Na Oscar Assenga,TANGA

BILIONI 10 zimelipwa kama sehemu ya fidia kwa wananchi ambao wameweza kupisha maeneo yao kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya Bomba la Mafuta Ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongeleani Tanga,Tanzania.


Hayo yalibainishwa na Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba wakati wa ziara ambayo aliambatana na Waziri wa Nishati na Maendeleo ya Madini wa Uganda, Dkt. Ruth Nankabirwa ya kujionea hatua ambayo imefikiwa ya ujenzi wa mradi huo katika eneo la Chongoleani Jijini Tanga.

Ambapo pia katika mradi huo zaidi ya wananchi 9800 waliopo katika mkoa wa Tanga wameweza kushiriki kwenye shughuli za ujenzi wa bomba la mafuta ghafi.

Naibu Waziri huyo alisema mradi huo kwa upande wa Tanzania umeweza kufikia asilimia 86 ya utekelezaji wake ukihusisha maeneo ya ulazaji wa mabomba,ujenzi wa matankiya kuhifadhia mafuta ghafi sambamba na eneo la gati ya kushushia mafuta hayo.


Aidha alisema kuwa mpaka sasa mradi huo upo katika hatua nzuri ya utekelezaji wake na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Julai mwaka huu.

Makamba alisema kuwa mradi huo utaongeza usambazaji wa mafuta nchini na kupunguza gharama za usafirishaji, na kuufanya uwe na tija kwa wananchi wa mkoa wa Tanga na Tanzania kwa ujumla.



Mradi huu umewanufaisha kwa kiasi kikubwa wananchi wa Tanzania tofauti na wenzetu wa uganda kutokana na eneo kubwa kuwa upande wa nchi yetu"alisema Naibu Waziri Makamba.


Hata hivyo Makamba alisema kwamba dhamira ya dhati ya Rais Dkt Samia Suluhu na Rais wa Uganda Yoweri Kaguta Museveni imewezesha utekelezaji mzuri wa mradi huo unaotarajiwa kuleta mabadiliko makubwa katika Nyanja za kiuchumi ,kijami,ajira na uboreshaji wa huduma za jamii


Kwa upande wake Waziri wa Uganda Nankabirwa alisema kuwa mradi huo umeweza tekelezwa katika viwango bora vya usalama huku ukizingatia ulinzi wa athari za kimazingira


"Tayari wananchi wetu wameweza wameweza kunufaika na sehemu ya kurudisha kwa jamii kwa kuwekewa miundombinu ya maji safi,ujenzi w barabara sambamba na shughuli za michezo kwa wananchi wanaoishi karibu na maeneo ya mradi huo"alisema Waziri huyo.

Aidha aliwataka wananchi wa nchi hizo mbili kuutunza na kuulinda mradi huo kwani utakapoanza kazi utaweza kuketa manufaa makubwa ya kiuchumi baina ya nchi hizi mbili.


Ziara hiyo ililenga kuona hatua za utekelezaji wa mradi huo na kuhakikisha kuwa unatekelezwa kwa viwango vya juu vya ubora na usalama.



 


Watoto waliokinzana na sheria na kupelekwa katika Shule ya Maadilisho ya Irambo iliyopo Wilaya ya Mbeya Vijijini mkoani Mbeya wamehimizwa kujutia makosa yao, kubadili mienendo na kuishi kwa utii na maadili mema mara baada ya kumaliza adhabu na kurejea katika jamii walizotoka.

Ushauri huo umetolewa na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum , Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi wakati wa ziara yake ya kutembelea na kukagua shule hiyo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali katika kuhakikisha watoto waliokinzana na sheria wanarekebishwa kimaadili na kisaikolojia.

“Hii ni fursa ya pili mliyopewa na Serikali itumieni kujitathmini, kujutia makosa na kuamua kubadilika ili mtakaporejea katika jamii muwe mfano wa kuigwa maana mnajua kabisa kutowasikiliza wazazi na jamii kumewasababisha wengi wenu kujiingiza katika vitendo vinavyopingana na sheria na hatimaye kujikuta mmefikishwa katika shule hii na naamini ndani ya miaka hiyo uliyopangiwa na Serikali naamini itawasaidia kubadilika” amesema Mhe. Mahundi.

Aidha, aliwasisitiza watoto hao kuwa utii, nidhamu na maadili mema ni nguzo muhimu zitakazowawezesha kujenga maisha bora na kuepuka kurudia makosa ya awali, huku akiahidi kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya malezi katika shule za maadilisho nchini.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini, Mhe. Patali Shida Patali, ameishukuru Serikali kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika eneo hilo, pia kukifanya kituo hicho kuwa katika jimbo lao ambapo kinasaidia watoto wa vijiji vyao na Tanzania nzima.

“Mheshimiwa Naibu Waziri kuwepo kwa kituo hiki sisi Mbeya Vijijini tunanufaika kwani tuna mahusianao mazuri na kituo hiki kwa kuwa kinatunufaisha katika masuala mbalimbali ikiwemo maji tunapata kwao, elimu za mashamba darasa tunazipata hapa pamoja na huduma za afya wanakijiji hutumia zahanati ya shule hii” amesema Mhe. Patali.

Awali akisoma taarifa ya shule hiyo, Meneja wa Shule ya Maadilisho Irambo John Meshack amesema kuwa, shule hiyo kwa sasa inahudumia watoto 28 wa kiume waliotoka maeneo mbalimbali ya Tanzania Bara na watoto hao wanapatiwa huduma muhimu ikiwemo elimu ya msingi, afya, stadi za maisha, malezi na michezo kwa lengo la kuwabadilisha tabia na kuwaandaa kurejea katika jamii wakiwa raia wema. 

Ziara ya Naibu Waziri Mahundi inalenga kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, viongozi wa kisiasa na taasisi za malezi katika kuhakikisha watoto waliokinzana na sheria wanapata marekebisho stahiki na kurejeshwa salama katika jamii.















 


Imeelezwa kuwa Serikali imefanya uwekezaji mkubwa kupitia mradi wa EASTRIP ili kukifanya Chuo cha Ufundi Arusha (ATC), kupitia Kituo cha Umahiri Kikuletwa, kuwa kitovu cha mafunzo ya nishati jadidifu kwa ukanda wa Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla. 

Akizungumza Januari 6, 2026 wakati wa ziara yake katika kituo hicho, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir alisema kuwa utekelezaji wa mradi wa EASTRIP utakifanya ATC kuwa kitovu cha mafunzo ya vitendo katika uzalishaji wa nishati safi ikiwemo nguvu ya maji, jua, upepo na bioanuwai. 

Alielekeza kuwa ujenzi wa mtambo wa kufua umeme utasaidia kutoa wahitimu wenye ujuzi unaohitajika, na kusisitiza umuhimu wa kuwahusisha wakufunzi na wanafunzi moja kwa moja katika ujenzi huo ili kuongeza uwezo wa kitaaluma na kuboresha mafunzo.

Aidha, Naibu Waziri alielekeza chuo kuendelea na kuimarisha mahusiano na viwanda pamoja na taasisi za elimu, sayansi na teknolojia ndani na nje ya nchi. Hatua hiyo inalenga kutoa fursa kwa watumishi na wanafunzi kushiriki katika tafiti za pamoja zinazoweza kujibu changamoto za kijamii na kiuchumi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Ufundi Arusha (ATC), Prof. Musa Chacha, alisema kuwa utekelezaji wa mradi wa EASTRIP umewezesha ujenzi wa kituo cha kufua umeme, umeongeza udahili wa wanafunzi hasa wa kike, na kuanzishwa kwa mitaala mipya 27. Pia umewezesha ujenzi wa miundombinu mipya katika Kampasi ya Kikuletwa pamoja na mitambo ya kisasa ya kufundishia na kujifunzia.

Prof. Chacha aliongeza kuwa ili kuhakikisha utekelezaji wa elimu amali unafanikiwa, chuo kimeweka mkakati wa kuhamasisha wanafunzi kupenda na kuchagua elimu amali hususan katika mafunzo ya nishati jadidifu.








Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, Mhe. Timontheo Mnzava, amewataka madiwani na wenyeviti wa vijiji kushirikiana kwa karibu katika kutatua migogoro ya ardhi ili kulifanya jimbo hilo kuwa mfano wa matumizi sahihi ya ardhi na kuimarisha amani kwa wananchi.

Mbunge Mnzava ametoa wito huo wakati akiendelea na ziara zake za kukutana na makundi mbalimbali ya jamii, kwa kushirikiana na viongozi wa Chama pamoja na Halmashauri. Katika kikao maalum alichokaa na madiwani pamoja na wenyeviti wa vijiji, walijadili masuala mbalimbali yenye lengo la kuimarisha utawala bora na maendeleo ya wananchi.

Katika kikao hicho, Mhe. Mnzava aliwapongeza madiwani kwa ushindi wao katika uchaguzi na kuwashukuru wenyeviti wa vijiji kwa kushiriki kikamilifu katika kulinda amani wakati wote wa zoezi la uchaguzi, Alisisitiza kuwa mchango wao ulikuwa mkubwa katika kuhakikisha maeneo yao yanabaki salama na yenye mshikamano.

Aidha, aliwakumbusha viongozi hao majukumu yao ya msingi, hususan kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi kwa vitendo, kwa kuzingatia maslahi ya wananchi waliowachagua.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mnzava alikemea vikali vitendo vya rushwa na matumizi mabaya ya mihuri katika maeneo yao, akisisitiza kuwa vitendo hivyo vinadhoofisha uaminifu wa wananchi kwa viongozi wao na kukwamisha haki. Akihitimisha kikao hicho, aliwataka madiwani na wenyeviti wa vijiji kuwa mstari wa mbele katika kulinda na kuitunza amani iliyopo, akisisitiza kuwa amani ni msingi muhimu wa maendeleo endelevu ya jimbo na taifa kwa ujumla.

 


Na Benny Mwaipaja, Zanzibar


Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, itaendelea kuboresha huduma za jamii ikiwemo sekta ya afya kwa wananchi wake.

Mhe. Balozi Omar ametoa kauli hiyo wakati akizindua Kituo cha Afya cha Kisasa cha Kinduni, kilicho gharimu shilingi bilioni 3.77, kilichokojengwa katika Wilaya ya Kaskazini B mkoa wa Kaskazini Unguja, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 62 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Alisema kuwa uwepo wa Kituo hicho cha Afya inathibitisha mafanikio makubwa katika sekta ya afya chini ya Uongozi wa Raisi wa Zanzibar wa Awamu ya nane, Mhe. Dkt Hussein Ali Mwinyi kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya katika ngazi zote za kijamii. 

“Serikali imeshajenga na kuweka vifaa katika  hospital 10 za wilaya katika wilaya za Unguja na Pemba, baada ya kuimarisha huduma katika ngazi ya wilaya zote, kuanzia mwaka 2023/2024 ambapo imeweka kipaombele katika kuimarisha miundombinu ya Afya ya msingi ili kutoa huduma bora zaidi ya Afya kwa jamii” alisema Mhe. Balozi Omar.

Alisema kuwa amefarijika kuona miundombinu ya afya inazidi kuimarika zaidi katika awamu ya nane ya Mhe. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi na kuwataka wananchi wakitunze  Kituo hicho ili kiwe chenye ubora na cha kuvutia siku zote ili kiendelee kutoa huduma bora za afya kwa muda mrefu na kuwahudumia Wananchi wengi zaidi.

Alisema kuwa Kituo hicho kitahudumia zaidi ya watu 19,546 wakiwemo watoto wenye umri wa chini ya mwaka mmoja 782, watoto wenye umri chini ya miaka mitano 2,834 na wanawake wenye umri wa kuzaa 5,336 kutoka shehia nne za Kinduni, Mkataleni, Mahonda na Mnyimbi pamoja na maeneo Jirani.

Akitoa taarifa ya ujenzi wa Kituo hicho cha afya Kinduni, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Mgereza Mzee Miraji, alisema kuwa Mradi huo unajengwa kwa fedha za Serikali kwa gharama ya shilingi za Tanzania bilioni 3.77 chini ya Mkandarasi Mazrui Building Contractors Ltd na unasimamiwa na Mshauri elekezi, Wakala wa Majengo Zanzibar (ZBA).

Alisema Ujenzi wa kituo hicho unahusisha jengo moja la gorofa moja (G+2) na baada ya kukamilika kwake kitakuwa kinafanya kazi saa 24, kitakuwa na uwezo wa kulaza wagonjwa 30 kwa wakati mmoja na kitakuwa kikitoa huduma mbalimbali kwa wananchi ikiwemo huduma za Kliniki na wagonjwa wa nje (OPD), huduma za Kliniki za mama na mtoto, maradhi ya pua, koo, masikio na macho, klinik ya magonjwa ya shinikizo la damu, kisukari, Ngozi, kinywa na meno.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Bw. Cassian Galoss Nyimbo, alisema kuwa Kitu cha Afya Kundini, ni cha kisasa kilichojengwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa fedha zake za ndani, ambacho kitatoa huduma za afya karibu na wananchi na kwamba hawatakwenda umbali wa zaidi ya kilometa 5 kupata huduma hizo.

Nao wananchi wa Kundini na Mahonda, waliishukuru Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kuwasogezea huduma za afya karibu nao kwa kuwajengea Kituo hicho kitakachotoa huduma za afya kwa mfumo wa kidigitali kwani tayari vifaa vya uchunguzi, matibabu na TEHAMA, vimeshafungwa.










Magesa Magesa ,Arusha .



Arusha .Mkuu wa mkoa wa Arusha ,CPA Amos Makalla amewataka wananchi kuhakikisha kuwa wanajiunga na bima ya afya kwa wote ili waweze kupata vipimo,matibabu,na dawa katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Ameyasema hayo jijini Arusha leo wakati akizindua sehemu maalumu ya kupokelea wagonjwa wa dharura pamoja na magonjwa yasiyoambukiza katika hospitali ya ALMC (Selian ) iliyopo jijini hapa .

Sehemu hiyo maalumu ya kupokelea wagonjwa hao imekarabatiwa na kuweka vifaa tiba na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI)  ambapo ukarabati pamoja na vifaa tiba umegharimu kiasi cha shs 200 milioni .


CPA Makalla aliwapongeza wananchi wa mkoa wa Arusha na mikoa jirani kujitokeza kwa wingi kupata huduma ya upimaji wa magonjwa ya moyo yanayotolewa na Tasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete ambayo imeweka kambi ya matibabu hospitalini hapo .


"kila binadamu ni mgonjwa mtarajiwa hivyo nawapongeza wananchi kwa kuwahi kukua afya zenu, kwani kwa kufanya hivyo mtaweza kupata matibabu ya haraka na kuepukana na magonjwa hayo yasiyoambukiza."amesema CPA Makalla. 


Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dokta Peter Kisenge amesema kuwa , Taasisi hiyo imekwisha  kufungua vituo sita katika maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo kituo hiki.cha hapa  Arusha ambacho kitahudumia mikoa ya kaskazini na mikoa jirani .

Dkt Kisenge amesema kuwa , kambi hiyo ya  uchunguzi wa magonjwa ya moyo ilianza desemba 29 na inatarajiwa kifikia tamati  januari 9, na kusema kuwa hadi sasa zaidi ya wagonjwa 1,200 wameshahudumiwa na walioonekana na tatizo kubwa walipewa rufaa ya kwenda makuu ya Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. 


Amesema kuwa, mwitikio wa wananchi ni mkubwa hali inayoonyesha kuwa wananch9 wengi wanakabiliwa na tatizo la moyo na kuwataka wananchi kuendelea kujitokeza kwa siku hizo chache zilizobakia .


"Bado tatizo la magonjwa yasiyoambukiza yamekuwa ni tishio kubwa kwa uhai wa mwanadamu hivyo umefika wakati sasa kwa wananchi kuchunguza afya zao mapema ili kuweza kutambua afya zao badala ya kusubiri  hadi dalili za ugonjwa husika kujitokeza kitendo ambacho kinakuwa ni changamoto kwenye suala la matibabu ."amesema Dkt Kisenge .

 Aidha ameshukuru hospitali hiyo ya ALMC (Selian) inayomilikiwa na kanisa la Kiinjili la.kilutheri Tanzania (KKKT)  pamoja na uongozi  wa kanisa hilo kwa kuwakubalia kuweka kituo cha kutoa huduma ya matibabu ya moyo katika hospitali hiyo kwani lengo la JKCI  ni kutaka kuona wananchi hawapotezi maisha  yao kwa tatizo la moyo.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Ngarenaro, Abdulaziz  Chande (Dogo Janja) amemshukuru Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha JKCI ili kuweza kuja kutoa huduma hiyo kwa siku zote hizo kwa  wananchi wa Arusha  na mikoa ya jirani.

"Mimi.nina mfano ulio hai baba yangu mzazi anasumbuliwa na tatizo la moyo na ilikuwa nikitakiwa kumpeleka  jijini Dar es Salaam mara mbili kwa mwezi ,lakini kufunguliwa kwa kituo hiki mkoani Arusha kimeleta faraja sio kwangu tu ila kwa wananchi wote wanaosumbuliwa na matatizo ya moyo kwani imewapunguzia gharama za kwenda kufuata huduma hiyo jijini Dar es Salaam. "amesema Dogojanja.

Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango (NPC), Dkt. Fred Msemwa (Kushoto) akiwa katika mazungumzo na Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango ya Zanzibar, Dkt. Afua Khalfan Mohamed (Katikati) alipotembelea ofisi hizo Zanzibar leo ( 6.1.2025). Kulia ni Mkurugenzi wa Utawala na Rasimali Watu, Bi.Maryam Ukki.

 


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Ally Gugu, amewahimiza wafanyakazi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, taratibu na miongozo iliyowekwa katika usajili na utambuzi wa wananchi.

Gugu alitoa wito huo tarehe 3 Januari, 2025, alipokuwa akifungua rasmi mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa NIDA uliofanyika katika Ukumbi wa Shule ya Uongozi ya Julius Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.

“Nawapongeza kwa utendaji mzuri wa kazi, lakini nawasisitiza muendelee kuzingatia sheria, taratibu na kanuni za usajili, kwani NIDA ni taasisi muhimu sana katika maendeleo ya taifa,” alisema Gugu.

Alisisitiza kuwa NIDA inatekeleza majukumu nyeti yenye maslahi makubwa kwa taifa, hivyo wafanyakazi wanapaswa kuonesha uzalendo na uadilifu katika kulinda na kusimamia vyema taarifa binafsi za wananchi walizokabidhiwa.

Aidha, aliwahimiza wananchi ambao bado hawajachukua vitambulisho vyao vya taifa kufika katika ofisi za NIDA za wilaya ili kuvichukua, akibainisha kuwa vitambulisho hivyo ni nyaraka muhimu za utambulisho na kwamba serikali imetumia gharama kubwa kuvizalisha.

Vilevile, Gugu aliipongeza NIDA kwa kuanzisha huduma ya Msimbo Mfupi (Short Code) inayowawezesha wananchi kupata mrejesho wa huduma za vitambulisho kupitia simu za mkononi bila malipo.

Alisema huduma hiyo itanufaisha zaidi wakazi wa maeneo ya vijijini kwa kuwawezesha kupata taarifa kuhusu hali ya usajili wao na taarifa binafsi wakiwa maeneo yao, bila ya kusafiri umbali mrefu hadi ofisi za wilaya.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, James Kaji, alieleza kuwa zaidi ya vitambulisho vya taifa 300,000 bado havijachukuliwa katika ofisi za NIDA za wilaya mbalimbali.

“Natumia fursa hii kuwasihi wananchi kwenda kuchukua vitambulisho vyao, kwani serikali imetumia fedha nyingi katika uzalishaji wake,” alisema Kaji.

Aidha, aliwashauri wananchi wenye makosa katika taarifa zao binafsi kutumia kibali maalum cha mwaka mmoja kurekebisha taarifa hizo, akisisitiza kuwa baada ya kibali hicho kuisha, hakutakuwa na muda wa nyongeza.

Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase,akizungumza wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua uendeshaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) wilayani humo kwa niaba ya Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Patrobas Katambi.

....

Serikali imewataka wakulima nchini kuhakikisha wanapeleka kakao yenye ubora sokoni ili kulinda bei nzuri inayoendelea kupatikana kwa sasa.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase, akizungumza kwa niaba ya Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Patrobas Katambi (Mb), wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua uendeshaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) wilayani humo, .

 DC Manase amesisitiza kuwa kuingiza kakao isiyo na viwango katika masoko kutasababisha bei kuporomoka, jambo ambalo litawaathiri wakulima kiuchumi. Amesema kuwa uaminifu wa mkulima katika kuzingatia vigezo vilivyowekwa ndiyo njia pekee ya kuhakikisha zao hilo linaendelea kuwa na ushindani na kupata masoko yenye tija ndani na nje ya nchi.

Aidha, DC Manase amewahimiza wakulima wa Kyela kuendelea kupanda miti kama mbinu madhubuti ya kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kulinda mazingira ya kijani. Amebainisha kuwa utunzaji wa mazingira ni kigezo muhimu kinachowezesha mazao ya wakulima kukubalika katika ngazi ya kimataifa, huku akisisitiza kuwa juhudi hizo pia zinasaidia wakulima kupata uaminifu wa kibenki na huduma nyingine za kifedha.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, ameeleza umuhimu wa utaratibu wa kukagua mizigo ghalani kabla ya kuifikisha mnadani. Akifafanua kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuhakikisha kile kinachouzwa kinafahamika kwa usahihi, jambo linalosaidia kuondoa migogoro kati ya wanunuzi na wauzaji.

Vilevile, amesema utaratibu huo wa ukaguzi umeleta matokeo chanya kwani hivi sasa hakuna malalamiko yanayotolewa na pande zote mbili katika mnyororo wa biashara.

Naye Naibu Msajili wa Udhibiti wa Vyama vya Ushirika, Bw. Collins Nyakunga, ameeleza kuwa vipaumbele vya sasa vya ushirika ni kuwekeza katika ujenzi wa viwanda ili kuongeza thamani ya mazao, hatua inayolenga kubadilisha taswira ya vyama vya ushirika ili viweze kutoa mchango mkubwa zaidi kwa wakulima kwa kuhakikisha wanapata faida kubwa kutokana na kazi yao.

Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase,akizungumza wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua uendeshaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) wilayani humo kwa niaba ya Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Patrobas Katambi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu,akielezea umuhimu wa utaratibu wa kukagua mizigo ghalani kabla ya kuifikisha mnadani wakati wa ziara ya Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase, kukagua uendeshaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) wilayani humo kwa niaba ya Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Patrobas Katambi.

Naibu Msajili wa Udhibiti wa Vyama vya Ushirika, Bw. Collins Nyakunga,akielezea  vipaumbele vya sasa vya ushirika ni kuwekeza katika ujenzi wa viwanda ili kuongeza thamani ya mazao, wakati wa ziara ya Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase, kukagua uendeshaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) wilayani humo kwa niaba ya Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Patrobas Katambi.

Sehemu ya washiriki wakisikiliza hotuba ya Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua uendeshaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) wilayani humo kwa niaba ya Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Patrobas Katambi.