📌Bilioni 7 kuwezesha maeneo 165 ya miji kupata huduma ya umeme Morogoro


Mkuu wa mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima ameipongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa utekekezaji wa miradi ya umeme maeneo ya Vijijini na Vitongoji hali iliyopelekea kuchochea uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

RC Malima ametoa pongezi hizo leo Februari 26, 2026 mkoani humo wakati akizungumza na Bodi ya Nishati Vijijini (REB) pamona na Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ilipomtembelea ofisini kwake kueleza utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini inayoendelea na iliyokamilika mkoani humo. 

"Nimeifahamu REA kwa mingi toka ilipoanzishwa rasmi. Hapa ilipofika leo hii lazima tujivunie sisi kama Watanzania kwa kuwa imeweza kufikisha umeme vijiji vyote na sasa utekekezaji unaendelea kwenye vitongoji vyote nchini," Amesema RC Malima.

Halikadhalika RC Malima ameipongeza Bodi ya REA na Menejimenti kwa kazi kubwa iliyofanyika kwa kusimamia miradi mbalimbali ya umeme katika mkoa huo ili Watanzania waweze kunufaika na nishati hiyo muhimu. 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Kingu ameeleza kuwa REA itaendelea kutekekeza miradi ya umeme vijijini wa weledi huku ikiwasimamia wakandarasi wa miradi hiyo ili waweze kuikamilisha miradi hiyo kwa wakati. 

"Sisi kama Bodi tunauhakika miradi inayoendelea tutaikamilisha kwa wakati kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan tayari imetoa fedha nyingi ili kuwezesha na kukamilisha miradi hiyo, " Ameongeza Mhe. Balozi Kingu. 

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa REA Mha. Hassan Saidy ameeleza kuwa kwa mkoa huo Wakala ipo mbioni kuongeza miradi ya ziada katika maeneo ya miji ambayo bado hayajafikiwa na huduma ya umeme ambapo takribani  maeneo 165 yatapatiwa huduma hiyo na wateja wa awali 1,750 watapatiwa huduma ya umeme ambapo Serikali imetoa takribani shilingi bilioni 7 kwa mkoa wa Morogoro kutekeleza miradi hiyo. 








 

Mbunge wa Jimbo la Kisarawe mkoani Pwani, Selemani Jafo, ameonesha kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi wa maji katika Kijiji cha Nyani, Kata ya Mafizi, akieleza kuwa hatua iliyofikiwa inaleta matumaini mapya kwa wananchi.

Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya BROADWAYS ENGINEERING CO LTD una thamani ya shilingi milioni 402.8 na hadi sasa umefikia asilimia 70 ya utekelezaji, jambo linaloashiria kuwa upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wa eneo hilo si wa muda mrefu tena.

Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji, mradi unahusisha ujenzi wa mnara wa tanki la maji lenye urefu wa mita 12 na uwezo wa kuhifadhi lita 50,000, pamoja na ujenzi wa vituo vitano vya kuchotea maji na ulazaji wa mtandao wa mabomba wenye urefu wa kilometa 16.167.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Dkt. Jafo alimpongeza mkandarasi kwa kufanya kazi kwa kasi na weledi mkubwa, akibainisha kuwa kampuni hiyo imeendelea na kazi hata kabla ya kupokea malipo yoyote, jambo alilolitaja kuwa ni uzalendo na kujitolea kwa maendeleo ya wananchi.

Kutokana na kasi hiyo, Jafo ameiiomba Wizara ya Maji kulipa kiasi cha shilingi milioni 279.1 kwa kazi zilizokamilika ili kumwezesha mkandarasi huyo kuendelea na hatua zilizobaki na kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

Mbali na mkandarasi, mbunge huyo pia amempongeza Meneja wa RUWASA Wilaya ya Kisarawe, Mhandisi Evangelista Kahwili, kwa usimamizi makini wa miradi ya maji ndani ya jimbo hilo, akisema nidhamu na ufuatiliaji wa karibu umechangia mafanikio yanayoonekana.

Wananchi wa Nyani na maeneo ya jirani wanatarajia kunufaika na mradi huo mara utakapokamilika, huku wakieleza kuwa utapunguza adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji na kuboresha afya pamoja na shughuli za kiuchumi katika eneo hilo.


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratous Ndejembi, ameitaka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuimarisha mipango yake katika ukusanyaji wa data sahihi, tathmini ya vitalu vya utafiti, na maandalizi ya Watanzania kushiriki kikamilifu katika miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG).

Mhe. Ndejembi ameyasema hayo wakati wa Kikao cha Tano cha Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi la PURA kilichofanyika mkoani Morogoro leo Februari 26, 2026.

 Amesisitiza kwamba sekta ya nishati ina nafasi ya kipekee katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo PURA inatakiwa kuhakikisha mipango yake inaendana na maono hayo.

“Sekta ya Nishati imetambuliwa kama moja ya vichocheo muhimu vya uchumi wa taifa. Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati zina wajibu mkubwa kuhakikisha upatikanaji endelevu, salama na wa uhakika wa rasilimali za mafuta na gesi asilia,” amesema Mhe. Ndejembi.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuongeza juhudi katika ukusanyaji na usimamizi wa data za kijiolojia na kufanya tafiti za awali, hasa ikizingatiwa kwamba maeneo makubwa ya nchi bado hayajafanyiwa utafiti wa kina.

“Takwimu sahihi ni msingi wa kuvutia uwekezaji na kuongeza ugunduzi wa rasilimali. Hatuwezi kuendeleza sekta bila taarifa za kutosha na tafiti madhubuti,” amesisitiza.

Waziri huyo pia ameagiza PURA kufanya tathmini ya kina katika vitalu vilivyopo, hususan katika ukanda wa Tanga, Ruvu, na maeneo mengine, ili kubaini iwapo wamiliki wa vitalu wanafanya shughuli za utafutaji kama inavyotakiwa.

 Ameongeza kuwa si vyema kwa vitalu kukaa mikononi mwa wawekezaji wasioendeleza shughuli za utafutaji, na mamlaka za udhibiti zinapaswa kuchukua hatua pale inapobainika hakuna maendeleo yanayofanyika kwa manufaa ya Taifa.

Akizungumzia mradi wa LNG, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuanza mapema kuandaa mkakati wa kujenga uwezo wa kitaasisi katika kusimamia mradi huo. 

Sambamba na hilo, amewahimiza kuandaa Watanzania kushiriki kikamilifu katika mnyororo wa thamani wa LNG, badala ya kusubiri utekelezaji wa mradi kuanza.

Awali katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amewataka PURA kusimamia majukumu yake ya msingi kama yanavyoainishwa katika malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.


















Na Munir Shemweta, WANMM

 

Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeyapatia ufumbuzi malalamiko ya muda mrefu ya viwanja mbadala kwa wananchi wa jiji la Dodoma.

 

Suluhisho hilo linafuatia malalamiko ya takriban wananchi 4000 wa jiji la Dodoma wanaodai viwanja na halmashauri ya jiji la Dodoma kuwapa ahadi bila kutekeleza mpaka sasa.

 

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 25 Februari 2026 na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo wakati akizungumza na wananchi wenye migogoro ya ardhi katika eneo la Mahomanyika lilopo kata ya Nzuguni jijini Dodoma.

 

Dkt Akwilapo amesema, eneo la Mahomanyika ni eneo la serikali hivyo lipangwe na kupimwa kwa ajili ya utatuzi wa migogoro ya meneo mbalimbali ya jiji la Dodoma pamoja na matumizi ya serikali.

 

"Eneo hili lenye mgogoro hapa Mahomanyika ni eneo la serikali hivyo lipangwe na kupimwa kwa ajili ya utatuzi wa migogoro na siyo ya hapa tu na mingine ya jiji la Dodoma na matumizi ya serikali" amesema.

 

Amesisitiza kuwa katika upangaji wa eneo hilo kipaumbele kiwe kutatua changamoto za wananchi wa jiji la Dodoma ambao kwa muda mrefu wamedai viwanja na jiji kuwaahidi bila ya kuwapatia.

 

Katika kufanikisha zoezi hilo, zimeundwa timu mbili kwa ajili ya upangaji na upimaji na pamoja na ile ya kushughulika na uhakiki wa wananchi wenye migogoro na kustahili kupatiwa  viwanja mbadala.

 

"Timu hizi zitaanza kazi mara moja na kazi hiyo itafanyika kwa muda wa siku sitini, miezi miwili kazi iwe imekamilika kila mtu kujua amepata nini na anaenda wapi" amesema.

 

Akigeukia uuzwaji viwanja 1,037 vilivyoingizwa kwenye mfumo wa TAUSI ili wananchi wapate viwanja vilivyopimwa katika eneo la Mahomanyika, Dkt. Akwilapo amuagiza Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma kuendelea na uuzaji viwanja kwa waombaji 352 pekee walioanza kulipa huku wale ambao hawajaanza kulipa maombi yao yasitishwe.

 

Eneo la Mahomanyika limekuwa na changamoto ya malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa wananchi wakidai ni wamiliki wa asili wa maeneo hayo jambo lililosababisha kuundwa kwa Timu (Timu ya DC) ambayo ilishirikisha wananchi, Vyombo vya Usalama na Wataalam ambapo timu hiyo ilibaini eneo husika ni eneo la Serikali.










Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amefungua semina ya Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoka Zanzibar na kusisitiza umuhimu wa kuimarisha usimamizi na uwajibikaji katika utekelezaji wa Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo.

Semina hiyo imefanyika Unguja, Zanzibar Februari 26, 2026 akieleza kuwa Mfuko wa Jimbo umechangia kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma za kijamii ikiwemo upatikanaji wa maji safi na salama, umeme, elimu, barabara na kukuza shughuli za biashara katika jamii.

Amesema mfuko huo ulianzishwa kwa lengo la kuwashirikisha wananchi katika kubuni na kutekeleza miradi ya maendeleo inayogusa mahitaji halisi ya majimbo yao, hivyo ni wajibu wa wabunge kuhakikisha wananchi wanashirikishwa kikamilifu ili miradi iwe na tija na uendelevu.

“Serikali inalenga kuwezesha utekelezaji wa miradi ya haraka yenye manufaa kwa wananchi, kuimarisha uwajibikaji na ushiriki wa jamii katika kupanga na kusimamia maendeleo pamoja na kupunguza pengo la maendeleo kati ya maeneo mbalimbali,” amesema Mhe. Abdulla.

Ameeleza licha ya kuwepo kwa sheria na miongozo ya matumizi ya fedha za mfuko huo, bado kuna changamoto za usimamizi katika baadhi ya halmashauri zilizosababisha kuibuka kwa hoja za ukaguzi.

Kutokana na changamoto hiyo amewataka watendaji wa halmashauri kusimamia ipasavyo fedha hizo ili kuepuka dosari na kuhakikisha thamani ya fedha inapatikana.

Aidha amezungumzia umuhimu wa kukusanya maoni kuhusu mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Jimbo ya mwaka 2009, kufuatia maelekezo yaliyotolewa baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ya utekelezaji wa mfuko kwa mwaka 2023/24 katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI.

Amesema Ofisi ya Makamu wa Rais imeombwa kuratibu upatikanaji wa maoni kutoka upande wa Zanzibar, hivyo akawahimiza wabunge kutumia semina hiyo kama jukwaa la majadiliano ya wazi na kitaalamu kwa lengo la kuboresha mfumo wa mfuko huo.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema semina hiyo ni hatua muhimu katika kuimarisha uelewa wa wabunge kuhusu utekelezaji na usimamizi wa Mfuko wa Jimbo.

Amesema maboresho yanayopendekezwa yanalenga kuhakikisha sheria na miongozo ya mfuko inaendana na hali halisi ya utekelezaji na kuongeza uwazi pamoja na ufanisi katika matumizi ya fedha za umma.

Semina hiyo imewakutanisha wabunge kutoka majimbo 50 ya Zanzibar pamoja na viongozi na watendaji kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais na Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, kwa lengo la kujadili kwa kina namna bora ya kuboresha utekelezaji wa Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo.







Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, ameielekeza Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuongeza kasi ya utafiti wa awali katika maeneo mapya ya mafuta na gesi asilia ili kuvutia wawekezaji na kuongeza mapato ya taifa.

Akizungumza leo Februari 26, 2026, wakati wa Mkutano wa Tano wa Baraza la Wafanyakazi uliofanyika mkoani Morogoro, Dkt. Mataragio amesema juhudi hizo zitachochea uwekezaji, kupanua ushiriki wa wazawa na kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya msingi ya taasisi hiyo.

Amesisitiza kuwa ni muhimu kwa PURA kuendelea kutambua na kuendeleza maeneo mapya ya miradi, kuyatangaza kwa wawekezaji pamoja na kusimamia kikamilifu majukumu yake kama yalivyoainishwa katika malengo ya kuanzishwa kwake.

Miongoni mwa majukumu hayo ni kusimamia na kufuatilia shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia kwa kuzingatia sheria na taratibu, kuishauri Serikali kuhusu masuala ya mkondo wa juu wa mafuta na gesi, pamoja na kutangaza vitalu vilivyowazi kwa ajili ya uwekezaji ili kuongeza ugunduzi wa rasilimali hizo nchini.

Dkt. Mataragio amesema hatua hizo zitasaidia kuongeza mchango wa sekta ya mafuta na gesi katika ukuaji wa uchumi wa taifa na kuimarisha usimamizi wa rasilimali kwa manufaa ya Watanzania.







Tume ya Ushindani (FCC) imesema itaendelea na mchakato wa marekebisho ya sheria zake kwa lengo la kuimarisha ulinzi wa walaji, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki unaochochea ukuaji wa uchumi na ajira nchini.

Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Ngasongwa amesema marekebisho hayo yanalenga kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa zisizo na ubora, matangazo ya upotoshaji pamoja na vitendo vinavyokwenda kinyume na misingi ya ushindani wa haki sokoni.
Amesema moja ya vipaumbele vya Tume hiyo ni kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia zinazoingia sokoni, akibainisha kuwa bidhaa hizo huathiri afya za wananchi, hupunguza mapato ya Serikali na kuwanyima wafanyabiashara halali fursa ya kukuza biashara zao.
“Jukumu letu ni kuhakikisha uchumi unakua kwa misingi ya ushindani wa haki. Matokeo yake ni kuongezeka kwa uwekezaji na ajira kwa wananchi,” alisema Ngasongwa.
Aidha, amesema FCC itaendelea kukutana mara kwa mara na waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali kwa lengo la kutoa taarifa sahihi kuhusu majukumu yake na kusikiliza changamoto za wananchi ili kuzipatia ufumbuzi kwa wakati.
Katika hatua nyingine, amesema kuna maboresho yanayofanyika kupitia TANOGA — muunganiko wa taasisi za Serikali za udhibiti pamoja na mawakala wa forodha — kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa bidhaa zinazoingia nchini.
Ngasongwa ameongeza kuwa taasisi hizo zinaelekea kuingia katika mfumo wa kidijitali utakaopunguza mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watumishi na wateja, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, kupunguza urasimu na kudhibiti mianya ya vitendo visivyo vya kiadilifu.
FCC imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali pamoja na sekta binafsi ili kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanabaki kuwa salama, yenye ushindani wa haki na yenye manufaa kwa wananchi.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa, akizungumza wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyoandaliwa na Tume hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, Februari 24, 2026.
Makamu wa Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Habari Mkoa wa Dar ea Salaam (DARPC) Mary Geofrey akitoa maelezo kuhusiana na semina ya FCC itavyochochea ushindani wa soko ,jijini Dar es Salaam.
Semanina ikiendelea 
Picha pamoja ya wafanyakazi wa FCC na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.
Picha pamoja ya waandishi wa Habari na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.