KIGOMA

Baraza la Ushindani(FCT), moja ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, imeendesha kikao cha kuwajengea uwezo watumiaji wa huduma, wadau na wafanyabiashara wa Mkoa wa Kigoma kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu haki za ushindani na taratibu za rufaa.

Kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa Lake Tanganyika Hotel na kuhudhuriwa na wadau kutoka sekta mbalimbali za biashara na huduma.

Akifungua kikao hicho, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Ndg. Deogratias Sangu, aliwataka wananchi kutumia elimu waliyoipata kuelewa haki zao katika ushindani na udhibiti wa soko. Alisema uelewa wa sheria na taratibu za ushindani utasaidia kupunguza migogoro isiyo ya lazima, kuimarisha uwajibikaji wa taasisi na kujenga mazingira ya Soko yenye usawa na haki.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa FCT, Mhe. Jaji Rose Ally Ebrahim, alisema Baraza lina jukumu la kusikiliza na kuamua rufaa zinazotokana na maamuzi ya Fair Competition Commission (FCC) pamoja na mamlaka za udhibiti wa sekta mbalimbali ikiwemo LATRA, EWURA, TCRA, TCAA na PURA.

Aliwahimiza wananchi wa Kigoma kulitumia Baraza hilo wanapokuwa hawajaridhishwa na maamuzi ya vyombo husika, akisisitiza kuwa mfumo wa rufaa umewekwa kisheria ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati na kwa uwazi.

“Watu wakijua wapi pa kupata haki, wanapunguza gharama za kuhangaika kutoka sehemu moja ya huduma hadi nyingine,” alisema Mhe. Jaji Ebrahim, akisisitiza kuwa elimu ya sheria ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha wananchi na wafanyabiashara kukua kiuchumi.

Wadau waliohudhuria kikao hicho waliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuendelea kuimarisha taasisi zinazolinda na kusimamia haki za wafanyabiashara na watumiaji wa huduma.

Walisema juhudi hizo zinaonyesha dhamira ya Serikali ya kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika uchumi kupitia mfumo wa ushindani ulio wazi, shindani na wa haki, unaochochea ukuaji wa biashara na ustawi wa taifa.

     

Na mwandishi wetu

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju amesema mradi wa jengo la wagonjwa Mahututi katika Hospitali ya Halmashauri hiyo litakapokamilika litaondoa adha kwa wananchi kusafiri takribani kilomita 160 kufuata huduma hizo katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga.

Akisoma taarifa ya mradi huo kwa Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, akiwa katika ziara yake ya kikazi wilayani Handeni, Ukwaju amesema uwepo wa jengo hilo ni juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za afya na kuwataka watendaji kuhakikisha miundombinu hiyo inatumika ipasavyo kuokoa maisha ya wananchi.

"Uwepo wa ICU hii utaondoa changamoto iliyokuwa inawakabili wagonjwa mahututi waliolazimika kusafirishwa umbali mrefu kupata huduma, hali iliyokuwa ikiongeza hatari kwa maisha yao pamoja na gharama kwa familia," amesema.

Awali, amefafanua kuwa Mradi wa ujenzi wa jengo la ICU ulianza Mei 6, 2024 na kukamilika Mei 25, 2025 kwa gharama ya zaidi ya Sh. milioni 426, ukitekelezwa na kampuni ya SWASH Construction Co. Limited kwa kushirikiana na CAREMED Gas Limited waliotekeleza mfumo wa gesi ya oksijeni.

Amesema Halmashauri tayari imelipia vifaa tiba vya awali vyenye thamani ya Sh. milioni 200 kupitia Bohari ya Dawa (MSD), huku ununuzi wa vifaa tiba vingine pamoja na awamu ya pili ya mfumo wa gesi ya oksijeni ukitarajiwa kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2026/2027.

Ujenzi wa jengo hilo ni sehemu ya maboresho ya miundombinu ya afya yaliyowezeshwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambapo alitoa Sh. milioni 900 kwa awamu ya pili kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa majengo mbalimbali ya hospitali hiyo.

Nao, wananchi wa Handeni wameeleza matumaini yao kuwa kuanza kwa huduma za ICU kutasaidia kuokoa maisha ya wagonjwa wengi, kuongeza ufanisi wa huduma za afya na kupunguza msongamano katika hospitali za rufaa za mkoa.


Na: OWM (KAM) - Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu amezindua Programu ya Nchi ya Kazi za Staha Awamu ya Tatu ya Mwaka 2025/2026 – 2029/2030 na Mkakati wa kukuza Kazi za Staha Kwa wafanyakazi wa nyumbani.

 


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Februari 12, 2026 amekagua na kuweka jiwe la msingi la Mradi wa ujenzi kituo cha kupokea na kupoza umeme cha MVA 60 Mkatata Tanga na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa  kilovolti 33.

Akiweka jiwe la msingi mradi huo, Dkt. Mwigulu amesema kutekelezwa kwa mradi huo ni jitihada za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika. 

"Nitoe rai kwa Wizara ya Nishati kuhakikisha kasi ya ukamilishwaji wa mradi huo na unakamilika kwa wakati ". Amesisitiza Mhe. Waziri Mkuu. 

Katika hatua nyingine ameiagiza Wizara ya Nishati kuwasiliana na Wizara ya Fedha ili kukamilisha malipo ya fidia kwa Wananchi takribani shilingi bilioni moja.

Ujennzi wa mradi huo ni shilingi bilioni 44 na unahusisha ujenzi wa vituo viwili vya kupokea, kupoza na kusambaza umeme vyenye uwezo wa MVA 60 huku kila kimoja kikiwa na MVA 30,  pamoja na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 33 kutoka kituo cha Mkata hadi kwa Msisi.

Kwa upande wake Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amemshukuru Mhe. Rais kwa kuwezisha upatikanaji wa fedha zitakazo tumika katika utekelezaji wa mradi huo.

“Utekelezaji wa mradi huu unakwenda kuondoa changamoto za umeme katika Wilaya za Handeni na Kilindi ambazo zinapata umeme kutokea Tanga mjiani ambapo ni umbali mrefu". Amesema Mhe. Ndejembi. 

Amefafanua kuwa kupitia miundombinu hiyo mipya, umeme utasafirishwa kutoka Mkata kwenda Msisi kwa umbali wa kilomita 45, hatua itakayoongeza uwezo wa usambazaji na kuimarisha huduma katika maeneo hayo.

Kuimalika kwa huduma ya umeme Wilaya za Handeni na Kilindi kutachochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi na kijamii.













 


Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi amesema mradi wa kimkakati wa ujenzi wa kituo cha kupoza umeme katika eneo la Mkata wilayani Handeni utagharimu shilingi bilioni 44.14 mpaka kukamilika kwake na utaimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Wilaya ya Handeni.

Akizungumza Februari 13, 2026 wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi, Waziri wa Nishati Mhe. Ndejembi amesema fedha hizo pia zitatumika kujenga njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 45 kutoka kituo cha Mkata hadi kijiji cha Kwamsisi.


Alieleza kuwa kwa muda mrefu wakazi wa Handeni walikuwa wakipata umeme kutoka Tanga, hali iliyosababisha upotevu mkubwa wa umeme njiani kutokana na umbali mrefu pamoja na kupungua kwa nguvu ya umeme. Kupitia mradi huu, sasa umeme utatoka Chalinze ambako ni karibu zaidi na Handeni, jambo litakaloongeza uthabiti wa huduma hiyo na kupunguza changamoto za kukatika mara kwa mara.

Kwa mujibu wa Waziri Ndejembi, kukamilika kwa kituo hicho kutaimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika wilaya za Handeni na Kilindi, kuchochea shughuli za uchimbaji wa madini ya graphite, kuvutia wawekezaji wapya na kuongeza mapato ya Shirika la Umeme kupitia wateja wakubwa watakaojiunga baada ya mradi kukamilika. Aidha, ajira zipatazo 120 zinatarajiwa kunufaisha wananchi wa eneo hilo.

Mradi huo unatekelezwa na kampuni ya TBEA kutoka China na utekelezaji wake ulianza Agosti 17, 2023 na unatarajiwa kukamilika Novemba 16, 2026.

Kwa upande wake, mkazi wa Kwamsisi, Rashid Hamza amesema awali ilikuwa vigumu kuendesha shughuli za kiuchumi kwa kutegemea umeme kutokana na kukatika mara kwa mara. Alisema matarajio yao ni kuona mradi huo ukikamilika kwa wakati ili kuwawezesha kuongeza uzalishaji na kipato kupitia matumizi ya nishati ya umeme.

Jiwe la msingi la mradi huo limewekwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mwigulu Nchemba kama dhamira ya Serikali ya kuendelea kuimarisha miundombinu ya nishati kwa maendeleo ya wananchi.