Na Oscar Assenga,TANGA
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dk. Batilda Burian, ametaka elimu ya kupinga rushwa ianze kutolewa kwa wanafunzi wa shule za msingi wakiwa na umri mdogo ili kuwajengea maadili ya uadilifu, uaminifu, uwajibikaji, uzalendo na kuipenda nchi yao.
Dk. Burian alitoa kauli hiyo Agosti 6, 2026, wakati wa fainali ya shindano la Chemsha Bongo Zuia Rushwa 2026 mkoani Tanga, lililofanyika katika Shule ya Ufundi Tanga (Tanga Technical Secondary School).
Alisema kuwafundisha wanafunzi masuala ya rushwa kuanzia wakiwa darasa la tatu kutawajengea msingi imara wa kuchukia na kukemea vitendo vya rushwa, hivyo kuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku.
Alisema wanafunzi tayari wanaonesha uelewa mkubwa kuhusu madhara ya rushwa kwa maendeleo ya taifa.
“Kama mlivyowasikia wanafunzi wakijieleza, wameonesha namna rushwa inavyodumaza maendeleo. Inaweza kusababisha kujengwa kwa madaraja mabovu kwa sababu ya kumpa kazi mkandarasi asiye na sifa. Mwisho serikali hudhani imetekeleza maendeleo, kumbe ni maendeleo ya magumashi,” alisema.

Dk. Burian, ambaye aliwakilishwa na Ofisa Elimu wa Mkoa wa Tanga, Emanuel Kisongo, alisema walimu wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa kwa wanafunzi kwa kuwalea katika misingi ya maadili mema na kuwafundisha athari za rushwa kwa jamii na taifa.
Kwa upande wake, Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Tanga, Ramadhan Ndwata, alisema shindano la Chemsha Bongo Zuia Rushwa 2026 linalenga kujenga kizazi chenye uadilifu kupitia wanafunzi wa shule za msingi.
Alisema maadili yanayojengwa kwa watoto yatawasaidia kukua wakiwa raia wanaochukia rushwa na kuzingatia misingi ya haki na uwajibikaji.
“Tunataka kujenga kizazi kitakachokuwa sehemu ya suluhisho la tatizo la rushwa badala ya kuwa sehemu ya tatizo. Vitendo vina nguvu kubwa katika kujenga maadili kuliko maneno pekee,” alisema.
Ndwata alisema kuanzishwa kwa klabu za wapinga rushwa katika shule za msingi kumeongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu masuala ya rushwa.
Alisema wakati wa mashindano hayo wanafunzi walikuwa wakisahihishana wenyewe kuhusu masuala yanayohusu rushwa, jambo alilosema ni ishara ya mafanikio ya programu hiyo na kwamba wako tayari kuwaelimisha wengine.
Aidha, aliwataka wazazi kushiriki kikamilifu katika malezi ya watoto kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kuendeleza elimu dhidi ya rushwa, akisema familia ina nafasi kubwa katika kujenga maadili ya kizazi kijacho.
Mratibu wa mashindano hayo Frank Mapunda alisema Shule ya Msingi Kombezi iliibuka mshindi wa kwanza na kujinyakulia kombe kubwa pamoja na fedha taslimu Sh200,000.
Alisema mshindi wa pili alikuwa Klabu ya Wapinga Rushwa ya Shule ya Msingi Bombo iliyopata kombe dogo na Sh150,000, huku Shule ya Msingi Chumbageni ikishika nafasi ya tatu na kujishindia ngao ya glasi pamoja na Sh100,000.
Nafasi ya nne ilichukuliwa na Klabu ya Wapinga Rushwa ya Shule ya Msingi Nguvumali iliyopata ngao ya plastiki pamoja na Sh50,000.
Mwalimu wa Shule ya Msingi Mkwakwani Faraja Mwagike alisema kuanzishwa kwa klabu za wapinga rushwa kumewaongezea wanafunzi uadilifu, ujasiri na kuwajengea msingi wa kuwa raia wema watakaoheshimu sheria na kutenda haki.
Naye mwanafunzi wa Shule ya Msingi Kisosora, Mariam Juma, alisema klabu hizo zimechangia kuwaelimisha wanafunzi kuhusu madhara ya rushwa kwa jamii na taifa.
“Ni muhimu wigo wa klabu hizi ukaongezwa ili wanafunzi wengi zaidi wanufaike na elimu hii na ujumbe uwafikie wote,” alisema.
Na. OWM–TAMISEMI, Kilosa
Wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa watanufaika na Shilingi Bilioni 1.2 zilizotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya ujenzi wa daraja la kisasa la chuma lenye urefu wa mita 30 katika Mto Nyameni, Kata ya Ulaya, mradi unaotekelezwa na TARURA wenye lengo la kuboresha usafiri na usafirishaji kati ya kata za Zombo, Nyameni na Ulaya.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, Agosti 6, 2026 alipokagua maendeleo ya ujenzi wa daraja hilo katika ziara yake ya kikazi ya kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo wilayani Kilosa.
"Mhe. Rais anawapenda wananchi wa Zombo, Nyameni na Ulaya. Ameonesha hilo kwa kutoa Bilioni 1.2 kujenga daraja hili litakalomaliza changamoto ya usafiri na usafirishaji iliyosababishwa na kuvunjika kwa daraja la zamani," amesema Prof. Shemdoe.
Amesema ujenzi wa daraja katika barabara ya Zombo–Nyameni–Ulaya umefikia asilimia 85 na unatarajiwa kukamilika Agosti 30, 2026, mara baada ya kuwasili kwa vyuma vya kukamilisha ujenzi, ambavyo vinatarajiwa kuingia nchini kwa njia ya meli.
Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emmanuel Ndyamkama, amesema ufungaji wa vyuma hivyo utafanywa na wahandisi wa TARURA mkoa wa Morogoro wenye uzoefu wa kazi kama hiyo iliyotekelezwa Mlimba, wilaya ya Kilombero.
Ameongeza kuwa daraja hilo litakuwa na njia mbili za watembea kwa miguu pamoja na uwezo wa kupitisha magari yenye uzito wa zaidi ya tani 40. Pia, daraja la kamba lililopo litahamishiwa eneo jingine lenye uhitaji ili kuongeza huduma ya kuvuka mto Nyameni.
Naye, mkazi wa kata ya Ulaya, Bi. Fatuma Mwalimu Chaubwa, amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha ujenzi wa daraja hilo na kumpongeza Mbunge wa Jimbo, Mhe. Denis Londo, kwa ufuatiliaji wake wa karibu wa utekelezaji wa mradi huo.
Daraja hilo linatarajiwa kurahisisha usafirishaji wa mazao na bidhaa kwenda sokoni, kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na elimu, kuongeza fursa za biashara na uwekezaji, pamoja na kuimarisha usalama wa wananchi wanaovuka mto Nyameni.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) wa CCM, Idara ya Organizesheni, Paul Chacha amesema uongozi wake utasimamia uchaguzi wa haki na usawa ndani ya chama, akisisitiza kuwa hakuna mwanachama atakayepokonywa haki yake kutokana na ushawishi wa fedha au mamlaka ya watu binafsi.
Akizungumza katika makao makuu ya CCM jijini Dodoma wakati wa mapokezi ya viongozi wapya walioteuliwa kushika nyadhifa mbalimbali ndani ya chama, Chacha amesema CCM ndiyo chama kilichojipanga zaidi nchini na kinaendelea kuwahakikishia Watanzania amani, maendeleo na matumaini ya maisha bora.
Amesema uchaguzi ndani ya chama unapaswa kuwa wa haki na uwazi ili kumpata kiongozi anayestahili kwa ridhaa ya wanachama, huku akiahidi kusimama imara kulinda misingi ya demokrasia bila kuyumbishwa na shinikizo lolote.
Chacha ametoa onyo kwa watu wanaokusudia kutumia fedha kujinufaisha kisiasa, akisema ni heri fedha hizo zikaelekezwa kwenye uwekezaji au biashara kuliko kutumika kuwarubuni wapiga kura.
Aidha, amesisitiza kuwa CCM haitamvumilia mtu yeyote atakayejaribu kununua kura au kushawishi wanachama kwa fedha ili kupata nafasi za uongozi, akibainisha kuwa hatua kali zitachukuliwa kwa wote watakaokiuka maadili ya chama.
Vilevile, amesema chama hakitasita kuwachukulia hatua watu wanaotumia nafasi au mamlaka ya ndugu zao kuingilia mchakato wa uchaguzi na kutoa maelekezo yanayokandamiza haki za wanachama.
Kwa mujibu wa Chacha, uchaguzi wa haki ndio msingi wa kupata viongozi wenye uwezo wa kukijenga chama na kuendelea kuwatumikia Watanzania kwa uadilifu na uwajibikaji.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Bi. Martha Chassama, ameendelea kutoa elimu kwa vitendo kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa kuandaa na kupika vyakula kwa kutumia majiko ya kisasa yanayotumia nishati safi, ikiwa ni sehemu ya shughuli za uelimishaji wa wananchi wanaotembelea banda la REA katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.
Akizungumza baada ya onesho hilo, Bi. Chassama amesema REA inaendelea kutekeleza kwa kasi miradi ya nishati safi ya kupikia nchini kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa nishati salama, nafuu na rafiki kwa mazingira, sambamba na kuboresha afya za wananchi na kuhifadhi mazingira.
“Nishati safi ya kupikia siyo tu suluhisho la kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, bali ni uwekezaji katika afya za wananchi, uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya uchumi wa familia. REA inaendelea kuhakikisha wananchi wanapata elimu na fursa ya kutumia teknolojia hizi za kisasa ili kuboresha maisha yao,” amesema Bi. Chassama.
Amefafanua kuwa maonesho hayo yanatoa fursa kwa wananchi kujionea kwa vitendo namna majiko ya kisasa yanavyofanya kazi, kufahamu manufaa yake pamoja na kupata elimu kuhusu teknolojia mbalimbali za nishati safi ya kupikia zinazotekelezwa na REA kwa kushirikiana na Serikali na wadau wa maendeleo.
Aidha, amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia yanachangia kupunguza athari za kiafya zitokanazo na moshi wa kuni na mkaa, kulinda mazingira kwa kupunguza ukataji wa miti, pamoja na kuokoa muda na gharama zinazotumika katika kutafuta nishati za kupikia.
Bi. Chassama amewahimiza wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nanenane kutembelea banda la REA ili kupata elimu kuhusu utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini, nishati safi ya kupikia na teknolojia za nishati jadidifu, zinazolenga kuboresha maisha ya Watanzania na kuchochea maendeleo endelevu.
Maonesho ya Nanenane ya mwaka 2026 yanaendelea katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma, yakitoa jukwaa kwa taasisi za umma na sekta binafsi kuonesha huduma, ubunifu na teknolojia zinazochangia maendeleo ya sekta ya kilimo na uchumi wa Taifa.



































.jpeg)



.jpeg)