Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kupitia Kanda ya Kaskazini, leo tarehe 5 Machi 2026 imetoa elimu kwa viongozi wa Wilaya ya Korogwe katika semina iliyofanyika katika ukumbi wa GMCC.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, George Mhina, alisema lengo ni kuwajengea viongozi uelewa kuhusu majukumu ya EWURA na maeneo inayoyadhibiti ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika semina hiyo, washiriki walipatiwa elimu kuhusu umuhimu wa uvunaji wa maji ya mvua, matumizi ya nishati safi ya kupikia, leseni za mafundi umeme, ujenzi wa vituo vya mafuta vijijini pamoja na namna ya kutatua migogoro katika sekta za maji na nishati.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Mhe. William Mwakilema amewasisitiza viongozi hao kuwa mabalozi wa elimu waliyoipata kwa kuhakikisha wanaifikisha kwa wananchi ili kuongeza uelewa na matumizi sahihi ya huduma za maji na nishati.

 

Dar es salaam –
Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir, ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi kutumia fursa ya huduma za ardhi zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki, akisisitiza umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi kama njia ya kujikomboa kiuchumi.
Mufti Zubeir alitoa kauli hiyo baada ya kufika katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika katika Ofisi za Ardhi za Mkoa wa Dar es Salaam, ambapo alipata hati ya ardhi huku akishuhudia namna wananchi wanavyohudumiwa katika kliniki hiyo ambayo inaendelea nchi nzima.
Akizungumza mara baada ya kupata huduma hiyo, Mufti Zubeir alisema hatua ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuandaa Samia Ardhi Kliniki yenye kulenga kuwapa kipaumbele wanawake ni jambo muhimu linalosaidia kuongeza usawa katika umiliki wa rasilimali muhimu kama ardhi.
Alisema wanawake wanapaswa kutumia kikamilifu fursa hiyo ili waweze kupata hati za ardhi na kujiimarisha kiuchumi.
“Wanawake wana haki ya kumiliki mali mbalimbali ikiwemo magari na mali nyingine, hivyo hakuna sababu ya kuwanyima nafasi ya kumiliki ardhi. Ni muhimu jamii, hususan wanaume, kuachana na mila kandamizi zinazowazuia wanawake kumiliki rasilimali,” alisema Mufti Zubeir.
Aidha, aliwataka wanaume kuwapa nafasi wanawake kumiliki ardhi ili kuongeza idadi ya wanawake wenye umiliki rasmi wa ardhi nchini, jambo ambalo litasaidia kuimarisha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.
Katika hatua nyingine, Mufti Zubeir alipongeza maandalizi mazuri yaliyofanywa na Ofisi ya Mkoa wa Dar es Salaam katika uendeshaji wa kliniki hiyo, kuanzia mapokezi hadi utoaji wa huduma kwa wananchi.
Alisema namna wateja wanavyohudumiwa kwa ufanisi ni jambo jema lenye manufaa kwa jamii na lina thawabu kubwa mbele za Mwenyezi Mungu, hususan katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Mufti Zubeir pia aliwaombea heri watumishi wanaotoa huduma katika kliniki hiyo ili waendelee kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na bidii.
Samia Ardhi Kliniki zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi, hususan kwa wanawake, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa Machi 8 kila mwaka.
 
 
 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule ameipongeza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuendesha zoezi la Samia Ardhi Kliniki linalofanyika nchi nzima.

Mhe. Senyamule ametoa pongezi hizo leo Machi 5, 2026 alipotembelea kliniki hiyo inayoendelea katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Dodoma.

“Nimekaa sijawahi kuona ubunifu wa jambo hili, na nimeambiwa linafanyika nchi nzima ya Tanzania. Hiki ni kitu cha pekee sana,” amesema Senyamule.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa mkoa wa Dodoma, awali aliposikia kuhusu kliniki hiyo alijiuliza kama kutapatikana wanawake wa kutosha kwenda kutatuliwa kero zao za ardhi, lakini hali imekuwa tofauti.

“Nilijiuliza kama wanawake watapatikana kwa wingi, lakini leo nimeshangaa kuona na kushuhudia kuwa sasa wanawake wengi wanamiliki ardhi,” amesema Senyamule.

Aidha, amesema kuwa kama jambo hilo lingefanyika miaka kumi au ishirini iliyopita, isingekuwa rahisi kupata wanawake wengi kwa sababu wengi hawakuwa na uelewa wa haki yao ya kumiliki ardhi.

“Kama ungelifanya jambo hili miaka kumi au ishirini iliyopita na kusema wanawake waje washughulikie kero zao za ardhi na kupata hati, usingewapata wengi kwa sababu wakati huo hatukuwa na uelewa kuwa sisi pia tunastahili kumiliki ardhi,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mhe. Senyamule amewaasa wanawake kutunza vizuri hati zao za ardhi, akieleza kuwa ardhi ya Dodoma ina thamani kubwa inayoongezeka kila siku.

“Ukishapata hati yako, itunze vizuri kwa sababu ardhi ya Dodoma ina thamani kubwa na thamani yake inaendelea kuongezeka kila siku,” amesema.

Sambamba na hilo, Mhe. Senyamule pia amekabidhi hati miliki kwa baadhi ya wanawake waliofika katika kliniki hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dodoma.

Samia Ardhi Kliniki ilianza rasmi tarehe 2 Machi 2026 katika mikoa yote nchini na inatarajiwa kuhitimishwa tarehe 7 Machi 2026 yenye Kauli Mbiu, Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi sasa.

 


📌Umegharimu bilioni 11 na kuingiza umeme gridi ya Taifa.

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenan Kihongosi ameipongeza Wizara ya Nishati kwa utekelezaji wa mradi wa umeme jua wenye thamani ya shilingi bilioni 11 unaoingiza megawati tano (5) katika Gridi ya Taifa.

Kihongosi ametoa pongezi hizo mara baada ya kutembelea mradi huo uliopo katika Kijiji cha Kayenze, Jimbo la Ushetu wilayani Kahama, akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Shinyanga.

“Naipongeza Wizara ya Nishati kwa mradi huu wenye tija ambao ni sehemu ya vielelezo vya utekelezaji wa miradi ya nishati safi kwa ajili ya wananchi. Kupitia mradi huu tunaendelea kuona dhamira ya Serikali ya kupeleka maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini,” amesema Kihongosi

Aidha, amemshukuru na kumpongeza Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake yaliyowezesha kukamilika kwa miradi mbalimbali ya kimkakati ikiwemo mradi wa Julius Nyerere unaozalisha megawati 2,115 pamoja na mradi wa umeme jua wa Kishapu ambapo awamu ya kwanza imekamilika na kuanza kuzalisha megawati 50.

Kihongosi pia amempongeza Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba pamoja na viongozi wengine  kwa usimamizi madhubuti unaoifanya sekta ya nishati kuwa imara na yenye utulivu, huku akisisitiza kasi ya utekelezaji wa miradi kuendelea.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati na Mbunge wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Salome Makamba amesema umeme unaozalishwa katika mradi huo unaingizwa kwenye Gridi ya Taifa kupitia njia ya msongo wa kilovolti 33 (33kV). Ameongeza kuwa mradi huo ulikamilika mwezi Mei 2025 na kuanza kufanya kazi mara moja.

Ameeleza pia kuwa pamoja na kusaidia kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme, mradi huo umechangia maendeleo ya jamii kwa kujenga jengo la zahanati katika Kijiji cha Kayenze kwa gharama ya shilingi milioni 130.

Kuhusu usambazaji wa umeme katika Jimbo la Ushetu, Mhe. Salome amesema Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha kwa ajili ya kusambaza umeme katika vitongoji 136 jimboni humo, huku vitongoji takriban 100 vilivyosalia vitakuwa vimefikiwa na huduma hiyo ifikapo mwaka 2030.











 


Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ametembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) katika maonesho ya mafanikio ya siku 100 za uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na utatuzi wa kero za wananchi.

Maonesho hayo ya siku tatu yamefunguliwa leo machi 5, katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma, yakishirikisha taasisi mbalimbali za Serikali ikiwemo TEMESA, ambapo imewasilisha mafanikio yao katika utoaji wa huduma kwa wananchi na kutoa elimu kuhusu majukumu yao.

Akiwa katika banda la TEMESA, Mhe. Senyamule alipata maelezo kuhusu shughuli mbalimbali zinazofanywa na TEMESA pamoja  na mafanikio ya Wakala kutoka kwa Meneja Masoko na Uhusiano kwa Umma, Bi. Martha Joachim.

Akitoa ufafanuzi huo, Bi. Martha amesema TEMESA imepiga hatua katika kuboresha utoaji wa huduma za kiufundi kwa taasisi za Serikali kupitia matumizi ya mifumo ya kisasa na ya kidijitali.

Ameeleza kuwa miongoni mwa mafanikio hayo ni matumizi ya Mfumo wa Usimamizi wa Kazi za Matengenezo (MUM), unaosaidia na kurahisisha ufuatiliaji wa shughuli za matengenezo kwa ufanisi zaidi.

“Mfumo huu umeongeza uwazi, ufanisi na kasi katika utoaji wa huduma za matengenezo, na kusaidia taasisi za Serikali kupata huduma bora zinazopelekea  kuwahudumia wananchi kwa ufanisi,” amesema.

Aidha, Bi. Martha ameongeza kuwa TEMESA inaendelea  kuboresha utendaji kazi wake, hasa katika huduma za matengenezo ya magari ya Serikali, usimamizi wa vivuko pamoja na miundombinu ya umeme katika taasisi mbalimbali za Umma.





Na Oscar Assenga,TANGA

Uzinduzi wa Kamati ya Ushauri wa Masuala ya Kisheria ngazi ya Mkoa itaanza Machi 9 hadi 15 katika viwanja vya Tangamano Jiji Tanga huku Jopo Mawakili wa Serikali 40 wanatarajiwa kusikiliza kero sugu za kisheria ambazo zitatolewa ufafanuzi wa kisheria na hatimaye kufungwa na hatimaye kuweza kuzimaliza.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Batilda Burian wakati akieleza kuhusu uzinduzi wa Kamati ya Ushauri wa Masuala ya Kisheria ngazi wa Mkoa Bila Malipo itakayofanyika kwenye viwanja vya Tangamano Jijini Tanga ikianza Machi 9 hadi 15 mwaka huu huku akiwataka wananchi wote .

Alisema kamati hizo zinalenga kutoka huduma kwa wananchi na watuumishi wa umma ,viongozi wa umma na wengine bila kubagua ili kutatua changamoto za kisheria zinazojitokeza huku akieleza itasadia kupunguza mashauri au migogoro dhidi ya Serikali katika ngazi ya mikoa na wilaya.

“Lakini kama mtakumbuka Rais Dkt Samia Suluhu alituma jopo la wanasheria kutoa Wizara ya sheria wakiongozwa na Waziri kwa ajili ya kuzindua kliniki za sheria mkoa lakini ofisi ya Mwanasheria mkuu wa Serikali alituma jopo la wanasheria kutoka ofisi yake na waliopo kwenye mikoa kushirikiana na wanasheria wengine wa kujitolea hapa Tanga”Alisema .

“Kama mtakumbuka hivi karibuni Waziri Mkuu alianza ziara ameenda Arusha na Manyara migiogoro ni mingi wenzetu hawa wamekuja kusaidia kutoa  suluhu za kisheria na kuwasaidia wananchi na zitakutanaisha mawakili wa serikali na taasisi mbalimbali kuwasaidia wananchi wenye changamoto mbalimbali”Alisema

Hata hivyo alisema kwamba huduma hiyo itawezesha kupunguza malalamiko kwa wananchi na hata jopo hilo likiondoka utaratibu huo utaendelea na zoezi hilo  litafanyika bila malipo kwa hiyo wananchi wajitokeze kwa wingi wenye malalamiko ikiwemo mabando yenye malalamiko yawabebe na yawe na vielelezo vya kutosha.

Alieleza kwamba hiyo yote ni ni muendelezo wa kazi nzuri anayoifanya Rais Dkt Samia Suluhu  na wanaendelea kumpongeza kuweza kulinda,kukuza na kutetea haki za wananchi wanyonge na kupinga vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora na kuhakikisha ukatili wa kijinsia unatokomezwa.

Mkuu huyo wa mkoa alisema pia  lakini kuheshimu utawala wa sharia ambao ndio msingi wa maendeleo kwenye mkoa huo wanaendeela kupongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuhakikisha kamati ya ushauiri wa kisheria kwenye mkoa wa Tanga inazinduliwa na kuanza kutioa huduma kwa wananchi wote bila kujali uwezo wao wa kifedha .



Mwisho.

Mkutano Mkuu wa 12 wa Umoja wa Maafisa Elimu wa Mikoa na Halmashauri Tanzania Bara (REDEOA) umeendelea kufanyika jijini Arusha kwa siku saba tangu ulipofunguliwa rasmi Machi 2, 2026 na Waziri wa Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Profesa Riziki Shemdoe.
Wanawake wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dar es Salam  wametembelea Gereza la Segerea na kutoa misaada mbalimbali kwa wafungwa, ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa kila mwaka Machi 8.
Ziara hiyo pia imekuwa muendelezo wa maadhimisho ya miaka 25 ya chuo hicho, ambapo taasisi imekuwa ikitekeleza shughuli za kurejesha kwa jamii kupitia matendo ya kijamii na misaada kwa makundi yenye uhitaji.
Akizungumza wakati wa kukabidhi misaada hiyo, Zena Hussein, Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC, aliyemwakilisha Mkuu wa Chuo, amesema wanamshukuru Mkuu wa  chuo kwa kuwawezesha kutekeleza jukumu hilo la kijamii, akieleza kuwa lengo ni kuonyesha upendo na mshikamano kwa wafungwa kama sehemu ya jamii.
Amesema kuwa, kama wanawake wafanyakazi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, wameona umuhimu wa kutambua kundi hilo na kujitoa kwa moyo wa huruma wakiamini kuwa si kila aliyepo gerezani ni mkosaji wa kukusudia, bali baadhi yao wamejikuta katika mazingira magumu yasiyotegemewa. Ameongeza kuwa misingi ya dini, kwa Waislamu na Wakristo, inahimiza kusaidia wahitaji na kuwa watoaji, hivyo wameamua kupeleka kile walichoweza kumudu.
Miongoni mwa misaada iliyotolewa ni sukari, mchele, unga, maharage, maji, dawa za usafi, khanga, mashuka ya watoto, ndala, mifagio, dawa za meno, mafuta ya kupaka, pedi za wanawake, nepi za watoto, maziwa ya watoto, vitabu vya dini ikiwemo Qur’an na Biblia pamoja na nguo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza la Wanawake Segerea, SSP Hamida Mussa Matimba, ameishukuru TPSC kwa msaada huo akisema vitabu vya dini vitakuwa nguzo muhimu katika kuwajenga wafungwa kiimani na kuwasaidia katika mchakato wa mabadiliko chanya.
Alieleza kuwa gereza hilo linaendesha programu mbalimbali za mafunzo ya ufundi stadi ikiwemo ushonaji, upishi, ufyatuaji wa matofali, ujenzi, ufundi magari na umeme, akisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha kila anayeingia gerezani anatoka akiwa na mabadiliko chanya ya kiimani, kimaadili na kiujuzi ili aweze kujitegemea anaporejea uraiani.
Aidha, aliwahimiza wanawake kuwa na moyo wa kusamehe ili kupunguza migogoro inayoweza kuishia kwenye vyombo vya sheria, akitolea mfano wa migogoro ya madeni katika vikundi vya mikopo. Pia alitoa wito kwa wazazi kuwalea vijana, hususan mabinti, katika misingi ya maadili na kuwajenga kuridhika ili kuepuka tamaa zinazoweza kuwaingiza katika matatizo ya kisheria.
Kaulimbiu ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka 2026 inasema: “Haki na usawa kwa wanawake na wasichana ni msingi jumuishi kufikia Dira 2050.” Ziara hiyo imeakisi dhamira ya wanawake wa TPSC ya kuadhimisha siku hiyo kwa vitendo vinavyogusa jamii moja kwa moja
Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC,Zena Hussein (kushoto) akikabidhi
Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC,Zena Hussein akizungmza wakati kukabidhi misaada huo.
Mkuu wa Gereza la Wanawake Segerea, SSP Hamida Mussa Matimba akizungumza  wakati wa kukabidhi misaada huo. 
 
 

Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:

“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”

(“Mimea ya Dawa na Harufu na Mchango Wake kwa Ustawi wa Binadamu: Njia ya Mbele ya Matumizi Endelevu”)

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.

Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:

• Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.

• Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.

• Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

• Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.

Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:

“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”

Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.

TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU 

Imetolewa na: Boniventura Mwalongo

Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO)

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), yatakiwa kuongeza kasi ya urasimishaji wa biashara na kuimarisha mifumo ya kidijitali ili kuchochea ufanisi na ukuaji wa uchumi kwani BRELA ni lango kuu la uwekezaji nchini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), Machi 04, 2026, wakati akifungua Baraza la wafanyakazi la BRELA na kuhimiza uwekezaji kwenye rasilimali watu, akitaka watumishi wapewe mafunzo na stahiki zao kwani ustawi wa wafanyakazi ndio siri ya mafanikio ya taasisi, na kuwataka watumishi kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, na uzalendo.

Waziri Kapinga amebainisha kuwa kwa mujibu wa tafiti mbalimbali za wadau, zaidi ya 80% ya biashara nchini zipo sekta isiyo rasmi, hivyo BRELA lazima iwe kinara wa kuzirasimisha, hatua ambayo itawawezesha Wajasiriamali wadogo kupata mikopo, masoko, na ulinzi wa kisheria.

Aidha, ameagiza kuhuisha mifumo ya TEHAMA ili iwe rafiki itakayopunguza gharama pamoja na muda wa mteja kupata huduma na kusisitiza kuwa mifumo hiyo lazima iwe na usalama wa taarifa wa hali ya juu na itumike kupata mrejesho wa haraka kutoka kwa wateja ili kuboresha utendaji.

Aidha, ameipongeza BRELA kwa ongezeko la usajili na makusanyo, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyakazi na kuitaka taasisi hiyo kugeukia mfumo wa uwezeshaji badala ya udhibiti pekee ili kukuza sekta binafsi nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa BRELA Bw. Godfrey Nyaisa amebainisha kuwa BRELA imevuka lengo la mapato kwa asilimia 105 na kutekeleza malengo kwa asilimia 78 katika nusu mwaka wa 2025/26, ambapo taasisi hiyo imewasilisha Shilingi bilioni 3.1 kwa Msajili wa Hazina, na kusema mafanikio hayo yanayotokana na mshikamano, kujituma na bidii ya watumishi.

Vilevile, amewasilisha Mpango Mkakati wa 2026–2031 unaolenga kuboresha za usajili na miundombinu, ikiwemo ujenzi wa ofisi za Dodoma na Kinondoni na kubainisha kuwa uongozi unaendelea kuimarisha maslahi ya watumishi kupitia muundo mpya wa mishahara na motisha ili kutatua changamoto za uhaba wa wafanyakazi na kuongeza tija.