Na; Mwandishi Wetu - Chato
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Profesa Mohammed Ali Sheikh, Ametoa wito kwa wataalam kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu kuwa na mbinu bora za kiutendaji zitakazowezesha programu hiyo kutekelezeka kwa kasi zaidi.
Ameyasema hayo Wilayani Chato Mkoani Geita Tarehe 12 Juni 2026 alipozungumza na wataalam wa programu wanaofanya kazi ya utekelezaji ya mapitio ya programu mara baada ya ziara yake maalum ya kutembelea kituo cha kuendeleza Ukuzaji viumbemaji cha Rubambagwe kilichopo Wilayani chato.
“Niwapongeze sana kwa kuchukua hatua za haraka baada na maagizo ya kikao cha Mawaziri kukaa pamoja kama wataaalamu na kuyafanyia kazi maagizo yale. Hii ni hatua muhimu sana inayoonesha ni kwa namna gani mnaweza kuwajibika kiutaalamu, mnapewa maelekezo na mnayatekeleza” Alisema.
Naibu Katibu Mkuu Sheikh alibainisha kuwa, kukutana kwa wataalamu hao ni hatua muhimu sana ya kukaa pamoja na kujaribu kujitathmini kuona kila kinachofanyika kinakwenda sawa ama vinginevyo, ‘’Niipongeze sana timu ya Uratibu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kuitisha kikao kazi hiki “Mnapoona kitu hakiendi hebu muitane muone namna ya kukifanyia kazi sisi kama watekelezaji wa Programu hii ni familia moja, Serikali ni moja na tunachotaka ni kufikia malengo na kumsaidia mtanzania katika kilimo na uvuvi kwa ukubwa wake” Alisisitiza
Alibainisha kuwa, kwa kufanya tathmini kunasaidia kujua wapi ulikwama na wapi pa kuboresha. Zaidi aliendelea alisema kuwa, kukua na kubadilika kwa teknolojia kufanya tathmini kunaweza kusaidia kwenda mbele zaidi, “lazima tusaidianae tuje na mbinu bora za utekelezaji katika utendaji wa mradi msione aibu kushauri na kutoa mapendekezo ya kiutendaji kuhusiana na Programu.” Alisema
Akizungumza katika kikao kazi hicho, Mhandisi Enock Nyanda, Mkurugenzi msaidizi sehemu ya Sekta za Uchumi na Uzalishaji Idara ya Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) alisema lengo mahususi ya wataalam kukutana katika kikao kazi hicho ni kuongeza kasi ya utekelezaji wa Programu ili kufikia malengo.
Na Mwandishi Wetu
Baraza la Ushindani Halali Zanzibar (ZFCT) limefanya ziara ya mafunzo katika Tume ya Ushindani ya Haki (FCC) kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu katika masuala ya ushindani wa biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na usimamizi wa mashauri yanayohusiana na ushindani.
Ziara hiyo iliyofanyika katika ofisi za FCC Juni 10, 2026 Jijini Dar es Salaam, imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa ya haki kwa wadau wote.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa alisema kuwa kubadilishana uzoefu na taasisi za ndani ya nchi ni muhimu katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa ushindani na kulinda maslahi ya watumiaji dhidi ya vitendo vinavyokiuka sheria za ushindani na biashara.
Alisema ujumbe wa ZFCT unapata fursa ya kujifunza namna FCC inavyotekeleza majukumu yake ya kudhibiti vitendo vya ushindani usio wa haki, kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia pamoja na mifumo ya uchunguzi na uendeshaji wa mashauri mbalimbali yanayofikishwa mbele ya taasisi hiyo.
Kwa upande wake, ujumbe wa ZFCT ukiongozwa na Msajili wa Baraza, Bi. Fatma Yahya alieleza kuridhishwa na mafunzo na uzoefu uliopatikana katika ziara hiyo, ukibainisha kuwa utaisaidia taasisi hiyo kuimarisha utendaji wake katika kushughulikia rufaa na mashauri yanayohusiana na ushindani wa biashara Zanzibar.
ZFCT ni chombo kinachoshughulikia mashauri na rufaa zinazotokana na maamuzi ya mamlaka za ushindani, ambapo wadau wasiokubaliana na maamuzi yaliyotolewa huwasilisha kesi zao kwa ajili ya kusikilizwa na kutolewa uamuzi.
Ziara hiyo pia ilitoa nafasi kwa wataalamu kutoka pande zote mbili kujadiliana changamoto na fursa zilizopo katika usimamizi wa ushindani wa biashara, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana katika kujenga uwezo wa kitaasisi na kuimarisha utekelezaji wa sheria zinazolinda ushindani wa haki katika soko.

Wakulima wa zao la pamba kutoka vijiji vya Mbutu, Iyogelo, Ilambakuki, Imalanguzu na Mwamakoma vilivyopo katika Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora, wamehamasika kufungua akaunti za benki na kusajili laini za simu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea malipo ya mazao yao kwa njia ya kidijitali. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi, usalama na uharaka wa malipo kwa wakulima.
Wakulima hao wamefungua akaunti kupitia Benki ya NMB pamoja na kusajili laini kupitia mtandao wa simu wa Mixx by Yas, hatua itakayowawezesha kupokea fedha zao kwa urahisi kupitia mifumo ya benki na huduma za kifedha za simu za mkononi.
Zoezi hilo limefanyika kwa kushirikiana na AMCOS za Ngw'ajojabi, Ngw'asabi na Mwamakoma AMCOS, likitekelezwa kufuatia waraka wa Mrajis wa Vyama vya Ushirika unaoelekeza malipo ya wakulima wa pamba kufanyika kupitia akaunti za benki na huduma za fedha kwa njia ya simu badala ya kutegemea fedha taslimu. Lengo ni kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati, kwa uwazi na kwa usalama zaidi.
Mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka siku hadi siku kufuatia juhudi za uhamasishaji zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali. Hadi kufikia Juni 10, 2026, jumla ya wakulima 506 wamejitokeza na kufungua akaunti pamoja na kujiunga na huduma za kifedha za simu, hatua inayoonesha uelewa na utayari mkubwa wa wakulima kupokea mabadiliko ya mfumo wa malipo ya kidijitali.
Aidha, uhamasishaji wa zoezi hilo umefanywa na Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Tabora, Peja Mhoja pamoja na Mrajis Msaidizi (Uhamasishaji), Ibrahim Kadudu, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wakulima kujiunga na mifumo rasmi ya kifedha ili kunufaika na malipo ya kisasa, salama na yenye tija.


Mkuu wa Tawi la Operation na Mafunzo wa JKT, Brigedia Jenerali Peter Mnyani,akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 12,2026 katika Mako Makuu ya JKT Chamwino Mkoani Dodoma kuhusu wito wa kuripoti makambini vijana waliochaguliwa kujiunga na mafaunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria 2026.
Na.Alex Sonna-CHAMWINO
Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa JKT Meja Jenerali Rajab Mabele amewataka Vijana waliohitimu kidato cha Sita kwa Mwaka 2026, Tanzania Bara na Visiwani ambao wamechaguliwa kujiunga na Mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa sheria ambao hawajaripoti kwenye kambi waliyopangiwa, kwenda kuripoti kwenye makambi yaliyokaribu nayo kuanzia juni 12 hadi Juni 15, 2026.
MHA. MRAMBA AKUTANA NA WADAU WA KIMATAIFA KUHARAKISHA MIRADI YA JOTOARDHI NA NISHATI SAFI YA KUPIKIA
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mha. Felchesmi Mramba, amefanya mazungumzo na wadau mbalimbali wa sekta ya nishati kuhusu fursa za kuendeleza miradi ya jotoardhi na kuimarisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini Tanzania.
Mazungumzo hayo yamefanyika pembeni mwa Mkutano wa Dunia wa Jotoardhi (World Geothermal Congress – WGC 2026) nchini Canada, ambapo Mha. Mramba alikutana na Bw. Yvan Champagne, Mwanzilishi na Mkurugenzi wa Hewa Ukaa wa Kampuni ya CarbonAI.
Katika kikao hicho viongozi hao wamejadiliana namna ya kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa miradi ya nishati safi ya kupikia pamoja na upatikanaji wa fedha kupitia mfumo wa hewa ukaa (carbon financing) kwa ajili ya kufadhili miradi hiyo.
Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mha. Mramba ameikaribisha CarbonAI kushirikiana na Serikali katika kutekeleza ajenda ya nishati safi ya kupikia na kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.
Amesema Serikali ipo tayari kushirikiana na taasisi na kampuni zenye teknolojia na uzoefu utakaosaidia kufikiwa kwa malengo ya maendeleo endelevu katika sekta ya nishati.
Aidha, Mha. Mramba amefanya mazungumzo na wadau mbalimbali wa nishati jadidifu, hususan katika eneo la jotoardhi, kuhusu fursa za kuharakisha maendeleo ya miradi ya rasilimali hiyo nchini.
Ameeleza kuwa Serikali inaendelea kuweka msisitizo mkubwa katika matumizi ya nishati jadidifu kama sehemu ya mkakati wa kuhakikisha asilimia 75 ya umeme nchini inazalishwa kutoka katika vyanzo vya nishati jadidifu ifikapo mwaka 2030.
Mkutano wa Dunia wa Jotoardhi (WGC 2026) umewakutanisha viongozi wa Serikali, Wataalam, wawekezaji na wadau wa Sekta ya Nishati kutoka sehemu mbalimbali duniani kwa lengo la kujadili maendeleo ya teknolojia, sera na uwekezaji katika miradi ya jotoardhi.
Na Hassan Kimweri, WAF – Tabora.
Jumla ya macho 996 yamefanyiwa uchunguzi kwa wagonjwa 823 wanaotarajiwa kufanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho katika kambi maalum ya madaktari bigwa iliyowekwa na Serikali kwa kushirikiana na Taasisi ya 'Helen Keller International' na wadau wengine wa sekta ya afya.
Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Igunga Mhe. Elizabeth Rwegasila amesema hayo leo wakati wa ufunguzi wa kambi ya madaktari bingwa wa macho iliyowekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Igunga mkoani Tabora ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha afya ya macho na kuondoa tatizo la upofu kwa wananchi.
"Idadi hii inaonesha ukubwa wa mahitaji ya huduma za macho kwa wananchi wa eneo hili, wanaonufaika na huduma hiyo wanapatiwa huduma mbalimbali muhimu ikiwemo usafiri kutoka majumbani mwao, malazi, chakula pamoja na huduma za matibabu kabla na baada ya upasuaji," amesema Mhe. Rwegasila
Aidha, amelishukuru Shirika la Helen Keller International kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za afya ya macho, akieleza kuwa mbali na kutoa huduma za matibabu, shirika hilo limechangia kuwajengea uwezo wataalamu wa afya ili kuendeleza huduma hizo hata baada ya mradi kukamilika.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Wizara ya Afya Dkt. Greater Mande amesema mtoto wa jicho ni miongoni mwa sababu zinazosababisha upofu kwa wananchi wengi, kupitia kambi hiyo wagonjwa wengi wamepata fursa ya kurejeshewa uwezo wao wa kuona na kuendelea na shughuli zao za kila siku.
Pia, Dkt. Mande amewahimiza wananchi watakaonufaika na huduma hizo kuwa mabalozi kwa jamii zao kwa kutoa taarifa kwa watu wengine wenye changamoto za macho ili waweze kujitokeza kupata matibabu wanapopata fursa hiyo.
Nae, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Boniface Marwa amesema wataendelea kushirikiana na wadau ili huduma hiyo ya upasuaji na mtoto wa jicho inakua endelevu na wananchi waendelee kupata huduma hizo pamoja na kuwashukuru Helen Keller kwa kuwasimesha wataalam wa eneo hilo.
Sambamba na hilo, Mkurugenzi wa Shirika ka Helen Keller International Dkt. Geogle kabona amesema msaada huo utaendelea kutolewa pamoja na kutoa huduma ya mafunzo kwa wataalamu wa eneo hilo pamoja na kutolewa kwa elimu ili jamii ipate uelewa huo.
"Tutaendelea kushirikiana na Serikali katika juhudi za kupunguza upofu unaozuilika na kuhakikisha wananchi wengiz zaidi wanaoata huduma bira za afya ya macho," amesema Dkt. Kabona.
Serikali imeendelea kuweka msukumo mkubwa katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi na mbadala nchini, hususan umeme na gesi asilia, katika sekta ya usafiri na matumizi ya majumbani, kupitia mapendekezo mapya ya hatua za kodi kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Akiwasilisha mapendekezo ya Serikali ya makadirio ya mapato na matumizi Bungeni, Waziri wa Fedha,Balozi Dkt Khamis Mussa Omar, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kifedha na kodi zinazolenga kupunguza gharama za uwekezaji na kuongeza matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira.
Kwa mujibu wa mapendekezo hayo, Serikali imeendelea kutoa msamaha wa ushuru wa bidhaa kwa magari yanayotumia umeme na gesi asilia kwa kuzingatia ukubwa wa injini, sambamba na msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye gesi asilia iliyoshindiliwa (CNG) inayotumika kwenye magari.
Aidha, Serikali imeondoa VAT kwenye vifaa vinavyotumika katika miundombinu ya gesi asilia (CNG), ikiwemo compressors, vifaa vya kupimia, mitambo ya kuhifadhi gesi, magari maalum ya usafirishaji na pampu za kujazia gesi. Hatua hiyo pia inahusisha msamaha wa kodi katika mnyororo mzima wa uzalishaji wa CNG pamoja na vifaa vinavyotumika kubadili magari kutoka mafuta ya petroli kwenda kwenye gesi au umeme.
Katika sekta ya uzalishaji wa ndani, Serikali imeweka pia msamaha wa VAT kwenye malighafi zinazotumika kutengeneza mitungi ya gesi kwa matumizi ya majumbani na magari, pamoja na kutoa unafuu wa ushuru wa forodha kwa waunganishaji na wazalishaji wa vyombo vya moto vinavyotumia nishati safi nchini chini ya kanuni za Jumuiya ya Afrika Mashariki za mwaka 2025.
Kwa mwaka wa fedha 2026/27, Serikali inapendekeza hatua zaidi ikiwemo msamaha wa VAT kwa vifaa vya vituo vya kuchaji magari ya umeme (EV charging stations), pamoja na kupunguza ushuru wa forodha kutoka asilimia 25 hadi asilimia 10 kwa magari yanayotumia umeme.
Pia, Serikali imependekeza msamaha wa VAT kwa mita janja za gesi ya kupikia (LPG smart meters) zitakazoingizwa nchini na kusambazwa na wasambazaji wa gesi pekee, sambamba na majadiliano ya kutoa unafuu wa kodi kwa waunganishaji wa magari ya umeme nchini ili kuchochea uzalishaji wa ndani.
Hatua hizo Serikali inasema, zinalenga kupunguza gharama za matumizi ya nishati safi, kuvutia uwekezaji katika sekta ya nishati mbadala, kuimarisha viwanda vya ndani, na hatimaye kulinda mazingira kupitia upunguzaji wa matumizi ya mafuta ya kisukuku.
Kwa ujumla, mkakati huu unaonekana kuwa sehemu ya mpango mpana wa Serikali wa kuhamia kwenye uchumi wa kijani unaotegemea nishati safi na endelevu nchini.

















