Standard Chartered Tanzania kwa kushirikiana na Nipe Fagio imeadhimisha miaka 20 ya programu ya kujitolea kwa jamii ya Standard Chartered duniani kwa kufanya zoezi la kila mwaka la usafi wa fukwe katika Ufukwe wa Silversand, Kunduchi.

Jumla ya washiriki 74, wakiwemo watoto 20, walishiriki katika zoezi hilo lililolenga kuchangia uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha ushiriki wa wafanyakazi katika shughuli za maendeleo ya jamii.

Akizungumza kuhusu shughuli hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Bank Tanzania, Geofrey Mchangila, alisema:

"Zoezi la mwaka huu lina umuhimu wa pekee kwetu kwani linafanyika wakati Standard Chartered inaadhimisha miaka 20 ya kujitolea kwa jamii duniani kote. Tunaamini kuwa mabadiliko ya kweli huanza pale watu wanapounganisha nguvu zao. 

Kupitia ushirikiano wetu na wafanyakazi, familia zao pamoja na Nipe Fagio, tunaendelea kuchangia kulinda ukanda wa pwani wa Tanzania na kujenga jamii zenye afya bora na mazingira endelevu kwa vizazi vijavyo."

Katika zoezi hilo, washiriki walisafisha eneo lenye ukubwa wa takribani mita za mraba 4,000 za ufukwe na kukusanya kilo 506 za taka zilizohifadhiwa katika mifuko 55. 

Uchambuzi wa taka zilizokusanywa ulionyesha kuwa plastiki, hususan povu la polystyrene na chupa za plastiki za vinywaji, ndizo zilikuwa taka zilizopatikana kwa wingi, hali inayodhihirisha umuhimu wa kuendelea kuchukua hatua za kudhibiti uchafuzi wa mazingira ya bahari.

Kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita, kupitia ushirikiano wake na Nipe Fagio, Standard Chartered Tanzania imefanikisha jumla ya kampeni tano za usafi wa fukwe, ikihusisha washiriki 594, kusafisha zaidi ya mita za mraba 32,000 za ukanda wa pwani na kukusanya karibu tani tano za taka.

Mpango huu ni sehemu ya mkakati mpana wa Standard Chartered wa kuendeleza uhimilivu wa mazingira na maendeleo endelevu, huku ukiunga mkono Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs), hususan Lengo la 13 la Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, Lengo la 14 la Kuhifadhi Maisha ya Chini ya Maji na Lengo la 17 la Kuimarisha Ushirikiano kwa Ajili ya Kufanikisha Malengo.

Standard Chartered inapoendelea kuadhimisha miaka 20 ya programu yake ya kujitolea kwa jamii, inaendelea kuwahamasisha wafanyakazi wake kutumia muda, ujuzi na utaalamu wao kuleta mabadiliko chanya na endelevu katika jamii na mazingira.










 


Serikali imetangaza kuanza kutoa vibali vya ujenzi na kufanya majadiliano na wamiliki wa ardhi na nyumba ambao wapo tayari kushiriki kwenye Mpango wa Uendelezaji Upya eneo la Sinza, huku ikisisitiza kuwa mchakato uliopita umefutwa ili kutoa nafasi ya kuanza upya kwa misingi ya uwazi, ushirikishwaji na kujenga maridhiano.

Kauli hiyo ilitolewa Julai 1, 2026 jijini Dar es Salaam na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo, alipokutana na wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kwa lengo la kuwafafanulia hatua za utekelezaji wa mpango huo na kusikiliza maoni yao.

Dkt. Akwilapo alisema Serikali imeamua kufungua ukurasa mpya baada ya kubaini kuwa mchakato uliopita uliacha malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi, hivyo vikao vyote vya awali vimefutwa na sasa mazungumzo yanaanza upya kwa ushirikiano na wananchi.

Alieleza kuwa ukuaji wa miji ni jambo lisiloepukika kutokana na ongezeko la watu na mahitaji ya makazi, hivyo Serikali ina wajibu wa kupanga matumizi ya ardhi kwa kuzingatia mahitaji ya sasa na ya baadaye.

Waziri huyo alisema Sinza ya sasa imebadilika kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka ya nyuma, jambo ambalo linahitaji mpango mpya wa maendeleo utakaoendana na hadhi yake kama eneo muhimu la makazi na biashara ndani ya Jiji la Dar es Salaam.

"Kama mwananchi anaona mpango huu haufai, hiyo ni haki yake, lakini ipo siku ataona umuhimu wake. Tusiporatibu maendeleo ya miji, tutakuwa na maeneo yasiyo na mpangilio na yenye miundombinu isiyokidhi mahitaji ya wananchi," alisema.

Dkt. Akwilapo alibainisha kuwa uendelezaji upya wa maeneo ya makazi si jambo geni nchini, kwani maeneo kama Posta, Kariakoo, Upanga, Oysterbay na Masaki yamepitia hatua kama hizo na yameendelea kuwa na thamani kubwa zaidi kutokana na upangaji mzuri wa matumizi ya ardhi.

Waziri huyo aliwataka wananchi kuwa makini na watu wasio waaminifu wanaoweza kutumia mchakato huo kuwahadaa au kuwasambazia taarifa zisizo sahihi kwa manufaa binafsi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, alisema mafanikio ya mpango huo yatategemea kiwango cha ushirikishwaji wa wananchi na kuzingatia maoni yao.

Alipendekeza muda wa ukusanyaji wa maoni uongezwe kwa miezi mitatu ili wananchi wengi zaidi wapate nafasi ya kuelewa mpango huo na kutoa maoni yao kabla ya hatua za utekelezaji kuanza.

"Wananchi wasikilizwe, maoni yao yazingatiwe na rasimu iboreshwe ili iakisi matakwa yao. Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan haiwezi kupora haki za wananchi bali itafuata sheria, kanuni na taratibu zote zinazotambuliwa," alisema Profesa Mkumbo.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga aliwataka wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kuwa watulivu na kutochukua maamuzi ya haraka ya kuuza maeneo yao kutokana na taarifa zisizo rasmi.

Alisema thamani ya ardhi katika eneo la Sinza imeongezeka maradufu hivyo wananchi wanapaswa kutambua fursa iliyopo badala ya kufanya maamuzi yatakayowagharimu baadaye.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Wamiliki wa Ardhi na Nyumba wa Sinza, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw. Asibwene Lumuli, alisema ushirikiano kati ya Serikali na wananchi ndio utakaohakikisha mpango huo unatekelezwa kwa mafanikio na kwa manufaa ya pande zote.






Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, leo Julai 1, ametembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba, yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza bandani hapo, Mhe. Kapinga ameipongeza TEMESA kwa kasi ya mabadiliko inayoenda nayo katika matengenezo ya magari na mabadiliko ya mifumo ya utoaji huduma.



“Nawapongeza sana kwa kazi nzuri mnazozifanya katika matengenezo ya magari na pia matumizi yenu ya mifumo katika utoaji huduma. Hongareni sana.” Amesema Mhe. Kapinga.

Waziri wa Viwanda na Biashara alipotembelea banda la TEMESA alipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na TEMESA, ikiwemo huduma za vivuko, umeme na elektroniki, matengenezo ya magari na mitambo, ushauri wa kihandisi pamoja na mifumo ya kidijitali na ubunifu unaolenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.



Maonesho hayo ya biashara yamebebwa na kauli mbiu isemayo “Hii ni Kubwa Kuliko” na yanatarajiwa kuzinduliwa rasmi siku ya ijumaa tarehe 3 Juni, 2026



TEMESA inaendelea kuwakaribisha wananchi, wadau na wageni wote kutembelea banda lake ili kujifunza kuhusu huduma zake, kupata ushauri wa kitaalamu na kufahamu mchango wa Wakala katika maendeleo ya sekta ya ufundi na umeme nchini.






Serikali ya Tanzania na Marekani zimesaini Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano katika Sekta ya Afya (MoU) ya miaka mitano yenye thamani ya zaidi ya dola za Marekani bilioni 3.14, hatua inayotarajiwa kuimarisha mfumo wa huduma za afya nchini huku ikijenga msingi wa kujitegemea katika utoaji wa huduma hizo.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb) , amesema Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yameonyesha mafanikio makubwa ya sekta ya viwanda na biashara pamoja na fursa zinazotolewa na Serikali kwa vijana na wanawake.

Waziri Kapinga amesema hayo akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Waziri Salum,  alipotembelea  maonesho hayo julai 01, 2026  yanayoshirikisha waoneshaji 3,722 kutoka nchi 23 ambayo yatafunguliwa rasmi Julai 3 na Rais wa Msumbiji, Mhe. Daniel Francisco Chapo, akiwa ameambatana na Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, amewataka Watanzania kutembelea maonesho hayo ili kujifunza kuhusu biashara, viwanda na fursa za kuongeza thamani ya mazao.

Amesema bidhaa nyingi zinazozalishwa na wanawake na vijana zinaonesha matokeo ya uwekezaji wa Serikali kupitia mikopo na programu za uwezeshaji.

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Baraza la Famasi limeanzisha mkakati wa kuimarisha ushirikiano na wahariri na waandishi wa habari nchini kwa kuwajengea uelewa kuhusu majukumu yake, hatua inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu huduma za dawa na usimamizi wa taaluma ya famasi ili kulinda afya ya jamii.
Wananchi, wanafunzi, wataalamu, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo wanatarajiwa kukutana jijini Mbeya Julai 3, 2026, katika mhadhara maalum wa hadhara utakaolenga kujadili nafasi ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) katika kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

 


Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amesisitiza umuhimu wa malezi na makuzi bora kwa watoto, akieleza kuwa ndiyo msingi wa kujenga kizazi chenye maadili, afya njema, elimu na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii na Taifa.

Akizungumza katika nyakati tofauti tarehe 1Julai, 2026 mkoani Mtwara, Naibu Waziri Mahundi amesema malezi ya mtoto ni jukumu la wazazi wote wawili, hivyo akawataka akina baba na akina mama kushirikiana kwa karibu katika kuwalea watoto wao badala ya kumwachia mzazi mmoja jukumu hilo.

"Malezi ya mtoto si jukumu la mama pekee, Baba na mama wanapaswa kushirikiana kwa upendo, uwajibikaji na mshikamano ili kuwajengea watoto msingi imara wa maisha kwa kuwa watoto wa leo ndiyo viongozi na nguvu kazi ya kesho, hivyo wanahitaji kulelewa katika mazingira salama na yenye maadili mema," amesema Naibu Waziri Mahundi.

Aidha, Naibu Waziri Mahundi amesema Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowainua wananchi kiuchumi kupitia fursa mbalimbali za uwezeshaji, hivyo amewahimiza wajasiriamali kutumia kikamilifu mikopo inayotolewa kupitia mabenki na taasisi za kifedha ili kukuza biashara zao, kuongeza kipato na kuboresha ustawi wa familia.

"Mikopo inayotolewa na Serikali ni fursa ya kujiletea maendeleo nawahimiza wajasiriamali kuitumia kwa malengo yaliyokusudiwa ili biashara zikue, kipato kiongezeke na hatimaye familia ziwe na uwezo wa kuwapatia watoto huduma bora za elimu, afya na lishe." amesema Naibu Waziri Mahundi.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Mahundi amempongeza Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, kwa kuanzisha kituo cha kulelea watoto katika Soko la Chuno, akieleza kuwa kituo hicho ni mfano wa ubunifu unaowasaidia wazazi, hususan wajasiriamali, kutekeleza shughuli zao za kiuchumi huku watoto wao wakipata huduma ya uangalizi katika mazingira salama.

Naibu Waziri Mahundi amesema uwepo wa kituo hicho umeleta nafuu kwa wazazi wanaofanya shughuli za biashara sokoni hapo, huku ukiwa sehemu ya jitihada za kuhakikisha watoto wanapata malezi na ulinzi stahiki wakati wazazi wao wakitafuta kipato cha kuendesha maisha ya familia.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana na Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini, Joel Nanauka, amesema elimu hiyo itaongeza uelewa wa jamii na kuwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika kujenga familia imara na Taifa lenye maendeleo endelevu.



Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Jumatano, Julai 1, 2026, amekagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, lililopo mjini Mugumu, mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani humo.

Akiwasilisha taarifa ya ujenzi huo, Msanifu Majengo wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Mara, Bw. Nicholas Jeje, alisema mradi huo unagharimu shilingi bilioni 4.5 zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Alisema ujenzi ulianza Aprili 10, 2025 na unatarajiwa kukamilika Aprili 9, 2028, huku utekelezaji wake ukiwa umefikia asilimia 42.

Alieleza kuwa jengo hilo litakuwa na ofisi 62, zikiwemo ofisi za Mkurugenzi wa Halmashauri na Mwenyekiti wa Halmashauri, pamoja na kumbi mbili za mikutano zenye uwezo wa kuchukua watu 50 na 110 mtawalia, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi, alimkaribisha Waziri Mkuu mkoani humo na kusema ziara hiyo itamwezesha kutembelea wilaya zote sita, halmashauri zote tisa na majimbo yote 10 ya uchaguzi yaliyopo mkoani Mara, ambapo pamoja na mambo mengine atakagua miradi ya maendeleo na kuzungumza na wananchi.








 

 

 Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Christine Grau, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, katika Ofisi ya Katibu Mkuu wa CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yamefanyika jana Juni 30,2026, ikiwa ni sehemu ya ziara ya kumuaga Balozi Grau anayehitimisha kipindi chake cha uwakilishi nchini Tanzania. Viongozi hao walitathmini ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya na kujadili namna ya kuuendeleza kwa manufaa ya pande zote mbili.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao walibadilishana mawazo kuhusu umuhimu wa kuimarisha misingi ya utawala bora, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa kama nguzo ya maendeleo endelevu ya Taifa. Katika muktadha huo, CCM ilisisitiza dhamira yake ya kuendelea kujenga Taifa linaloongozwa kwa misingi ya haki, uwajibikaji na utulivu wa kisiasa.

Pia, ilitambua changamoto zilizojitokeza nchini katika kipindi cha Uchaguzi Mkuu uliopita na umuhimu wa hatua ambazo Serikali inaendelea kuzichukua katika kuimarisha imani ya wananchi, ikiwemo kuundwa kwa Tume ya Uchunguzi, Tume ya Upelelezi wa Jinai na hatua nyingine za kisheria zinazolenga kuhakikisha ukweli, uwajibikaji na haki vinaendelea kutawala katika kulinda amani na mshikamano wa Taifa.

Aidha, ilielezwa kuwa ajenda ya kuendelea kuimarisha demokrasia nchini, ikiwemo mchakato wa Katiba Mpya ambao umeainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, inabaki kuwa sehemu muhimu ya maono ya muda mrefu ya kuimarisha utawala bora na mshikamano wa Taifa.

Viongozi hao pia walitambua nafasi ya vijana katika mustakabali wa maendeleo ya Tanzania na umuhimu wa kuhakikisha kizazi hicho kinaendelea kuwa sehemu ya safari ya Taifa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na ujenzi wa uchumi wenye ushindani na maendeleo jumuishi.

CCM inathamini ushirikiano wake na Umoja wa Ulaya na inaamini kuwa ushirikiano huo utaendelea kuimarika kwa kuzingatia misingi ya kuheshimiana, maslahi ya pamoja na dhamira ya pamoja ya kuendeleza maendeleo endelevu ya Tanzania.







 

 


HALMASHAURI za Wilaya, Miji na Jiji mkoani Tanga, zimeagizwa kuzuia vyanzo vinavyosababisha hoja zinazoibuliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). 

Agizo hilo limetoa leo Juni 30, 2026 na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt Batilda Burian, alipozungumza kwenye vikao maalum vya kujadili hoja za CAG katika Baraza la Madiwani wa Halmashauri za Lushoto na Bumbuli.

Amesema, taarifa za CAG kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, inaonesha halmashauri hizo zimefanikiwa kupata hati inayoridhisha, ikiwa ni Ishara ya ufanisi, weledi na kujituma kwa watumishi na watendaji.

Amesema, hali hiyo inapaswa kuendelezwa ili kufikia malengo msingi ya Serikali katika kutoa huduma bora kwa wananchi.


Hata hivyo, Mhe. Balozi Dkt Batilda amesema, pamoja na mafanikio hayo, halmashauri hizo zinatakiwa kudhibiti vitendo vinavyosababisha hoja za ukaguzi.

Awali, taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Nje, Mkoa wa Tanga, Hamu Mwakasola, ilieleza kuwa kutolewa hati inayoridhisha haimaanishi kuwepo mifumo mizuri ya udhibiti wa ndani, bali kutokuwepo dosari kubwa wakati wa ukaguzi.

“Inamaanisha hapakuwa dosari kubwa zilizobainika wakati wa ukaguzi ambazo zingemzua Mkaguzi kutoa maoni, au kumlazimu kutoa hati yenye mashaka au hati mbaya,” amesema

Naye Katibu Tawala Mkoa (RAS) wa Tanga, Rashid Mchatta, pamoja na mambo mengine, amewahimiza watumishi na umma, kuendeleza mahusiano mema ili kuongeza ufanisi na tija mahali pa kazi.

Amesema, viongozi, watendaji na watumishi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wanapaswa kutambua ‘uzito’ wa hadhi ya Ofisi ya CAG katika ukaguzi wa hesabu uliopo katika ngazi za kimataifa.

Mchatta amesema utambuzi wa ubora huo utachangia kuboresha utendaji kazi na kupunguza kwa kiasi kikubwa hoja za ukaguzi, hali itakayoifanya CAG kutekeleza vema wajibu wake wa ushauri wa kitaalamu kwa taasisi husika.  


 


📌 Waziri Ndejembi asema mradi utaimarisha Gridi ya Taifa na kuongeza uwezo wa kusafirisha umeme

📌 Mradi unatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026

📌 MD TANESCO asema Shirika limevunja rekodi kwa kuunganisha wateja zaidi ya laki nane mwaka 2025/26


Mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma wenye urefu wa kilometa 345 umefikia asilimia 89 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026, hatua itakayoongeza uwezo wa kusafirisha umeme na kuimarisha uthabiti wa Gridi ya Taifa.

Akikagua maendeleo ya Mradi huo Julai 1, 2026, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb), amesema mradi huo ni miongoni mwa uwekezaji wa kimkakati wa Serikali unaolenga kuimarisha miundombinu ya usafirishaji wa umeme nchini na kuongeza uwezo wa Gridi ya Taifa kuhudumia mahitaji yanayoendelea kuongezeka.

Amesema njia hiyo ya kusafirisha umeme ina umuhimu mkubwa kutokana na kuwezesha usafirishaji wa umeme unaozalishwa na Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere chenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115.

Aidha, Waziri Ndejembi amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miradi ya umeme ili kuhakikisha huduma ya umeme wa uhakika inaendelea kuwafikia Watanzania na kukidhi mahitaji ya sekta mbalimbali za uzalishaji.

“Serikali imeona mahitaji ya umeme nchini yanazidi kuongezeka, hivyo ujenzi wa njia hii ya umeme ni muhimu sana kwani utaleta uthabiti katika Gridi ya Taifa,” amesema Mhe. Ndejembi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Razalo Twange, amesema ongezeko la uwekezaji katika miundombinu ya umeme limechangia kuongezeka kwa idadi ya wateja wanaounganishiwa huduma, ambapo katika mwaka wa fedha 2025/26 Shirika limeandika historia kwa kuwaunganishia umeme zaidi ya wateja laki nane.

“Haijawahi kutokea tangu Tanzania ipate uhuru. Hii inaonesha mahitaji ya umeme yameongezeka, na hivyo sisi tunaendelea kuongeza miundombinu ya umeme,” amesisitiza Bw. Twange.

Awali, akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Meneja wa Mradi, Mha. Newton Mwakifamba, amesema kazi zinaendelea vizuri na zinatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026, kwa mujibu wa ratiba ya mkataba.