Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Bw. Patience Ntwina (kushoto) akibadilishana nyaraka na Mkurugenzi Mtendaji wa MISA TAN Bi. Elizabeth Riziki baada ya kutia saini mkataba wa ushirikiano baina ya taasisi hizo mbili.
KILINGE Salama (Safe Space) kilichoandaliwa na Mtandao wa Kijinsia Tanzania (TGNP) Chamwibua Diwani, Farida Abdallah ambaye ni Diwani wa wilaya ya Mtwara ambapo ameeleza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wanawake viongozi ikiwemwo kukatishwa tamaa ili wasiweze kugombea nafasi mbalimbali za uongozi.
Akizungumza leo Machi 28, 2024 wakati wa kilinge salama kilichofanyika katika ukumbi wa TGNP jijini Dar es Salaam, Diwani huyo ambaye aliishia kidato cha pili na kupata ujauzito huku akimpote Mama yake mzazi amewaasa wanawake kutokukata tamaa pale yanapojitokeza maneno ya kukatisha tamaa pale yanapojitokeza wakati wa harakati za kutafuta nafasi za uongozi.
“Wakati nawania nafasi ya uongozi watu walikuja kunikatisha tamaa ili ni sigombee….. hata kwenda kumshawishi Mme wangu ili anikatishe tamaa lakini hawakufanikiwa….” Amesema Farida.
Kwa Upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Lilian Liundi akizungumza wakati wa kufungua Kilinge salama ambapo ni mazingira ambayo ni rasmi au yasiyo rasmi ambayo wanawake na wasichana wanapata nafasi ya kujadili kwa uhuru masuala yao, amesema kuwa Katika mwezi Machi wa wanawake, TGNP imekuwa ikiandaa vilinge hivyo ili kuhamasisha wanawake kuingia katika nafasi za uongozi.
“Mategemeo yangu ni kwamba mwisho wa siku ya leo tutaungana kwa pamoja kuendelea kusimamia Agenda ya mwanamke na uongozi katika mkoa wetu wa Dar es Salaam.”
Pia Mkurugenzi Mtendaji Lilian ameweka bayana takwimu za Wenyeviti wa vijiji kuwa ni asilimia 2.1, Wenyeviti vitongoji ni asilimia 6.7 na Wenyeviti mitaa ni asilimia 12.6.
Kwa upande wa Wabunge wa kuchaguliwa, wanawake ni 25 ya Wabunge 264 ambayo ni sawa na asilimia 9.5 tu ya Wabunge wote, idadi ya Wabunge wanawake wa Viti Maalumu ni 113 ambayo ni sawa na asilimia 29 ya Wabunge wote. Jumla ya Wabunge Wanawake ni 142 sawa na asilimia 37 ya idadi ya Wabunge wote ambao ni 393 ambapo ili kufikia 50 kwa 50 ya uongozi wa Wanawake Viongozi lazima ifikiwe kwa kutoa elimu kwa wanawake na wasichana waweze kuwania nafasi mbalimbali za uongozi.
Lilia pia ameeleza kuwa malengo ya Kilinge salama kwa Wasichana na Wanawake ni kukaa pamoja na viongozi wanawake wanaochipukia na viongozi wanawake wenye uzoefu, kuandika na kusambazi kestoria za safari za uongozi za wanawake viongozi mahiri ili kuonesha michango waliyonayo katika maendeleo ya nchi.
Pia kutoa hamasa kwa viongozi wanawake wanaochipukia au wanawake wanaotamani kuwa viongozi.
Kilinge Salama kwa Wanawake na Wasichana pamoja na viongozi leo ni kutoka mkoa wa Dar es Salaam, halmashauri za Ilala, Kinondoni na Temeke, Mtwara, Lindi na Pwani.
Na Ashrack Miraji
Mkuu wa Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro Kasilda Mgeni ameagiza Maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wilayani humo kutumia ubunifu, weledi pamoja na busara katika kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi kwa baadhi ya wafanyabiashara ambao sio waadilifu.
Mkuu huyo wa wilaya amebainisha hayo katika kikao cha kamati ya ushauri wa kodi cha wilaya na kusisitiza kuwa mfanyabiashara yeyote atakaye bainika kuendelea kukiuka kulipa kodi taarifa iwasilishwe Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yake.
Amesema suala la ulipaji kodi ni wajibu wa kila mwananchi kisheria ili kusaidia Serikali kupanga shughuli za kuwaletea wananchi wake maendeleo, akihimiza TRA kuwa wabunifu katika ukusanyaji mapato na kufanya operesheni za mara kwa mara kwa wafanyabiashara wote wilayani humo.
“TRA fanyeni operesheni za mara kwa mara kwa wafanyabiashara wote ambao wapo ndani ya wilaya ya Same na wanaostahili kutumia mashine za Kielektroniki (EFD) basi wanakuwa nazo na kwa wale ambao watakuwa wakaidi baada ya kuwafuatilia na kuwapa elimu basi sheria iweze kuchukua mkondo wake juu yao kwani hao ni wahujumu uchumi wa serikali”.
Kwa upande wake meneja wa TRA wilaya ya Same Eliapenda Mwanri amesema ufanisi wa utendaji unatokana na ziara za mara kwa mara za mkuu wa wilaya na kamati yake ya usalama ya kuwatembelea wafanyabiashara katika biashara zao kusisitiza utoaji wa risiti za kielektroniki, ulipaji wa kodi kwa wakati pamoja na kusikiliza na kutatua kero na changamoto za kibiashara, pia kupata maoni ya kuboresha biashara zao.
Kwa mwaka wa fedha 2023/24 TRA wilaya ya Same imekusudia kukusanya shilingi bilioni 4. 6 (4,637,450,937.77) sawa na ongezeko la asilimia 48% ikilinganishwa na makusanyo ya mwaka 2022/23 ambapo lengo lilikuwa ni shilingi bilioni 3.6 (3, 685, 320, 179.62).
Katika kipindi cha mwezi Julai 2023 hadi Februari 2024 imekusanya kiasi cha shilingi bilioni 2.2 (2, 240, 762, 028. 53) sawa na ufanisi wa asilimia 74.2% ya lengo la kukusanya shilingi bilioni 3.0 (3, 021, 651, 706. 79. na makusanyo haya sawa na ongezeko la asilimia 8.2 ikilinganishwa na kipindi kama hiko mwaka 2022/23 ambayo yalikuwa Shilingi Bilioni 2.0 (2, 070, 285, 159. 60).
Kocha Mkuu wa Timu ya Tabora United Denis Laurence amesema kuwa katika kipindi cha siku saba tangu alipojiunga na Timu anaridhishwa na viwango vya wachezaji kutokana na kujituma kwao kwenye mazoezi uwanjani.
Kocha Laurence amesema kuwa ameshangwaza kuona wachezaji kwa kipindi kifupi tangu alipojiunga na Timu hiyo yenye Makazi yake Mkoani Tabora wanamuonesha ushirikiano wakutosha nakusikiliza kila anachowaelekeza kwenye uwanja wa mazoezi na kwamba hajapata changamoto yoyote hadi sasa.
Ameongeza kuwa ushirikiano ambao wachezaji wanampa unatoa taswira njema kuelekea kwenye michezo tisa ya Ligi Kuu ya NBC Soka Tanzania Bara pamoja na michuano ya Kombe la Azam Sport Federation dhidi ya Singida Fountain Gate kufanya vizuri kwani ndio mkakati uliopo kwa sasa kama Timu.
“Nafurahi kuona wachezaji wananisikiliza vizuri, tunakwenda sawa ,tunazungumza Lugha moja , kwa huumuda mfupi ambao nimekuwa nao hapa kwangu ni maajabu, wanafuata ninachowaambia lakini pia wanafanyia kazi, hii kwangu ni kubwa sana kama kocha, muhimu nazidi kuwasisitiza kila mmoja ananafasi kwenye kikosi changu cha kwanza” amesema Kocha Laurence.
Ukiangalia kila mmoja anauwezo mkubwa, nahii ni kawaida kwa wachezaji wa Afrika, muhimu ninachokifanya ni kuwaweka kwa pamoja wacheze kitimu ili tuweze kushinda, morali na hari zao zipo juu hivyo ninafurahia sana kuwepo na wachezaji wangu mazoezini na mazingira yote kwa ujumla.
Aidha katika hatua nyingine Kocha Laurence amesema kuwa hadi sasa tayari ameshapata kikosi chake cha kwanza lakini akasisitiza sio ndio kitadumu milele hapana kwani mfumo wake ni kuhitaji kila mmoja aweze kucheza kweye michezo hii iliyosalia kabla ya kumalizika kwa msimu wa 2023/2024.
Tabora United itakuwa ugenini siku ya Aprili Nne katika Uwanja wa CCM Kirumba Mwanza ikiwakabili Singida Fountain Gate kwenye mchezo wa ASFC na badae Aprili 14 katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya JKT Tanzania utakaopigwa katika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi hapa Mjini Tabora.
Imetolewa leo Machi 28
Na Christina Mwagala
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano
Tabora United
Serikali kupitia Wizara ya Afya inaendelea kuimarisha ubora wa huduma za Afya ya mama na mtoto katika vituo 25 vinavyotoa huduma ya upasuaji wa dharura wa kumtoa mtoto tumboni (CEmONC) katika Mkoa wa Dar Es Salaam ili kupunguza vifo vitokanavyo na Uzazi.
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amesema hayo leo Machi 28, 2024 wakati akifungua mafunzo elekezi kazini juu ya huduma za Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto katika Mkoa wa Dar Es Salaam ambapo mafunzo hayo ni endelevu yanayotolewa nchini nzima ili kupunguza vifo vya mama mjamzito na mtoto.
“kuimarisha ubora wa huduma za Afya ya mama na mtoto katika vituo 25 vya Afya vinavyotoa huduma ya upasuaji wa dharura wa kumtoa mtoto tumboni yaani (CEmONC) tutakua tumetatua asialimia 84 ya changamoto za Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto kwa Mkoa wa Dar Es Salaam.” Amesema Waziri Ummy
Amesema, mafunzo haya ni muhimu sana ambayo yamesaidia kupunguza vifo katika katika Mkoa wa Tabora ambapo kwa mwaka 2023 vifo vya watoto wachanga vimepungua kutoka vifo 50 hadi vifo Vinne kwa miezi Mitatu, lakini pia mafunzo hayo yanasaidia kupeana mbinu mbalimbali za kuwahudumia vizuri wagonjwa ili kuendelea kupunguza vifo vitokanavyo na Uzazi.
“Mkoa wa Dar Es Salaam kwa Mwaka 2023 kulikua na vifo vya wajawazito 219, vifo vya watoto wachanga 1,701 hivyo tunaamini kupitia mafunzo haya tutapunguza takwimu hizi za vifo kwa zaidi ya asilimia 50, inawezekana.” Amesema Waziri Ummy
Aidha, Waziri Ummy amezitaka Halmashauri kutenga fedha kwa ajili ya kuwawezesha watoa huduma waliopatiwa mafunzo hayo ili waweze kwenda kutoa mafunzo hayo kwenye vituo vyao vya Afya vinavyotoa huduma ya upasuaji wa dharura wa kumtoa mtoto tumboni (CEmONC) vilivyobakia pamoja na Zahanati.
Pia, Waziri Ummy amezitaka kila Hospitali pamoja na Vituo vya Afya vinavyotoa huduma ya upasuaji wa dharura wa kumtoa mtoto tumboni (CEmONC) zianzishe wodi maalumu ya watoto wachanga inayofanya kazi kwa kuwa na vifaa tiba pamoja na watoa huduma waliojengewa uwezo.
“Jambo jingine nataka nisisitize, tutoe taarifa sahihi za vifo vya wajawazito, vifo vya watoto wenye umri chini ya miaka Mitano, vifo vya watoto wenye umri chini ya Mwaka Mmoja pamoja na takwimu sahihi za vifo vya watoto wachanga wenye siku 0-28.” Amesema Waziri Ummy
Mwisho, Waziri Ummy amesema, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anataka hadi kufika Mwaka 2027 tuwe tumepunguza vifo vya watoto wachanga kutoka 24 katika kila vizazi hai 1,000 hadi kufikia 12 katika kila vizazi hai 1,000 “hii inawezekana kupitia mafunzo haya, hatutamuangusha Rais Dkt. Samia.”
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hayo yameelezwa na msemaji wa familia ya hayati Edward Sokoine, Bw. Lembris Kipuyo alipokutana na kuzungumza na waandishi wa habari leo Machi 28, 2024 jijini Dodoma, kwa lengo la kuwaalika watanzania wote kwenye ibada maalum ya kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine.
Amesema ibada hiyo iliyoandaliwa na familia ikishirikiana na Taasisi ya Hayati Edward Moringe Sokoine itafanyika siku ya Ijumaa Aprili 12, 2024, saa 3:00 asubuhi katika Kijiji cha Enguik, Monduli Juu mkoani Arusha.
“Ibada hiyo ya kumbukumbu ya Hayati Sokoine itawashirikisha viongozi mbalimbali wa serikali wakiongozwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesema Bw. Kipuyo.
Amesema lengo kubwa la kuanzishwa kwa Taasisi ya Hayati Edward Moringe Sokoine ni kuenzi mema aliyoyafanya kwani aliacha alama kubwa ambayo taifa linamkumbuka hadi leo na kueleza kuwa taasisi hiyo imejikita katika masuala ya elimu, kilimo, hifadhi ya mazingira, vyanzo vya maji pamoja na afya.
Bw. Kipuyo amesema,“Hayati Sokoine alikuwa mzalendo wa kweli, alipenda taifa lake na wananchi wake, alihakikisha kwamba rasilimali za nchi zinatumika na watanzania wote, aliwatumikia wananchi bila kubagua na alikuwa na hofu ya Mungu katika kufanya kazi zake.”
Hayati Sokoine alikuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika vipindi viwili wakati wa uongozi wa awamu ya kwanza.
Hayati Sokoine alizaliwa Agosti 01, 1934, kijijini Enguik, Monduli Juu wilayani Monduli, mkoani Arusha na kufariki Aprili 12, 1984 kwa ajari ya gari katika kata ya Dakawa wilayani Mvomero mkoani Morogoro akitokea bungeni jijini Dodoma.
Mahakama ya Wilaya ya Mbulu imemhukumu Melkiadi Zakaria Tlehema aliyekuwa Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Hayloto kata ya Nambris, Wilaya ya Mbulu Mkoa wa Manyara.
Mshtakiwa ametiwa hatiani kwa makosa mawili ambayo ni Ubadhirifu na Matumizi Mabaya ya Madaraka, makosa hayo ni kinyume na kifungu cha 28 na kifungu cha 31cha Sheria Ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa sura ya 329 kama ilivyofanyiwa marejeo Mwaka 2022.
Hukumu hiyo dhidi ya Melkiadi Zakaria Tlehema, shauri la Uhujumu Uchumi Na 03/2023, imetolewa chini ya Mhe.Vitalis Eusebius Kapugi, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbulu – Machi 2, 2024.
Mshtakiwa ameamriwa kulipa faini ya shilingi 200,000/= au kwenda jela miezi mitano. Pia mshtakiwa ametakiwa kurejesha fedha alizofanyia ubadhirifu kiasi cha shilingi 1,869,500/=.
Mshatikiwa alifanya ubadhirifu kwenye fedha hizo kupitia makusanyo ya fedha za wananchi kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Msingi Hyloto.
Hata hivyo, Mshtakiwa amelipa faini na kurejesha kiasi cha fedha alichofanyia ubadhirifu hivyo ameachiwa huru.