Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt.Mosses Kusiluka amesema kuwa serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Raisi Daktari Samia Suluhu Hassan imeipa kipaumbele cha kwanza sekta ya TEHAMA nchini kwa kuendeleza mifumo mbalimbali na kuhakikisha huduma zinapatikana kirahisi.

Katika kufanikisha hilo pia serikali imeendelea kuwekeza katika sekta hiyo na kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kuweka rekodi nzuri ya kutambuliwa kimataifa katika kutoa huduma nzuri ya serikali mtandao.

Ameyasema hayo leo wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha Sita cha Serikali Mtandao (eGA) kinachoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa (AICC) mkoani Arusha. 

"Kuwepo kwangu hapa leo ni kuonyesha  umuhimu wa serikali ya awamu ya Sita  ambayo imeipa umuhimu wa kipekee TEHAMA,Mheshimiwa Raisi wetu Daktari Samia  Suluhu Hassan  anaishi TEHAMA na anaitumia kwa kiasi ambacho watu wengi hawawezi kufahamu kwahiyo TEHAMA ni kipaumbele cha kwanza kwenye Utekelezaji wa Ajenda ya serikalimtandao"Alisisitiza Balozi  Kusiluka

Aidha amesema kuwa Tanzania ni nchi yenye mafanikio makubwa duniani kwenye matumizi ya TEHAMA,hatua kubwa imepigwa na mafanikio ya eGa ni kielelezo kizuri cha azma ya serikali  kutumia teknolojia  kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi  hali ambayo inapelekea huduma kupatikana kwa wakati.

Nae Mhandisi Benedict  Ndomba  ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) amesema kuwa kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kitakuja na maazimio ya pamoja ya kuboresha huduma ya serikali mtandao, kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utendaji kazi na kujenga serikali mtandao.

Mhandisi Ndomba amewahikikishia washiriki eGA itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa kuendelea kuijenga serikali Mtandao.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Bodi  ya Wakurugenzi  Mamlaka  ya Serikali Mtandao (eGA), Daktari Mussa Kissaka amesema kuwa serikali ilianzisha mamlaka hiyo ili kuratibu  na kusimamia  jitihada za serikali mtandao pamoja na kuhakikisha kuwa uzingatiaji wa sera,sheria,kanuni na  miongozo na viwango ya serikali mtandao kupitia taasisi za umma huku  lengo likiwa ni kujenga  serikali mtandao kupitia teknolojia za kisasa kwa  ajili ya kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Jumla ya washiriki 1400 wanashiriki mkutano huo ambao unajumuisha wadau mbali mbali kutoka serikalini na sekta binafsi kwa lengo la kuboresha serikali mtandao.











Na.Alex Sonna-DODOMA

WAZIRI  wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mhe. Anthony Mavunde , amevitaka vikundi vilivyonufaika na mkopo wa shilingi bilioni mbili uliotolewa kwa wajasiriamali wa jimbo hilo, kutumia fedha hizo kama zilivyokusudiwa ili kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mikopo hiyo jijini Dodoma, Mhe.Mavunde amesema kuwa  azma ya serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata nyenzo na mitaji ya kuwawezesha kupanua na kuendeleza shughuli zao za kiuchumi.

Amesema kuwa  Mkopo huo umefadhiliwa na CRDB Bank kupitia CRDB Bank Foundation katika programu ya imbeju inayolenga kuwawezesha wajasiriamali wadogo na wa kati.

"Tumieni vizuri  mikopo hiyo kwa kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za ujasiriamali ili iweze kuleta tija, kuwaimarisha kiuchumi na hatimaye kurejeshwa kwa manufaa ya wengine."amesema Mhe.Mavunde

Mhe.Mavunde amesema kuwa  mikopo hiyo ni kama mbegu inayohitaji kutunzwa na kuendelezwa ili izae matunda yenye manufaa kwa mkopaji na jamii kwa ujumla.

“Mikopo hii ni mbegu. mkizitumia vizuri zitazaa matunda na kuwainua kiuchumi, lakini pia zitawawezesha wengine kupata fursa kama hii baada ya ninyi kurejesha kwa wakati,” amesisitiza 

Aidha ameongeza kuwa dhamira yake ni kuona wananchi wa mtumba wanaachana kabisa na mikopo umiza maarufu kama ‘mikopo ya kausha damu’ na badala yake wanatumia fursa rasmi za kifedha zenye masharti nafuu na rafiki kwa maendeleo yao.

“Wananchi wa mtumba wakae mkao wa kula. kuna mipango mingi ya kuwawezesha kiuchumi inaendelea kuja, na lengo letu ni kuhakikisha kila mmoja anapata fursa ya kujikwamua,” ameongeza

Hata hivyo amewataka wanufaika kuchangamkia fursa hizo kila zinapojitokeza na kuhakikisha wanarejesha mikopo kwa wakati ili wengine nao wapate kunufaika na mpango huo.

kwa upande wake, Mkurugenzi mtendaji wa CRDB Bank Foundation,Bi. Tully Esther Mwambapa, amesema kuwa  taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na serikali kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuyawezesha makundi tofauti ya wananchi kiuchumi.

Amesema kuwa  lengo la programu ya imbeju ni kuwajengea uwezo wajasiriamali kwa kuwapatia mitaji pamoja na elimu ya usimamizi wa biashara ili waweze kuendesha miradi yao kwa tija na ufanisi.

" Hadi sasa taasisi hiyo imetoa mikopo ya mitaji wezeshi yenye thamani ya shilingi bilioni 22.1, huku zaidi ya wajasiriamali milioni moja wakinufaika nchini kote."amesema 

Amesema kuwa  mikopo hiyo imekuwa chachu ya kuboresha ustawi wa kiuchumi wa jamii na kuchangia katika ukuaji wa pato la taifa kupitia shughuli za uzalishaji mali zinazofanywa na wanufaika.

Baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wameishukuru CRDB  kwa kuwagusa moja kwa moja katika maisha yao na kuahidi kuitumia mikopo hiyo katika shughuli za uzalishaji mali pamoja na kuirejesha kwa wakati ili iweze kuwafikia watu wengi zaidi katika maeneo mbalimbali nchini.

hafla hiyo imeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kuimarisha uchumi wa wananchi wa mtumba na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya taifa.



Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam


Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais (Uwekezaji) Dkt. Fred Msemwa ametoa wito kwa vijana hususani walioko vyuo vikuu kujenga utamaduni wa kujifunza kuhusu uwekezaji, kwa kuwa wana faida ya kuwa na uwezo wa kiutendaji na utimamu wa kimwili.

Dkt. Msemwa, ametoa wito huo leo katika hafla ya uzinduzi wa Klabu ya Uwekezaji kwa Vijana (YIC) katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Dar es Salaam, ambapo amesisitiza kuwa Dira 2050 imewapatia vijana umuhimu mkubwa kwa kuwaona wao kama rasilimaliwatu Muhimu.

“Dira inawatambua nyinyi kama rasilimali muhimu ya Taifa, inasisitiza kuwaandaa kuwa na ujuzi wa hali ya juu ili muiwezasha nchi kushindana kimataifa.” Alisema Dkt. Msemwa.

Katika mazungumzo yake na vijana hao, aliwapa changamoto ya kujiwekea msingi imara wa kiuchumi, akawafundisha nguzo nne muhimu zilizohusisha; kuwa na malengo, kujenga mtizamo sahihi, kujifunza kuweka akiba na kuwekeza, na kujifunza tabia ya kufanya zaidi.

Vile vile, Katibu Mkuu amewakumbusha kuwa Elimu ya Fedha, Ujasiriamali, Uwekezaji kwenye mifuko ya kijamii, na ujuzi wa Kuanzisha na Kusimamia Biashara, iliyokuwa ikitolewa katika hafla hiyo ilikuwa muhimu kwa kuwa inajibu changamoto zao binafsi na za jamii.

Ufunguzi wa Klabu hiyo, ni sehemu ya utekelezaji wa program ya uwajibikaji kwa jamii (CSR) wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) unaolenga kukuza elimu ya fedha, ujasiriamali na utamaduni wa uwekezaji miongoni mwa vijana na wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini.













Na Oscar Assenga, TANGA

WAZIRI Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amefanya ziara ya kutembelea utekelezaji wa mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki unaotekelzwa eneo la Chongoleani Jijini Tanga huku akiridhishwa na kasi ya utekelezaji wake unaoendelea kwa kuzingatiwa viwango vilivyowekwa.

Nchemba aliyasema hayo wakati akizungumza katika ziara yake eneo la Chongoleani Jijini Tanga linapoishia Bomba la Mafuta ambalo litasafirisha mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi eneo la Chongoleani licha ya kuwepo kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wake.

Alisema kwamba kwamba mradi huo wa kimkakati ambao utagharimu Dola za Marekani Bilioni 5.65 ni kielelezo cha Undugu Kati ya Tanzania na Uganda ambapo mradi huo umefikia asilimia 81 ya utekelezaji wake

Ambapo alisema changamoto hizo ni pamoja na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko 19 pamoja na mtikisiko wa uchumi wa dunia lakini akabainisha kuwa hatua zilizochukuliwa zimewezesha mradi huo kuendelea bila kuathiri ubora na malengo yake.
"Mradi umepiga hatua lakini wakati wa utekelezaji wa mradi huu kulikuwepo na changamoto ikiwemo dunia kupita kwenye misikusuko ya kiuchumi na mabadilio ya sera za kiuchumi lakini umeendelea kutekelezwa kwa kasi jambo ambalo linaendelea kuipa heshima nchi yetu pamoja na ndugu zetu tunaotekeleza mradi huo kwa pamoja "Alisema

Mradi huo wa EACOP una urefu wa takribani Kilomita 1,444 ukianzia Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani Tanzania na unatarajiwa kusafirisha mafuta ghafi kutoka maeneo ya uzalishaji ya Uganda hadi kwenye Kituo cha Kuhifadhi na Kusafirisha mafuta eneo la Chongoleani Jijini Tanga.

Alisema kwamba mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati katika ukanda wa Afrika Mashariki ukilenga kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi pamoja na

Aidha Waziri Mkuu huyo aliwatahadharisha watu wanaoanzisha makampuni na kuyaita ya wazawa huku yakiwa yanamilikiwa na wageni ili kunufaika na fursa ya “Loal Content” ya ushirikishwaji wa watanzania mradi kwamba watakapogundulika watafungiwa na hawatafanya kazi tena hapa nchini kwani hivyo ni kuwatapeli watanzania na kuwaibia fursa

Awali akizungumza katika ziara hiyo,Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba alisema kwamba katika mradi huo ulianza mwaka 2022 na unatarajiwa kukamilika Julai 2026 huku akieleza Serikali kwa kushirikiana na EACOP imekamilisha zoezi la kuthamini na utwaaji wa ardhi ya mradi.

Alisema kwamba hadi kufikia Januari 2026 Jumla ya Sh. Bilioni 35.06 zimetumika kulipa stahiki ya fidia kwa wananchi 9,869 kati ya wananchi 9,927 sawa na asilimia 96.4 kwa wanaopisha eneo la mradi na mkoani Tanga wananchi 1,688 wamefidiwa na kulipwa Jumla ya Bilioni 10.49.

Aidha alisema wananchi 294 wamenufaika kwa kujengewa nyumba 340 za makazi mbadala na wameshakabidhiwa nyumba zao hapa Tanga walionufaika ni wananchi 43.

Alisema kwamba wananchi wa Mkoa wa Tanga waliopatiwa udhamani wa chakula ni 1,200 huku wananchi 191 wameshiriki mafunzo ya ufugaji wa kuku,nyuki na ujasiriamali ili kuongeza kipato.

Makamba alisema katika mkoa huo miundombinu iliyojengwa ni pamoja na kituo kimoja cha Afya na kituo kimoja cha kupunguza mgandamizi wa mafuta ghafi kilichopo Handeni,Matenki Mawili ya Kuhifadhia Mafuta yaliyopo Tanga na Gati ya kupakia mafuta na kituo kikuu cha kuongeza ulinzi wa bomba la mafuta.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian alisema wana Tanga wanamshukruu Rais kwa jinsi ambavyo maono yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni kwamba mradi umekuwa mzuri na shughuli zimekwenda vizuri na wananchi wa Tanga wamepata ajira.

Alisema pia kwa waliopitiwa na mradi waliweza kupata fidia bila kuwepo kwa changamoto yoyote lakini waliweza kusaidiwa na mashamba yaliyoguswa waliweza kulimiwa huku akiwashukuru EACOP kuna maeneo walikwenda kwa sababu walikwenda na utaalamu wakarudi kumueleza kuna changamoto ya uharibifu wa panya wa mazao iliwasaidia nao kuwaeleza wizara na hivyo kuondosha changamoto hiyo.

Mkuu wa Mkoa alisema kwamba zaidi vijana wa Tanga wameweza kushirikiana na wahandisi na wanashukuru mradi upo salama na hawajapata changamoto yoyote ya watu kupata madhara na suala la mazingira kwa sababu mradi umekwenda kwenye bahari wamehakikisha maeneo yenye uoto asili waliweza kuzingatia na hata kuchepusha ili wasiharibu na wanazingatia mazingira ya bahari.





Na Hadija Bagasha - Tanga


Imeelezwa kuwa ongezeko la mifarakano na kuvunjika kwa ndoa nyingi kwenye jamii imekuwa chanzo kikuu cha mmomonyoko wa maadili kwa watoto wengi na kwamba changamoto za kifamilia zimekuwa zikiathiri kwa kiasi kikubwa makuzi ya watoto na kuwaingiza katika hatari ya kuharibika kitabia na hata kuathirika kisaikolojia.


Kauli hiyo imetolewa na Mchungaji Ibrahim Joram wakati wa mahafali ya nne ya Chuo cha Theolojia na uongozi cha Eclea Kampasi ya Tanga, ambapo alisisitiza kuwa athari za kuvunjika kwa ndoa haziishii kwenye mgawanyiko wa mali au makazi, bali huacha alama ya kudumu katika nafsi za watoto.

Kwa mujibu wa mchungaji huyo, watoto wanaokulia katika mazingira yenye migogoro ya mara kwa mara au wazazi waliotengana hukosa msingi imara wa malezi na mwongozo wa karibu kutoka kwa pande zote mbili za wazazi ambapo hali hiyo huwafanya baadhi yao kukosa upendo, uangalizi na haki ya msingi ya kusikilizwa na kueleweka, jambo linaloweza kuwafanya watafute faraja au uthibitisho nje ya familia, wakati mwingine kujiingiza katika makundi au matendo yasiyofaa.


Kwa upande wake Katibu mkuu wa huduma ya Eclea Tanzania Reverine Mdimi, alieleza kuwa watoto wengi baada ya wazazi kutengana hujikuta wakikumbwa na msongo wa mawazo, hasira, huzuni au kukosa mwelekeo sahihi wa maisha hivyo bila msaada wa karibu wa wazazi, walezi au jamii, watoto hao huweza kujiingiza katika mienendo mibaya inayoweza kuharibu mustakabali wa maisha yao.


Wakizungumza katika mahafali hayo, wachungaji waliwataka wazazi kujijenga kiimani na kiroho ili kuimarisha misingi ya ndoa na familia na kwamba imani thabiti humsaidia mzazi kuwa na uvumilivu, busara na uwezo wa kusuluhisha migogoro kwa njia ya mazungumzo badala ya kuishia katika kuvunjika kwa ndoa.


Naye mchungaji Joas Stephano wa makanisa ya pentecoste motomoto aliwahimiza wanandoa kutafuta ushauri wa kitaalamu na wa kiroho mapema wanapokumbana na changamoto, ili kulinda ustawi wa watoto wao.


Kwa upande wa taasisi za elimu ya dini, wachungaji hao walibainisha kuwa mafunzo yanayotolewa katika Chuo cha Eclea hayalengi tu masomo ya kitheolojia, bali pia yanatoa elimu ya maisha.


"Eclea inatoa masomo rasmi yanayohusika na mambo kama hayo moja msamaha na maridhiano, mbili ndoa na malezi bora ni mafunzo tunayoyatoa kwa kina zaidi pamoja na kutoa ushauri wa kijinsia kwa maana tunawashauri watu namna gani bora ya kutatua migogoro ya kifamilia hasa kwenye eneo hili la ndoa na familia, "akisisitiza Mchungaji Mdimi.


Walieleza kuwa viongozi wa dini wanaohitimu masomo ya kidini wanatarajiwa kuwa mwanga katika jamii, wakifundisha si tu neno la Mungu, bali pia misingi ya malezi bora, maadili na utatuzi wa migogoro ya kifamilia.


Mahafali hayo yalikuwa fursa ya kuwakumbusha wahitimu kuwa huduma yao kwa jamii inapaswa kuanzia katika kuimarisha familia, ambayo ndiyo msingi wa taifa lolote huku Wachungaji wakiwahimiza wahitimu kuwa mabalozi wa amani na maridhiano, wakisaidia kurejesha matumaini kwa familia zinazokumbwa na misukosuko na kulinda kizazi dhidi ya athari za kuvunjika kwa ndoa.


Kuvunjika kwa ndoa ni changamoto inayoweza kuzuilika endapo wazazi watachukua hatua za makusudi kujenga upendo, mawasiliano na imani ndani ya familia. Ni wito kwa jamii nzima kusimama pamoja kulinda maadili ya watoto, kwani mustakabali wa taifa huanzia katika uimara wa familia.