiaji wengi nchini.